Wapiga Mbiu ya Ufalme Waripoti
Kudumisha Imani Katika Nyumba Iliyogawanyika
MTUME Paulo alionya Wakristo kwa upole hivi: “Jitunze nafsi yako, na mafundisho yako. Dumu katika mambo hayo; maana kwa kufanya hivyo utajiokoa nafsi yako na wale wakusikiao pia.” (1 Timotheo 4:16) Katika bara moja la Mashariki, ‘kudumu’ katika mafundisho ya Biblia kulitokeza baraka nzuri sana kwa Bi. L——baada ya yeye kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova.
Bi. L——na mume wake, wote wawili walitoka kwenye jamaa za Kihindu. Bibi mwenyewe alitembelewa na Mashahidi wa Yehova katika 1959, na baada ya kujifunza Biblia pamoja nao, akakubali ukweli wa Neno la Mungu. Ndipo yeye akamtolea ushuhuda mume wake na watu wengine wa ukoo. (Linganisha Yohana 1:40, 41.) Mume wake hakuonyesha kupendezwa, lakini dada yake wa kimnofu R——alijiunga katika funzo hilo. Katika 1961 yeye na dada yake walibatizwa kuonyesha wakfu wao kwa Yehova. Watoto wa Dada L——walipoendelea kukua, yeye alijifunza pamoja nao na kuwapeleka mikutanoni. Binti wa umri mkubwa zaidi, S——, alipoacha shule, aliweka maisha yake wakfu kwa Yehova, akabatizwa, na kuolewa na Shahidi mmoja. Hata hivyo, baada ya muda fulani yeye na mumeye wakawa wasiotenda. Mwana aliye wa umri mkubwa zaidi alisonga mbele kupata elimu ya juu zaidi na kuingia katika ushirika mbaya. Halafu akaoa msichana Mkatoliki na kukoma kushirikiana pamoja na watu wa Yehova. Kwa upande ule mwingine, binti aliye mchanga zaidi aliweka wakfu maisha yake kwa Yehova na kubatizwa baada ya kuacha shule.
Dada L——aliendelea kuwatolea ushuhuda watu wa ukoo wake. Dada mwingine wa kimnofu akapendezwa, lakini mume wake akampinga vikali, hata akaharibu Biblia na vitabu vyake. Yeye hakuruhusiwa kupeleka watoto wake watatu mikutanoni, lakini alijifunza pamoja nao kwenye maskani yao. Baada ya muda yeye pia alijiweka wakfu na kubatizwa, kwa kukabiliana na upinzani imara kutoka kwa mume wake. Mwishowe, watoto wake wote watatu wakawa Mashahidi waliojiweka wakfu na kubatizwa.
Kwa wakati uliopo, Dada L——aliendelea kuwatolea ushuhuda watu wa ukoo wa kimnofu. Aliponena pamoja na ndugu yake na mkeye, ndugu huyo hakuonyesha upendezi wowote, lakini mke wake alisikiliza. Baada ya kupata maarifa ya kutosha ya Biblia, mke huyo alijiweka wakfu kwa Mungu na kuonyesha hivyo kwa kubatizwa katika maji.
Dada L——alimtolea ushuhuda ndugu mwingine wa kimnofu, ambaye aliupinga ukweli. Lakini mke wake, pamoja na binti yao, alianza kujifunza. Binti huyo alipelekwa Kanada akapate mafunzo zaidi ya kimwili lakini akaendelea na funzo lake la Biblia na ushirika pamoja na Mashahidi huko. Mwishowe, yeye pia alichukua msimamo kwa ajili ya ukweli na akabatizwa. Aliolewa na ndugu painia katika Kanada, na baba na mama yake wakahudhuria arusi ile. Ushirika pamoja na akina ndugu katika Kanada ulikuwa na athari nzuri sana juu ya baba yule.
Matokeo ya Kutolea Jamaa Yake Ushuhuda
Jitihada za uaminifu za Dada L——zilibarikiwa na Yehova. Baada ya muda fulani binti yake aliye mchanga zaidi aliacha kazi yake yenye mshahara mnono, akaanza kazi ya nusu-siku, na kuanza kutumikia Yehova akiwa mhudumu wa wakati wote. Binti aliye na umri mkubwa zaidi pamoja na mume wake walianza kujifunza na kuhudhuria mikutano tena na wakawa watendaji katika huduma. Mwanaye aliyekuwa ameoa msichana Mkatoliki na kupeperukia mbali kutoka kwenye ukweli alianza pia kujifunza tena na mwishowe akaweka maisha yake wakfu kwa Yehova na kubatizwa. Mwanaye aliye mchanga zaidi akajiweka wakfu pia na kubatizwa halafu akachukua msimamo wake kuhusu suala la kutokuwamo. (Isaya 2:4) Alihukumiwa kifungo cha miaka mitatu katika gereza la kijeshi, lakini muda wote huo akatoa ushuhuda thabiti sana mbele ya baraza la mahakimu. Baba yake, ambaye ni mume wa Dada L——, alivutiwa sana na msimamo ambao mwana wake alichukua hivi kwamba yeye sasa akapendezwa na akaanza kuhudhuria mikutano.
Kwa kweli, miaka 29 ya utumishi mwaminifu wa Dada L——katika nyumba iliyogawanyika imekuwa yenye kutosheleza na kuthawabisha kama nini! Sasa yeye anashangilia kuhesabu washiriki wa kijamaa na watu wa ukoo 18 ambao wamebatizwa. Jambo hilo lililoonwa na liwe chanzo cha kuwatia moyo na kuwafariji wengi wa ndugu na dada zetu ambao, wakiwa chini ya mastakimu zinazofanana na hizo, wanalazimika kuvumilia na kudumisha imani katika nyumba zilizogawanyika.—1 Petro 2:19, 20; 1 Wakorintho 7:12-16.