Sisi Tuligeukia Chanzo cha Uadilifu wa Kweli
Kama ilivyosimuliwa na Erwin Grosse
MIAKA michache iliyopita, asubuhi ya mapema ilikuwa ikinipata nikiwa kwenye kiwanda kikubwa cha kuundia meli katika Kiel, Ujeremani, nikigawa vikaratasi na kuuza Rote Fahne, gazeti la KPD/ML.a Wakati ule ule ningekuwa nikijaribu kuvuta wafanya kazi na wakurufunzi ili wahusike katika majadiliano. Ilikuwa kazi ya bure kujaribu kuwasadikisha kauli zangu za kikomunisti.
Hata hivyo, sikuacha jambo hilo linivunje moyo. Mimi nilikuwa nimegundua mradi maishani: kusaidia kutokeza hali za uadilifu kupitia mapinduzi makubwa ulimwenguni. Ni jinsi gani nilivyofikia kuwa na rai hiyo? Je! mradi huo maishani ungeridhisha njaa yangu ya kutaka uadilifu?
Kutafuta Uadilifu
Njia ya maisha ya wazazi wangu ilikuwa kujikaza kabisa wakitafuta ufanisi wa vitu vya kimwili, nayo haikunivutia kamwe. Sisi vijana tulikuwa tukitafuta kitu bora. Mitindo mipya ya maisha ilikuwa ikijaribiwa, na makusudi mapya maishani yakawa yakitangazwa. Wakati huo, vita ya Vietnam na msukosuko wa wanafunzi ndiyo mambo yaliyokuwa yakitangazwa sana magazetini. Kwetu ilionekana kwamba watu wasio na hatia walikuwa wakitoa uhai wao ili kulipia ukichaa wa fahari ya umashuhuri ya wanasiasa na wabepari. Hali hiyo ililemea sana akili yangu, nami nikaanza kuchukia mfumo wa kibepari.
Pia nilielekeza kisogo changu kwenye dini zenye kuimarika sana. Jambo moja lililonipata nikitumikia katika kani za kijeshi za Ujeremani Magharibi ndilo lililonisaidia kufanya uamuzi huo. Mbinu za kijeshi tulizokuwa tukijihusisha nazo zilikatizwa ili tufanye utumishi wa kambi, na askari-jeshi waligawanywa wawe vikundi-vikundi vya Wakatoliki na Waprotestanti. Kwenye umalizio wa utumishi huo, makasisi wa madhehebu yote mawili walibariki ile mizinga mizito-mizito! Nilishtuka. Je! kwani silaha hizo hazikujengwa ili kuua? Na wakati mimi nilipofundishwa shuleni, kwani sikuwa nimefundishwa hivi: “Usiue”?—Kutoka 20:13.
Nilihisi kwamba Karl Marx alisema kweli alipoita dini “kasumba ya watu” kwa sababu ilifanya watu wawe hoi walipotakiwa kufuata mapendezi ya ubepari. Kwa hiyo baada ya mimi kuondoka jeshini, nilijiuzulu kanisani na kuanza masomo ya ukawaida ya kujifunza mawazo ya Marx na Lenin. Pia nilisoma vitabu vya Mao Tsetung. Yote hayo yaliimarisha usadiki wangu kwamba mapinduzi makubwa ulimwenguni ndiyo tu yangeweza kung’oa uovu pamoja na mizizi yao. Ni kwa njia hiyo tu, mimi nikawaza, kwamba jamii mpya ya kibinadamu ingeweza kutokea ikiwa na uadilifu.
Chama cha KPD/ML kilinipa mazoezi ya kuvutia wafanya kazi wafuate mafundisho ya Lenin na kuwatolea vikaratasi na Rote Fahne. Pia nilienda nikiwa na beramu na kuendesha magari yenye vipaaza-sauti kwenye maandamano ya kuteta. Hata hivyo, watu walikuwa na rai ya kwamba nilikuwa mfuasi wa hivi hivi tu wa chama hicho. Kabla halmashauri kuu haijaweza kunikubali niwe mshiriki, ilikuwa lazima nijithibitishe mwenyewe, nitumikie chama kwa muda fulani na kukiunga mkono kifedha.
Kazi Tofauti—Mtamauko Wenye Uchungu!
Nilikuwa nimepewa mazoezi kuwa mchora ramani za uhandisi, lakini nilipendezwa zaidi na sanaa ya wachora-picha wa usoshalisti, nami niliona ni laiti ningeweza kujishughulisha kwa kuvumbua maarifa mapya ya kikazi kama wao. Kwa hiyo, nikajaza ombi la kutaka nafasi kwenye Koleji ya Sanaa ya Berlin Magharibi. Nilikubaliwa na nikaanza kusomea sanaa katika Februari 1972.
Hapo tena niliwasiliana na chama na muda si muda nikawa nimesimama mbele ya malango ya kiwanda nikiuza Rote Fahne. Pia nilijifanyizia mwenyewe karatasi kubwa za kuteta katika maandamano na nikachora picha za Marx, Engels, Lenin, na Mao Tsetung katika bendera nyekundu.
Nilikuwa nimepiga moyo konde nisifunge ndoa kamwe—yaani, mpaka wakati nilipokutana na Linda. Nilipata kwamba yeye alikuwa na sifa moja iliyo haba, uaminifu, na hiyo ikafanya nibadili nia. Miezi mitano baadaye tukawa mtu na mkeye, tukianza ile ambayo ingekuwa ndoa yenye upatano.
Hapo kwanza, mimi niliishi pamoja na kikundi cha vijana walioshikilia maoni mbalimbali ya kutaka mapinduzi. Tulikuwa na mazungumzo ya mambo ya aina nyingi, lakini kulikuwako pia mzozano na uhasama. Hali ilikuwa ile ile katika vile vyama tofauti vya kikomunisti. Kila kimoja kilishikilia maoni ya kwamba vingine vyote havikuelewa vizuri wazo la ukomunisti na vilipaswa kujiunga na chama kilicho “cha kweli.” Mapambano yakawa tayari!
Ndani ya chama changu mwenyewe, mapambano kati ya wenye kutaka na wasiotaka mapinduzi yalikuwa jambo la kikawaida. Washiriki mashuhuri walijaribu kupinduana vyeo. Mimi nilichoshwa na mapigano na ufidhuli huo, na pole kwa pole hiyo ikaniongoza kuvunja ukamatano wote pamoja na chama. Sikuona maana ya kuhusika pamoja na kitu ambacho kwa kweli hakingeweza kuleta badiliko lolote. Lile wazo bora la ukomunisti lilikuwa limejithibitisha kwa matendo kuwa lisiloweza kufikiwa! Lakini katika moyo wangu nilibaki nikiwa mfuasi wa Marx.
Linda Aniambia Juu ya Mungu
Usiku mmoja, nilipokuwa nikiendesha gari kutoka Kiel kwenda Berlin, Linda alinishtua. Yeye alisema: “Mimi nasadiki kwamba kuna Mungu, nami namwitikadi kwa kina cha moyo wangu.” Hilo ndilo jambo ambalo sikutarajia kabisa kusikia! Linda alikuwa ameunga mkono mawazo yangu ya ufuasi wa Marx.
Ukafuata ubishi mkali juu ya jinsi mazingira ya kijamii huathiri watu na juu ya mawazo ya Marx. Mawazo ya Marx hutokeza hoja ya kwamba mwanadamu hupata sehemu yote ya maisha yake ya kiroho, ya kiakili, na kiadili kutokana na mazingira yake ya kijamii. Tokeo ni kwamba, mwanadamu huyo “mpya” hutokea kwa kupata elimu ya mawazo ya kikomunisti na kwa kupatwa na badiliko chanya katika mazingira. Hata hivyo, Linda alikuwa fundi aliyezoezwa kimaabara, naye alijua mengi zaidi! Yeye angeweza kuthibitisha kwamba tabia ya mwanadamu inaongozwa pia na umbo lake la urithi wa chembe za tabia. Tulikatiza mazungumzo yetu ili kuepuka ugomvi.
Wakati wa safari moja ya baadaye, Linda alihisi tena tamaa ya kuongea nami juu ya Mungu. Kwa rai yangu, nadharia ya mageuzi ilihakikisha kwamba kila kitu kilitokana na asili ya kimwili na kwa nasibu kabisa. Linda alitaja kanuni za sayansi inayohusu utendaji unaobadilisha joto kuwa nishati na nishati kuwa joto, sheria ya nguvu zinazodumisha vitu katika kikao na mwendo mmoja usiogeuka kabla ya kuguswa na kani nyingine ya kutoka nje, na akataja sheria nyingine za kimwili ili kuthibitisha kwamba ni lazima kuwe kuna mwanzishi wa uhai. Mimi niligandamana na kauli zangu. Hata hivyo, falsafa yangu juu ya maisha na mawazo yangu yalikuwa tayari yamechanika-chanika!
Mwaka mmoja ukapita. Asubuhi moja ya Jumapili Linda alichomoa kitabu kinene na kuanza kunisomea. Ilikuwa hadithi ya mwanamume mmoja aliyeangusha mti, akatumia nusu yao kufanyiza sanamu isiyo na uhai halafu akaisihi hivi: “Uniokoe.” Uelezaji huo wa kustaajabisha kuhusu dini ulinivutia sana. Ebu wazia mshangao wangu nilipojua kwamba uelezaji huo ulitoka katika Biblia.—Isaya 44:14-20.
Nikaomba mke wangu anieleze mengi zaidi. Yeye akafanya hivyo kwa muda wa saa tano—akianza na anguko la mwanadamu katika Edeni na kumalizia kuhusiana na kurudishwa kwa Paradiso ambako kumeelezwa katika kitabu cha Ufunuo. Hiyo ilimwacha Linda akiwa amechoka sana, lakini mimi nilihisi kama kwamba magamba yenye kunifunika macho yalikuwa yameanguka na kwamba niliweza kuona waziwazi kwa mara ya kwanza. Kiasili, nikataka kujua Linda alikuwa amejifunzia wapi yote hayo.
Yeye akaniambia kwamba alipokuwa na umri wa miaka 14, alikuwa amejifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova katika Berlin na hata akabatizwa baadaye. Alipokuwa na miaka 18, alilazimika kuhamia mbali kwa sababu ya kazi yake ya kuajiriwa, na la kuhuzunisha ni kwamba, yeye aliiacha njia ya ukweli. Ndipo aliporudi Berlin, akahusika katika siasa za wataka-mapinduzi. Furaha ambayo sasa aliipata katika ndoa yetu ilimsukuma amtafute Mungu upya. Lakini je! angemsamehe makosa yake? Yeye alijua kwamba njia peke yake ya kuhifadhi uhai wetu na furaha ya ndoa yetu ilikuwa kurudia Mungu kwa kutubu. Lakini mimi nilikuwa bado sijafikia hatua hiyo. Nilihitaji wakati mwingi zaidi.
Mgeuko wa Kuelekea Upande Unaofaa
Jioni moja ya kiangazi, tulitazama jua likichwea jijini kwa rangi ya kidhahabu. Linda akasema: “Labda tunaweza kuona shangwe ya mambo kama hayo kwa muda kidogo, Erwin. Lakini je! Mungu atatuweka tukiwa hai wakati atakapoingilia mambo? Sisi tunampa sababu gani ya kufanya hivyo?” Hiyo ilinigutusha nikarudiwa na fahamu. Nilikuwa nimejifunza jambo fulani juu ya Yehova lakini ni wazi halikuwa la kutosha. Kwa hiyo mimi nikaamua kabisa kumgeukia yeye.
Muda mfupi baada ya hapo, tukiwa sokoni tuliona mwanamke mzeemzee katika kiti-magurudumu akiwa ameshika Mnara wa Mlinzi. Tukamwomba atuambie nyakati za mikutano kwenye Jumba la Ufalme la kwao, na macho yake yakaanza kung’aa. Yeye alitushika sana mikono: “Nafurahi kwamba vijana kama nyinyi mnataka kujua Biblia,” yeye akasema-sema. Kwa kujawa na shangwe nyingi sana, aliketi wima katika kiti-magurudumu chake na kumkumbatia Linda. Sisi tukakubali kuchukua magazeti fulani na kuahidi kuja kwenye mkutano ambao utafuata.
Tuliwasili muda mfupi kabla haujaanza. Mimi nilikuwa na nywele ndefu na ndevu na nilivalia suruali-jini na fulana. Linda alivalia vazi samawati la arusi ya shangazi yake la tangu miaka 30 iliyopita. Mimi niliona mwanamume mmoja aliyevalia jaketi na tai akiwa amesimama kwenye mwingilio na nikafikiri: ‘Mbeja halisi huyu! Lo, mwanzo gani huu!’ Hata hivyo, yeye alionyesha urafiki, akasema: “Tumekuwa tukiwatarajia nyinyi.” Niligutuka lakini nikasema kwake hivi: “Sisi tungependa funzo la Biblia.” Wala jambo hilo halikumshangaza. “Limekwisha pangwa tayari,” yeye akajibu. Tukaingia ndani, tukiwa tumeudhika kidogo.
Mkutano ulipokuwa ukiendelea, nilihisi mara kadhaa kama kwamba msemaji alikuwa akinena na mimi binafsi. Na baadhi ya waliokuwa kundini walishangaa wakati Linda alipochomoa Mnara wa Mlinzi aliokuwa ametayarisha mapema kwa ajili ya funzo. Baada ya saa zile mbili, dada yule mzeemzee alikuja akatukumbatia, uso wake uking’aa shangwe. Yeye ndiye aliyekuwa ameeneza habari za kuja kwetu. Mipango ilifanywa kwa ajili ya funzo la Biblia pamoja na ndugu aliyekuwa ametukaribisha, na miezi tisa baadaye, siku ya Aprili 4, 1976, mimi nikaonyesha wakfu wangu kwa Yehova kwa kuzamishwa katika maji.
Niliterema kama nini kupata kumjua yule Mmoja aliyeahidi hivi: “Tazama, nayafanya yote kuwa mapya”! (Ufunuo 21:5) Na ni jinsi gani Muumba ataleta uadilifu wa kweli? Mithali 2:21, 22 inaandaa jibu: “Maana wanyofu watakaa katika nchi [dunia, AW], na wakamilifu watadumu ndani yake. Bali waovu watatengwa na nchi, nao wafanyao hila watang’olewa.”
Ijapokuwa hapo kwanza mimi nilisimama nikiwa na Rote Fahne mbele ya malango ya kiwanda, sasa nilisimama siku za Jumamosi katika Barabara ya Karl Marx katika Berlin Neukolln nikiwa na Mnara wa Mlinzi. Sasa ningeweza kunena juu ya jambo fulani ambalo hakuna mfumo wowote wa kibinadamu ungeweza kutolea watu: uhai wa milele. (Yohana 17:3) Nilijifunza jinsi “wanyofu” wanavyozoezwa hata sasa kujivika “utu mpya, ambao kupitia maarifa sahihi unafanywa mpya.” (Wakolosai 3:10, NW) Elimu hiyo iliyo kwa ajili ya ulimwengu mpya haitakosa mafanikio!
Kwa habari ya Linda, yeye sasa amepiga moyo konde asigeuke tena kutoka kwenye Chanzo cha uadilifu wa kweli. Peter na Reni, waliotufunza njia za Yehova, walitambua kile alichohitaji kiroho na wakamsaidia kufanya maendeleo.
Miradi Mipya Katika Kijia cha Uadilifu
Kwenye koleji, ilionekana wazi kwamba hawakukubaliana na itikadi ambazo mimi sasa nilizifuata kwa bidii nyingi. Profesa wa darasa langu, aliye mchora-picha maarufu, alionyesha kwamba ningelazimika kuamua kati ya sanaa na imani yangu mpya. Kwa hiyo mimi nikaacha uchoraji-picha na kutafuta kazi ambayo ingetusaidia kufikia mradi wetu mpya: utumishi wa painia. Kwa kufikiria jambo hilo, Linda na mimi tulimtajia-tajia Yehova tamaa yetu mpya. Tulipeleka fomu za maombi yetu nusu-mwaka kabla ya tarehe tuliyopanga kuanza, Septemba 1, 1977.
Eeh, haikuwa rahisi, lakini kwa msaada wa Yehova tulifikia mradi wetu. Kwa wakati uliopo, tangu Januari 1, 1985, Linda na mimi tumekuwa tukitumikia tukiwa mapainia wa pekee—kwa hiyo tamaa nyingine yenye kuwaka imetimizwa. Kutumia imara yetu yote kusaidia watu wajifunze kijia cha uadilifu wa kweli kunatutosheleza sana.
Namna gani juu ya tamanio langu kubwa la uadilifu? Je! limetoshelezwa? Ndiyo. Leo mimi najua maana halisi ya maneno ya Yesu kwenye Mathayo 5:6, NW: “Wenye furaha ni wale wanaohisi njaa na kiu kwa ajili ya uadilifu, kwa kuwa wao watajazwa.”
[Maelezo ya Chini]
a Kommunistische Partei Deutschlands/Marxisten-Leninisten (Chama cha Ukomunisti Ujeremani/Wafuasi wa Marx na Lenin).