Vijana Ambao Watumikia Mungu
JE! WEWE waona si jambo la kawaida vijana wazuri kutoa wakati wao, bila malipo, ili waje kwenye mlango wako kuongea juu ya Mungu? Je! yaonekana ikishangaza kwamba, katika muda wenye ongezeko la kutoamini, watoto hujiunga na wazazi wao katika kuongea na wengine juu ya ahadi nzuri sana za Biblia kuhusu wakati ujao wenye furaha?a
Katika yaliyo mengi ya yale makundi zaidi ya 60,000 ya Mashahidi wa Yehova kotekote duniani, utapata vijana wengi. Wao hawaendi kwenye shule ya Jumapili ya kila juma wala darasa la kufunzwa katekisimu. Bali, vijana hawa hunufaika na hata hushiriki katika mikutano ya kundi. Wadogo-wadogo waweza kutoa maelezo sahili. Wasiofika umri wa utineja hutumia malikizo ya shule wakisaidia majirani kujifunza juu ya Mungu na ahadi zake nzuri sana kwa wakati ujao.
Kwa kweli utendaji huo wa kiujana si jambo jipya kamwe. Biblia husema juu ya wanaume na wanawake vijana waaminifu, na pia vijana na watoto wadogo, walioweka vielelezo vya kutokeza katika kutumikia Mungu.
Kitabu cha Biblia cha Zaburi kilitabiri “andamano la wanaume vijana,” wakiwa wenye kuburudisha na wengi sana kama “matone ya umande,” katika utumishi wa kumcha Mungu. Pia ilisema juu ya “wanaume vijana” na “mabikira” wakisifu jina la Mungu. (Zaburi 110:3; 148:12, 13, NW) Yaelekea kwamba, vijana fulani walikuwa miongoni mwa wale waliokuwapo wakati roho takatifu ya Mungu ilipomiminwa juu ya waamini kwenye Pentekoste 33 W.K. Siku hiyo watu karibu 3,000 walilipokea Neno kwa moyo na kubatizwa. Mtume Petro alisema tukio hili la kugutusha lilikuwa utimizo wa unabii wa Yoeli: “Wana wenu na binti zenu watatoa unabii na wanaume wenu vijana wataona njozi na wanaume wenu wazee wataota ndoto.”—Matendo 2:4-8, 16, 17, 41, NW.
Vielelezo vingine vya Kibiblia vya watu waliotumikia Yehova Mungu katika ujana wao ni kutia na Samweli, Mfalme Daudi mwadilifu, manabii wa Biblia wajulikanao sana Yeremia na Danieli, na vilevile Timotheo mwaminifu. Toleo hili lina makala tatu zinazoshughulika na baadhi ya vielelezo hivi vya Kibiblia. Utaona kutokana na makala hizo ni kwa nini vijana, na vilevile watu wenye umri mkubwa zaidi, huona kutumikia Mungu ni jambo lipasalo kuchukuliwa kwa uzito na kwa nini wao hutumia wakati mwingi sana wakisaidia jirani zao wafanye hivyo hivyo.
[Maelezo ya Chini]
a Uchunguzi wa maoni ya watu uliofanywa katika 1985 ulipata kwamba ni asilimia 12 tu ya Waamerika waliozaliwa tangu 1946 waliosema kwamba walikuwa na “imani nyingi sana” wakiwa na umri wa miaka 16.