Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w89 1/15 kur. 21-24
  • Mahari—Wakristo Wawe na Rai Gani Kuihusu?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mahari—Wakristo Wawe na Rai Gani Kuihusu?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Jinsi Inavyoweza Kuathiri Baba
  • Jinsi Inavyoweza Kuathiri Bibi-Arusi na Bwana-Arusi
  • Dumisha Rai Yenye Usawaziko
  • Je, Wajua?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2022
  • Kupatana juu ya Mahari ya Kiasi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • “Ndoa ya Kidesturi” Katika Ghana
    Amkeni!—1996
  • Kutayarisha Kwa Ajili Ya Ndoa Yenye Mafanikio
    Siri ya Furaha ya Familia
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
w89 1/15 kur. 21-24

Mahari​—Wakristo Wawe na Rai Gani Kuihusu?

ILE desturi ya kale ya kulipa mahari ingali inazoewa katika mabara mengi. Katika visa vilivyo vingi, malipo yanafanywa kwa namna ya pesa, pamoja na zawadi za vitu vyenye thamani. Thamani yenyewe hutofautiana mahali na mahali na kutoka jamaa moja hadi jamaa nyingine, ikitegemea hadhi ya kijamii, elimu, na mambo mengine. Kiasi cha kutoa huwekwa na sheria katika nchi fulani fulani, ingawa ni watu wachache wanaofuata bei ile ya kiwango kilichowekwa.

Ufikirio wa uangalifu unaonyesha kwamba desturi ya ki-siku-hizi inahusisha ndani mengi kuliko kulipa mahari. Kwa sababu hiyo, ni hekima kufikiria jinsi jambo hilo linavyoweza kukuathiri wewe Mkristo.

Katika Papua New Guinea, malipo ya mahari ni kama kuhamisha rasilmali kutoka kikundi cha jamaa ya mtu, kile cha jamaa kubwa ya bwana-arusi inayohusisha ndani hata watu wa ukoo, kuzipeleka kwenye kikundi cha watu kama hao wa upande wa bibi-arusi wa ndoa ile. Malipo hayo yanaweza kuanzia dola 100 hadi dola 46,000, ikitegemea utajiri wa jamaa ya bwana-arusi. Katika Sri Lanka, hali ni kinyume. Ni lazima wazazi wa bibi-arusi wampe bwana-arusi mahari. Hiyo inaweza kutia ndani vito vya thamani, mali, nyumba, na pesa taslimu. Ili mali isitoke katika jamaa hiyo, desturi ni kuoa binamu wa kwanza.

Katika sehemu nyingi za Afrika, malipo ni moja la matakwa ya kidesturi yanayofanya mkataba wa ndoa ukamilike na kuwa halali. “Miongoni mwa Waigbo,” anasema baba mmoja Mnaijeria ambaye binti yake alikuwa akitayarishwa kwa ajili ya ndoa, “kulipa mahari kunahitajiwa sana ili ndoa iwe na utambuzi wa kitamaduni. Kukubaliwa kwayo ni kionyesho cha kwamba jamaa ya msichana imetoa idhini. Kunaridhisha dhana ya watu kuhusu ndoa. Kwa sababu hiyo, hata ndoa iliyofanyiwa mkataba kanisani au katika idara ya serikali ya uandikishaji haingetambuliwa katika jumuiya ya kienyeji ikiwa mahari haikulipwa.”

Jinsi Inavyoweza Kuathiri Baba

Miongoni mwa Waafrika hao, malipo yalikuwa wonyesho wa kwamba mwanamume ana uwezo wa kudumisha riziki ya jamaa. Washiriki wa jamaa yake wangezuru wazazi wa msichana ili kupiga bei ya kwanza inayohusiana na mahari. Katika maeneo mengi mambo yameacha kuwa hivyo, kwa maana sasa akina baba hupiga bei halisi kwa kuomba mahari ya kadiri kubwa zaidi wawezayo kupata. Kiasi kutoka karibu dola 12, kinachowekwa na sheria za maeneo fulani ya Naijeria, hadi dola 1,400 au zaidi hudaiwa. Huenda pesa au zawadi zikatarajiwa hata kabla ya ziara ya kwanza ya wazazi wa mwenye kuchumbia. Halafu, kama vile ilivyo katika Zaire, huenda ikawa za ziada zilipwe ili ‘kufungua kufuli katika kinywa cha baba,’ yaani, kumfanya akubali kushauriana kuhusu bei atakayopewa kwa ajili ya bintiye. Hata baada ya donge fulani kulipwa, malipo na zawadi nyinginezo zinaweza kudaiwa.

Mazoea ya jinsi hiyo yanaweza kutia moyo kuwa na pupa ya pesa. Hata hivyo, Biblia inasema: “Shina moja la mabaya ya kila namna ni kupenda fedha.” (1 Timotheo 6:10) Kwa sababu ya pupa, watu wanaweza kuwa wanyakuzi, na hiyo huleta kukosa upendeleo wa Mungu. Biblia inatuambia kwamba hakuna “mtu mwenye pupa​—maana yake kuwa mwabudu-sanamu​—aliye na urithi wowote katika ufalme wa Kristo na wa Mungu.”​—Waefeso 5:5, NW; linganisha Mithali 20:21; 1 Wakorintho 5:11; 6:10.

Hata hivyo, hakuna ubaya wa kumpa baba mahari kama kionyesho cha kulipia upotevu wa binti aliyemlea na kumwelimisha. Anayetarajia kuwa mwana-mkwe angeweza kuona malipo hayo kuwa kifananishi cha uthamini wake kwa mazoezi ambayo mchumba wake wa kike alipewa. Hata hivyo, wazazi fulani hujaribu kurudishiwa kiasi chote walichotumia, wakihisi kwamba binti zao walioolewa hawatasaidia kuelimisha watoto walio wachanga zaidi. Wazazi wa jinsi hiyo hutafuta mahari ya juu zaidi kadiri iwezekanavyo, kana kwamba binti zao ni bidhaa za mauzo tu. Lakini wao wana deni la kuwapa watoto wao malezi mema. Fahari yao inapaswa kuwa katika utimizo wa wajibu huo, wala si katika kuona ni kiasi gani wanachoweza kurudishiwa kwa namna ya pesa au kwa kujipatia sifa kupitia mahari kubwa mno. Badala ya kuongoza wazazi wafikirie faida za kimwili ambazo watoto wanaweza kuleta, Biblia inasema hivi: “Haiwapasi watoto kuweka akiba kwa wazazi, bali wazazi kwa watoto.”​—2 Wakorintho 12:14.

Madai yanayofanywa na baba fulani wenye kujiita Wakristo hupuuza uwezo wa kifedha wa wachumba vijana wa Kikristo. Kwani, kuna visa ambamo akina baba fulani wamekataa matoleo ya kiasi kinachofaa waliyopewa na ndugu Wakristo kwa sababu wanaume walimwengu waliwapa zaidi! Baadhi yao hata huacha mashauriano hayo yafanywe na walimwengu wa ukoo wao, ambao hudai bei kubwa mno. Wakati upiga-pigaji huo wa bei unapoendelea, hali ingeweza kusukuma vijana hao waingie katika uasherati. Hivyo ndivyo huwa miongoni mwa walimwengu. Mara nyingi hutukia kwamba vijana wenye kutatizika wanaotaka kufunga ndoa hutumia mimba kama njia iliyo rahisi zaidi ya kulazimisha jamaa ya msichana ikubali kiasi ambacho mchumba anaweza kulipa.

Wakristo hawapaswi kutenda jinsi hiyo. Neno la Mungu linaharamisha uasherati, na wale wanaoutenda wangeweza kuondoshwa katika kundi. (1 Wakorintho 6:9; Waebrania 13:4) Baba hawezi kujiondolea lawama ikiwa madai yake ya unyakuzi yanachangia anguko la bintiye katika ukosefu wa adili. Lawama hilo lingeweza kuathiri kwa uzito msimamo wake katika kundi. Vilevile, kukubali kiasi chochote cha pesa kutoka kwa mlimwengu ili aoe binti Mkristo aliyejiweka wakfu si jambo la kitheokrasi. Kufanya hivyo kunafanya ndugu asistahili angalau mapendeleo fulani ya pekee katika kundi. Wazazi Wakristo wanapaswa kutaka vijana wao wabaki wakiwa imara katika kundi la Kikristo na wanapaswa kuwasaidia kudumisha mwenendo safi. Inawapasa kutamani kwamba binti zao waolewe katika ndoa yenye furaha “katika Bwana tu,” na waume ambao pia wanapenda Yehova na wana staha ya kina kirefu kwa sheria na kanuni zake.​—1 Wakorintho 7:39.

Si jambo la Kikristo mtu kuiona mahari kama njia ya kuunda pesa kutokana na mtoto wake mwenyewe, kwa njia ya unyakuzi akitoza zaidi ya kadiri inayofaa. Lazima baba Mkristo ajilinde dhidi ya pupa na ubinafsi, kwa maana hiyo ingeweza kuathiri kwa uzito hali yake ya kiroho na mapendeleo yake katika kundi.​—1 Wakorintho 6:9, 10.

Jambo la kufurahisha ni kwamba, akina baba wengi Wakristo wameonyesha ufikirio katika kiasi cha mahari ambayo wameomba, na hiyo inafunua mwelekeo bora. Baadhi yao hata wamechagua kutokuomba mahari yoyote, ili kujilinda dhidi ya kutumia vibaya desturi hiyo na kusababisha matatizo ya kiroho.

Jinsi Inavyoweza Kuathiri Bibi-Arusi na Bwana-Arusi

Katika visa kadhaa, pupa ya msichana ndiyo iliyotokeza uvutano wa kiasi cha mahari iliyowekwa na wazazi. Kuna wale wanaoomba arusi yenye gharama nyingi na ya kujionyesha sana, hata wakifanyia wazazi wao choko-choko ya daima ili iwe hivyo. Wengine hudai kwamba wazazi wao wanunue vyombo vya gharama kubwa kwa utumizi wa nyumba mpya. Ili baba atimize madai hayo, huenda akahisi akihitajika kabisa kuongeza mahari.

Hiyo, nayo, inamtilia kani bwana-arusi aanze maisha yake ya ndoa akiwa chini ya lemeo la madeni yaliyotokana na arusi ya gharama kubwa na fanicha iliyo ghali. Neno la Mungu linasema kwamba “hekima ya kutoka juu ni . . . yenye kiasi.” Vijana wanaotaka kufunga ndoa wanapaswa kuacha “kiasi chao kijulikane kwa watu wote” kwa kupanga arusi isiyoweka lemeo zito la kifedha juu ya mtu yeyote.—Yakobo 3:17; Wafilipi 4:5, NW.

Baada ya arusi, mke angeweza kuanza kupima upendo ambao mumeye anao kwake kulingana na kadiri ya mahari aliyolipa. Huenda mke huyo akahisi yeye si salama ikiwa mumeye alilipa kiasi kidogo. Mke huyo angeweza kusababu ya kuwa ikitukia kwamba mumeye achoke naye na atake kumfukuza, mume huyo angefanya hivyo kwa utayari, kwa kuwa angekuwa na nia ya kupoteza kile kiasi kidogo alicholipa. Ni kweli kwamba waume fulani wamefukuza wake zao warudie wazazi wao kwa sababu mbalimbali, kama vile kutoweza kuzaa watoto au kwa kuonyesha roho ya uasi. Hilo ndilo jambo ambalo huwa wakilitia moyo wale wanaosema hivi kwa kijana mwanamume ambaye ametoka sasa hivi kulipa mahari: “Umenunua mke.” Ikiwa alilipa bei kubwa, yeye angeweza kushawishwa kuwa na rai ya kwamba mke wake ni mtumishi aliyenunuliwa, badala ya huyo kuwa ni rafiki msiri sana. Pia, kwa sababu mbalimbali, akina baba wamerudisha mahari na kushurutisha binti zao kuwaacha waume zao.

Kuna wale wanaotoa ubishi kwamba mahari kubwa husaidia kuvunja moyo jambo hilo kwa sababu ya ugumu wa kuweza kurudishiwa au kurudisha kadiri kubwa ya pesa. Wao wanahisi pia kwamba bei kubwa hupunguza wingi wa ndoa za mapema, kwa maana huchukua muda mrefu mwanamume kuokoa pesa za kufunga ndoa. Wao wanahisi kwamba mafikirio hayo hutokeza waume wakomavu wenye kujali madaraka, na ndoa zenye imara nyingi zaidi.

Ingawa huenda hiyo ikawa kweli katika visa fulani, msingi wa imara ya ndoa ya Kikristo haupasi kuwa mafikirio hayo ya vitu vya kimwili. Uaminifu wa mume Mkristo haupasi kutegemea kiasi cha vitu vya kimwili ambavyo huenda akapoteza ndoa ile ikivunjika. Badala ya hivyo, yeye anapaswa kuongozwa na kanuni hii ya Kimaandiko: “Kitu ambacho Mungu amefungia nira pamoja mtu asikitenganishe.” (Mathayo 19:6, NW) Badala ya kuwa na rai ya kwamba wake ni mali ya kununuliwa, waume wanaamriwa ‘wawape heshima.’ (1 Petro 3:7) Yesu alisema kwamba mwanamume na mwanamke wanakuwa “mnofu mmoja” wakati wanapofunga ndoa. (Mathayo 19:5; Mwanzo 2:24, NW) Biblia inashauri waume wapende wake zao, wawajali sana na kuwatunza, sawa na vile wanavyofanyia miili yao wenyewe. (Waefeso 5:28, 29) Zaidi ya hilo, kipimo halisi cha upendo wa mwanamume kinapasa kuwa kwa jinsi yeye anavyotendea mke wake katika miaka ile ya baada ya arusi. Mume awe au asiwe amelipa mahari yoyote, ikiwa yeye anatunza mke wake na ni mshikamanifu katika upendo wake, je! mtu yeyote angeweza kutia shaka kwamba anampenda?

Mahari inaweza pia kuathiri rai ya mume kuhusu wazazi wa mke wake. Akiwa amekwisha lipa mahari kubwa, yeye angeweza kukata shauri kwamba hana deni jingine lolote kwao, hata wakitumbukia katika uhitaji. Hata hivyo, Biblia inasema hivi: “Mjane akiwa ana watoto au wajukuu, na wajifunze kwanza kuyatenda yaliyo wajibu wao kwa jamaa zao wenyewe, na kuwalipa wazazi wao. Kwa kuwa hili lakubalika mbele za Mungu.” (1 Timotheo 5:4) Wakristo wanafuata shauri hilo, lakini tatizo linaweza kutokea ikiwa mume anaruhusu uhakika wa kwamba alilipa mahari upotoshe hisia yake ya kujali daraka.

Dumisha Rai Yenye Usawaziko

Mazoea fulani yanayohusiana na mahari yangeweza kufanyiza matatizo ya pekee kwa mwanamume kijana atakayeoa dada wa kiroho ambaye wazazi wake si Wakristo. Wao wangeweza kumtaka ashiriki katika mila zinazotegemea kuabudu mababu na kuitikadi katika kutokufa kwa nafsi. (Mhubiri 9:5, 10; Ezekieli 18:4) Lakini je! yeye angeweza kufanya hivyo bila kupoteza upendeleo wa Mungu na baraka ambayo Yehova huweka akibani kwa ajili ya wale ambao ‘wametakatisha nafsi zao kwa kutii kwao ule ukweli’? (1 Petro 1:22; Ufunuo 18:4, NW) Akikabiliana na madai ya jinsi hiyo, ni lazima Mkristo aliyejiweka wakfu apige moyo konde ‘kutii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.’​—Matendo 5:29, NW.

Maelezo yaliyotangulia kuhusu unyakuzi, kuepuka uasherati, na kufunga ndoa na waitikadi wenzi peke yao yanatumika kwa usawa ule ule wakati ambapo jamaa ya bibi-arusi ndiyo yenye kuandaa mahari. Msichana Mkristo na wazazi wake hapaswi kuongozwa na viwango vya kilimwengu katika kuchagua mume. Kuolewa na mtu asiye Mkristo ni kitendo cha kutotii Mungu. Kupitia Musa, Yeye aliambia hivi Waisraeli: “Binti yako usimpe mwanawe mume, wala usimtwalie mwanao mume binti yake.” (Kumbukumbu 7:3, 4; 1 Wakorintho 7:39) Ni wazi kwamba haingefaa wanaume au wanawake vijana walio Wakristo wajitangaze katika karatasi-habari za watu wote ya kwamba wanatafuta wenzi wa ndoa wanaostahili. Wao wanapaswa kutafuta wenzi wa ndoa wenye kustahili miongoni mwa ndugu na dada zao Wakristo.

Ndoa ni mpango mtakatifu wa Yehova, na sisi sote tunapaswa kuongozwa na yale anayosema juu yayo katika Neno lake. Upendo wenye juhudi nyingi sana kwa Yehova, watoto wetu, na waitikadi wenzetu unapasa kutuongoza tujiondoshe kabisa kwenye mazoea yote yanayovunja mambo yanayofaa na yaliyo mema. (Zaburi 119:105; Waebrania 4:12) Hakika baraka ya Yehova itaendelea kuwa pamoja na wale wanaoacha Neno lake liwaongoze katika maamuzi yanayohusu si bei ya kununua bibi-arusi na mahari tu bali pia mambo mengine yote ya maisha.​—Mithali 10:22.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki