Muono-Ndani Juu ya Habari
Je! Ni Ufunguo wa Kupata Furaha?
“Magumu ni miaka miwili, furaha ni milele.” Huu ndio msemo unaotumika sasa miongoni mwa wanafunzi Wachina katika Japani, kulingana na karatasi-habari ya Kijapani Yomiuri Shimbun. Wakiwa na matazamio ya kutajirika, wanafunzi hawa hukopa pesa ili waje Japani, kwa kuamini kwamba huko kuna pesa nyingi kama mvua. Wanatumaini kwamba kwa kufanya kazi za nusu-wakati kwa miaka miwili wakiwa bado wanaenda shuleni, huenda wakaokoa yeni milioni mbili (karibu dola 15,400 za United States) halafu warudi nyumbani wakaishi katika raha mustarehe muda wote uliobaki.
Jambo hilo la kutegemea pesa ili ziwe ufunguo wa kupata furaha limeenea ulimwenguni pote. Uchunguzi uliofanywa hivi majuzi miongoni mwa vijana katika 9 kati ya nchi 11 ulifunua kwamba ‘“pesa’ ndilo jambo kubwa zaidi” kati ya mambo yanayowatia wasiwasi na kuwahangaisha, inasema Asahi Evening News.
Hata hivyo, je! kuweka tegemeo katika mali ndilo jambo ambalo kwa kweli litaufungua mlango wa kupata furaha? Mfalme Sulemani mwenye hekima alionya kwamba “apendaye fedha hatashiba fedha.” (Mhubiri 5:10; 7:12) Kutanguliza pesa hakutokezi uradhi wa kweli, wala hakutoi uhakikisho kamili juu ya kupata usalama wakati ujao. Mathalani, Biblia inasema, “fedha yao wala dhahabu yao havitaweza kuwaokoa katika siku ile ya ghadhabu ya Bwana [Yehova, NW].” (Sefania 1:18) Hata hivyo, kwa utofautisho, mtunga zaburi Daudi aliandika hivi:“Mwenye furaha ni mwanamume kakawana ambaye ameweka Yehova kuwa tegemeo lake.” Kumtegemea Yehova, si pesa, ndio ufunguo wa kupata furaha milele.—Zaburi 40:4, NW; Isaya 30:18.
Ugumu Wenye Matatizo Mawili ya Ubatizo
Matatizo mawili yametokezwa kuhusiana na kubatizwa kwa vitoto vichanga katika nyakati za majuzi ndani ya Kanisa la Uingereza. La kwanza linahusu ubatizo “unaofanywa ovyoovyo tu,” ambao kasisi mmoja aliueleza kuwa ni aina fulani ya “kupigwa chanjo ya kiroho.” La pili ni hesabu inayoongezeka ya makasisi wanaokataa kubatiza watoto wachanga ambao wazazi wao hawaliungi mkono Kanisa la Uingereza kwa kuwa watendaji.
Makasisi wengi wanang’amua kwamba mara nyingi wazazi hawataki kuhudhuria kanisa wala hawangetaka watoto wao wafanye hivyo. Mbona basi wabatize vitoto vichanga? “Wanataka watoto wao wachanga wapewe jina la ukristo,” inaeleza The Times, “sawa na vile wanavyotaka kutoa au kupokea zawadi za siku ya kuzaliwa, kupamba nyumba zao wakati wa Krismasi . . . Ni sehemu ya utamaduni wao: si lazima jambo hilo liwe na sababu fulani.”
Kasisi mmoja alijiuzulu kwa sababu alifikia kukata shauri kwamba mabatizo ya vitoto vichanga hayapasi kufanywa. Alisema: “Mtu mmoja tu anayeweza kujikabidhi wajibu huo kumwelekea Kristo ni mtu mwenyewe.” Yeye angaliweza kuongezea kwamba Yesu Kristo alikuwa na miaka 30 alipobatizwa na kwamba neno la Kigiriki la ubatizo, ba·pti.zo, linamaanisha kuchovya au kuzamisha. Baada ya kubatizwa katika Mto Yordani, Yesu alikuja “juu kutoka ndani ya maji.” (Marko 1:10; Mathayo 3:13, 16, NW) Biblia haitaji mahali popote juu ya kunyunyiza maji juu ya vitoto vichanga. Kwa kuwa ubatizo ni ufananisho wa wakfu wa mtu kwa Mungu akiwa mfuasi wa hatua za nyayo za Kristo, huo si uamuzi unaoweza kufanywa na kitoto kichanga.
Vizuia-Mimba na Wakatoliki
Upinzani wa Kanisa Katoliki kwa utumizi wa vizuia-mimba ulitiliwa nguvu na John Paul 2 kwenye Mkutano wa Pili wa Kimataifa uliohusu Theolojia ya Kiadili ambao ulifanywa Roma katika Novemba uliopita. Kulingana na karatasi-habari ya Jiji la Vatikani, L’Osservatore Romano, yeye alisema hivi:“Hiyo si kanuni ya mwongozo iliyovumbuliwa na mwanadamu. Imeandikwa na mkono wa ubuni wa Mungu katika maumbile yenyewe ya mtu-binadamu. Kuitilia shaka ni kama kukataa kutii Mungu kwa akili ya uelewevu wetu,” na kwa hiyo, yeye anaongezea kwamba, “haiwezi kutiliwa shaka na mwanatheolojia aliye Mkatoliki.”
Lakini barua ile ya kipapa Humanae Vitae, iliyotajwa na Papa John Paul na kuandikwa na Paul 6 miaka 20 hivi iliyopita, “ilitiliwa shaka papo hapo na hesabu kubwa ya wanatheolojia,” inasema karatasi-habari ya Kiitalia La Stampa, na ilipuuzwa na “Wakatoliki walio wengi.”
Ni wazi kwamba kushikilia mambo mno kuhusiana na suala la kupanga uzazi kumeleta ukosefu wa muungamano kati ya wanatheolojia na kuvuruga hisia za Wakatoliki wenye mioyo myeupe. Mgawanyiko unaoendelea kuhusu utumizi wa namna yoyote ya vizuia-mimba hata kulimharakisha John Paul kuhimiza wanatheolojia wote wanene “lugha ile ile moja.” Hata hivyo, tofauti na dai la papa kwamba msimamo wa kanisa kuhusu vizuia-mimba ‘uliandikwa na mkono wa ubuni wa Mungu,’ karatasi-habari ya Kiitalia La Repubblica inasema kwamba “hakuna mstari wowote unaotajwa kutokana na zile Injili wala Agano la Kale ili kuhalalisha kanuni hiyo ya mwongozo.”
Biblia haizungumzi mahali popote juu ya kutumia vizuia-mimba wala juu ya kupanga uzazi katika ndoa, wala haisemi kwamba Wakristo wana wajibu wa kuzaa watoto. Neno la Mungu linaacha suala hilo la kupanga jamaa liwe la dhamiri ya kila Wakristo wawili waliofunga ndoa. Kwa kufanya iwe lazima kufuata amrisho lao kuhusu kupanga uzazi, Kanisa Katoliki ‘limeyapita yale yaliyoandikwa.’—1 Wakorintho 4:6.