Wapiga Mbiu ya Ufalme Waripoti
‘Kuwaka Roho’ Katika Meksiko
“NCHI nzima yaonekana kuwa imewaka na kuvuma sana kwa utendaji mwingi.” Ndivyo iandikavyo ofisi ya tawi ya Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi katika Meksiko, nalo elezo hilo ni la kweli kama nini! Utendaji wenye kuvuma sana katika bara hilo washuhudizwa na jambo la kwamba kufikia Agosti, kulikuwa kumekuwako vilele 70 mfululizo mwezi baada ya mwezi, vikifikia kiwango cha juu zaidi cha wahubiri 277,436. Kwa kuongezea, mafunzo ya Biblia zaidi ya 400,000 yaliripotiwa, na hudhurio la Ukumbusho mwaka uliopita likafika 1,046,291. Ni msingi mzuri kama nini wa ukuzi wakati ujao!
Jambo kubwa la 1989 lilikuwa badiliko katika hali ya kutambuliwa kwa Mashahidi wa Yehova katika Meksiko. Tokeo ni kwamba, Biblia ingeweza kutumiwa katika kazi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba kwa mara ya kwanza, na mikutano ingeweza kufunguliwa kwa sala. Jambo hili lilipata matokeo mara hiyo. Katika muda wa miezi miwili, hesabu ya wahubiri iliruka kwa zaidi ya 17,000.
Shangwe ya akina ndugu kuhusu tukio hili yaonekana katika maelezo yao. Mmoja aliandika hivi: “Barua hiyo iliposomwa katika kundi, ilikatizwa mara mbili na makofi ya kujitolea. Lilikuwa jambo la kusisimua!” Mwingine alisema hivi: “Hatungeweza kuzuia machozi ya shangwe. Matokeo yamedhihirishwa na maendeleo ya kufika bila kuchelewa. Kila mmoja hutaka awepo kwa ajili ya sala ya kufungua.”
“Katika eneo letu,” akasema Shahidi mwingine, “mwanamke ambaye ni mtendaji katika programu ya funzo la Biblia la Kanisa Katoliki alieleza hivi: ‘Ikiwa [Mashahidi] walituduwaza kwa maelezo yao na magazeti yao tu, sasa kwa vile wao wanafungua Biblia kwenye milango, hatujui tutafanya nini!’”
Mashahidi wa Yehova katika Meksiko hukazia pia kutoa ushahidi wa vivi hivi kwa kutumia Biblia. Dada mmoja alifikia mwanamke na kuulizwa naye ana maoni gani kuhusu utoaji mimba. Shahidi alijibu hivi: “Maoni yangu si ya maana kama yale yasemwayo na Biblia.” Baada ya kusoma maandiko kadhaa, dada akasababu hivi: “Uhai ni wa maana sana kwa Muumba, hata uhai wa wale ambao hawajazaliwa bado.”
Ndipo bibi huyo akakiri kwamba alikuwa akitarajia kupata kitoto chake cha kwanza, lakini uchunguzi mbalimbali wa kikliniki ulidokeza kwamba kitoto hicho kingekuwa cha hali isiyo ya kikawaida. Daktari wa mwanamke huyo alimtaka atoe mimba, na mume wake akakubali, lakini bibi mwenyewe hakuwa na uhakika. Mhubiri huyo alizidi kusababu mambo pamoja naye kutokana na Biblia, akampa jina lake, kisha wakaachana.
Miaka mitano baadaye kwenye mkusanyiko wa wilaya, mume na mke wenye mtoto wa miaka minne walitaka kuona dada yule na mume wake. Alikuwa ni mwanamke yule yule! Ilikuwa imekuwaje? Baada ya maongeo yake pamoja na Shahidi yule, mwanamke huyo aliamua kumzaa mtoto wake. Daktari wake alikataa kumwona tena, na mume wake hata akatisha kumwacha ikiwa mtoto huyo angezaliwa akiwa ameumbuka mwili. Wakati wake wa kuzaa ulipofika, yeye alienda kutafuta msaada kwa daktari yeyote yule ambaye angeweza kumpata kwanza.
Mara tu baada ya mtoto yule kuzaliwa, daktari alisema hivi: “Pongezi, mama! Una kisichana cha kupendeza.” Kwa kutoamini aliyosikia, akamwomba daktari achunguze mtoto huyo kwa uangalifu. Halafu mwanamke huyo akamsimulia daktari hadithi yake. Daktari huyo hakuwa na mengi ila kusema kwamba: “Huu ni muujiza.” Mwanamke yule akafurahi sana kwamba yeye alikuwa amekuwa na moyo mkuu wa kustahi maoni ya Yehova kuhusu utakato wa uhai, naye akampa mtoto wake mzuri na mwenye afya jina la dada yule. Mara tu alipokwisha kuwa na imara ya kutosha, aliwatafuta Mashahidi na kuanza kujifunza Biblia pamoja nao. Katika muda wa chini ya mwaka mmoja, yeye na mume wake walibatizwa.
Mtume Paulo alihimiza hivi: “Wakeni roho. Mwe watumwa kwa ajili ya Yehova.” (Warumi 12:11, NW) Mashahidi wa Yehova katika Meksiko, kama Wakristo wa kweli kila mahali, huitikia himizo hilo kwa moyo wao wote. Ndiyo sababu nchi nzima imewaka na inavuma sana utendaji wa kiroho. Yehova huwabariki sana watu wake wenye imani!