Tembea Kama Ufundishwavyo na Yehova
“Unipe mafundisho, Ee Yehova, juu ya njia yako. Mimi nitatembea katika ukweli wako. Unganisha moyo wangu uwe kitu kimoja ili kuogopa jina lako.”—ZABURI 86:11, NW.
1, 2. Ni nini husukuma Mashahidi wa Yehova kukataa kutiwa damu mishipani?
“LABDA Mashahidi wa Yehova hufanya jambo la haki kukataa vitu vilivyofanyizwa kwa damu, kwa maana ni kweli kwamba viini fulani viwezavyo kusababisha maradhi vyaweza kupitishwa na damu iliyotiwa mishipani.”—Gazeti la kitiba la Kifaransa litokealo kila siku, Le Quotidien du Médecin, Desemba 15, 1987.
2 Watu fulani wasomao elezo hilo huenda wakawa walihisi kwamba bahati tu ndiyo iliyofanya Mashahidi wa Yehova wakatae kutiwa damu mishipani muda mrefu kabla haijajulikana kwa ujumla jinsi huko kutiwa damu kuwezavyo kuwa hatari, hata kuua. Lakini msimamo ambao Mashahidi wa Yehova wamechukua kuhusu damu haukutokea kwa aksidenti, wala hiyo si sheria iliyovumbuliwa na farakano fulani la dini ya kiajabu, msimamo unaotokana na kuhofu kwamba damu si salama. Bali, Mashahidi hukataa damu kwa sababu ya kupiga moyo konde watembee kwa utii mbele za Mfundishaji Mkuu wao—Mungu.
3. (a) Daudi alihisije juu ya kumtegemea Yehova? (b) Ni tokeo gani ambalo Daudi alitazamia kwa sababu ya kumtumaini Mungu?
3 Mfalme Daudi, aliyehisi tegemeo lake juu ya Mungu, alipiga moyo konde afundishwe naye na ‘kwenda katika kweli yake.’ (Zaburi 86:11) Wakati mmoja Daudi alishauriwa kwamba kama angeepuka kuwa na hatia ya damu machoni pa Mungu, ‘nafsi yake ingeweza kuthibitika kuwa imefungiliwa katika mfuko wa uhai pamoja na Yehova.’ (1 Samweli 25:21, 22, 25, 29, NW) Kama vile watu walivyofungilia vitu vya thamani kuvilinda na kuvihifadhi, ndivyo uhai wa Daudi ungeweza kulindwa na kuhifadhiwa na Mungu. Kwa kukubali ushauri huo wa hekima, Daudi hakutafuta kujiokoa kwa jitihada za kibinafsi bali alimtumaini yule Mmoja ambaye yeye alikuwa na deni lake kwa uhai wake: “Utanijulisha njia ya uzima; mbele za uso wako ziko furaha tele; na katika mkono wako wa kuume mna mema ya milele.”—Zaburi 16:11.
4. Kwa nini Daudi alitaka kufundishwa na Yehova?
4 Akiwa na mtazamo huo, Daudi hakuhisi kwamba angeweza kibinafsi kuchagua ni sheria zipi za kimungu zilizokuwa halali au zilizohitaji kutiiwa. Mtazamo wake ulikuwa: “Ee BWANA [Yehova, NW], unifundishe njia yako, na kuniongoza katika njia iliyonyoka.” “Unipe mafundisho, Ee Yehova, juu ya njia yako. Mimi nitatembea katika ukweli wako. Unganisha moyo wangu uwe kitu kimoja ili kuogopa jina lako. Nakusifu wewe, Ee Yehova Mungu wangu, kwa moyo wangu wote.” (Zaburi 27:11, UV; 86:11, 12, NW) Nyakati fulani kutembea katika ukweli mbele za Mungu kungeweza kuonekana kuwa jambo lisilo na mafaa au kungeweza kumaanisha kujidhabihu sana, lakini Daudi alitaka kufundishwa katika njia ifaayo na kutembea katika hiyo.
Kafundishwa Juu ya Damu
5. Ni jambo gani ambalo Daudi angekuwa ajua juu ya msimamo wa Mungu kuhusu damu?
5 Yastahili sisi tuangalie kwamba kuanzia uvulana na kuendelea, Daudi alikuwa amefundishwa maoni ya Mungu juu ya damu, na maoni hayo hayakuwa fumbo la kidini. Watu waliposomewa Sheria, Daudi angekuwa amesikia jambo hili: “Uhai wa mwili u katika hiyo damu; nami nimewapa ninyi hiyo damu juu ya madhabahu, ili kufanya upatanisho kwa ajili ya nafsi zenu; kwani ni hiyo damu ifanyayo upatanisho kwa sababu ya nafsi. Kwa hiyo naliwaambia wana wa Israeli, Hapana mtu miongoni mwenu aliye na ruhusa kula damu, wala mgeni aketiye kati yenu asile damu.”—Walawi 17:11, 12; Kumbukumbu 4:10; 31:11.
6. Kulikuwaje na uhitaji wenye kuendelea watumishi wa Mungu wafundishwe juu ya damu?
6 Kwa muda ambao Mungu alitumia Israeli wakiwa watu wake wakusanywa, wale waliotaka kumfurahisha walihitaji kufundishwa juu ya damu. Kizazi baada ya kizazi cha wavulana na wasichana Waisraeli walifundishwa hivyo. Lakini je! fundisho hilo lingeendelea baada ya Mungu kulikubali kundi la Wakristo, akiwajumlisha kuwa “Israeli wa Mungu”? (Wagalatia 6:16) Ndiyo, kweli kweli. Maoni ya Mungu juu ya damu hayakubadilika. (Malaki 3:6) Msimamo wake uliotajwa juu ya kutotumia damu vibaya ulikuwako kabla ya lile agano la Sheria kutendeshwa kazi, nao uliendelea baada ya Sheria hiyo kukomeshwa.—Mwanzo 9:3, 4; Matendo 15:28, 29.
7. Kwa nini kufundishwa na Mungu juu ya damu ni kwa maana kwetu?
7 Heshima kwa damu ni jambo kuu kwa Ukristo. ‘Je! huko si kutia chumvi?’ huenda watu fulani wakauliza. Hata hivyo, ni jambo gani lililo kuu kwa Ukristo ikiwa si dhabihu ya Yesu? Na mtume Paulo aliandika hivi: “Katika yeye huyo [Yesu], kwa damu yake, tunao ukombozi wetu, masamaha ya dhambi, sawasawa na wingi wa neema yake.” (Waefeso 1:7) The Inspired Letters, kilichotafsiriwa na Frank C. Laubach, chaufasiri hivi mstari huo: “Damu ya Kristo ilitulipia na sasa sisi ni mali Yake.”
8. Ni jinsi gani “umati mkubwa” wategemea damu kwa uhai?
8 Wote watumainiao kuokoka “dhiki kubwa” inayokaribia sana na kuonea shangwe baraka za Mungu katika dunia-paradiso huitegemea damu ya Yesu iliyomwagwa. Ufunuo 7:9-14, NW, waeleza juu yao na kusema hivi juu ya jambo ambalo tayari wamefanya: “Hawa ndio wale ambao huja kutoka dhiki kubwa, na wamefua majoho yao na wameyafanya meupe katika damu ya Mwana-Kondoo [Yesu].” Iangalie lugha iliyopo hapa. Haisemi kwamba hawa ambao waokolewa kupitia ile dhiki walikuwa ‘wamemkubali Yesu’ wala ‘kutia imani katika yeye,’ ingawa kwa uhakika hayo ni mambo muhimu. Yasonga mbele hatua moja zaidi na kusema kwamba ‘walifua majoho yao na kuyafanya meupe katika damu ya Yesu.’ Hiyo ni kwa sababu damu yake ina thamani yenye kukomboa.
9. Kwa nini kumtii Yehova kuhusu damu ni jambo zito sana?
9 Kuzingatia ubora wa thamani hiyo husaidia Mashahidi wa Yehova kuazimia kutotumia damu vibaya, hata ikiwa tabibu adai kwa moyo mweupe kwamba kutia damu mishipani ni muhimu kwa uhai. Huenda yeye akawa aamini kwamba manufaa ziwezazo kutokana na kutia damu mishipani zina uzito mwingi kuliko hatari za afya ambazo zatokezwa na damu yenyewe. Lakini Mkristo hawezi kupuuza hatari iliyo mbaya hata zaidi, ile hatari ya kupoteza kibali cha Mungu kwa kukubali kitendo cha kutumia damu vibaya. Wakati mmoja Paulo alisema juu ya wale ‘wafanyao dhambi kusudi baada ya kuupokea ujuzi wa ile kweli.’ Kwa nini dhambi yoyote ya namna hiyo ilikuwa nzito sana? Kwa sababu mtu wa jinsi hiyo ‘amemkanyaga Mwana wa Mungu, na kuihesabu damu ya agano aliyotakaswa kwayo kuwa ni kitu ovyo.’—Waebrania 9:16-24; 10:26-29.
Saidia Wengine Wafundishwe
10. Ni nini kisukumacho kupiga kwetu moyo konde ili kushika mwiko wa damu?
10 Sisi ambao huthamini dhabihu ya ukombozi ya Yesu hujihadhari tusizoee dhambi, kuikataa thamani yenye kuokoa uhai ya damu yake. Tukiisha kulifikiria jambo hilo kabisa, sisi hung’amua kwamba kule kushukuru Mungu tu kwa ajili ya uhai kwapasa kutuongoze tukatae jambo lolote la kuacha kuzifuata sheria zake adilifu, ambazo tuna hakika zilitolewa kwa kuzingatia moyoni masilahi zetu bora—masilahi zetu bora za muda mrefu. (Kumbukumbu 6:24; Mithali 14:27; Mhubiri 8:12) Ingawa hivyo, namna gani watoto wetu?
11-13. Ni maoni gani yenye makosa ambayo wazazi fulani Wakristo wanayo juu ya watoto wao na damu, na kwa nini?
11 Ingawa wazao wetu ni watoto wachanga au ni wachanga mno wasiweze kuelewa, Yehova Mungu aweza kuwaona kuwa safi na wenye kukubalika kwa msingi wa ujitoaji wetu. (1 Wakorintho 7:14) Hivyo basi ni kweli kwamba vitoto vichanga katika nyumba ya Kikristo huenda vikawa havijaelewa na kufanya chaguo juu ya kutii sheria ya Mungu juu ya damu. Hata hivyo, je! sisi tunafanya yote tuwezayo ili kuvifundisha katika jambo hilo muhimu? Wazazi Wakristo wapaswa kufikiria hilo kwa uzito, kwa maana wazazi fulani huonekana ni kama wana mtazamo wenye makosa juu ya watoto wao na damu. Wengine wao huonekana kuhisi kwamba kwa kweli wao hawawezi kudhibiti (kuwa na amri) sana juu ya kama watoto wao wadogo watatiwa damu mishipani. Kwa nini wao huwa na maoni hayo yenye makosa?
12 Mabara mengi yana sheria au mashirika ya kiserikali ya kulinda watoto walioachiliwa ovyo na kutumiwa vibaya. Watoto wa Mashahidi wa Yehova hawaachiliwi ovyo wala kutumiwa vibaya wakati wazazi waamuapo dhidi ya kuruhusu mwana au binti yao mpendwa apewe damu, wakati ule ule wakiomba utumizi wa matibabu ya badala ambayo tiba ya ki-siku-hizi yaweza kuandaa. Hata kwa maoni ya kitiba, huko si kuwaachilia ovyo wala kuwatumia vibaya, zikifikiriwa zile hatari zinazokubaliwa wazi za matibabu ya kutia damu mishipani. Huo ni utumizi wa haki ya kupima hatari zenye kuhusika halafu kuchagua matibabu.a Hata hivyo, maandalizi ya kisheria yamegeukiwa na wanatiba fulani wakitafuta mamlaka ya kulazimisha kutia damu katika mishipa ya asiyetaka kutiwa.
13 Wakiwa na habari kwamba huenda ikawa rahisi kwa wanatiba kuungwa mkono na mahakama ili kutia damu katika mishipa ya mtoto, huenda wazazi fulani wakahisi kwamba jambo hilo halimo mikononi mwao, kwamba hakuna jambo ambalo wazazi waweza au wahitaji kufanya. Hayo ni maoni yenye makosa kama nini!—Mithali 22:3.
14. Daudi na Timotheo walifundishwaje katika ujana wao?
14 Tumeona kwamba Daudi alifundishwa katika njia ya Mungu kuanzia ujana wake na kuendelea. Hiyo ilimtayarisha kuuona uhai kuwa zawadi kutoka kwa Mungu na kujua kwamba damu huwakilisha uhai. (Linganisha 2 Samweli 23:14-17.) Timotheo alifundishwa katika kufikiri kwa Mungu “tangu utoto.” (2 Timotheo 3:14, 15) Je! wewe hukubali kwamba hata Daudi na Timotheo walipokuwa chini ya ule ambao leo ni umri wa kisheria wa utu uzima, ni lazima wawe waliweza kujieleza vema juu ya masuala yaliyohusu mapenzi ya Mungu? Vivyo hivyo, muda mrefu kabla ya kufikia umri wa mtu mzima, Wakristo vijana leo wapaswa kufundishwa katika njia ya Mungu.
15, 16. (a) Ni maoni gani yamesitawi katika mahali fulani-fulani juu ya haki za watoto? (b) Ni nini kilichoongoza hadi mtoto mmoja kupewa damu?
15 Katika mahali fulani-fulani mtoto aitwaye mkomavu eti hupewa haki zifananazo na zile za watu wazima. Kwa msingi wa umri au kufikiri kwa ukomavu, au mambo yote mawili, huenda kijana akaonwa kuwa amekomaa kadiri ya kutosha kujifanyia maamuzi yake mwenyewe juu ya matibabu. Hata ambapo hiyo siyo sheria, mahakimu na wakuu huenda wakayapa uzito mwingi matakwa ya kijana awezaye kueleza waziwazi uamuzi wake thabiti juu ya damu. Kinyume cha hilo, mahali ambapo kijana hawezi kueleza imani zake waziwazi na kwa ukomavu, huenda mahakama ikahisi ni lazima iamue lionekanalo kuwa jambo bora zaidi, kama vile iwezavyo kufanyia mtoto mchanga.
16 Kijana mwanamume mmoja alikuwa amejifunza-funza Biblia akiacha-acha kwa miaka kadhaa lakini hakubatizwa. Ijapokuwa alikuwa amebaki na majuma saba tu kutoka umri ambapo yeye angepata ile “haki ya kujikatalia matibabu yeye mwenyewe,” hospitali moja yenye kumtibu kansa ilitafuta kuungwa mkono na mahakama ili imtie damu mishipani dhidi ya matakwa yake na yale ya wazazi wake. Yule hakimu mwenye kudhamiria alihoji-hoji kijana mwanamume huyo juu ya imani zake juu ya damu na kumwuliza maswali ya msingi, kama majina ya vitabu vya kwanza vitano vya Biblia. Kijana mwanamume huyo hakuweza kuvitaja wala kutoa ushahidi wenye kusadikisha kwamba alielewa kwa nini alikataa damu. Kwa kuhuzunisha, hakimu alitoa mamlaka ya kutia damu mishipani, akieleza hivi: “Katao [lake] la kutokubali kutiwa damu halina msingi wa uelewevu mkomavu wa imani zake mwenyewe za kidini.”
17. Ni msimamo gani ambao msichana mmoja wa miaka 14 alichukua juu ya kupewa damu, kukiwa na tokeo gani?
17 Huenda mambo yakageuka kuwa tofauti kwa mtoto aliyefundishwa vema katika njia za Mungu na mwenye kutembea kwa utendaji katika ukweli Wake. Mkristo mchanga zaidi alikuwa na namna ile ile ya kansa isiyopatikana mara nyingi. Msichana huyo na wazazi wake walielewa na kukubali matibabu yenye urekebisho ya kutumia kemikali kutoka kwa mtaalamu kwenye hospitali maarufu. Na bado, kesi ilipelekwa mahakamani. Hakimu aliandika hivi: “D.P. alishuhudia kwamba angekinza kutiwa damu mishipani kwa njia yoyote ambayo angeweza. Msichana huyo aliona kutiwa damu mishipani kuwa ni kuuvamia mwili wake na akakulinganisha na kulala mwanamke kinguvu. Aliiomba Mahakama iheshimu chaguo lake na kumruhusu aendelee kuwa kwenye [hospitali] bila kutiwa damu mishipani kwa agizo la Mahakama.” Fundisho la Kikristo alilokuwa amepokea lilimsaidia wakati huo mgumu.—Ona sanduku.
18. (a) Msichana mgonjwa alichukua msimamo gani imara juu ya kupokea damu? (b) Hakimu aliamua nini juu ya matibabu yake?
18 Msichana wa miaka 12 alikuwa akitibiwa ugonjwa wa kujazana kwa chembe nyeupe za damu zisizokomaa. Shirika la masilahi ya watoto lilipeleka jambo hilo mahakamani ili aweze kulazimishwa kutiwa damu. Hakimu alikata shauri hivi: “L. ameambia mahakama hii waziwazi na uso kwa uso kwamba, jaribio likifanywa kumtia damu mishipani, yeye atapigana na huko kutiwa damu mishipani kwa nguvu zote awezazo kupata. Msichana huyo amesema, nami namwamini, kwamba atapiga makelele na kujing’ang’ania na kwamba atakivuta kile chombo cha kudunga sindano kimtoke mkononi na atajaribu kuiharibu damu iliyo katika mfuko wenye kuning’inia juu ya kitanda chake. Mimi nakataa kutoa agizo lolote ambalo lingempitisha mtoto huyu katika hilo tatizo kubwa . . . Kwa habari ya mgonjwa huyu, matibabu yaliyonuiwa na hospitali yashughulikia maradhi yale katika maana ya kimwili tu. Yakosa kushughulikia mahitaji yake ya kihisia-moyo na imani zake za kidini.”
Wazazi—Fundisheni Vema
19. Ni wajibu gani wa pekee ambao wazazi wapaswa kutimiza kuelekea watoto wao?
19 Mambo hayo yaliyoonwa yana ujumbe wenye nguvu kwa wazazi watamanio kwamba wote katika familia yao waishi kulingana na sheria ya Mungu juu ya damu. Sababu moja kwa nini Abrahamu alikuwa rafiki ya Mungu ilikuwa kwamba Yeye alijua kwamba mzee huyo wa ukoo ‘angeamuru wanawe, na nyumba yake baada yake waishike njia ya Yehova, wafanye haki.’ (Mwanzo 18:19) Je! haipasi kuwa hivyo kwa wazazi Wakristo leo? Ikiwa wewe ni mzazi, je! unafundisha watoto wako wapendwa kutembea katika njia ya Yehova ili sikuzote ‘wawe tayari kumjibu kila mtu awaulizaye habari za tumaini lililo ndani yao, lakini wakifanya hivyo kwa upole na kwa hofu’?—1 Petro 3:15.
20. Ni jambo gani hasa ambalo twapaswa kutaka watoto wetu wajue na kuamini juu ya damu? (Danieli 1:3-14)
20 Ingawa ingekuwa vema watoto wetu wapashwe habari juu ya hatari za maradhi na hatari nyingine za kutiwa damu mishipani, kufundisha watoto wetu katika sheria kamilifu ya Mungu juu ya damu hakumaanishi hasa kujaribu kukaza kikiki ndani yao hofu juu ya damu. Kwa kielelezo, ikiwa hakimu angeuliza msichana kwa nini hataki kupewa damu na jibu lake sana-sana liwe kwamba yeye huiona damu kuwa hatari mno au yenye kuogopesha, tokeo lingeweza kuwa nini? Huenda hakimu huyo akakata shauri kwamba msichana huyo hajakomaa tu na ni mwoga kupita kiasi, kama vile angeweza kuogopa sana kupasuliwa ili aondolewe kidole cha utumbo hivi kwamba angelia na kukinza upasuaji huo ambao hata wazazi wake wanauona kuwa ndio umfaao kabisa. Zaidi ya hilo, mapema kidogo tuliona kwamba sababu ya msingi ya Wakristo kukataa kutiwa damu mishipani si kwamba damu ina uchafu bali kwamba hiyo ni yenye thamani kubwa kwa Mungu aliye Mpaji-Uhai wetu. Watoto wetu wapaswa kujua hilo, na pia kwamba hatari ziwezekanazo kutokea kitiba za damu zaongezea uzito wa msimamo wetu wa kidini.
21. (a) Wazazi wapaswa kujua nini juu ya watoto wao na maoni ya Biblia juu ya damu? (b) Wazazi waweza kusaidiaje watoto wao kuhusiana na damu?
21 Ikiwa wewe una watoto, je! una uhakika kwamba wao hukubaliana na msimamo huo wenye msingi wa Biblia juu ya kutiwa damu mishipani na kwamba waweza kuueleza? Je! wao kweli huamini msimamo huo ni mapenzi ya Mungu? Je! wao husadiki kwamba kuvunja sheria ya Mungu kungekuwa jambo zito sana hivi kwamba lingeweza kutia hatarini tazamio la Mkristo la uhai wa milele? Wazazi wenye hekima watapitia mambo hayo pamoja na watoto wao, wawe ni wachanga sana au wakaribia kuwa watu wazima. Wazazi waweza kufanya vipindi vya mazoezi ambamo kila kijana akabili maswali yawezayo kutokezwa na hakimu au mkuu wa hospitali. Mradi si kumfanya kijana arudie kwa kumbukumbu la akili mambo ya hakika au majibu fulani yaliyochaguliwa. Ni jambo la maana zaidi wajue mambo ambayo wao wayaamini, na kwa nini. Bila shaka, kwenye usikizi wa kesi mahakamani, wazazi au wengine wangeweza kueleza habari juu ya hatari za damu na kupatikana kwa matibabu badala. Lakini kile ambacho hakimu au mkuu angeelekea kutafuta kujua kwa kusema pamoja na watoto wetu ni kama wao wanaelewa kwa ukomavu hali na machaguo waliyo nayo na pia kama wao wana viwango vyao wenyewe vya kiadili na masadikisho imara.—Linganisha 2 Wafalme 5:1-4.
22. Ni nini liwezalo kuwa tokeo la kudumu la kufundishwa kwetu na Mungu juu ya damu?
22 Sisi sote twahitaji kuthamini na kushikilia maoni ya Mungu juu ya damu kwa kuazimia sana. Ufunuo 1:5, NW, hueleza juu ya Kristo kuwa yule ‘ambaye hutupenda sisi na ambaye alifungua sisi kutoka madhambi yetu kwa njia ya damu yake mwenyewe.’ Ni kwa kukubali thamani ya damu ya Yesu tu kwamba twaweza kupata msamaha kamili wenye kudumu wa dhambi zetu. Warumi 5:9 husema wazi hivi: “Basi zaidi sana tukiisha kuhesabiwa haki [waadilifu, NW] katika damu yake, tutaokolewa na ghadhabu kwa yeye.” Basi, ni jambo la hekima kama nini sisi na watoto wetu tufundishwe na Yehova juu ya jambo hilo na tupige moyo konde kutembea katika njia yake milele!
[Maelezo ya Chini]
a Ona broshua How Can Blood Save Your Life?, iliyochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc., kurasa 21-2, 28-31.
Mambo Makuu ya Kufundisha
◻ Ni maoni gani tupaswayo kuwa nayo juu ya kufundishwa na Yehova?
◻ Kwa nini kutii sheria ya Mungu juu ya damu ni jambo la maana sana?
◻ Kwa nini ni muhimu vijana waweze kueleza waziwazi na kwa imara masadikisho yao juu ya damu?
◻ Wazazi Wakristo waweza kusaidiaje watoto wao wafundishwe vizuri katika sheria ya Yehova juu ya damu?
[Sanduku katika ukurasa wa 17]
MAHAKAMA ILIVUTIWA
Uamuzi wa mahakama ulisema nini kuhusu D.P. aliyetajwa katika fungu la 17?
“Mahakama ilivutiwa sana na uelewevu, utulivu wa hisia, fahari, na mkazo wa kijana huyu wa miaka 14-1/2. Huenda yeye akawa aligutushwa na ugunduzi wa kwamba alikuwa na namna hatari ya kansa . . . Hata hivyo, huyo aliyekuja kwenye Mahakama kushuhudia alikuwa kijana mkomavu. Alionekana alikuwa amekaza fikira waziwazi juu ya kazi ngumu iliyomkabili. Alikuwa amehudhuria vipindi vyote vya kupewa mashauri, akakubalia mpango fulani wa matibabu, akakuza ufikirio fulani wenye kupatanika vizuri juu ya jinsi yeye kama binadamu angekabili tatizo hili la kitiba, naye akaijia Mahakama na lile ombi lenye kugusa hisia: onyesheni heshima kwa uamuzi wangu . . .
“Kuongezea ukomavu wake, D.P. ameeleza sababu za uamuzi wake ambazo zatosha kuifanya Mahakama iuheshimu. Kiroho, katika maoni ya kiakili, kiadili, na kihisia-moyo yeye angedhuriwa na mpango wa matibabu ambao ungehusisha kutiwa damu mishipani. Mahakama itaheshimu chaguo lake la mpango wa matibabu.”
[Picha katika ukurasa wa 16]
Hakimu au msimamizi wa hospitali huenda akataka kujua jambo ambalo kijana Mkristo huamini hasa, na kwa nini