Maisha Yetu Yenye Kuthawabisha Tukiwa Wamisionari Katika Afrika
Kama ilivyosimuliwa na John Miles
TAMASHA inayohusika ni hifadhi ya wanyama katika kaskazini-magharibi mwa Zimbabwe. Mke wangu, Val, na mimi tunaendesha gari kuelekea maporomoko-maji yanayojulikana sana kuwa Victoria Falls. Hapana, sisi si watalii. Sisi ni wamisionari na tumetumwa hapa kufanya kazi miongoni mwa Waafrika wenyeji. Tunapopiga kona moja, kumbe, ndovu mmoja mkubwa sana ndiye yule amesimama kando ya barabara. Mimi nazimisha gari na kuchomoa kichwa nje dirishani ili nipige picha. Nikiwa karibu kupiga picha nyingine Val anapiga ukelele hivi:
“Anatujia!”
Mimi nafanya haraka kuwasha gari, lakini linakataa kuwaka. Lo, ni muhali ulioje! Ndovu yule anafikia kikomo cha kutukimbilia na kurudi nyuma ili atukanyage-kanyage. Kwa wakati unaofaa kabisa enjini inawaka tena nasi tunakwepa kuingia vichakani. Kwa nasibu, hakuna mawe wala miti ya kuzuia ukimbizi wetu. Tunaamua kumwachia huyo Bw. Jumbo haki ya kuimiliki njia hiyo nasi tunasonga mbele kwa kufuata njia tofauti.
Tamasha nyingine. Wakati huu sisi tumo katika nchi yenye milima-milima ya Lesotho, Afrika kusini. Ni alasiri ya Jumapili katika mji mkuu, Maseru. Sisi tunarudi kwenye maskani yetu baada ya kufurahia kikusanyiko cha Kikristo pamoja na waitikadi wenzetu wa kienyeji. Kwa ghafula, tunashambuliwa na majizi vijana wawili. Mmoja ananipiga konde na yule mwingine ananirukia mgongoni. Mimi namtikisia mbali, naye amgeukia Val, akishika upesi mkoba wake. Val anaita kwa sauti kubwa: “Yehova! Yehova! Yehova!” Mara hiyo, mwanamume huyo anaachilia mkoba wa Val na kurudi nyuma akiwa amekodoa macho kwa kuduwaa. Mwenye kunipiga konde arudi nyuma pia—ngumi zake zikiwa zinapiga hewa. Sisi tunafanya haraka kwenda zetu, nasi tunatusha pumzi sana tunapokuta waitikadi wenzetu kwenye kituo cha basi.—Mithali 18:10.
Kila kimoja cha vituko vilivyotangulia kutajwa kilichukua muda wa dakika chache tu, lakini vimo miongoni mwa kumbukumbu nyingi zisizosahaulika za miaka 32 iliyopita ya kuwa kwetu wamisionari katika Afrika. Sisi tulifikaje hapa? Kwa nini tukawa wamisionari? Je! yamekuwa maisha yenye kuthawabisha?
Mwamerika Aliye Kibarua wa Shamba Ajifunza Ukweli
Yote yalianza katika 1939 wakati nilipokutana na Val Jensen katika Yakima, Washington, U.S.A. Wakati huo, mimi nilifanya kazi katika shamba moja, na Val aliajiriwa kuwa mtunza nyumba. Mara nyingi yeye alikuwa akiongea nami juu ya Biblia. Jambo moja lililonivutia lilikuwa elezo lake la kwamba hell si mahali penye moto. (Mhubiri 9:5, 10; Matendo 2:31; Ufunuo 20:13, 14) Ingawa mimi sikwenda kanisani, nilijua mambo ambayo viongozi wa kidini walifundisha juu ya hell, na yale ambayo Val alinionyesha kutokana na Biblia yalisikika kuwa ya kiakili.
Baba na mama ya Val walikuwa wamekuwa Mashahidi wa Yehova katika 1932. Val pia alianza kujifunza Biblia, na alibatizwa katika Septemba 1935. Baada ya sisi kufahamiana, Val alinialika niende mikutanoni kwenye Jumba la Ufalme. Mimi nilikubali na nikafurahia ushirika pamoja na watu niliokuta huko, yaani, wakati wo wote ambapo kazi ya shamba ingeniruhusu kwenda. Maisha ya shamba bado yalikuja kwanza katika maisha yangu. Ingawa hivyo, pole kwa pole nilianza kuwa na rai nzito juu ya mikutano, na Mashahidi wa mahali pale walinialika kushiriki katika kazi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba. Kufanya hivyo katika mji wa maskani ya kwetu kulionekana kuwa mtihani mkubwa mno kwangu. Lakini mimi niliupita.
Mambo mawili ya kukumbukika yalitukia katika 1941. Katika Machi, nilibatizwa kuwa shahidi aliye wakfu wa Yehova, na baadaye Val na mimi tukafunga ndoa. Halafu, katika Oktoba 1942, tukaanza katika kazi ya kuhubiri wakati wote tukiwa mapainia katika sehemu ya kusini mashariki ya Dakota ya Kaskazini.
Sisi hatutasahau kamwe jambo lililotukia mwaka uliofuata. Lilikuwa hatua kubwa katika historia ya Mashahidi wa Yehova. Katika Februari 1, 1943, mazoezi ya umisionari yalianza kwa ajili ya darasa la kwanza la ile ambayo wakati huo iliitwa Koleji ya Biblia ya Gileadi ya Mnara wa Mlinzi. Miezi miwili baadaye sisi tulihudhuria “Mwito Kwenye Kitendo” kusanyiko katika Aberdeen, Dakota ya Kusini. Baraka za utumishi wa misionari katika mabara ya kigeni zilisimuliwa, na tamaa ya kuhudhuria Gileadi na kuwa wamisionari ikaamshwa katika mioyo yetu.
Kufanya Kazi Kuelekea Ule Mradi wa Utumishi wa Misionari
Miaka tisa ingepita kabla sisi hatujafikia mradi wetu. Katika wakati huo, tulikuwa na mapendeleo mengine mazuri ya utumishi, na pia vipingamizi fulani. Baada ya kupainia kwa mwaka mmoja na nusu katika Dakota ya Kaskazini, tulijaza ombi la eneo la upainia katika Missouri. Ombi hilo lilikubaliwa, nasi tukalowea katika jiji la Rolla. Eneo letu lilitia ndani sehemu nzima ya Manispaa ya Phelps ambako kulikuwa na Shahidi mmoja tu mtendaji. Sisi tulitumia huko miaka mitatu yenye kufurahika na tukashiriki katika kuanzishwa kwa kundi moja.
Ndipo tulipoelekeana uso kwa uso na tatizo lililofifisha matumaini yetu ya kuwa wamisionari. Mali zetu zilimalizika. Usimamizi mbaya na ukosefu wa imani kwamba Yehova angetuandalia ulisababisha tuache kupainia. Madhumuni yetu yalikuwa kwamba tuache kwa miezi michache tu, lakini mwaka mmoja na nusu ulipita kabla hatujaanza kupainia tena. Wakati huu sisi tulipiga moyo konde tusirudie makosa yetu ya wakati uliopita. Mgawo wetu mpya ulikuwa pamoja na kundi moja katika mji wa Reardan katika Mkoa wa Washington mashariki. Kazi ya nusu-siku ilikuwa ngumu kupatikana, kwa hiyo sisi tulihitaji kumtegemea sana Yehova ili atuandalie mahitaji yetu ya kila siku.—Mathayo 6:11, 33.
Eneo letu lilitia ndani miji kadhaa midogo-midogo katika ujirani huo. Siku moja tulilazimika kufunga safari ya kilometa 130 ili tuzuru watu tukiwa na ujumbe wa Ufalme. Petroli tuliyokuwa nayo haikuwa ya kutosha lakini hatukuacha jambo hilo lituzuie. Tulipokuwa njiani kutoka mjini, tulisimama kwenye ofisi ya posta, nawe unafikiri tulipata nini? Barua moja ilikuwa ikitungojea hapo kutoka kwa binamu yangu aliyekuwa ndiyo sasa tu ameanza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi. Ilikuwa na hundi ya pesa za kutosha kujazia tangi letu na kubakia. “Sisi tulitaka kutoa upaji huu uwe wa Mji wa Boy,” wao wakaandika, “lakini tukaamua ninyi mliuhitaji zaidi ya Baba Flanagan.” Walisema kweli kabisa!
Maono kama hayo yalikazia ukweli wa ahadi ya Yesu: “Tafuteni ufalme [wa Mungu] kwa uendelevu, na vitu hivi [mahitaji ya kimwili] vitaongezwa kwa ninyi.” (Luka 12:31, NW) Hayo yalikuwa mazoezi yenye kuthamanika ambayo yangetusaidia tuendelee tujapopatwa na matatizo mengine.
Majira mamoja ya kipupwe, tulikuwa na kiasi kidogo tu cha makaa-mawe. Je! sisi tungeruhusu hali hiyo ibadili hali yetu ya kupiga moyo konde kuendelea kupainia? Tuliweka jambo hilo kwa Yehova katika sala na tukaenda kulala. Saa kumi na mbili ya asubuhi iliyofuata, mlango wetu ulipigwa hodi! Alikuwa ndugu mmoja na mke wake ambao, baada ya kurudi kutoka safari ya kwenda kwa watu wa ukoo wao, walikuwa wameamua kutuzuru. Sisi tulichokora-chokora moto uliokuwapo, tukaweka kipande cha mwisho tulichokuwa nacho cha makaa-mawe, na kutayarisha birika ya chai. Tulipokuwa tukifurahia ushirika wao, ndugu yule akauliza kwa ghafula hivi, “Ninyi mna makaa-mawe ya kadiri gani?” Val na mimi tulitazamana na kuanza kucheka. Makaa-mawe ndicho kitu kile hasa tulichohitaji mara hiyo. Wao walitupa sisi dola kumi, ambazo katika siku hizo zingelipia angalau nusu tani ya makaa-mawe.
Katika pindi nyingine kusanyiko la mzunguko lilikuwa likikaribia, na tulikuwa na dola tano tu mkononi. Pia, leseni ya gari letu ingehitaji kulipiwa mara tu baada ya kusanyiko hilo. Sisi tuliamua kuweka kwanza mambo yaliyo ya kwanza na kuhudhuria kusanyiko hilo. Shukrani ziende kwa roho ya ukarimu ya akina ndugu, tulirudi kwenye mgawo wetu tukiwa na dola 15. Leseni hiyo iligharimu dola 14.50!
Sisi tulifurahia utumishi wetu wa painia katika mashariki ya Washington, na hatimaye hesabu fulani ya jamaa tulizojifunza nazo Biblia zikawa mashahidi washikamanifu wa Yehova. Hata hivyo, baada ya kuwa katika mgawo huo miaka miwili nilipokea barua kutoka Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi ikitaarifu kwamba mimi nilikuwa nimependekezwa kutumikia nikiwa mhudumu mwenye kusafiri, yaani, mmoja anayeyazuru na kuyatia moyo makundi ya Mashahidi wa Yehova katika mzunguko. “Ikiwa utawekwa rasmi, je! wewe utakubali mgawo huu?” Sosaiti ikauliza, ikiongezea hivi: “Tafadhali tujulishe mara moja.” Ni wazi kwamba jibu langu lilikuwa ndiyo. Kuanzia Januari 1951, tulitumia mwaka mmoja na nusu katika mzunguko wenye eneo kubwa sana lenye kuhusisha ndani nusu ya magharibi mwa Dakota ya Kaskazini na nusu ya mashariki mwa Montana.
Wakati wa kipindi hicho, tulipokea mshangazo mwingine—mwaliko wa kuhudhuria darasa la 19 la Gileadi! Je! tamaa yetu ingetimizwa mwishowe? Loo jamani, barua nyingine ikafuata ikisema kwamba darasa lilikuwa limejazwa ndugu kutoka nchi nyinginezo. Hicho kilikuwa kipingamizi, lakini sisi hatukuachwa! Miezi michache baadaye, tulipokea mwaliko kwenye darasa la 20 nasi tukakubaliwa humo katika Septemba 1952.
Kutoka Gileadi Kwenda Afrika
Tulithamini kama nini wema wa Yehova katika kutuleta tuwe pamoja na wanafunzi zaidi ya mia moja kutoka sehemu nyingi za dunia—Australia, New Zealand, India, Thailand, Ufilipino, Skandinavia, Uingereza, Misri, na Ulaya ya Kati. Hiyo ilitusaidia tuone kadiri ambayo Yehova alikuwa akihubirisha ule ujumbe wa Ufalme.—Mathayo 24:14.
Wakati wa kuwa kule Gileadi ulipita haraka, nasi tukahitimu katika Februari 1953. Tukiwa pamoja na wanne wengine, tuligawiwa kwenda Rhodesia ya Kaskazini (ambayo sasa ni Zambia) katika Afrika. Ingawa hivyo, Sosaiti ilituruhusu kwa fadhili tukae katika United States kwa ajili ya mkusanyiko wa kimataifa ambao ungefanywa Yankee Stadium baadaye mwaka huo katika Julai. Wakati wa miezi iliyotangulia mkusanyiko huo na kwa kitambo fulani baadaye, mimi nilitumikia nikiwa mwangalizi wa mzunguko katika Oklahoma ya mashariki.
Katika Novemba 1953, Val na mimi, pamoja na wamisionari wengine sita, tulipanda meli ya shehena yenye kuelekea Afrika. Tulifika nchi kavu kule Durban, Afrika Kusini, na kusafiri kaskazini kwa gari-moshi kwenda Rhodesia ya Kusini (ambayo sasa ni Zimbabwe). Hapo wawili walituacha wakaanze migawo yao katika Salisbury (ambayo sasa ni Harare), na tuliobakia tukasonga kwenda Kitwe, Rhodesia ya Kaskazini.
Val na mimi tuligawiwa kwenda kwenye mji wa Mufulira ulio na migodi ya madini ambako kulikuwa na jamaa chache zenye kupendezwa lakini bila kundi. Yehova alibariki kazi yetu ya kuhubiri nyumba kwa nyumba. Tulianza mafunzo mengi ya Biblia na baada ya muda mfupi watu kadhaa wenye kupendezwa wakaanza kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Baada ya miezi kadhaa tuliitwa tujazie nafasi-wazi kwenye ofisi ya tawi ya Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi katika Luanshya. Baadaye, tulipewa mgawo mwingine tutumikie tukiwa wamisionari katika Lusaka. Tulipokuwa huko, mimi nilitumikia mara kwa mara nikiwa mwangalizi wa mzunguko kwa ajili ya ile hesabu ndogo ya makundi yenye kunena Kiingereza.
Maisha ya Kuthawabisha Katika Sehemu za Vichakani
Halafu, katika 1960, sisi tulihamishwa kwenda Rhodesia ya Kusini ambako mimi niligawiwa kutumikia nikiwa mwangalizi wa wilaya miongoni mwa ndugu weusi. Kwa sehemu, hiyo ilihusisha ndani kuzuru makundi na kufanya uangalizi juu ya makusanyiko ya mzunguko na mikusanyiko ya wilaya. Yaliyo mengi ya makundi hayo yalikuwa katika sehemu za mashambani, kwa hiyo ilikuwa lazima sisi tujifunze kuishi huko vichakani. Tulihisi kwamba ikiwa ndugu zetu wangeweza kuishi vichakani hata sisi tungeweza.
Ofisi ya tawi ya Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi ilitupa sisi kifaa cha gari aina ya pikapu la tani moja na nusu. Sehemu ya nyuma ilikuwa imefunikwa kwa shiti ya metali ikiwa na milango maradufu ya kuingizia mizigo. Madirisha yaliyokuwa kati ya sehemu ya dereva na upande wa nyuma yalikuwa ya kadiri inayotosha tu kupita ndani, nayo yalifunikwa kwa mapazia ya plastiki. Vifaa vyetu vya kinyumbani vilikuwa kitanda kilichojengwa ndani pamoja na godoro sponji-sponji. Tulikuwa na kabati za muundo wa masanduku na stovu yenye kuwashwa kwa kutumia mafuta-taa. Pia tulikuwa na kifaa chenye kubebeka cha kuchukulia nguo na hema.
Muda mfupi baada ya kuanza mgawo wetu katika sehemu ya magharibi ya nchi, mimi niliumwa na mdudu asiyejulikana. Yeye alisababisha mguu wangu ufure na kuniletea homa kali. Kuongezea ubaya, hali ya hewa iligeuka kuwa mbaya na mvua ikaanza kunya kweli kweli. Mimi nilikuwa nikitoka jasho sana hata ikawa lazima matandiko yabadilishwe mara nyingi. Karibu usiku wa manane, Val aliamua kwamba napaswa kuona daktari. Yeye aliendesha gari kuelekea barabara kuu, lakini gari likakwama katika matope. Ikawa lazima mimi nitikisike kweli kweli wakati Val alipokuwa akifanya jitihada za kujaribu kulisukuma mbele au nyuma. Aliposadiki kwamba hangeweza kufanya jambo lolote jingine, yeye alijifungilia blanketi la mwisho lililobaki likiwa kavu na akajiunga nami katika gari huku ile mvua ikiwa bado inagonga chini kweli kweli.
Asubuhi kukawa na kitulizo. Mimi nilikuwa nikihisi nafuu, mvua ilikuwa imeacha kunya, na akina ndugu waliowasili kutayarisha kusanyiko walisukuma gari letu wakaliondoa katika matope. Katika Bulawayo ndugu wengine wenye fadhili walinipeleka hospitali, na baada ya matibabu niliweza kurudi na kuendelea na mipango ya kusanyiko.
Ilikuwa katika kipindi hicho, tulipokuwa tukisafiri kati ya makundi, kwamba tukapatwa na ule mkabiliano pamoja na ndovu. Tulikabiliana pia na viumbe wengi wadogo zaidi. Baadhi ya wageni wenye kuzuru hema letu, mbali na mainzi na mbu, walikuwa chungu wa mavuno. Katika muda mfupi sana, wao wangeweza kutoboa vitundu katika nguo au kitambaa cha namna yoyote kilichoachwa kikiwa ardhini. Aina mbalimbali za mijusi na buibui wa mawindo waliotuzuru walikuwa wasiodhuru, lakini fira aliyeingia ndani aliondoshwa humo haraka. Pia nge walikuwa wasiokaribishwa. Val anaeleza kwamba hisia inayopata mtu anapoumwa nao ni kama kupigiliwa kwa nyundo nzito msumari mwekundu uliokuwa ndani ya moto. Sharti yeye ajue hivyo. Yeye ameumwa mara nne!
Labda vitu hivyo vinafanya maisha ya vichakani yasikike kuwa yasiyothawabisha hata kidogo, lakini sisi hatuna rai hiyo. Kwetu sisi, yalikuwa maisha ya mahali peupe penye hewa safi, yenye utendaji na afya, na zile baraka za kiroho zinayapita kwa mbali mambo yoyote ya kukosa starehe za kimwili.
Sikuzote lilikuwa jambo la kuimarisha imani kuona jitihada iliyofanywa na ndugu wa mashambani kuhudhuria mikutano. Kundi moja lilikuwa la vikundi viwili vyenye kuishi kilometa 23 mbali mbali, kukiwa na kijia kimoja tu cha kuviunganisha. “Jumba la Ufalme” lao, lililokuwa katikati wa vikundi hivyo, lilikuwa mti mmoja mkubwa uliowapa kivuli ukiwa na mawe ya kukalia. Akina ndugu kutoka kila kikundi walitembea kilometa 11.5 kutoka pande zote mbili ili wahudhurie mikutano yao mara mbili kwa juma. Sisi tunakumbuka pia wale mume na mke wazee-wazee waliotembea kilometa 120 wakiwa na masanduku ya nguo na blanketi zao ili kuhudhuria kusanyiko la mzunguko. Hivyo ni vielelezo viwili tu vya jinsi ndugu Waafrika wanavyothamini lile onyo la upole, ‘kutoacha kukusanyika pamoja.’—Waebrania 10:25.
Katika maeneo fulani wenyeji walitia shuku juu ya kusudio letu, baadhi yao hata wakiona uchungu juu ya kukaa kwetu katika ujirani wao. Katika pindi moja, mimi nilipiga hema karibu na uwanja wa kusanyiko katika kisehemu chenye kuzungukwa na nyasi ndefu. Baada ya kipindi cha kusanyiko kuwa kimemalizika nasi tukawa kitandani kwa muda wa saa kadha, mimi niliamshwa na kelele fulani nje. Kwa kutumia kurunzi (tochi) yangu niliweza kung’amua umbo la mtu fulani akiwa amesimama nyuma ya mti mdogo.
“Wewe unataka nini?” nikaita kwa sauti. “Kwa nini wewe unajificha nyuma ya mti huo?”
“Sh-h-h ndugu,” likaja jibu, “sisi tulisikia watu fulani wakisema wangewasha moto kwenye nyasi hizi. Kwa hiyo sisi tumepanga kitengenezo kuwe na walinzi wa kuwalinda ninyi wakati wa usiku.”
Wao hawakuwa wametuambia juu ya hatari hiyo ili wasivuruge usingizi wetu. Na bado walikuwa na nia ya kukosa usingizi wao ili watulinde sisi salama! Kusanyiko lilipoisha alasiri ya Jumapili, wao walipanga kwamba gari moja liendeshwe likiwa mbele yetu na jingine likiwa nyuma yetu mpaka tulipoondoka kwenye lile eneo la hatari.
Lilikuwa jambo la kuthawabisha pia kuona thamani ambayo watu hao wanyenyekevu wanaweka juu ya Biblia. Kundi moja tulilotumikia lilikuwa katika eneo moja ambamo wanakijiji walikuza njugu. Wakati wa juma, tulibadilishana fasihi na Biblia kwa masanduku ya njugu zisizoondolewa maganda. Ziara yetu ilipomalizika, tulipakia vifaa vyetu, fasihi, na njugu na kuanza kusafiri kwenye sehemu ile nyingine ya kusanyiko. Muda mfupi baada ya kuondoka kwenye eneo hilo, tuliombwa tusimame kwa sababu mtu fulani alikuwa akijaribu kutufikia. Tulisimama na kungojea. Kumbe akawa ni bikizee mwenye kubeba sanduku la njugu juu ya kichwa chake. Alipotufikia, yeye alikuwa amechoka mno hata akaanguka chini na kulazimika kulala hapo mpaka alipoweza kuanza kupumua kikawaida. Ndiyo, yeye alitaka Biblia! Sisi tukalazimika kuondoa-ondoa karibu kila kitu, lakini ilikuwa raha kutosheleza tamaa yake. Biblia nyingine moja ikawa ndiyo hiyo katika mikono yenye upendo—na sanduku moja zaidi la njugu likawa ndilo hilo ndani ya sehemu ya kubebea mizigo ya gari letu!
Lilikuwa jambo zuri sana pia kuona jinsi Yehova alivyotokeza waangalizi wa mizunguko ili kuzuru yale makundi mengi katika sehemu zile za vichaka vya Kiafrika. Wakati huo ilikuwa vigumu Sosaiti kupata ndugu wenye kustahili wasiokuwa na wajibu mbalimbali wa kijamaa. Kwa hiyo halikuwa jambo lisilo la kikawaida mwangalizi mwenye kusafiri kwenda kutoka kundi mpaka kundi, kwa basi au kwa kuendesha baiskeli, akiwa na mke wake na watoto wawili au watatu, masanduku ya kuchukulia nguo, blanketi, na fasihi. Kwa kweli ndugu hao na jamaa zao walifanya kazi kwa bidii na bila malalamiko ili kutumikia makundi. Lilikuwa pendeleo kubwa kutumikia pamoja nao.
Katika 1970 vita ya wenyewe kwa wenyewe ilianza kusababisha matatizo kwa akina ndugu, na suala la kutokuwamo likawa likitia wengi wao kwenye mitihani mikali ya ushikamanifu. (Yohana 15:19) Sosaiti iliwaza ilikuwa vizuri zaidi kubadili mgawo wangu ili nisifanye hali izidi kuwa mbaya kwa akina ndugu bila sababu. Kwa hiyo, katika 1972, mimi niliitwa nitumikie kwenye afisi ya tawi katika Salisbury. Hiyo ilinipa fursa ya kusaidia ujenzi wa afisi mpya ya tawi. Muda fulani baadaye niligawiwa kuwa mwangalizi wa mzunguko kwa ajili ya makundi yaliyotapakaa sana yenye kunena Kiingereza. Hiyo ilitaka kuyasafiri marefu na mapana ya Zimbabwe. Katika maeneo fulani hali ilikuwa hatari sana hata tukalazimika kusafiri tukiwa katika misafara iliyopangwa kitengenezo na serikali na tukiwa tunalindwa na jeshi kwa kusaidiwa na ndege na helikopta.
Mhamo Wetu Kwenda Kwenye Paa ya Afrika
Ndipo lilipokuja badiliko jingine kubwa la mgawo ili tutumikie katika Maseru, mji mkuu wa Lesotho. Hiyo ni nchi ya milima-milima, ambayo nyakati nyingine inaitwa paa ya Afrika, na ina mahali pengi penye uzuri wa kimandhari.
Ingawa sisi tunathamini na kufurahia mandhari ya nchi, hilo silo lililokuwa kusudi letu la kuja hapa. Sisi tupo hapa kusaidia kutafuta “vitu vyenye kutamanika” vinavyonenwa kwenye Hagai 2:7, NW. Hii ni nchi ndogo yenye idadi ya wakaaji milioni moja na nusu tu. Tulipowasili katika 1979, Mashahidi 571, kwa wastani, walikuwa wakishiriki katika kuhubiri “habari njema hizi za ufalme” kila mwezi. (Mathayo 24:14, NW) Julai huu uliopita, 1986, tulifikia kilele kipya cha watangazaji wa Ufalme 870 na hivi majuzi lile kundi katika Maseru lilikua kufikia hatua ambapo lililazimika kugawanywa sehemu mbili.
Hivi majuzi zaidi, katika Aprili 1988, tulifurikwa na shangwe kwa kufikia kilele cha watangazaji Ufalme 1,078. Kwa sasa kazi inazidi kuwa na maendeleo katika ile migawo yetu ya zamani ya umisionari ya Zambia na Zimbabwe. Tulipowasili katika Afrika mara ya kwanza yapata miaka 35 iliyopita, kulikuwa na jumla ya watangazaji wa Ufalme 36,836 katika nchi hizo mbili. Leo tarakimu yenyewe ni 82,229. Pendeleo la kushiriki kwa njia ndogo katika maongezeko hayo limekuwa thawabu nzuri sana kwetu.
“Onjeni mwone ya kuwa BWANA [Yehova, NW] yu mwema,” akaandika mtunga zaburi Daudi. (Zaburi 34:8) ‘Mwonjo’ wetu wa utumishi wa misionari umetusadikisha juu ya ukweli wa maneno hayo. Kwa uhakika, muda wote wa tangu 1942 wakati ambapo sisi tulianza katika utumishi wa wakati wote tukiwa pamoja, maisha zetu zimejawa na mibaraka kwa kuwa tumeupata wema tele wa Yehova. Kungali kuna kazi nyingi ya kufanya. Sisi ni wenye shukrani kama nini kwa Yehova kwamba bado tuna kipimo fulani cha imara na afya ya kutumia katika utumishi wake!
[Picha katika ukurasa wa 24]
John Miles pamoja na Val, mke wake