Mapokeo ya Kidini Je! Ni Kuabudu Mungu Katika Ukweli?
“SALGA, salga, salga” (“Kuja nje, kuja nje, kuja nje”). Hicho ndicho kilio cha huzuni kinachotoka kwenye uwanja wa makaburi ulio na giza katika kisiwa cha Janitzio katika Ziwa Pátzcuaro, Meksiko. Huko Mhindi Mtaraskani anayefuata imani zake kwa bidii anamsihi-sihi mfu wa ukoo wake kwa msaada wa sala iliyoandikwa. “Tasbihi Takatifu na ivunje minyororo inayokufunga wewe,” yeye anaombeleza.
Hiyo ndiyo Siku ya Wafu. Kuanzia saa za mapema, wanawake na watoto wamepamba makaburi yao ya kijamaa kwa majani ya maua na fremu za mbao zilizorembwa. Mbele ya makaburi wameweka matoleo ya matunda na vitamutamu vingi vya kuokwa. Na sasa wanavumilia baridi ya usiku ili waimbe-imbe sala au wafanye kesha la unyamavu katika ile nuru hafifu ya maelfu ya mishumaa yenye kusinzia-sinzia iliyowashwa kwa ajili ya wafu.
Jambo hilo lenye kuonekana la kigeni au hata la upuuzi kwa mtazamaji wa nje ni pokeo la kidini la watu hawa ambalo limeheshimiwa kwa muda mrefu: mwadhimisho wa Kikatoliki wa Siku ya Nafsi Zote Zilizokufa. Katika mabara mengi ya Latini Amerika, pokeo huongoza maelfu ya waitikadi wamiminike kwenda kwenye nyanja za makaburi na kutolea wafu wao sala za kuandikwa, na zawadi.
Latini Amerika pia ina mapokeo mengi sana kuhusu mifano ya kidini. Mifano ya Kristo na Mariamu inapatikana kila mahali, ikiremba maskani na maduka yaliyo mengi. Ukipanda basi utaona picha ndogo-ndogo za Mariamu zikiwa zimewekwa juu ya kiti cha dreva. Sanamu-umbo za Mariamu, zikiwa zimerembwa kwa nuru za rangi zenye kuwaka-waka badala ya kurembwa kwa mishumaa, zinakuwa hata zimebandikwa kwa kuelekeana na kichochoro cha katikati ya basi.
Katika Kolombia maumbo makubwa sana ya Kristo na ya Mariamu yanakodoa macho kutazama chini kutoka kwenye vimo virefu sana vya milima juu ya majiji mengi. Kile kilele maarufu cha Monserrate kina kanisa fulani juu yacho lililojaa mifano yenye kupewa kicho kingi. Wakati wa majuma maalumu yaliyo matakatifu, maelfu ya wakaaji wa Bogota hupanda kwenye kileleta hicho cha miamba-miamba, wengine wao wakiwa wanatambaa kwa magoti yaliyochomwa-chomwa na kutoka damu.
Mifano, misalaba, sherehe—hayo ni sehemu ya mapokeo ya kidini ambayo yamekuwa njia ya maisha iliyothibitika kwa watu kote kote ulimwenguni. Mapokeo hayo yamepokezwa kutoka kizazi hadi kizazi, na watu wanaelekea kuwa na rai ya kwamba ni matakatifu.
Je! Ni Kuabudu Katika Ukweli?
Ingawa labda walio wengi wanatosheka kufuata mapokeo bila kutia shaka, kwa wengi wanaodai kuwa Wakristo mapokeo hayo yanatokeza utatanishi wenye kusumbua. Ingawaje, Yesu Kristo mwenyewe ndiye aliyesema hivi: “Waabuduo halisi watamwabudu Baba katika roho na kweli.” (Yohana 4:23) Hata hivyo, ni wazi kwamba mapokeo mengi ya kidini yametolewa katika desturi za kidini zisizo za Kikristo, au angalau yanafanana nazo kwa njia ya kugutusha sana. Mathalani, Siku ya Nafsi Zote Zilizokufa ni kama inalingana kabisa na sherehe ya Kibuddha ya “Ullambana,” siku ambayo imewekwa kando iwe ya “wonyesho wa heshima ya watoto kwa mababu wa zamani waliokufa na kufunguliwa kwa maroho kutoka kwenye utumwa wa ulimwengu huu.” (The New Encyclopcedia Britannica, chapa ya 1976, Micropaedia, Buku 1, ukurasa 260) Je! kweli wafuasi wa mapokeo hayo wanaabudu katika ukweli?
Watu fulani wanatoa ubishi kwamba kukubaliwa kwenyewe kwa mapokeo ili yawe ndani ya kanisa kunatetea uhaki wayo. Baraza la Pili la Vatikani lilisema hivi katika 1965: “Uhakika wa kila jambo ambalo Kanisa limefunuliwa hautokani na Andiko takatifu tu. Kwa hiyo pokeo takatifu na pia Andiko takatifu vinapasa kukubaliwa na kuheshimiwa sana kwa bidii na kicho cha kadiri inayolingana.
Ingawa hivyo, namna gani ikiwa kuna mahitilafiano ya msingi kati ya pokeo lililofanyizwa na binadamu na Andiko lililovuviwa na Mungu? Kwa kujibu, acheni tutazame sana mapokeo kwa msaada wa shauri la Biblia.