Wapiga-Mbiu wa Ufalme Waripoti
“Neno la Mungu Likaenea”
KUTANIKO la Kikristo lilikua upesi sana kutoka washiriki 120 hivi hadi zaidi ya 3,000 baada ya kufanyizwa kwalo. (Matendo 1:15; 2:41) Biblia hueleza kwamba “neno la Mungu likaenea; na hesabu ya wanafunzi ikazidi sana katika Yerusalemu.” (Matendo 6:7) Baada ya miaka michache tu, hilo kutaniko lililofanyizwa karibuni likawa tengenezo lililoenea hadi mabara mengineyo kukiwa na Wakristo katika Afrika, Asia, na Ulaya.
Kutaniko la Kikristo leo vilevile linakua upesi. Mathalani, katika Mexico, idadi ya wapiga-mbiu wa Ufalme imekua kwa zaidi ya 130,000 hadi 443,640 katika muda wa miaka mitano pekee! Katika 1995 mtu 1 kati ya watu 59 katika Mexico alihudhuria Ukumbusho wa kifo cha Kristo kama vile unavyoadhimishwa na Mashahidi wa Yehova. Hata hivyo, mavuno ya kiroho hayajaisha katika nchi hiyo, kama ionyeshwavyo na ono lifuatalo.—Mathayo 9:37, 38.
Katika mji mmoja wa jimbo la Chiapas, hakuna mtu aliyekuwa amekubali funzo la Biblia nyumbani pamoja na Mashahidi wa Yehova, hata baada ya wao kuwa wamehubiri habari njema katika eneo hilo kwa miaka ipatayo 20. Kwa wazi watu wengi wa mji huo walitishwa na mtu fulani aliyekuwa na sifa mbaya ya kuwa mjeuri. Wao walihofu itikio lake ikiwa angaligundua kwamba walikuwa wakijifunza Biblia pamoja na Mashahidi.
Mashahidi wawili wenye moyo mkuu waliohamia eneo hilo waliamua kushughulikia tatizo hilo kwa kwenda moja kwa moja kwa mwanamume huyo. Walipowasili nyumbani kwake, mke wake alifungua mlango na kusikiliza kwa makini ujumbe wao. Yeye alipendezwa hasa na kile ambacho Biblia husema kuhusu kuishi katika paradiso duniani. Lakini akakiri kwamba mume wake angefanya mambo yawe magumu sana kwake ikiwa angejifunza Biblia. Hao Mashahidi walieleza kwamba kama asingechunguza kwa uangalifu kile ambacho Biblia husema, yeye asingejifunza kamwe jinsi ya kumtumikia Mungu na kufurahia maisha duniani milele. Yeye akakubali funzo la Biblia.
Kama ilivyotazamiwa, mume wake hakupendezwa na uamuzi wake. Alimkataza mke asitumie gari lake ili kuhudhuria mikutano ya Kikristo, ingawa aliruhusiwa alitumie kwa mambo mengineyo. Ujapokuwa upinzani wa mume, yeye alitembea kwa ukawaida hadi Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova la karibu zaidi, lililokuwa umbali wa kilometa kumi. Upesi wengine mjini waliona moyo wake mkuu na azimio lake. Watu wakaanza kusikiliza wakati Mashahidi walipozuru nyumba zao. Wengine hata wakaanza kuandamana na huyo mwanamke kwenye mikutano. Baada ya wakati mfupi, wale Mashahidi walikuwa wakiongoza mafunzo 20 hivi ya Biblia katika mji huo!
Rafiki ya mwanamke huyo aliamua pia kujifunza Biblia ujapokuwa upinzani wa mume wake. Kwa kushangaza, yeye alitiwa moyo kufanya hivyo na mume wa yule mwanamke wa kwanza. Baada ya mume huyo kuongea na mume wake, upinzani uliisha. Kwa hiyo ikawa kwamba baada ya miaka 20 mbegu ya kweli ya Biblia ikachipuka hatimaye, kukiwa na watu zaidi ya 15 wakijifunza Biblia na kuhudhuria mikutano ya Kikristo, kutia na wale wanawake wawili, ambao sasa wanatangaza habari njema.y