Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w91 12/1 kur. 2-5
  • Je! Kweli Dini Inahitajiwa?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! Kweli Dini Inahitajiwa?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Ukuzi wa Uulimwengu
  • Kurudi Nyuma kwa Uulimwengu
  • Upendezi Uliofanywa Upya Katika Dini
  • Sehemu ya 19: Karne ya 17 hadi ya 19 Jumuiya ya Wakristo Yamenyana na Badiliko la Ulimwengu
    Amkeni!—1990
  • Nani Anayependezwa na Dini?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Je! Dini Yoyote Ni Nzuri vya Kutosha?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Dini Ina Faida Gani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
w91 12/1 kur. 2-5

Je! Kweli Dini Inahitajiwa?

JE! DINI ina maana kwako? Je! wewe, labda, ni mshirika wa kikundi cha kidini au wa kanisa fulani? Ikiwa ndivyo, wewe una hali moja na watu wengine wengi walioishi huko nyuma katika 1844, mwaka ambao mwanafalsafa Mjerumani Karl Marx aliandika hivi: “Dini . . . ndiyo kasumba ya watu.” Katika siku hizo karibu kila mtu alienda kanisani na dini ilikuwa na uvutano mkubwa katika kila cheo cha kijamii. Leo, hali hiyo imebadilika sana, na dini ina uvutano mdogo sana au haina uvutano wowote katika maisha ya mamia ya mamilioni ya watu. Ikiwa unaenda kanisani, yaelekea wewe ni kati ya wachache wafanyao hivyo katika jumuiya yako.

Ni nini kilichosababisha badiliko hilo? Kwanza, Karl Marx alisitawisha falsafa ya kupinga dini iliyokuja kuwa maarufu sana. Marx yaonekana aliona dini kuwa kizuizi cha maendeleo ya kibinadamu. Alidai kwamba mahitaji ya ainabinadamu yangepatikana vizuri zaidi kwa kufuatia mambo ya kimwili, falsafa ambayo haikuachia Mungu wala dini ya kimapokeo nafasi yoyote. Hilo lilimwongoza ataarifu hivi: “Jambo la kwanza linalotakiwa kwa furaha ya watu ni kuondolewa kwa dini.”

Falsafa ya Marx ya kufuatia vitu vya kimwili ilikuzwa zaidi na Msoshalisti Mjerumani Friedrich Engels na Vladimir Lenin mwongozi Mkomunisti wa Urusi. Ilikuja kuitwa falsafa ya Umaksi-Ulenini. Mpaka hivi karibuni, zaidi ya theluthi moja ya ainabinadamu iliishi chini ya tawala za kisiasa zilizoifuata kwa kadiri kubwa au ndogo falsafa hiyo ya kutoamini kuna Mungu. Wanaume na wanawake wengi wangali wakiishi chini ya tawala hizo.

Ukuzi wa Uulimwengu

Mweneo wa falsafa ya Kikomunisti silo jambo peke yake lililodhoofisha uvutano wa dini kwa ainabinadamu. Maendeleo katika sayansi yalikuwa na uvutano pia. Kwa mfano, mweneo wa nadharia ya mageuzi ulisababisha wengi kutilia shaka kuwapo kwa Muumba. Na kulikuwako mambo mengine.

Encyclopœdia Britannica yataja “ugunduzi wa maelezo ya kisayansi kwa matukio ambayo zamani yalionwa kuwa yalisababishwa na mambo yanayopita uwezo wa kiasili” na “kuondolewa kwa uvutano wa dini madhubuti katika maeneo ya utendaji kama vile utibabu, elimu na sanaa.” Matukio kama hayo yamesababisha ukuzi wa “uulimwengu.” Uulimwengu ni nini? Unafasiliwa kuwa “mtazamo wa maisha . . . wenye msingi wa wazo kwamba dini na nadharia za kidini zapasa kupuuzwa au kuwekwa mbali makusudi.” Uulimwengu una uvutano mkubwa katika nchi za Kikomunisti na zisizo za Kikomunisti pia.

Lakini uulimwengu na falsafa ya Umaksi-Ulenini hazikudhoofisha uvutano wa dini peke yavyo. Ni lazima makanisa ya Jumuiya ya Wakristo yashiriki lawama hiyo. Kwa nini? Kwa sababu kwa karne nyingi yametumia vibaya mamlaka yao. Na yalikuwa yamefundisha mafundisho yenye msingi wa mapokeo yasiyo ya Kimaandiko na falsafa za kibinadamu badala ya Biblia. Kwa hiyo, wengi katika makundi yao walikuwa wamedhoofika sana kiroho wasiweze kushindana na shambulio la uulimwengu.

Isitoshe, makanisa yenyewe kwa kadiri kubwa yalishindwa hatimaye na uulimwengu. Katika karne ya 19, wanachuo wa kidini katika Jumuiya ya Wakristo walitokeza namna ya uchambuzi wa juu zaidi uliofanya wengi wasiamini sifa ya Biblia ya kwamba ni Neno la Mungu lililopuliziwa roho. Makanisa, kutia na Kanisa Katoliki la Kiroma, yalikubali nadharia ya mageuzi. Naam, bado walidai kuamini uumbaji. Lakini waliacha nafasi wazi ya uwezekano wa kwamba mwili wa mwanadamu ulitokea kwa mageuzi, hali nafsi tu ndiyo iliyoumbwa na Mungu. Wakati wa miaka ya 1960, Uprotestanti ulitokeza theolojia iliyotangaza “kifo cha Mungu.” Makasisi wengi wa Kiprotestanti waliachilia mtindo-maisha wa kufuatia mambo ya kimwili. Walipendelea ngono kabla ya ndoa na hata ngono kati ya watu wa jinsia moja. Wanatheolojia wengine Wakatoliki walikuza theolojia ya ukombozi, wakichanganya Ukatoliki pamoja na falsafa ya kimapinduzi ya Umaksi.

Kurudi Nyuma kwa Uulimwengu

Hivyo, uulimwengu ukapata kuenea sana, hasa katika miaka ya 1960, na hadi karibu na katikati ya miaka ya 1970. Kisha mambo yakabadilika tena. Dini ilionekana kana kwamba yarudia hali ya kupendwa, ingawa kwa kadiri kubwa, haikuwa hivyo kwa makanisa ambayo yamekuwapo tangu zamani. Kuzunguka ulimwenguni kote, miaka ya mwisho ya 1970 na miaka ya 1980 ilishuhudia ukuzi wa ghafula wa vikundi vipya vya kidini.

Kwa nini mwinuko mwingine tena wa dini? Mwanasoshiolojia Mfaransa Gilles Kepel alitaarifu kwamba “watu walioelimishwa kilimwengu wasio makasisi . . . hudumisha kwamba utamaduni wa kilimwengu umewaongoza kwenye kikomo na kwamba kwa kudai uhuru wao mbali na Mungu, watu wanavuna kile ambacho wamepanda kwa kiburi na majivuno yao, yaani, uhalifu wa watoto, talaka, UKIMWI, matumizi mabaya ya dawa za kulevya, [na] kujiua.”

Kurudi nyuma kwa uulimwengu kumezidi kuongezeka tangu lile lionekanalo kuwa angamio la falsafa ya Umaksi-Ulenini la hivi karibuni. Kwa watu wengi falsafa hiyo ya kutoamini kuna Mungu ilipata kuwa dini ya kweli. Ebu wazia basi, fadhaa ya wale walioitumaini! Ripoti moja ya Washington Post kutoka Moscow ilinukuu mtu mmoja aliyekuwa zamani mkuu wa Shule ya Upili ya Chama cha Kikomunisti ambaye alisema hivi: “Nchi huishi si kwa kutegemea uchumi na mashirika yayo tu, bali pia kwa kutegemea fikira zayo za kutungwa na kwa kutegemea mababa walioianzisha. Jamii yoyote ya watu huingiwa na hisia za kuwa hoi igunduapo kwamba fikira zayo zilizo kubwa zaidi hazitegemei yaliyo kweli bali zategemea propaganda na mawazio tu. Lakini hilo ndilo linalotupata sisi sasa katika kile kisa cha Lenin na mapinduzi.”

Alipokuwa akisema kuhusu ulimwengu wa Kikomunisti na wa kibepari, Edgar Morin mwanasoshiolojia na mwanafalsafa Mfaransa alikiri hivi: “Tumeona si angamio tu la wakati ujao mwangavu uliowekewa watu wa kawaida bali tumeona pia angamio la maendeleo ya jumuiya ya kilimwengu yaliyopasa kupatikana kwa urahisi na kiasili, ambamo sayansi, fikira nzuri, na demokrasi zilipasa ziendelee kwa urahisi. . . . Sasa hakuna maendeleo yanayohakikishiwa sasa. Wakati ujao tuliotumaini umeangamia.” Hayo ndiyo maoni ya ubatili ya wengi walioweka imani katika jitihada za wanadamu kutokeza ulimwengu ulio bora zaidi bila Mungu.

Upendezi Uliofanywa Upya Katika Dini

Hali hii ya kufunguka macho ulimwenguni pote inasababisha idadi fulani ya watu mmoja mmoja wenye mioyo myeupe watambue uhitaji wa kuwa na upande wa kiroho maishani mwao. Wanaona uhitaji wa dini. Lakini hawatosheki na makanisa ambayo yamekuwapo tangu zamani, na wengine hata hutilia shaka dini zilizo mpya—kutia ndani madhehebu ya kuponyesha watu, vikundi vya karama za roho, vifarakano vya sirisiri, na hata vikundi vya waabudu wa Shetani. Ushupavu wa dini pia unazidi kuwa na hali isiyopendeza. Kwa hiyo, naam, dini inarudia hali ya kupendwa kwa njia nyingi. Lakini je, hali hiyo ya kurudia dini ni jambo zuri kwa wanadamu? Kwa kweli, dini yoyote hutosheleza kweli kweli mahitaji ya kiroho ya ainabinadamu?

[Picha katika ukurasa wa 3]

“Dini ndiyo kitulizo cha kiumbe kinachoonewa, ndiyo kisisimua-moyo cha ulimwengu usio na moyo wa huruma, na ndiyo kichangamsha nafsi cha hali yenye kuhuzunisha nafsi. Ndiyo kasumba ya watu”

[Hisani]

Photo: New York Times, Berlin—33225115

[Picha katika ukurasa wa 4]

Karl Marx na Vladimir Lenin waliona dini kuwa kizuizi kwa maendeleo ya kibinadamu

[Hisani]

Musée d’Histoire Contemperaine—BDIC (Universitiés de Paris)

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 5]

Mawazo ya Umaksi-Ulenini yalikuwa yameamsha matumaini ya juu sana katika mioyo ya mamilioni ya watu

[Hisani]

Musée d’Histoire Contemporaine—BDIC (Universitiés de Paris)

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 2]

Picha ya jalada: Garo Nalbandian

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki