Sasa Mwisho wa Uhalifu Uko Karibu!
WAPELELEZI hutafuta kutatua vitendo vya uhalifu kwa kuchunguza vidokezo vyenye kufunua utambulishi na makusudio ya wenye kuvitenda. Njia na mbinu stadi zitumiwazo na mpelelezi huzungumzwa na riwaya zipendezwazo sana ulimwenguni pote. Ingawa huenda hatimaye yeye akafanikiwa kumpata mhalifu, kwa ujumla kazi ya mpelelezi huanza baada ya tukio lenyewe, baada ya uhalifu ule kuwa umetendwa.
Kama iwezavyo kuonwa na ongezeko la uhalifu, kwa kila mhalifu mwenye kunaswa, kuna wengine wengi ambao hugeukia uhalifu. Kwa hiyo ili kukomesha kabisa uhalifu, mengi zaidi yahitajiwa kuliko kutatua makosa yale tu yaliyokwisha kufanywa. Ni nini kitakachozuia watu wasiwe wahalifu?
Uhalifu wahusiana na maadili. Hatuwi na ugumu wowote kukubali kwamba kuua, kunajisi, na vitendo vingine vya jeuri ni uhalifu. Lakini namna gani kudanganya wakati wa kujaza mambo ya kodi? Kitendo cha jinsi hiyo ni cha uhalifu pia, kwa maana ni kinyume cha viwango vya kiadili vya ufuataji haki. Kumaliza uhalifu kikamili kwapasa kumaanishe kufutilia mbali vitendo vyote vilivyo kinyume cha maadili yale ya msingi.
Fikiria vielelezo vitatu vya Biblia ambavyo zaidi ya kukazia kisababishi cha uhalifu vyakazia pia jinsi utakavyokomeshwa kabisa.
Hofu ya Kimungu Dhidi ya Husuda
Tafadhali angalia maneno ya mtunga zaburi Asafu: “Naliwaonea wivu [husuda, NW] wenye kujivuna, nilipoiona hali ya amani ya wasio haki.” (Zaburi 73:3) Ndiyo, kuhusudu ufanisi na mtindo-maisha wa mhalifu hushawishi wengi wajifuatishe njia za kutotii sheria. Kuufanya uhalifu uvutie sana katika televisheni na magazeti huufanya ukubalike zaidi badala ya kuchochea chuki ya lililo baya.
Hata hivyo, mwandikaji aliyevuviwa wa Mithali ahimiza hivi: “Moyo wako usiwahusudu wenye dhambi; bali mche BWANA [Yehova, NW] mchana kutwa.” Kusudio na tamaa ya mtu ndiyo mambo hasa yaliyo mzizi wa tatizo lenyewe. Njia yenye matokeo zaidi ya kuyazuia ni kusitawisha hofu ya kimungu ya kuepuka kutomfurahisha Yehova Mungu. “Maana bila shaka iko thawabu; na tumaini lako halitabatilika.”—Mithali 23:17, 18.
Imani Dhidi ya Pupa
Katika masika ya 33 W.K., Yesu alikuwa anasafiri kupitia mji wa Yeriko. Huo ulikuwa ndio mji wa nyumbani kwao Zakayo, ambaye Luka mwandikaji wa Gospeli amweleza kuwa ni “mkubwa mmoja katika watoza ushuru [kodi, NW],” akiongeza kwamba alikuwa “tajiri.” Wilaya yenye rutuba iliyozunguka Yeriko ilikuwa eneo kuu la ukusanyaji-kodi, na kama ionyeshwavyo na maneno ya Zakayo mwenyewe, utendaji wake akiwa mkubwa mmoja kati ya wakusanya-kodi ulimwandalia fursa za kufanya unyakuzi. Lakini Zakayo hakubaki akiwa mhalifu.—Luka 19:1-8.
Yeye alipiga mbio kuutangulia umati uliokusanyika kumzunguka Yesu na kwa sababu ya kimo chake kidogo akatafuta mahali palipomfaa kwa kupanda juu ya mkuyu-mforsadi. Yesu alimwona na kumwambia Zakayo ashuke, kwa maana Yeye angekaa naye muda ambao angekuwa Yeriko. Baadaye, maneno ya Zakayo yalipiga mbiu kwamba alikuwa na mwelekeo uliobadilika: “Nusu ya mali yangu nawapa maskini, na ikiwa nimenyang’anya mtu kitu kwa hila namrudishia mara nne.” Kurudisha pesa hizo zilizonyakuliwa kungehusisha gharama kubwa. Kwa kuahidi kufanya hivi, Zakayo alipiga mbiu kwamba alikuwa mwenye imani katika Yesu. Ndiyo, maoni yake yaliyobadilika yalileta tokeo lenye kuonekana, mrudisho wa kile alichokuwa amechukua kiharamu kuongezea mara tatu nyingine za thamani hiyo, ikifanya rudisho hilo liwe la mara nne. Hivyo Zakayo alirekebisha kosa alilokuwa amefanya na akazidi hapo, akithibitisha kwamba alibadili njia yake ya maisha kwa moyo mweupe.—2 Wakorintho 7:11.
Watu Ni wa Maana Kuliko Mali
Gavana Mroma Pilato alisema hivi juu ya Yesu Kristo mshtakiwa: “Sioni neno lililo ovu katika mtu huyu.” (Luka 23:4) Badala ya kugeukia mwenendo wa uhalifu ili apate mali, katika muda wote wa huduma yake ya kidunia, Yesu alionyesha upendezi wenye upendo katika watu. “Alipowaona makutano, aliwahurumia, kwa sababu walikuwa wamechoka na kutawanyika kama kondoo wasio na mchungaji. Ndipo alipowaambia wanafunzi wake, Mavuno ni mengi, lakini watenda kazi ni wachache. Basi mwombeni Bwana wa mavuno, apeleke watenda kazi katika mavuno yake.” (Mathayo 9:36-38) Kwa uwazi, Yesu alitanguliza watu mbele ya mali, hata mbele ya faraja na mapendezi yake mwenyewe. Twaona hilo pia kutokana na nia yake ya kujitoa sana ili kuwatunza wanafunzi na umati uliomtafuta-tafuta ili awape maagizo na msaada. (Mathayo 8:20; 14:13-16) Katika jambo hili, Yesu alituachia kiolezo tukifuate.—1 Petro 2:21.
Je! leo yawezekana watu wafuate kielelezo hicho, kuwachukua wanadamu wenzao kuwa wenye thamani kuliko bidhaa za kimwili? Twaweza kujibu ndiyo. Fikiria Mashahidi wa Yehova, ambao sasa ni zaidi ya milioni tatu na robo. Wao hutafuta kuwa na akili ya Kristo na kuonyesha jambo hilo kimatendo. Daima wao hujitahidi kuondoa kabisa katika mioyo yao zile tamaa mbovu ambazo huwaongoza watu wengine wengi kwenye uhalifu. Kabla ya kuwa Mashahidi, walipokuwa wakijifunza Biblia na kukuza upendo kwa Mungu, kufanya hivyo kuliwagusa baadhi yao waliokuwa wamekuwa ni wahalifu; kulisukuma hesabu fulani kati yao wafanye marudishio kwa ajili ya vitendo vya uhalifu walivyokuwa wametenda. Hapana, wao hawakufanya hivyo ili watangazwe sana mbele ya watu bali ili wawe na mahusiano yenye amani pamoja na Yehova Mungu na hivyo wanufaike na fadhili zisizostahiliwa zake kama zilivyoonyeshwa kupitia dhabihu ya ukombozi ya Yesu Kristo.—1 Wakorintho 2:16; 6:11; 2 Wakorintho 5:18-20.
Kwa kuwapenda jirani zao, Wakristo hao wanatumia wakati kuzuru watu wengine na kuwaeleza jinsi jamaa hizo zaweza kutazama mbele kwenye uhai katika hali za Paradiso chini ya Ufalme wa Mungu. Kila juma Mashahidi wa Yehova hufanya mikutano ya ukawaida kwenye Majumba ya Ufalme yao. Mwizi mmoja aliyejiungama mwenyewe alikubali mwaliko wa kuhudhuria ili aone mikutano hiyo ikoje. Yeye asimulia hivi: “Kwa uchache, mimi nilishangaa sana. Mambo hayakukosa upendezi wala kuchosha kama nilivyokuwa nimetazamia. Ni wazi kwamba uchangamfu na upendo, ulioonekana sana, ulikuwa wa kweli. Na uthamini ambao Mashahidi wote walionekana kuwa nao kwa ajili ya mambo ya kiroho ulikuwa wa kutokeza. Yeye alivutiwa sana hata akaendelea kufanya ushirika, na hiyo ikamsaidia kujirekebisha. Kama wewe umehusika au hujahusika katika uhalifu, ushirikianapo na watumishi wa Mungu, wewe pia utapata kupendezwa kikweli hivyo na watu badala ya kupendezwa na mali.—Mathayo 22:39.
Uhalifu—Je! Tayari Umekomeshwa Kabisa?
Ikiwa watu hawatendi tena wakiwa wahalifu, je! hii yamaanisha kwamba wao ni wakamilifu? Sivyo kabisa. Mashahidi wa Yehova, kama mtu mwingine yeyote, huteswa na dhambi iliyorithiwa kutokana na mzazi wetu wa kwanza wa kibinadamu, Adamu. (Warumi 5:12; 1 Yohana 1:8) Lakini sasa wao wameungamana katika kutumikia Mungu, kama ionyeshwavyo katika kazi yao ya kuhuburi na kufundisha ulimwenguni pote. Hii yatoa ushahidi wenye nguvu juu ya kutimizwa kwa unabii wa Isaya: “Itakuwa katika siku za mwisho, mlima wa nyumba ya Bwana [Yehova, utawekwa imara juu ya milima, . . . na mataifa yote watauendea makundi makundi.” (Isaya 2:2) Kweli kweli, mamilioni wanamiminika kwenye ibada ya Yehova iliyokwezwa, wakitafuta kuagizwa katika njia zake. Wewe waweza kuwa mmoja wa wale ambao wanufaika kwa kushirikiana na watu ambao waepuka uhalifu.
Kukomeshwa Kabisa kwa Uhalifu—Matazamio Yaliyopo
Kwa kweli utendaji ulioongezeka wa kufanya uhalifu siku yetu ni dalili ya kukaribia kwa hatua ya kimungu ya kuingilia mambo ili kuondoa waovu wote, kutia na wahalifu wote. “Maana watenda mabaya wataharibiwa . . . Maana bado kitambo kidogo asiye haki hatakuwapo, utapaangalia mahali pake wala hatakuwapo.” (Zaburi 37:9, 10) Sasa mwisho wa uhalifu uko karibu kweli kweli, kwa maana tunaukaribia wakati ambapo yule mhalifu wa awali, Shetani Ibilisi, atafungwa na kutiwa katika abiso. (Ufunuo 20:1-3, NW) Lapasa liwe jambo la kusisimua kama nini kujua kwamba karibuni kuhofu uhalifu na umivu lenye kuumiza watu yatakuwa mambo ya zamani!
Hata hivyo, namna gani mamilioni ya watu ambao watafufuliwa warudi kwenye uhai duniani? (Matendo 24:15) Wakiendelea na utu na njia zile zile walizokuwa nazo kabla ya kufa kwao, je! hawatafyatua wimbi jipya la uhalifu? Hakuna uhitaji wa kuhofu hivyo. Yesu alimwahidi mwizi mmoja ufufuo, akisema hivi: “Mimi nakuambia wewe leo, Wewe utakuwa pamoja na mimi katika Paradiso.” (Luka 23:43, NW) Kwa uhakika hii yaonyesha kwamba wafufuliwa watapaswa kufanya mabadiliko; ama sivyo ulimwengu mpya haungekuwa paradiso.
Sawa na vile wahalifu wagumu wahitajivyo kurudishwa upya kabla ya kuweza kulowea katika jumuiya bila kufanyiza matatizo, ndivyo chini ya Ufalme wa Mungu programu pana sana ya kielimu itakavyosaidia raia wawe washika-sheria. (Ufunuo 20:12, 13) Wakiwa na faida ya wazi ya kuwa wamezungukwa na wakaaji wa Paradiso, ambao wanatii sheria za Mungu, wafufuliwa watapata hali zenye kurekebiwa vizuri kiuchumi. (Isaya 65:21-23) Watawekwa watawala wenye haki, na watu wowote wenye kuendelea tu kufanya makosa wataondolewa waache kuwa hai. (Isaya 32:1; 65:20) Kwa hiyo kuna sababu tele ya kutegemea kwamba, mwishowe, uhalifu utakwisha.
Ingawa tungali twaishi katikati ya ulimwengu wenye uhalifu, wewe waweza kuonyesha kwa uhakika tegemeo katika Yehova, ambaye aahidi kuthawabisha watumishi wake waaminifu kwa uhai mkamilifu katika Paradiso. Fanya hivyo sasa kwa kujifaidi na mpango wa funzo la Biblia la nyumbani lisilo la malipo ambalo hutolewa na Mashahidi wa Yehova. (Yohana 17:3) Wakati ule mwingine ukutanapo nao, kwa nini usiwaombe wakueleze mengi zaidi? Au waweza kuandikia anwani iliyo karibu zaidi na wewe katika ukurasa wa 2 wa gazeti hili. Kwa uhakika yastahiki kujitahidi, kwa maana tazamio zuri sana lililopo ni kwamba sasa mwisho wa uhalifu uko karibu!
[Picha katika ukurasa wa 5]
Imani ya Zakayo ilimsukuma arudishe alivyokuwa amenyakua
[Picha katika ukurasa wa 7]
Programu ya kielimu itawafundisha raia za Ufalme wa Mungu wawe wenye kutii sheria