Wapiga Mbiu ya Ufalme Waripoti
“Ukweli Utawaweka Nyinyi Huru”—Na Kuleta Furaha
KATIKA UINGEREZA, ukweli wa Biblia umewaweka huru watu zaidi ya 113,000, na wengi zaidi wanaupokea ukweli kwa furaha nyingi kila siku. Maneno ya Yesu yanatimia kikweli: “Nyinyi mtajua ule ukweli, na ule ukweli utawaweka nyinyi huru.” (Yohana 8:32, NW) Uhuru huu hutokeza furaha, kama linavyoonyesha ono lifuatalo.
◻Penny alipokuwa katika huduma ya nyumba kwa nyumba, yasimulia ofisi ya tawi, bibi mzee-mzee alimwambia yeye kwa ghafula sana, “Mimi nina shughuli.” Penny akajibu kwamba angerudi tena. Siku chache baadaye, Penny alikuwa akirudi kwenye nyumba zisizokuwa na watu katika wakati ambao haikuwa kawaida yake kufanya hivyo, naye akafika kwenye nyumba ile ile bila kukusudia. Bibi huyo mzee-mzee alifungua mlango akamwalika Penny ndani. “Nilijua ungerudi,” akasema, “nami nimekuwa nikikungojea.” Walizungumza juu ya tumaini la Ufalme, na bibi huyo akasema alitumaini kwamba lingethibitika kuwa kweli. Yeye alikuwa na miaka 79, na mume wake alikuwa amekufa miaka mitatu kabla ya hapo. Bibi huyo hakuwa amepokea faraja yoyote kutoka kanisa lake na hakuweza kuona sababu ya kuishi na alitaka kufa. Baadaye, Penny alipokwisha kuanza funzo la Biblia pamoja naye, bibi huyo alimwambia Penny kwamba alikuwa amekuwa akifikiria kujiua lakini alijua ni kosa kufanya hivyo. Alikuwa amempelekea Mungu sala ili ampe faraja na kumsaidia apate tena tumaini. Alipokuwa akijifunza, mtamauko wake ulibadilika pole kwa pole ukawa tumaini, akiwa na usadikisho wa kina kirefu na shukrani kwa Yehova. Alikatiza ukamatano wake wa maisha yote pamoja na kanisa, akabatizwa kwenye umri wa miaka 80, na sasa ni mhubiri wa kawaida mwenye bidii kubwa. Kwa kweli, ukweli wa Neno la Mungu umemweka huru na kumletea furaha kubwa.
◻ Ukweli kuhusu Ufalme wa Mungu huleta uhuru wa kutoka kwenye utumwa wa dini bandia. Waweza pia kubadili utu wa mtu, na mara nyingi badiliko hili huvutia wengine na kuwasaidia wao wauone ukweli, kama linavyoonyesha ono lifuatalo.
Mwanamke kijana alipiga hodi kwenye mlango wa nyumba ya Shahidi mmoja na kuomba funzo la Biblia. Ilikuwaje hata akafanya hivyo? Wazazi wa mwanamke huyo walikuwa wakijifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova, na tokeo la funzo hilo juu ya wazazi wake—hasa baba yake —lilikuwa la kutazamisha na kuvutia sana hata binti huyo akastaajabu kweli kweli. Baba yake, aliyekuwa amekuwa akivuta sigareti 80 kwa siku, aliacha kabisa kuvuta alipoelezwa kwamba Yehova hakukubalia jambo hili. Ilikuwa ni karibu mara tu baada ya hapo kwamba aliwarudishia waajiri wake akiba nzima ya bidhaa alizokuwa ameiba kwao kwa kipindi fulani. Binti huyo alihisi kwamba ni lazima apeleleze kitu chochote hicho ambacho kingeweza kuathiri wazazi wake kwa njia hiyo. Sasa wazazi wamebatizwa, na binti huyo anahudhuria mikutano yote.
Ukweli ambao Yesu alipigia mbiu uliwaletea furaha wale waliotangulia kutajwa, na wengine wasiohesabika. Inaweza kufanya ivyo hivyo kwa wowote wenye kukubali ukweli wa Biblia na kuutumia katika maisha zao.—Zaburi 19:7, 8.