Desturi za Ngono Zenye Kuchukiza za Kale na za Ki-Siku-Hizi
IBADA ya Moleki mmojapo miungu ya Wamoabu ilikuwa yenye kutia karaha jinsi gani? Paolo Mantegazza anaandika katika kitabu chake The Sexual Relations of Mankind (Ngono za Aina ya Binadamu) kwamba Wamoabu wa nyakati za Biblia walifanya vitendo vibaya vya ngono “katika korasi, walipokuwa wakicheza dansi kuzunguka sanamuumbo ya Moloki yenye kung’aa kwa moto mwingi, baada ya vile vinywa saba vya shaba vya mungu yule kunyafua matoleo ya waaminifu, matoleo yaliyotia ndani unga, hua-turturi, aina za mwana-kondoo, kondoo dume, ndama, ng’ombe dume, na vivulana wadogo.” Yeye anaongezea hivi: “Yeyote ambaye amesoma Biblia lazima akumbuke laana mbaya sana ambazo Musa aliwatolea wale Waebrania waliofanya uasherati na Moloki. Baali-Fegori pia, au Bel-fegori [Baali wa Peori], ambaye ndiye mwenye uungu aliyependwa sana na Wamidiani, alipokewa na Wayahudi kwa idili yenye kupita kiasi, na kidhehebu chake kilikuwa kibaya sana kama vile kawaida za ibada ya Moloki.”—Walawi 18:21; New World Translation Reference Bible, maelezo ya chini; 20:2-5; Hesabu 25:1-5; Yeremia 32:35.
“Idili yenye kupita kiasi” ya Wayahudi hao ina ulinganifu leo katika “adili mpya” ambayo ilitokea, hasa katika United States na mabara mengine ya Jumuiya ya Wakristo, katika miaka ya 1960.
Katika kukadiria athari ya muda mrefu ya mabadiliko makubwa ya kufanya ngono, Madakt. Alexandra na Vernon H. Mark, watungaji-wenzi wa kitabu The Pied Pipers of Sex, walitoa maoni yao katika sehemu ya “Kusema Wazi” katika Medical World News, Houston, Texas, U.S.A. Katika 1985 waliandika hivi:
“Kwa muda wa miaka 25 iliyopita, jamii ya watu imeshuhudia badiliko lenye kutazamisha katika desturi za ngono. . . . Kugeuza huku kwa adili ya kitamaduni kumeitwa mabadiliko makubwa ya kufanya ngono.” Baada ya kuwataja majina maprofeshenali wa kitiba wanaohusika katika badiliko hili la mitazamo inayohusu ngono, waandikaji walijulisha wazi hivi: “Kwa kukadiria wachangaji wao mmoja mmoja, [wanatiba hawa] wamefanyiza matokeo makubwa ajabu juu ya jamii ya watu na mashirika yayo. Badala ya sisi kuwa na deni la kuwashukuru waelekezaji hawa wa mambo ya ngono, tunahitaji kupunguza uvutano wao kwa kuendeleza msimamo timamu na uliosawazika kuhusiana na mazoea ya ngono na ulinzi wa afya ya watu wote.
“Kuuruhusu utendaji kamili wa yale mabadiliko makubwa ya kufanya ngono bado hakujatokeza manufaa yoyote ya kadiri kwa nchi nzima—isipokuwa kama tunafikiria manufaa ya pato la kifedha ambalo kumetokeza. Lakini kwa kukazia kwayo ngono kuwa tafrija na mchezo wa kutazamwa, hayo mabadiliko makubwa yametokeza matatizo mengi ambayo yanatisha kutuletea chafuko la kijamii—moja likiwa ugonjwa unaotokana na uasherati. Ugonjwa unaotokana na uasherati si pigo jipya, lakini sasa umekuwa tauni, ukitokeza aina mpya ya bakteria ngeni na vitu vinavyofanana na virasi. Ugonjwa wa vilengelenge vya viungo vya uzazi ambao hauponi, katika watu wazima, umesababisha vifo vya vitoto vichanga kutokana na meningoencephalitis (uvimbe unaowasha katika bongo na ngozi inayofunika ubongo). UKIMWI. . . umeweza kuingia katika sehemu kubwa ya jamii yetu na katika mishipa ya damu ya majeruhi wasio na hatia kupitia damu iliyochangwa ikiwa na maambukizo.”
Waandikaji hawa wanafikia mkataa huu: “Ushuhuda unaoongezeka ukiwashtaki viongozi wa mapinduzi ya ngono ni wa ajabu. Wao waliahidi kupata shangwe, ukombozi, na afya njema. Wameleta taabu, magonjwa, na hata kifo.” Biblia inaonyesha wazi msimamo wa viongozi hao. Kwa kielelezo, 1 Wakorintho 6:9, 10 inataarifu hivi: “Au hamjui ya kuwa wadhalimu hawataurithi ufalme wa Mungu? Msidanganyike; waasherati hawataurithi ufalme wa Mungu, wala waabudu sanamu, wala wazinzi, wala wafiraji, wala walawiti.”—Ona pia Yuda 7.