Biblia—Ni Takatifu Kweli?
NI WATU wangapi leo wanaoiona Biblia kuwa takatifu, Neno la Mungu? Katika kipindi hiki cha kutia shaka, wengi huiona kuwa ya kikale kabisa na isiyotumika, wakishuku kama kwa kweli ni takatifu. Hata viongozi fulani wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo hufundisha kwamba Biblia imejaa hadithi na hekaya. Wao hushuku ‘kama ufafanuzi wa historia wa kibiblia ni mmoja ambao mtu mwenye akili aweza kukubali.’—The Interpreter’s Dictionary of the Bible, Buku 2, Ukurasa 611.
Wanachuo mashuhuri wanaeneza shaka kuhusu kama inafaa kurejezea Biblia kuwa Neno la Mungu. Mmoja alisema kwamba “kama mtu anataka kutumia aina ya lugha ya Neno la Mungu, maneno yanayofaa kwa Biblia yangekuwa Neno la Israeli, Neno la baadhi ya Wakristo wa mapema walioongoza.” (The Bible in the Modern World, ya James Barr) Wewe unafikiriaje? Je! Biblia ni Neno la Mungu? Ni takatifu kweli?
Nani Aliandika Biblia?
Kuandikwa kwa Mwanzo, kitabu cha kwanza cha Biblia, kwa kawaida kunasifiwa Musa, Mwebrania aliyeishi miaka 3,500 hivi iliyopita. Kulingana na Biblia yenyewe, watu 40 hivi kutoka kwa aina za maisha mbalimbali walishiriki katika kuandika Maandiko yaliyosalia, tokeo likiwa mkusanyo wa vitabu, au vijisehemu 66 vya Biblia. Hata hivyo, watu hao hawakujiona kuwa watungaji wenyewe wa Biblia. Mwandishi mmoja alisema hivi: “Kila andiko, [ni] lenye pumzi ya Mungu.” (2 Timotheo 3:16) Mwingine aliandika hivi juu ya waandishi wa Biblia: “Wanadamu walinena yaliyotoka kwa Mungu, wakiongozwa na Roho Mtakatifu [roho takatifu, NW].”—2 Petro 1:21.
Hilo lawaweka waandishi katika jamii ya makatibu, au makarani, wenye kudhibitiwa, au kuongozwa, na Mungu. Kulingana na Biblia, kwa kawaida mwandishi aliruhusiwa kuchagua maneno yake mwenyewe katika kueleza habari iliyotolewa kimungu. (Habakuki 2:2) Hiyo ndiyo sababu kuna mitindo mingi ya kuandika katika Biblia. Lakini kuandikwa kwayo sikuzote kuliongozwa na Mungu.
Ni kweli, madai ya waandishi hawa ya kupuliziwa roho kimungu yakiwa yenyewe si uthibitisho kwamba Biblia ni ujumbe wa kimungu kwa ainabinadamu kutoka kwa Muumba. Hata hivyo, kama Aliye Juu Kabisa ndiye Mtungaji wa Biblia au siye yapasa kuonekana wazi kwa uchunguzi wa uangalifu na usiopendelea wa kitabu hicho chenyewe. Je! Biblia yatoa uthibithisho wa kutungwa kimungu? Kwa kweli, twaweza kusema kwa uhakika kwamba Biblia ni takatifu?