Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w98 9/15 kur. 24-27
  • Kupatana juu ya Mahari ya Kiasi

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kupatana juu ya Mahari ya Kiasi
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kanuni za Biblia Zenye Kupatana na Akili
  • Ni Nani Apaswaye Kufanya Mapatano?
  • Kuepuka Tabia Zisizo za Kikristo
  • Vielelezo vya Kiasi
  • Faida za Kuwa na Kiasi
  • Je, Wajua?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2022
  • Mahari—Wakristo Wawe na Rai Gani Kuihusu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • “Ndoa ya Kidesturi” Katika Ghana
    Amkeni!—1996
  • Kutayarisha Kwa Ajili Ya Ndoa Yenye Mafanikio
    Siri ya Furaha ya Familia
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
w98 9/15 kur. 24-27

Kupatana juu ya Mahari ya Kiasi

LEO, sawa na ilivyokuwa katika nyakati za Biblia, tamaduni fulani hutaka mahari ilipwe kabla mwanamume hajamwoa mwanamke. “Nitakutumikia miaka saba kwa kumpata Raheli, binti yako mdogo,” Yakobo akamwambia Labani ambaye angekuja kuwa baba-mkwe wake. (Mwanzo 29:18) Kwa sababu Yakobo alimpenda Raheli, yeye alitoa kiasi kikubwa sana—kilicholingana na mshahara wa miaka saba! Labani alikubali toleo hilo lakini akamkenga Yakobo ili amwoe binti yake mkubwa, Lea. Labani aliendelea kushughulika na Yakobo kwa ujanja. (Mwanzo 31:41) Binti za Labani hawakumheshimu kwa sababu alikazia faida za kimwili. “Hakutufanya kama wageni, maana ametuuza, naye amekula fedha zetu kabisa?” wakauliza.—Mwanzo 31:15.

Kwa kusikitisha, katika ulimwengu wa leo wenye kufuatia vitu vya kimwili, wazazi wengi ni kama Labani. Na wengine ni wabaya zaidi. Kulingana na gazeti moja la Afrika, mapatano ya ndoa fulani hufanywa “kwa minajili tu ya akina baba wenye pupa kujifaidi.” Kisababishi kingine ni mkazo wa kiuchumi ambao huwashawishi wazazi fulani wawaone binti zao kuwa njia ya kuondolea mbali matatizo ya kifedha.a

Wazazi fulani huwakawiza binti zao wasiolewe kwa sababu wanamngoja atakayetoa kiasi kikubwa zaidi. Hilo laweza kutokeza matatizo mazito. Ripota wa gazeti katika Afrika Mashariki aliandika hivi: “Vijana huamua kutoroka kwa siri na wapenzi wao ili kuepuka kudaiwa mahari ya juu na wakwe wagumu.” Ukosefu wa adili katika ngono ni mojawapo ya matatizo yanayosababishwa na kudaiwa kwa kiasi cha juu cha mahari. Isitoshe wanaume wengi vijana hufanikiwa kumnunua mke lakini huachwa katika deni kubwa sana. “Wazazi wapaswa kuwa wenye kiasi,” akahimiza mfanyakazi wa kijamii wa Afrika Kusini. “Hawapaswi kudai kiasi kikubwa. Wenzi waliooana karibuni wahitaji kujikimu. . . . Basi mbona kumfilisi kijana?”

Wazazi Wakristo waweza kuwekaje kielelezo cha kuwa wenye kiasi, wenye kukubali sababu, wanapopatana juu ya malipo au upokeaji wa mahari? Jambo hili ni zito, kwa kuwa Biblia huamuru hivi: “Hali yenu ya kukubali sababu na ijulikane kwa watu wote.”—Wafilipi 4:5.

Kanuni za Biblia Zenye Kupatana na Akili

Iwapo wazazi Wakristo wataamua kufanya mapatano juu ya mahari au la ni uamuzi wa kibinafsi. Wakiamua kupatana, mapatano hayo yapaswa kufanywa kulingana na kanuni za Biblia. “Acheni namna yenu ya maisha iwe bila upendo wa fedha,” lasema Neno la Mungu. (Waebrania 13:5) Endapo kanuni hii haidhihiriki katika mapatano kuhusu ndoa, huenda mzazi Mkristo akawa anajidhihirisha kuwa kielelezo kisichofaa. Wanaume wenye madaraka katika kutaniko la Kikristo wapaswa kuwa wenye “kukubali sababu,” si ‘wapenda-fedha’ au “wenye pupa ya pato lisilo la haki.” (1 Timotheo 3:3, 8) Mkristo atozaye kiasi kikubwa cha mahari kwa pupa bila toba aweza hata kutengwa na ushirika wa kutaniko.—1 Wakorintho 5:11, 13; 6:9, 10.

Kwa sababu ya matatizo yanayotokezwa na pupa, serikali fulani zimetunga sheria ambazo hudhibiti mahari. Kwa mfano, sheria moja katika nchi ya Afrika Magharibi ya Togo husema mahari “yaweza kulipwa kwa bidhaa au kwa pesa taslimu au njia zote mbili.” Sheria iliongeza kusema: “Kiasi cha mahari hakipasi kamwe kuzidi jumla ya 10,000 F CFA (dola 20 za Marekani).” Kwa kurudia-rudia, Biblia huwaamuru Wakristo wawe raia wenye kutii sheria. (Tito 3:1) Hata iwapo serikali haitekelezi sheria kama hiyo, Mkristo wa kweli atataka kutii. Atadumisha dhamiri safi mbele za Mungu na hatakuwa sababu ya kukwaza wengine.—Waroma 13:1, 5; 1 Wakorintho 10:32, 33.

Ni Nani Apaswaye Kufanya Mapatano?

Katika tamaduni fulani, huenda namna ambayo mapatano ya mahari hufanywa ikapingana kabisa na kanuni nyingine muhimu. Kulingana na Biblia, baba ndiye mwenye daraka juu ya mambo ya nyumba yake. (1 Wakorintho 11:3; Wakolosai 3:18, 20) Hivyo, wale wenye vyeo vyenye madaraka kutanikoni wapaswa kuwa wanaume wenye “[ku]simamia watoto na watu wa nyumbani mwao wenyewe kwa njia bora.”—1 Timotheo 3:12.

Hata hivyo, huenda ikawa kawaida katika jamii kuacha mapatano ya muhimu ya ndoa yafanywe na watu wa jamaa ya kichwa cha familia. Na watu hao wa jamaa hudai kiasi fulani cha mahari. Hili hutahini nyumba za Kikristo. Wakidai kufuata desturi, vichwa fulani vya familia wameruhusu watu wa jamaa wasioamini kudai kiasi kikubwa sana cha mahari. Nyakati nyingine hili limefanya msichana Mkristo aolewe na mtu asiyeamini. Hilo lapingana na himizo la kwamba Mkristo apaswa kuoa au kuolewa “katika Bwana tu.” (1 Wakorintho 7:39) Kichwa cha familia anayewaruhusu watu wa jamaa yake wafanye maamuzi yenye kuhatarisha hali njema ya kiroho ya watoto wake, hawezi kuonwa kama “mwenye kusimamia nyumba yake vizuri.”—1 Timotheo 3:4.

Kama ilivyokuwa katika kisa cha mzee wa ukoo Abrahamu aliyemcha Mungu, vipi ikiwa baba Mkristo hashiriki moja kwa moja katika mapatano ya ndoa ya mmoja wa watoto wake? (Mwanzo 24:2-4) Endapo mtu mwingine achaguliwa kufanya hili, baba Mkristo apaswa kuhakikisha kwamba mpatanishi huyo afuata maagizo yanayopatana na kanuni za Biblia. Isitoshe, kabla hatua zozote hazijachukuliwa katika kufanya mapatano juu ya mahari, wazazi Wakristo wapaswa kufikiria mambo kwa uzito na kutojiruhusu wenyewe wavutwe na mila au kudai kusikopatana na akili.—Mithali 22:3.

Kuepuka Tabia Zisizo za Kikristo

Biblia hulaumu majivuno na “wonyesho wa mtu wa kujivunia njia yake ya kutegemeza maisha.” (1 Yohana 2:16; Mithali 21:4) Hata hivyo, watu fulani wenye kushirikiana na kutaniko la Kikristo wameonyesha tabia hizo katika mapatano yao ya ndoa. Wengine huiga ulimwengu kwa kujionyesha katika kulipa au kupokea kiwango kikubwa cha mahari. Kwa upande mwingine, ofisi moja ya tawi ya Watch Tower Society yaripoti hivi: “Waume fulani hawaonyeshi heshima wakati familia inapodai kwa kiasi, wakiwaona wake zao kama walionunuliwa kwa bei ya ‘mbuzi.’”

Wakristo fulani wamepatwa na pupa ya kiasi kikubwa cha mahari na jambo hili limehuzunisha. Kwa kielelezo, fikiria ripoti hii kutoka ofisi nyingine ya tawi ya Watch Tower Society: “Kwa kawaida ni vigumu kwa ndugu waseja kuoa au dada kupata wenzi. Tokeo limekuwa ongezeko la visa vya kutenga na ushirika kwa sababu ya ukosefu wa adili katika ngono. Ndugu fulani huenda kwenye migodi wakatafute dhahabu au almasi ambazo waweza kuziuza ili wapate mali inayotosha kuoa. Hilo laweza kuwachukua mwaka mmoja au miwili au zaidi, na kwa kawaida wao hudhoofika kiroho wanapokwenda mbali na ushirika wa akina ndugu na wa kutaniko.”

Ili kuepuka matokeo hayo yenye kuhuzunisha, wazazi Wakristo wapaswa kufuata kielelezo cha waliokomaa kutanikoni. Ijapokuwa hakuwa mzazi, mtume Paulo alishughulika na waamini wenzake kwa kiasi. Alikuwa mwangalifu asije akamtwika yeyote mzigo wenye kulemea wa gharama kubwa. (Matendo 20:33) Kwa kweli, wazazi Wakristo wapaswa kufikiria mfano wake usio na ubinafsi wanapofanya mapatano juu ya mahari. Bila shaka, Paulo alivuviwa na Mungu kuandika haya: “Kwa muungano iweni waigaji wangu, akina ndugu, na fulizeni kuwaangalia wale wanaotembea katika njia ilinganayo na kielelezo mlicho nacho katika sisi.”—Wafilipi 3:17.

Vielelezo vya Kiasi

Kwa habari ya mapatano ya ndoa, wazazi wengi Wakristo wameweka kielelezo kizuri cha kuwa wenye kiasi. Fikiria kisa cha Joseph na mke wake Mae, wanaotumika wakiwa waeneza-evanjeli wa wakati wote.b Wanaishi katika mojawapo ya Visiwa vya Solomon ambapo mapatano ya mahari huwa tatizo nyakati nyingine. Ili kuepuka magumu hayo, Joseph na Mae walipanga binti yao Helen aolewe katika kisiwa jirani. Walifanya vivyo hivyo kwa habari ya binti mwingine, Esther. Joseph alikubali mkwe wake Peter alipe mahari iliyokuwa chini kiwango ambacho kwa kufaa kingeweza kukubalika. Alipoulizwa sababu ya kufanya hivyo, Joseph alieleza: “Sikutaka kumwekea mzigo wenye kulemea mkwe wangu ambaye ni painia.”

Mashahidi wengi wa Yehova katika Afrika wameweka vielelezo vizuri pia katika kuwa na kiasi. Katika maeneo fulani, washiriki wa jamii zilizopanuka kwa ujumla hutarajia kulipa kiasi kikubwa cha pesa kabla ya mapatano hususa ya kiasi cha mahari. Na ili ampate bibi-arusi, huenda bwana-arusi akatarajiwa kuahidi kwamba atalipa mahari ya wakati ujao ya ndugu mchanga wa mchumba wake.

Tofauti na hili, fikiria kielelezo cha Kossi na mke wake Mara. Hivi karibuni, binti yao, Beboko, aliolewa na mwangalizi asafiriye wa Mashahidi wa Yehova. Kabla ya ndoa hiyo, watu wa jamaa waliweka mkazo mkubwa ili kupata fungu lao la mahari kubwa. Hata hivyo, wenzi hao walisimama imara na kukataa madai hayo. Badala yake, walifanya mapatano moja kwa moja na atakayekuwa mkwe wao, wakiitisha kiasi cha chini zaidi kwa ajili ya binti yao na kisha kurudisha nusu ya kiasi hicho kwa wenzi hao wachanga watumie kutayarisha siku ya arusi yao.

Kielelezo kingine katika nchi hiyohiyo chahusisha Shahidi mchanga aitwaye Itongo. Hapo awali, familia yake iliomba mahari ya kiasi. Lakini watu wa jamaa wakadai kiasi hicho kiongezwe. Hali ilikuwa ya wasiwasi, na ilionekana kwamba watu hao wa jamaa wangefaulu. Ijapokuwa kwa kawaida yeye huwa mwogamwoga, Itongo alisimama na kwa heshima akataarifu kwamba yeye alikuwa ameazimia kuolewa na Mkristo mwenye bidii aitwaye Sanze, kama ilivyokuwa imepangwa. Kisha akasema kwa ujasiri, “Mbi ke” (yaani, “Uamuzi umefikiwa”) na kuketi. Aliungwa mkono na mama yake Mkristo, Sambeko. Hakukuwa na mazungumzo mengine, na wenzi hao wakaoana kama ilivyokuwa imepangwa awali.

Kuna mambo ambayo wazazi Wakristo wenye upendo huhangaikia, kuliko zile faida za kimwili zinazotokana na mahari. Mume mmoja katika Kamerun aeleza hivi: “Mkwe wangu hutumia kila fursa kuniambia kile nilichokusudia kumpa kama mahari, nikitumie kwa mahitaji ya binti yake.” Wazazi wenye upendo huhangaikia pia hali njema ya kiroho ya watoto wao. Kwa kielelezo, fikiria Farai na Rudo, ambao huishi Zimbabwe na hutumia wakati mwingi katika kazi ya kuhubiri na kueneza habari njema za Ufalme wa Mungu. Ijapokuwa hawachumi mshahara wowote wao walitoa binti zao wawili kwa kiasi kidogo sana ya kile huitishwa kwa kawaida. Kwa nini? Wao walitaka binti zao wafaidike kutokana na kuolewa na wanaume wampendao Yehova kikweli. “Kile tulichoona kuwa cha muhimu ni hali ya kiroho ya binti zetu na wakwe zetu pia,” wakaeleza. Jinsi inavyoburudisha! Wakwe waonyeshao hangaiko lenye upendo kwa mambo ya kiroho na ya kimwili ya watoto wao waliofunga ndoa wanastahili kupongezwa sana.

Faida za Kuwa na Kiasi

Joseph na Mae wa Visiwa vya Solomon walibarikiwa kwa ukarimu wao na uangalifu ambao walishughulikia ndoa za binti zao. Hivyo, wakwe wao hawakutumbukizwa katika deni. Badala yake, wenzi wa ndoa zote mbili wameweza kutumia miaka mingi katika kazi ya wakati wote ya kueneza ujumbe wa Ufalme. Akumbukapo yaliyotokea, Joseph asema hivi: “Maamuzi ambayo mimi na familia yangu tulifanya yametokeza baraka nyingi. Kweli kuna nyakati kumekuwa na mkazo mwingi sana kutoka kwa wale ambao hawakuelewa, lakini nina dhamiri safi na kuridhika nionapo watoto wangu wakiwa na shughuli nyingi na wenye nguvu katika utumishi wa Yehova. Wao pia ni wenye furaha, na mke wangu na mimi tuna furaha kwelikweli.”

Faida nyingine imekuwa uhusiano mzuri kati ya wakwe. Kwa kielelezo, Zondai na Sibusiso ni wafanyakazi wa kujitolea wakiwa na wake zao, ambao ni dada za kimwili, katika ofisi ya tawi la Zimbabwe ya Watch Tower Society. Baba-mkwe wao Dakarai, ni mweneza-evanjeli wa wakati wote asiyepata mshahara wowote. Wakati wa kipindi cha mapatano juu ya kiasi cha mahari, yeye alisema angekubali chochote kile ambacho wangeweza kupata. “Twampenda sana baba-mkwe wetu,” Zondai na Sibusiso wasema, “nasi tungefanya yote tuwezayo tumsaidie endapo atakuwa katika uhitaji.”

Ndiyo, kuwa na kiasi katika mapatano ya mahari, huchangia furaha ya familia. Kwa kielelezo, waliooana karibuni hawatakuwa na deni, ikifanya iwe rahisi kwao kuzoea maisha ya ndoa. Hili limewezesha wenzi wengi wachanga kufuatia baraka za kiroho, kama vile kutumikia kwa wakati wote katika kazi ya uharaka ya kuhubiri na kufanya wanafunzi. Hili nalo humletea utukufu Mwanzilishi wa ndoa mwenye upendo, Yehova Mungu.—Mathayo 24:14; 28:19, 20.

[Maelezo ya Chini]

a Katika tamaduni fulani, hali ni kinyume. Wakwe hutazamia kupewa mahari kutoka kwa wazazi wa bibi-arusi.

b Majina yamebadilishwa katika makala hii.

[Sanduku katika ukurasa wa 27]

WALIRUDISHA MAHARI

Katika jamii fulani, bibi-arusi na wazazi wake hudharauliwa ikiwa kiasi cha mahari ni cha chini. Hivyo, kiburi na tamaa ya kuonyesha hadhi ya familia ya mtu wakati mwingine huwa nia ya kufanya mapatano ya kiwango cha juu cha mahari. Familia moja katika Lagos, Nigeria, huandaa tofauti yenye kutokeza. Mkwe wao Dele, aeleza haya:

“Familia ya mke wangu ilinistarehesha kutokana na matumizi mengi ambayo huwa kawaida ya sherehe ya kitamaduni ya utoaji wa mahari, kama vile kununua namna-namna nyingi za mavazi yenye bei kubwa. Hata familia yangu iliwapa mahari, msemaji wao aliuliza hivi: ‘Je wataka kumchukua msichana huyu awe mke au awe binti?’ Familia yetu kwa pamoja ikajibu: ‘Twataka kumchukua awe binti.’ Baada ya hilo tulirudishiwa mahari hayo katika bahasha ileile.

“Mpaka leo hii, nathamini jinsi wakwe wangu walivyoshughulikia arusi yangu. Ilinifanya niwaheshimu sana. Mtazamo wao bora sana wa mambo ya kiroho hunifanya niwaone kuwa watu wa jamaa walio karibu sana. Hili liliathiri sana mtazamo wangu kuelekea mke wangu. Nimekuza uthamini wenye kina kwake kwa sababu ya namna familia yake ilivyonitendea. Tunapokuwa na kutoelewana, mimi sikuruhusu kuwe tatizo. Mara nikumbukapo familia anayotoka, kutopatana huko hupungua.

“Familia yao na yetu zimeunganishwa kwa vifungo vya kirafiki. Hata sasa, miaka miwili baada ya arusi yetu, baba yangu bado huipelekea zawadi na vyakula familia ya mke wangu.”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki