Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w90 4/15 kur. 4-7
  • Amani ya Ulimwengu—Itamaanisha Nini Hasa?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Amani ya Ulimwengu—Itamaanisha Nini Hasa?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kumalizwa kwa Silaha—Njia ya Mungu!
  • Amani Nyumbani
  • Amani na Hali Njema Yako Binafsi
  • Amani ya Kweli—Kutoka Chanzo Gani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Jinsi Ambavyo Amani Yaweza Kupatikana Duniani
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Amani ya Kimungu kwa Wale Wanaofundishwa na Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
  • Acha “Amani Ya Mungu” Ilinde Moyo Wako
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
w90 4/15 kur. 4-7

Amani ya Ulimwengu—Itamaanisha Nini Hasa?

AMANI ya ulimwengu aliyo nayo Mungu akilini inatia ndani mengi zaidi ya kuacha mapigano katika tufe lote au hali ya kuogopa vita ya nyukilia. Hilo ni wazi kutokana na namna Biblia inatumia neno “amani.”

Kwa kielelezo, katika Maandiko ya Kiebrania (“Agano la Kale”) neno la amani ni sha.lohmʹ. Namna ya neno hili imetumiwa kwenye Mwanzo 37:14, NW ambapo mzee wa ukoo Yakobo anamwambia mwanae Yosefu hivi: “Ona kama ndugu zako ni salama na wenye afya na kama kundi la kondoo ni salama na lenye afya, urudi uniletee habari.”a Sha.lohmʹ limetumiwa tena kwenye Mwanzo 41:16, NW ambapo limetafsiriwa “hali njema.”

Kwa hiyo katika maana ya Kibiblia, amani ya kweli inatia ndani si kukomeshwa tu kwa uhasama bali pia afya, usalama, na hali njema. Toleo letu lililotangulia lilionyesha kwamba binadamu hawawezi kutatua tatizo la jinsi ya kuleta amani. Yesu Kristo tu, yule “Mwana-Mfalme wa Amani,” ndiye atasuluhisha mambo yote na kuleta amani ya kweli duniani. (Isaya 9:6, 7, NW) Fikiria, kwa kielelezo, unavyosema unabii wa Biblia kwenye Zaburi 72:7, 8 NW juu ya utawala wake: “Katika siku zake mwadilifu atachipuka, na wingi wa amani mpaka mwezi uwe haupo tena. Naye atakuwa na raia toka bahari mpaka bahari na toka Mto mpaka miisho ya dunia.” Ebu wazia—afya, usalama, hali njema kwa kadiri ya ulimwenguni pote! Hakuna patano la kisiasa lingeweza kutimiza hilo. Ni Ufalme wa Mungu tu unaweza, nao utatimiza hata zaidi. Biblia hutupatia miono midogo kadhaa yenye kusisimua ya kiunabii ndani ya amani hii ya ulimwengu ya wakati ujao. Acheni tufikirie baadhi yayo.

Kumalizwa kwa Silaha—Njia ya Mungu!

Zaburi 46:8, 9 husema: “Njoni myatazame matendo ya BWANA [Yehova, NW], jinsi alivyofanya ukiwa katika nchi. Avikomesha vita hata mwisho wa dunia; avunja uta, akata mkuki, achoma moto magari.” Maneno “uta,” “mkuki,” na ‘gari,’ ni kifananishi cha silaha ya vita au mashine zozote za vita. Hivyo Yehova anafika mbali zaidi ya kuwekea silaha mipaka au hata kumaliza silaha kabisa. Yeye anaondolea mbali kabisa silaha za nyukilia, mizinga, vifaru, virusha makombora, vikombora, vilipukaji vya plastiki, bunduki, bunduki za mkononi—chochote kinachoweza kutisha amani ya tufe lote.

Hata hivyo, silaha pekee hazisababishi vita. Kwa kawaida, chanzo cha vita ni ile asili isiyokamilika ya kibinadamu yenye chuki, pupa, au jeuri. (Linganisha Yakobo 4:1-3.) Kwa hiyo Ufalme wa Mungu utashambulia chanzo hiki cha vita kwa kuondoa sifa hizo za kiutu katika watu. Jinsi gani? Kwa njia ya programu ya elimu ya tufe lote. “Dunia itajawa na kumjua BWANA [Yehova, NW], kama vile maji yanavyoifunika bahari.”—Isaya 11:9.

Wakiwa ‘wamefundishwa na Yehova’ hivyo, ainabinadamu hawataona tena tofauti za rangi za kijamii kuwa msingi wa pambano, uhasama, au dharau. (Yohana 6:45) “Mungu hana upendeleo,” na wakaaji wa dunia wataonyesha sifa yake ya kutokuwa na upendeleo. (Matendo 10:34) Pia Ufalme utaondolea mbali uwezekano wowote wa pambano la kitaifa kwa kuondolea mbali mipaka ya kitaifa. ‘Toka bahari mpaka bahari na mpaka miisho ya dunia,’ wote wataapa utii wao wa moyo wa kupenda na wenye shukrani kwa utawala wa Kristo.—Zaburi 72:8, NW.

Ili amani hiyo idumu, Ufalme utaondolea mbali pia ile kani yenye kugawanya zaidi katika historia ya kibinadamu: dini bandia. (Sefania 2:11) Ainabinadamu wataunganishwa katika ibada yao ya yule Mungu mmoja tu wa kweli. (Isaya 2:2, 3) Udugu wa ulimwenguni pote utaimarika!

Amani Nyumbani

Hata hivyo, amani ya ulimwengu ingekuwa na thamani gani ikiwa makao ya faragha yangekuwa nyanja za vita ambako matukano, maneno yenye kuumiza, na vitisho vingekuwa vikirushwa huku na huku nyakati zote. Ndivyo ilivyo katika jamaa nyingi leo. Jamaa nyingine huficha uhasama ulioimarika sana nyuma ya kisetiri cha unyamavu usio na upendo.

Kwa hiyo amani ya kweli lazima itie ndani utulivu wa nyumbani. Chini ya programu ya elimu ya Ufalme, waume na wake watafundishwa kushugulikiana kwa upendo na staha. (Wakolosai 3:18, 19) Watoto watafundishwa ‘kuwatii wazazi wao katika kila jambo.’ (Wakolosai 3:20) Hakutakuwa na matineja waasi wa kutatiza na kusumbua wazazi wao. Utii utakuwa ndio kawaida, ushirikiano utakuwa ndiyo kanuni. Kuwa na watoto karibu kutapendeza na kuwaona kutaleta shangwe.

Leo, mibano ya kiuchumi huzidisha sana mikazo ya jamaa, kwa kuwa wazazi wote wawili wanawajibishwa kubeba mizigo mizito ya kazi ya kuajiriwa. Lakini chini ya utawala wa Kristo, jamaa zitaondolewa mizigo mizito yenye kulemea ya kifedha—kodi za nyumba zilizoongezwa sana, malipo makubwa mno ya amana, kodi zenye kuongezeka, ukosefu wa kazi za kuajiriwa. Kazi yenye kuridhisha, na kupendeza itakuwa tele. Wala hakuna atakayelazimika kuwa bila makao. Angalia jinsi unabii kwenye Isaya 65:21-23 unavyokazia mambo hayo ya hakika: “Nao watajenga nyumba, na kukaa ndani yake . . . Hawatajenga, akakaa mtu mwingine ndani yake; hawatapanda, akala, mtu mwingine. . . Wateule wangu wataifurahia kazi ya mikono yao muda wa siku nyingi. Hawatajitaabisha kwa kazi bure, wala hawatazaa kwa taabu; kwa sababu wao ni wazao wa hao waliobarikiwa na BWANA [Yehova, NW], na watoto wao pamoja nao.”

Ebu wazia ukiishi katika mazingira ambayo hayakushambulii kwa kuona, kusikia, minuko ya vitu vyenye kuoza mijini! Ebu wazia ukiishi juu ya shamba lenye rangi kijani-kibichi—shamba lako— lililolimwa vizuri kabisa, likatiwa mandhari nzuri, likatunzwa vizuri. Ebu wazia ukipumua hewa yenye kuburudisha kwa kuwa ni safi na kutakata; ukisikia, si ule mchanganyiko wa sauti zenye kuchukiza za ustaarabu wa ki-siku-hizi, bali sauti za kiasili zenye kuburudisha. Ni kweli, watu mmoja mmoja walio katika hali nzuri tayari wanaonea shangwe baadhi ya mambo haya. Lakini chini ya Ufalme wa Mungu, hali zenye amani za kuishi zitaonewa shangwe na wote. Hakutakuwako maskini, wenye njaa, wala wasiopendelewa.—Zaburi 72:13, 14, 16.

Biblia inaahidi zaidi kwamba “kwa habari ya waovu, watakatiliwa mbali.” (Mithali 2:22, NW) Hiyo yamaanisha kuondolewa kabisa kwa uhalifu. Mtoto wako aliye mdogo ku-pita wote akienda kucheza, hutahitaji kuwa na wasiwasi juu ya wasumbuaji watoto na wateka nyara wenye kuvizia gizani, magari yenye kwenda kasi huku na huku bila kudhibitiwa yakiendeshwa na madereva walevi, au magenge yenye kuzurura ya vijana waliotiwa kichaa na dawa za kulevya. Watoto wako watacheza pasipo hatari na kwa usalama kamili.

Amani na Hali Njema Yako Binafsi

Mwishowe, kuna ule upande wa hali njema ya kibinafsi. Hata hali za Paradiso hazipunguzi uchungu wa kansa au maumivu ya yabisi kavu. Kwa hiyo amani ya kweli lazima itie ndani kufutiliwa mbali kwa maradhi, ugonjwa, na kifo. Je! jambo kama hilo lawezekana? Alipokuwa duniani, Yesu Kristo alionyesha kwa kurudia-rudia uwezo wake juu ya udhaifu wa kibinadamu. (Mathayo 8:14-17) Kutoka mahali pake panapofaa pa kimbingu, Kristo ataweza kufanya miujiza duniani pote! “Ndipo [wakati huo, NW],” yaahidi Biblia, “macho ya vipofu yatafumbuliwa, na masikio ya viziwi yatazibuliwa. Ndipo mtu aliye kilema ataruka-ruka kama kulungu, na ulimi wake aliye bubu utaimba.”—Isaya 33:24; 35:5, 6.

Hata hivyo, kampeni ya Kristo dhidi ya mateso ya kibinadamu haitakomea hapo. Mtume Paulo anaeleza hivi kwa habari ya utawala wa Kristo: “Maana sharti amiliki yeye, hata awaweke maadui wake wote chini ya miguu yake. Adui wa mwisho atakayebatilishwa ni mauti.” (1 Wakorintho 15:25, 26) Hii inamaanisha kubatilisha uharibifu mwingi ulioletwa na kifo juu ya ainabinadamu tokea mwanzo wenyewe. Kama vile Yesu Kristo mwenyewe alivyoeleza: “Saa yaja, ambayo wote waliomo makaburini wataisikia sauti yake [Kristo]. Nao watatoka.” (Yohana 5:28, 29) Hivyo mamilioni yasiyohesabika ambao wameishi na kufa katika mateso watapata fursa ya kushiriki amani ya ulimwengu inayokuja.

Je! wewe utaishiriki? Mashahidi wa Yehova wanakuhimiza ujifunze zaidi juu ya yale yanayofundishwa na Biblia kwa habari hii.b Taraja la amani ya ulimwengu ni lenye kusisimua mno, ni halisi mno, lisiweze kupuuzwa. Uwe na uhakika kwamba ukijitahidi kujifunza na kutumia Neno la Mungu, ‘Mungu wa amani atakuwa pamoja nawe’—milele!—Wafilipi 4:9.

[Maelezo ya Chini]

a Kwa uhalisi, “Ona amani ya ndugu zako na amani ya kundi la kondoo.”

b Funzo la Biblia la nyumbani la bure laweza kupangwa kwa kuwaandikia watangazaji wa gazeti hili.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Yehova atakomesha vita “hata mwisho wa dunia”

[Hisani]

USAF Official Photo

[Picha katika ukurasa wa 6]

Waume na wake watafundishwa kushughulikiana kwa amani

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki