Wewe Unataka Uhalifu Umalizwe?
WATU wote wanaoheshimika watajibu ulizo hilo kwa kusema NDIYO. Wanataka kuona uhalifu (uvunjaji sheria) ukimalizwa.
Wazee fulani waliooana wa jiji moja la Amerika walitaka kuona uhalifu ukimalizwa. Walikuwa wakikaribia umri wa miaka 80, walikuwa wameacha kufanya kazi na walikuwa na mali za kuwatosha. Ndipo walipojiua!
Kwa sababu gani? Kibarua walichoandika kabla ya hapo kilieleza hivi: “Sisi hatutaki tena kuishi tukiwa na woga.” Walikuwa wameshambuliwa na kunyang’anywa mali juma chache kabla ya hapo. Tena kabla ya tukio hilo, walikuwa wametendwa uhalifu. Waliona walikuwa wazee mno wasiweze kuhama, kwa hiyo wakajiua kwa sababu hawakutaka kuishi wakiwa na woga.
Ni kweli kwamba walitenda tendo la kupita kiasi kwa sababu ya kuogopa uhalifu. Lakini tendo lao linaonyesha mambo ambayo yametukia miaka ya karibuni. Uhalifu na jeuri zimeongezeka sana karibu kila mahali ulimwenguni. Kwa mfano, katika United States matendo makubwa ya uhalifu zaidi ya milioni kumi na moja yanatendwa kila mwaka. Mamilioni mengine ya matendo hayo hayaripotiwi.
Ni jambo gani linaloweza kumaliza mambo hayo? Watu wengine wanaona kwamba mambo yatakuwa mazuri zaidi kukiwa na sheria nzuri zaidi. Lakini, yako maelfu ya sheria nzuri katika vitabu yako maelfu ya sheria nzuri katika vitabu vya nchi zote, tena sheria mpya zinaanza kutumiwa kila mwaka. Na bado uhalifu na jeuri zinaendelea kuenea.
Watu wengine wanaona kwamba mambo hayo yatamalizika kukiwa na mapolisi wengi zaidi, mahakimu wengi zaidi na magereza mengi zaidi. Ingawa watu hao na magereza hayo yameongezeka, uhalifu pia umeongezeka. Kwa kweli, uhalifu umefanywa na watu ao hao, hata magerezani. Mara nyingi maafisa wafisadi wanafanya iwe vigumu kwa wakuu wengine kuhakikisha kwamba sheria zinafuatwa.
Je! njia mpya za kupeleleza uhalifu zinaweza kumaliza mambo hayo? Jambo linalosikitisha ni kwamba, njia mpya ya kumaliza uhalifu ikianzwa, wahalifu nao wanaanza kutayarisha njia zao wenyewe za kuiweza.
Je! uhalifu utamalizwa umaskini ukimalizwa? Kama umaskini hasa ndio unaoleta uhalifu, kwa sababu gani matendo mengi zaidi ya uhalifu yanapatikana katika mataifa yaliyo tajiri? Kwa kawaida uhalifu unaongezeka upesi zaidi katika maeneo ya matajiri kuliko unavyoongezeka katika miji ya maskini. Watu wenye vyeo vya namna zote wanafanya matendo ya uhalifu, si maskini peke yao.
Ebu fikiri hivi: Kama wanadamu wangalikuwa na uwezo wa kumaliza uhalifu, je! sasa wasingalikuwa wamekwisha umaliza? Je! inafaa kweli kutazamia wanadamu wamalize uhalifu?
Kwa hekima Neno lililoongozwa na Mungu, Biblia, linatushauri hivi: “Msiwatumainie wakuu, wala binadamu ambaye hakuna wokovu kwake.” (Zab. 146:3) Basi tutatumaini nani? Neno ilo hilo la Mungu linajibu hivi: “Mtumaini [Yehova] kwa moyo wako wote, wala usizitegemee akili zako mwenyewe.”—Mit. 3:5.
Lakini kumtumaini Mungu kutamalizaje uhalifu? Kwanza, Neno la Mungu linatufahamisha waziwazi sababu gani uhalifu na jeuri zinaongezeka sana wakati wetu. Biblia inatuambia: “Lakini ufahamu neno hili, ya kuwa siku za mwisho kutakuwako nyakati za hatari.” Naam, mambo yote tunayoona yakitimiza unabii wa Biblia yanaonyesha kwamba tunaishi katika mwisho wa kipindi fulani. Tunaishi katika wakati uliotabiriwa kwamba watu zaidi na zaidi wangekuwa wavunja sheria, wasiojiweza, wakali sana, wenye vichwa vigumu, wapenda pesa, wasiotaka mambo ya Mungu, wakati ambao watoto wasingetii wazazi, wakati unaosemwa na unabii kwamba, “watu wabaya na wadanganyaji wataendelea, na kuzidi kuwa waovu.”—2 Tim. 3:1-13.
Mambo tunayoona yakitukia wakati wetu yanaonyesha wazi kwamba ulimwengu huu umo katika kipindi chenye uharibifu wa tabia njema kilichotabiriwa kwamba kingetokea muda mfupi tu kabla ulimwengu wenyewe haujamalizika. Hali za ulimwengu zinaonyesha waziwazi kabisa kwamba taratibu ya mambo iliyopo inakaribia kikomo chake.
Lakini, Biblia inatuambia kwamba wanadamu sio peke yao wanaoongeza uhalifu. Kama wanadamu peke yao ndio wanaohusika, wangalikuwa wameweza kumaliza uhalifu. Lakini Neno la Mungu linatuambia kwamba watu fulani wanaomzidi mwanadamu nguvu wanafanya kazi. Watu gani? Shetani Ibilisi na mashetani wake.
Ibilisi? Mashetani ati? Ni kweli kwamba watu wengi hawaamini kuna mashetani, kwa sababu hawawezi kuonekana. Lakini wanaamini kwamba kuna nguvu zisizoonekana kama upepo, umeme, nguvu za uvutano, joto, baridi, upendo, chuki. Tunajua kwamba mambo hayo yako kwa sababu tunaweza kuona matokeo yao.
Basi, tunajua kwamba mashetani wako kwa sababu tunaona matokeo ya kazi yao. Uhalifu na jeuri zimeongezeka sana kila mahali kwa sababu wanaongoza jamaa ya kibinadamu vibaya. Maongozi yao ni mengi sana hivi kwamba Biblia inamwita Shetani “mungu wa dunia hii.”—2 Kor. 4:4.
Tena, ni nani anayefaa zaidi kutueleza habari za kuwako kwa wakuu hao wasioonekana? Ni nani anayejua habari nyingi zaidi juu ya kazi ya Shetani—wanadamu, au Muumba ulimwengu, Mwenye Nguvu Zote?
Lakini kwa sababu gani maongozi ya mashetani yameongezeka sana siku zetu? Ni kwa sababu muda ambao Mungu ameruhusu uovu uwepo unakaribia kumalizika. Shetani na mashetani wake wanajua kwamba wamo katika ‘siku zao za mwisho.’ Ndiyo sababu Biblia inasema yafuatayo juu ya kizazi chetu: “Ole wa nchi na bahari! kwa maana yule Ibilisi ameshuka kwenu mwenye ghadhabu nyingi, akijua ya kuwa ana wakati mchache tu.”—Ufu. 12:12.
Lakini, Biblia haituelezi sababu tu ya uhalifu kuenea. Inatueleza pia jinsi utakavyomalizwa. Karibuni muda ambao Mungu ameruhusu uovu uwepo utakwisha, naye ataonyesha ana uwezo na anapenda mambo ya haki kwa kuondoa uhalifu katika dunia nzima. “Waovu watatengwa na nchi, nao wafanyao hila watang’olewa.” Mchochezi mkuu wa uhalifu, yaani, Shetani Ibilisi, ataondolewa pia: “Mungu wa amani atamseta Shetani chini ya miguu yenu upesi.”—Mit. 2:22; Rum. 16:20.
Baada ya wahalifu wote kuondolewa, taratibu mpya yenye kujawa na amani na usalama italetwa. Halafu maisha yatakuwaje? “Wataketi kila mtu chini ya mzabibu wake, na chini ya mtini wake; wala hapana mtu atakayewatia hofu,” yasema ahadi ya Mungu.—Mik. 4:4.
Basi, wewe unataka uhalifu umalizwe? Utamalizwa kwa njia ya Mungu, tena karibuni. Unataka kupata faida? Basi inakupasa ujue jinsi ya kutimiza matakwa ya Mungu uweze kuishi katika taratibu yake mpya inayokuja, ambayo haitakuwa na uhalifu.
[Blabu katika ukurasa wa 12]
“Watu wangu watakaa katika kao la amani; na katika maskani zilizo salama, na katika mahali pa kupumzikia penye utulivu.”—Isa. 32:18.