Abudu Muumba, Si Kilichoumbwa
“Ni Yehova Mungu, wako ambaye ni lazima wewe uabudu, na kwa yeye peke yake ni lazima wewe utoe utumishi mtakatifu.”—LUKA 4:8, NW.
1. Neno “kuabudu” limefafanuliwaje, na ibada ya kweli inapasa kutolewaje?
NENO “kuabudu” linafafanuliwa katika kamusi hivi: “Kuchukua kitu kwa staha, heshima, au ujitoaji mkubwa, hata wa kupita kiasi.”a Nani anapaswa kupewa ibada hiyo? Yesu Kristo alisema: “Ni lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili zako zote.” (Mathayo 22:37, NW) Pia, alipopewa toleo la falme zote za ulimwengu akifanya “kitendo [kimoja tuj cha ibada” kwa Shetani, Yesu alikataa, akijulisha wazi hivi: “Ni Yehova Mungu wako ambaye ni lazima wewe uabudu, na kwa yeye peke yake ni lazima wewe utoe utumishi mtakatifu.” (Luka 4:7, 8, NW) Kutokana na maneno na vitendo vya Yesu, ni wazi kwamba aliye wa kuabudiwa ni Yehova Mungu tu. Ibada hiyo inatia ndani “utumishi mtakatifu,” kwa maana “imani pasipo matendo imekufa.”—Yakobo 2:26.
2. Kwa nini inafaa kuabudu Muumba peke yake?
2 Kuabudu Yehova hivyo kunafaa kwa sababu ndiye Mwenye Enzi Kuu Zaidi wa ulimwengu wote mzima, Muumba wa mbingu za kustaajabisha sana na dunia pamoja na namna zote za uhai uliomo. Akiwa hivyo, ndiye peke yake anayestahili kuheshimiwa na wanadamu kwa “staha, heshima, au ujitoaji mkubwa, hata wa kupita kiasi.” Biblia inataarifu hivi: “Umestahili wewe, Bwana wetu [Yehova, NW] na Mungu wetu, kuupokea utukufu na heshima na uweza; kwa kuwa wewe ndiwe uliyeviumba vitu vyote, na kwa sababu ya mapenzi yako vilikuwako, navyo vikaumbwa.” (Ufunuo 4:11) Kwa uhakika, hakuna mwanadamu wa kikawaida tu, hakuna kitu kilicho au kisicho na uhai, kingestahili hiyo “staha, heshima, au ujitoaji.” Yehova tu ndiye anayestahili “ujitoaji wa pekee.”—Kutoka 20:3-6, NW.
Uharaka Maalumu
3. Kwa nini kuna uharaka maalumu kwamba sisi tuabudu Mungu?
3 Kwa sababu tunaishi katika kipindi cha hukumu, sasa kuna uharaka maalumu wa kuabudu Mungu ifaavyo. Matokeo ya milele yanaendelea kuamuliwa. Neno la Mungu la kiunabii linatuambia kwamba katika hizi “siku za mwisho” za mfumo uliopo wa mambo, Kristo Yesu amewasili katika utukufu wa kimbingu “na malaika wote pamoja naye.” Kwa kusudi gani? Yesu mwenyewe alitabiri kusudi hilo, akisema: “Mataifa yote yatakusanywa mbele yake, na yeye atatenga watu mmoja kutoka kwa mwingine, sawa na vile mchungaji hutenga kondoo watoke kwenye mbuzi.” Kondoo wataondoka “kuingia katika uhai wa milele.” Mbuzi wataondoka “kuingia katika kukatiliwa-mbali kwa milele.”—2 Timotheo 3:1-5; Mathayo 25:31, 32, 46, NW.
4. (a) Paulo anatambulishaje wale watakaoharibiwa daima kwenye mwisho wa ulimwengu huu? (b) Ni mwelekeo gani unaoonyeshwa na wale watakaopata uhai wa milele?
4 Mtume Paulo aliandika juu ya “kufunuliwa kwake Bwana Yesu kutoka mbinguni pamoja na malaika wa uweza wake; katika mwali wa moto; huku akiwalipiza kisasi wao wasiomjua Mungu, na wao wasioitii Injili ya Bwana wetu Yesu; watakaoadhibiwa kwa maangamizi ya milele.” (2 Wathesalonike 1:7-9) Hivyo, uharibifu wa milele ndilo tokeo la watu washupavu wa kimbuzi, wasiotaka kujua juu ya makusudi ya Mungu au wanaokataa kuchukua hatua wakiwa na fursa. Lakini “uhai wa milele” ndilo tokeo la watu wanyenyekevu wa kikondoo, wanaotaka kujua juu ya Yehova, wanaosikiliza maagizo yake, halafu wanajitiisha kwenye penzi lake. Biblia inasema: “Ulimwengu unapitilia mbali na ndivyo na tamaa yao, bali yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anabaki milele.”—1 Yohana 2:17, NW; ona pia 2 Petro 2:12.
5, 6. (a) Ni lazima mtu afanye nini ili apate ukweli juu ya Yehova na makusudi yake? (b) Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba watafutaji wa ukweli watakutana na ukweli hata kama hali yao ni nini maishani?
5 Watu wa kikondoo wana nia ya kudhabihu wakati, nishati, na mali za kimwili wautafute ukweli. Wao hufanya inavyosema Mithali 2:1-5: “Mwanangu, kama ukiyakubali maneno yangu, na kuyaweka akiba maagizo yangu; hata ukatega sikio lako kusikia hekima, ukauelekeza moyo wako upate kufahamu; naam, ukiita busara, na kupaza sauti yako upate ufahamu; ukiutafuta kama fedha, na kuutafutia kama hazina iliyositirika; ndipo utakapofahamu kumcha Bwana [Yehova, NW], na kupata kumjua Mungu.”
6 Nia ya kutafuta Yehova ndiyo hutenga watu wa kikondoo watoke kwa walio wa kimbuzi. “Ukimtafuta, ataonekana nawe; ukimwacha, atakutupa milele.” (1 Mambo ya Nyakati 28:9) Hivyo, hata kama mtu ni wa rangi au utaifa gani, hata kama ana elimu gani, kama ni tajiri au maskini, akiutafuta kwa moyo mweupe ukweli unaohusu Mungu, ataupata. Wakiwa kwenye mtazamo wao wa kimbingu, Kristo na malaika zake watahakikisha kwamba mtafutaji anakutana na ukweli, hata kama anaishi wapi. Utafutaji huo utathawabishaje? Yesu alisema: “Hii ndiyo maana ya uhai wa milele, kutwaa kwao maarifa ya kukujua wewe, Mungu wa kweli mmoja tu, na ya yeye uliyemtuma, Yesu Kristo.”—Yohana 17:3, NW; ona pia Ezekieli 9:4.
Kuepuka Ibada ya Kiumbe
7, 8. (a) Kuabudu wanadamu kuna hatari gani? (b) Eleza juu ya ‘staha, heshima, au ujitoaji wa kupita kiasi’ ambao Mariamu anapewa.
7 Watu wengi duniani pote wanachukua wanadamu—walio hai au wafu—kwa ‘staha, heshima, au ujitoaji wa kupita kiasi.’ Ingawa huenda wakawa wanahisi hiyo ni sehemu ya ibada yao kwa Mungu, kwa kweli inawapotosha kutoka kwenye ibada ya kweli. Hiyo inawafungulia njia ili kuamini kanuni zilizopokewa na kujihusisha katika mazoea yaliyo kinyume cha penzi la Mungu. Kielelezo kimoja cha kutokeza ni jinsi Mariamu, mama ya Yesu, anavyoonwa na mamilioni ya watu katika mabara ya Katoliki ya Kiroma na pia ya Katoliki Orthodoksi ya Mashariki.
8 Mifano na aikoni za Mariamu huinamiwa katika mwelekeo wa ibada, na katika kanuni rasmi iliyopokewa ya kanisa, Mariamu hutajwa kuwa “Bikira Mariamu Theotokos.” Neno the·o·toʹkos humaanisha “mzaa-Mungu” au “mama ya Mungu.” New Catholic Encyclopedia inasema: “Mariamu ndiye mama ya Mungu. . . . Ikiwa Mariamu siye kweli aliye mama ya Mungu, basi Kristo si Mungu wa kweli na pia mwanadamu wa kweli.” Hivyo, kama sehemu ya kanuni yao iliyopokewa ya Utatu, dini hizi hufundisha kwamba Yesu alikuwa Mungu Mwenye Nguvu Zote akiwa katika umbo la binadamu, hiyo ikimfanya Mariamu awe “mama ya Mungu.” Chanzo icho hicho kinaongezea kwamba ujitoaji kwa Mariamu unatia ndani: “(1) kicho kingi sana, au utambuzi wa heshima kuu juu ya fahari ya huyo Bikira mtakatifu aliye Mama ya Mungu; (2) kumwomba sana msaada, au kumwomba Bibi Mheshimiwa wetu afanye uombezi wake wa kimama na kimalkia kwa ajili yetu; . . . na sala za faragha [kwa Mariamu].”
9. Je! Biblia inafundisha kwamba Mariamu alikuwa “mama ya Mungu”?
9 Hata hivyo, neno the·o·toʹkos halionekani katika Maandiko yaliyovuviwa. Na hakuna mahali ambapo Biblia inasema Mariamu alikuwa “mama ya Mungu.” Yesu hakufundisha hivyo, wala Wakristo wa karne ya kwanza. Zaidi ya hilo, Biblia inaonyesha wazi kwamba Yesu hakuwa Mungu Mwenye Nguvu Zote akiwa katika umbo la binadamu bali alikuwa Mwana wa Mungu.b Kweli kweli, Mariamu alipotaarifiwa na malaika kwamba angezaa mwana, aliambiwahivi: “Roho takatifu itakuja juu ya wewe, na nguvu ya Aliye Juu Zaidi itakaa juu ya wewe kama kivuli. Kwa sababu hiyo pia kile chenye kuzaliwa kitaitwa kitakatifu, Mwana wa Mungu.” (Luka 1:35, NW) Kwa hiyo Yesu alikuwa Mwana wa Mungu, wala hakuwa ndiye Mungu mwenyewe akiwa katika umbo la binadamu. Hivyo, Mariamu alikuwa mama ya Yesu akiwa mwana wa Mungu, si mama ya Mungu akiwa katika umbo la binadamu. Ndiyo sababu wala Yesu wala wanafunzi wake hawakumwita kamwe Mariamu “mama ya Mungu.”
10, 11. (a) Ni vielelezo gani vinavyoonyesha jinsi Yesu alivyomwona mama yake? (b) Mitume na wanafunzi wa Yesu walimwonaje mama yake?
10 Jinsi Yesu alivyomwona mama yake inaonyesha kwamba cheo cha mama huyo ni cha kadiri tu. Kwenye karamu ya ndoa katika Kana, usimulizi wa Biblia unatuambia hivi: “Divai ilipopunguka mama ya Yesu alisema kwake hivi: ‘Wao hawana divai.’ Lakini Yesu akasema kwa yeye: ‘Mimi nina nini na wewe, mwanamke?’ “Hapa “Roman Catholic Douay Version” ya Biblia husomwa hivi: “Mwanamke, hiyo ni nini kwangu mimi na kwako wewe?” (Yohana 2:3, 4, NW) Pindi nyingine, mtu fulani alisema kwake hivi: “Lenye furaha ni tumbo la uzazi lililokubeba na matiti ambayo wewe ulinyonya!” Hiyo ilikuwa fursa nzuri sana Yesu ampe mama yake heshima maalumu na kuonyesha kwamba wengine wanapaswa kufanya ivyo hivyo. Badala ya hivyo, Yesu alisema: “Sivyo, bali, Wenye furaha ni wale wanaosikia neno la Mungu na kulishika!”—Luka 11:27, 28, NW.
11 Marejezo hayo yanaonyesha kwamba Yesu alijiangalia asimpe Mariamu ujitoaji au heshima asiyostahili au asimwite kwa mtajo wowote wa cheo maalumu. Hakuruhusu uhusiano wao ushawishi maoni yake. Na mitume na wanafunzi walifuata kielelezo chake, kwa maana katika maandishi yao yaliyovuviwa hamna mahali ambamo Mariamu anapewa heshima, mtajo wa cheo, au umashuhuri asioustahili. Ingawa walimstahi kuwa mama ya Yesu, hawakuzidi hapo. Kwa uhakika hawakumtaja kuwa “mama ya Mungu.” Walijua kwamba Yesu hakuwa Mungu Mwenye Nguvu Zote akiwa katika umbo la binadamu na, hivyo, haingewezekana Mariamu awe mama ya Mungu, cheo ambacho kinazidi sana kile ambacho Neno la Mungu linamruhusu Mariamu.
Kiibada cha Mungu-Mama
12. Ni mahali gani na wakati gani wazo lilipositawi kwamba Mariamu alikuwa ndiye “mama ya Mungu”?
12 Basi wazo hili lilianzia wapi? Lilipenya polepole ndani ya Jumuiya ya Wakristo yenye uasiimani katika karne za tatu na nne za Wakati wa Kawaida wetu. Hasa ndivyo ilivyokuwa baada ya mwaka 325 W.K. wakati Baraza la Nikaya lilipochagua kufuata kanuni iliyopokewa isiyo ya Kimaandiko, kwamba Kristo alikuwa Mungu. Wazo hilo la kimakosa lilipokubaliwa, ikawa rahisi zaidi kufundisha kwamba Mariamu alikuwa “mama ya Mungu.” Kuhusu hilo, The New Encyclopcedia Britannica inataarifu hivi: “Ule mtajo wa cheo [‘mama ya Mungu’] unaonekana ni kama ulitokea katika utumizi wa ibada, labda katika Alexandria, wakati fulani katika karne ya 3 au ya 4 . . . Kufikia mwisho wa karne ya 4, Theotokos ilikuwa imejiimarisha katika sehemu mbalimbali za kanisa.” New Catholic Encyclopedia inataarifu kwamba kanuni hiyo iliyopokewa ilikubaliwa rasmi “tangu Baraza la Efeso katika 431.”
13. Inaelekea ni nini kilichoshawishi Baraza la Efeso katika 431 W.K. kupiga mbiu kwamba Mariamu ni “mama ya Mungu”?
13 Inafaa kujua ni mahali gani na sababu gani baraza hilo lilikutana. Kitabu The Cult of the Mother-Goddess, kilichotungwa na E. 0. James, kinataarifu hivi: “Baraza la Efeso lilikusanyika katika basilika ya Theotokos katika 431. Katika mahali hapo hasa, zaidi ya penginepo pote, katika jiji hilo lenye sifa mbaya sana ya kuomba Artemi, au Diana kama vile Waroma walivyomwita, ambapo mfano wake ulisemwa kuwa ulianguka kutoka mbinguni, chini ya uvuli wa hekalu lile kubwa lililowekwa wakfu kwa Magna Mater [Mama Mkubwa] tangu 330 B.C. na ambapo, kulingana na pokeo, palikuwa na kao la muda la Mariamu, cheo hicho cha ‘mzaaMungu’ hakingeweza kukosa kuungwa mkono.”
14. Historia inashuhudizaje kwamba kanuni hii iliyopokewa ina chanzo cha kipagani?
14 Basi sawa na vile ilivyo kuhusu Utatu, kanuni iliyopokewa ya “mama ya Mungu” ni fundisho la kipagani linalosingizia kuwa imani ya Kikristo. Ilikuwa sehemu kubwa katika dini za kipagani karne kadhaa kabla ya Kristo. The New Encyclopcedia Britannica inataarifu hivi chini ya kichwa “mungu-mama”: “Kitu chochote kati ya unamna-namna wa miungu ya kike na vifananisha-umama vinavyohusu nguvu za kubuni, uzaliwa, nguvu za uzazi, muungano katika ngono, malezi, na kawaida inayojirudiarudia ya ukuzi. Mtajo huo umetumiwa pia kuhusu maumbo yanayotofautiana sana kama yale yanayoitwa Venasi ya zile Enzi za Kutumia Vifaa vya Mawe na ya Bikira Mariamu. . . . Hakuna utamaduni wowote ambao haujatumia kifananisha-mama fulani kuonyesha jinsi miungu yao ilivyo. . . . Mama huyo ndiye mlinzi na mlezi wa mtoto aliye mungu na, kwa maelezo ya urefusho, ndiye mlinzi na mlezi wa aina yote ya binadamu.” Hivyo, padri Mkatoliki Andrew Greely anasema hivi katika kitabu chake The Making of the Popes 1978: “Kifananisho cha Mariamu kinahusianisha Ukristo moja kwa moja na dini za kale [za kipagani] za miungu-mama.”
Ibada Isiyofaa
15. (a) Ni nini kilichositawi katika Jumuiya ya Wakristo kuhusu Mariamu? (b) Kulingana na Biblia, ni nani peke yake anayeweza kutuombea kwa Mungu?
15 Kudai kwamba Mariamu alikuwa “mama ya Mungu” kunampandisha kwenye cheo ambapo wanadamu wangeelekea kumwabudu, na ndivyo imetukia kwa karne kadhaa. Mamia ya mamilioni ya watu katika mabara mengi wamempelekea sala au wakazipeleka kupitia yeye na kuipa mifano na aikoni zake ujitoaji wa ibada. Ingawa huenda wanatheolojia wakajaribu kutoa udhuru wa jambo hilo kwa kusema kwamba hicho kicho kingi kwa Mariamu ni njia isiyo ya moja kwa moja tu ya kuabudu Mungu, hayo si maoni ya Mungu. “Mungu ni mmoja, na mpatanishi kati ya Mungu na wanadamu ni mmoja, Mwanadamu Kristo Yesu.” (1 Timotheo 2:5; 1 Yohana 2:1, 2) Yesu mwenyewe alisema: “Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi.”—Yohana 14:6.
16. Petro na Yohana walieleweshaje wazi kwamba Yehova peke yake ndiye wa kuabudiwa?
16 Kumpa Mariamu ujitoaji kwa njia iliyo au isiyo ya moja kwa moja, kumpelekea sala, kuinamia mifano na aikoni zake, ni kuabudu kilichoumbwa badala ya kumwabudu Muumba. Ni ibada ya sanamu, na Wakristo wanaagizwa ‘waikimbie ibada ya sanamu.’ (1 Wakorintho 10:14) Wakati Kornelio asiye Myahudi alipomwinamia mtume Petro kwa heshima nyingi mno, angalia lililotukia: “Petro alipokuwa akiingia Kornelio akatoka amlaki akamwangukia miguu, akamsujudia. Lakini Petro akamwinua, akasema, Simama, mimi nami ni mwanadamu.” (Matendo 10:25, 26) Haikufaa kuinamia mwanadamu kwa ibada, na Petro hangekubali hivyo. Pia, baada ya kupokea njozi kutoka kwa malaika, mtume Yohana aripoti hivi: “Nilianguka chini ili niabudu mbele ya nyayo za malaika ambaye alikuwa akionyesha mimi vitu hivi. Lakini yeye aambia mimi: ‘Uwe mwangalifu! Usifanye hivyo! Mimi ni mtumwa mwenzako tu na wa ndugu zako ambao ni wanabii na wa wale ambao wanashika maneno ya hatikunjo hii. Abudu Mungu.”’ (Ufunuo 22:8, 9, NW) Ikiwa hata malaika wa Mungu hapasi kuabudiwa, sembuse wanadamu au mifano yao.
17. Ensaiklopedia moja ya Kikatoliki inakiri tokeo la kumheshimu mno Mariamu huenda likawa nini?
17 Jambo la kwamba kumpa Mariamu ujitoaji huo huenda kukatokeza ibada isiyofaa linakiriwa na The Catholic Encyclopedia. Chapa ya mapema ya kitabu hiki ilitaarifu hivi: “Haiwezekani kukana kwamba ujitoaji ambao watu wengi walipenda kumpa Bikira Mbarikiwa uliambatana na mambo ya kupita kiasi na matumizi mabaya.”
18. Kanuni hiyo iliyopokewa ambayo si ya Kimaandiko ingetoka kwenye chanzo gani?
18 Kanuni hiyo iliyopokewa ambayo si ya Kimaandiko ingetoka kwenye chanzo gani? Ni lazima chanzo hicho kisichoonekana kiwe ni Hasimu wa Mungu, Shetani Ibilisi. (Yohana 8:44) Kwa nini yeye angeendeleza fundisho hilo? Ili kumpunguzia heshima na kumshusha Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, ili kuwapandisha cheo wanadamu, na kusababisha mvurugo. Linapotosha watu watoke kwenye ibada ya kweli na kusababisha wategemee viumbe kwa wokovu. Kwa karne kadhaa limeongezea pia mamlaka ya makasisi juu ya watu wa kikawaida, waliofundishwa kwamba ni lazima wawaheshimu mno viongozi wao wa kidini kwa sababu makasisi peke yao ndio walioijua theolojia hiyo ya kutatanisha.
19, 20. (a) Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba kabla hukumu za Mungu hazijafikilizwa, watu wa kikondoo wataupata ukweli? (b) Ni maswali gani yatakayositawishwa katika makala inayofuata?
19 Hata hivyo, Yesu alitabiri hivi: “Habari njema ya ufalme itahubiriwa katika ulimwengu wote, kuwa ushuhuda kwa mataifa yote; hapo ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mathayo 24:14) Na Yehova anaahidi kwamba kupitia kuhubiriwa kwa Ufalme, yeye atakusanya watu wote wa kikondoo ‘awafundishe njia zake ili waweze kwenda katika mapito yake.’ (Isaya 2:2-4) Kwa sababu wanakusanywa kwenye ibada iliyotakata ya Yehova, Yesu alisema hivi juu yao: “Mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru.” (Yohana 8:32) Kwa hiyo wanaotafuta ukweli wataupata na kuwekwa huru watoke kwenye mafundisho ya dini bandia yanayozuia watu kufanya penzi la Muumba.
20 Kuna mafundisho na mazoea mengine ya kidini yenye kukubaliwa kwa wingi ambayo yamepotosha watu kutoka ibada ya kweli ya Muumba, wakikipa kilichoumbwa ujitoaji wao. Ni nini baadhi yayo, na matokeo yayo yamekuwa nini? Ibada ya kweli inahusisha nini ndani? Makala inayofuata itachunguza maswali haya.
[Maelezo ya Chini]
a Webster’s Ninth New Collegiate Dictionary, 1986.
Wewe Ungejibuje?
◻ Yesu alionyeshaje wazi kwamba Yehova peke yake ndiye wa kuabudiwa?
◻ Kwa nini sasa kuna uharaka maalumu kuabudu ifaavyo?
◻ Kwa nini Mariamu hapasi kupewa heshima asiyostahili?
◻ Lilianzia wapi lile wazo la kwamba Mariamu ndiye “mama ya Mungu”?
◻ Mitume Petro na Yohana walikaziaje kwamba Yehova peke yake ndiye wa kuabudiwa?
na “imani pasipo matendo imekufa.”—Yakobo 2:26.