Kushikamana Kwa Ukaribu Na Tengenezo La Mungu
KAMA ILIVYOSIMULIWA NA ROY A. RYAN
Sandhill, Missouri, iliitwa hivyo kwa kufaa, kwa kuwa ilikuwa tu kilima kikubwa cha mchanga katika tambarare ya mashambani yenye vilima-vilima. Kijiji hiki chenye njia panda kilikuwako kilometa 5 magharibi mwa mji Rutledge nacho kilikuwa na nyumba nane au tisa tu, kanisa la Kimethodisti, na chumba kidogo cha mhunzi. Hapo ndipo nilipozaliwa Oktoba 25, 1900.
BABA yangu ndiye aliyekuwa mhunzi wa kijiji hicho. Ingawa wazazi wangu walienda kanisani mara chache sana, Mama alianza kuniagiza niende shule ya Jumapili kwenye kanisa la Kimethodisti. Sikupenda jina Methodisti, nikiamini kwamba mtu apaswa aitwe Mkristo; na hata hivyo nilisitawisha kiu ya kweli ya Biblia na upendezi katika uhai wa milele.
Nilipokuwa mwenye umri wa miaka 16, nilienda kufanya kazi kwenye njia ya gari-moshi ya Santa Fe. Mmoja wa Wanafunzi wa Biblia wa Kimataifa (kama Mashahidi wa Yehova walivyojulikana wakati huo) jina lake Jim alikuja kufanya kazi katika kikundi chetu cha wafanyakazi wa njia ya gari-moshi hiyo, na yeye nami tulifanya kazi pamoja mara nyingi. Jim aliongea, nami nikasikiliza yale aliyokuwa nayo ya kusema juu ya Biblia. Yalisikika kuwa mazuri kwangu, kwa hiyo nikamwomba kama ningeweza kuazima kimoja cha vitabu vyake.
Jim aliniazima buku la kwanza la Studies in the Scriptures, lililochapiswa na C. T. Russell wa Wanafunzi wa Biblia wa Kimataifa. Nilipoirudisha, nilimfanya aniletee buku nyinginezo. Muda mfupi baadaye, Jim akaacha kazi kwenye njia ya gari-moshi, nami nilimwona tena barabarani huko Rutledge, akichukua maagizo kwa kitabu Scenario of the Photo-Drama of Creation chenye picha. Baadaye akanikaribisha kwenye mikutano ya kikundi iliyokuwa ikifanywa nyumbani mwake. Kila Jumapili, nilitembea zile kilometa 5 hadi Rutledge kwenda mkutanoni.
Gazeti Golden Age (sasa Amkeni!) lilipotolewa katika 1919, nilitaka kuanza katika huduma ya shambani. Mwanafunzi wa Biblia mwingine mpya na mimi tulikuwa na nia ya kuligawanya gazeti hilo jipya kutoka nyumba kwa nyumba. Tulihisi hofu kwa kadiri fulani juu ya kutembelea watu wa mji wetu, kwa hiyo tulipanda gari-moshi na kwenda kwenye mji uliokuwa karibu. Tulipowasili asubuhi, kila mmoja wetu alienda zake na kugonga milango hadi alasiri, hata ingawa hatukuwa na mazoezi yoyote katika kazi hiyo. Nilichukua maagizo ya maandikisho mawili, moja kutoka kwa mwanamume niliyefanya kazi naye kwenye reli.
Katika Oktoba 10, 1920, nilibatizwa ziwani karibu na Rutledge. Wazazi wangu walipinga kuhusika kwangu na Wanafunzi wa Biblia wa Kimataifa. Hiyo ilikuwa kwa sababu ya upinzani wenye kuchochewa na makasisi uliowapata Wanafunzi wa Biblia katika miaka ya vita ya 1914-1918. Hata hivyo, baadaye, baba yangu alianza kuhudhuria mikutano mingine ya Wanafunzi wa Biblia, na alisoma The Golden Age pia. Kabla ya kufa, mama yangu alipata kuwa mwenye upendelevu zaidi kwa uelewevu wetu wa kweli ya Biblia. Hata hivyo hakuna yeyote katika familia yetu aliyefanya kweli hiyo iwe mali yake mwenyewe.
Wakati wa Kujaribiwa
Katika siku hizo za mapema, kulikuwako watatu tu zaidi ya mimi waliohudhuria kwa ukawaida mikutano ya funzo la Biblia katika Rutledge. Hao watatu waliliacha tengenezo hatimaye. Mmoja alikuwa msemaji mzuri kabisa, ambaye angetoa hotuba za Biblia za watu wote katika eneo hilo. Hata hivyo, akawa mwenye kiburi juu ya uwezo wake mbalimbali na kuliona kuwa jambo la kumshusha cheo kushiriki katika kuhubiri nyumba kwa nyumba kama Wakristo wa mapema walivyokuwa wamefanya.—Matendo 5:42; 20:20.
Hao watatu walipoacha kushiriki pamoja na Wanafunzi wa Biblia wa Kimataifa, nakumbuka nikihisi kama mtume Petro wakati Yesu aliposema na watu juu ya ‘kula mwili wa Yesu na kunywa damu yake.’ Wakiwa wamekwazwa na fundisho lake, wengi wakati huo wakamwacha. Kwa hiyo, Yesu aliwauliza mitume: “Je! ninyi nanyi mwataka kuondoka?” Petro akajibu: “Bwana! Twende kwa nani? Wewe unayo maneno ya uzima wa milele.”—Yohana 6:67, 68.
Ingawa Petro hakuelewa kikamili yale Yesu aliyomaanisha kwa ‘kula mwili wa Yesu na kunywa damu yake,’ yeye alitambua kwamba Yesu alikuwa na maneno ya uhai. Hivyo ndivyo nilivyohisi kuhusu tengenezo. Lilikuwa na kweli hata ingawa sikuzote sikuelewa kikamili kila kitu nilichosoma katika vichapo. Hata hivyo, wakati wowote jambo fulani liliposemwa ambalo sikuelewa, sikufanya ubishi juu yalo. Baadaye, jambo hilo lilieleweshwa wazi, au nyakati nyingine maoni yalirekebishwa. Nilifurahi sikuzote kwamba nilikuwa nimengojea kwa saburi kueleweshwa wazi huko.—Mithali 4:18.
Marekebisho Ili Kupainia
Katika Julai 1924, nilihudhuria mkusanyiko wa kimataifa huko Columbus, Ohio. The Golden Age liliueleza kuwa “mkusanyiko wa Wanafunzi wa Biblia ulio mkubwa zaidi uliofanywa katika enzi zote.” Hapo azimio lenye kusisimua “Shtaka” lilikubaliwa. Habari iliyopokewa na roho iliyodhihirishwa kwenye mkusanyiko huo ilinitia moyo kuwa mhudumu wa wakati wote, au painia.
Niliporudi kutoka mkusanyiko huo, niliacha kazi yangu ya reli ya gari-moshi, na Mwanafunzi wa Biblia mwenzangu pamoja na mimi tukaanza kutumikia tukiwa mapainia. Hata hivyo, baada ya muda wa mwaka mmoja, afya ya wazazi wangu ikawa mbaya zaidi kufikia kadiri ambayo walihitaji msaada wangu. Niliacha kupainia na nikapata kazi katika kampuni ya mabomba ya kusafirisha mafuta, lakini kwa kuwa watu waliokuwa wakifanya kazi huko hawakuwa na uvutano mzuri, niliacha kazi hiyo na kuanza biashara ya kufuga nyuki na kuuza asali.
Kufikia vuli ya 1933, wazazi wangu wote wawili walikuwa wamekufa, wakiniacha nikiwa bila wajibu wowote. Kwa hiyo katika masika ya 1934, nilimpa mtu mwingine nyuki zangu, nikajenga gari-nyumba dogo ambamo ningeweza kuishi, na kuanza tena katika huduma ya wakati wote nikiwa painia. Mwanzoni nilifanya kazi pamoja na Shahidi mzee-mzee katika ujirani wa Quincy, Illinois. Baadaye nikahamia Missouri tena, ambapo nilijiunga na kikundi cha mapainia.
Katika 1935 kulikuwako ukame mkali sana katika Magharibi ya kati, na kwa kuwa tulikuwa tukifanya kazi katika eneo lililokuwa la kilimo peke yake, hali ilikuwa ngumu sana. Hakuna yeyote aliyekuwa na pesa zozote, kwa hiyo mara nyingi watu wenye shukrani walitupa vyakula au vitu vingine tulipowaachia vichapo.
Kupainia Kusini
Katika kipupwe hicho tulihamia Arkansas kuiepuka baridi. Tuliweza kugawanya vichapo vingi zaidi katika eneo hilo na kupokea vifaa vyote vya mkebeni ambavyo tungeweza kutumia. Mara nyingi tulikubali vitu vingine ambavyo tungeweza kuuza na kupata pesa, kutia ndani vyombo vya zamani vya aluminiamu, shaba nyeupe au shaba nyekundu ya zamani, vyombo vya kupoza joto katika gari na betri za gari za zamani. Hizo zilitupa pesa za petroli kwa gari langu la Fodi Modeli A, ambalo tulitumia katika huduma.
Tulitumikia katika maeneo ya Newton, Searcy, na Carroll katika Uwanda wa Juu wa Ozark wenye milima-milima. Mambo tuliyoona tulipokuwa tukihubiri miongoni mwa watu wa mlimani wa Arkansas yangeweza kujaza kitabu kimoja kama yangeandikwa. Kwa kuwa siku hizo barabara zilikuwa za kale au hazikuwako, tulifanya sehemu kubwa ya kazi yetu kwa miguu. Mapainia wengine katika kikundi chetu walikuwa wakienda kwa farasi kuwafikia watu katika maeneo ya juu zaidi ya milima hiyo.
Wakati mmoja tulisikia kuhusu mtu wenye kupendezwa aitwaye Sam, ambaye hatimaye tulimpata akiishi juu ya mlima mmoja. Alitukaribisha kwa uchangamfu na akafurahi tukae kwake hadi kuamkia keshoye. Ingawa mke wa Sam hakupendezwa na ujumbe wetu, mwana wake Rex, mwenye umri wa miaka 16, alipendezwa. Tulipoondoka, Sam alitukaribisha turudi tena. Kwa hiyo majuma mawili baadaye, tulikaa pamoja nao tena.
Tulipokuwa tukiondoka mara ya pili, mke wa Sam ndiye aliyetukaribisha turudi. Alisema kwamba tulikuwa na uvutano mzuri kwa Rex. “Yeye hutumia usemi mchafu,” akaeleza, “na sidhani ameutumia usemi huo mara nyingi jinsi hiyo tangu wakati nyinyi vijana mmekuwa hapa.” Miaka mingi baadaye nilikutana na Rex tena wakati alipohudhuria shule ya misionari ya Gileadi katika South Lansing, New York. Maono kama hayo yameniletea uradhi mwingi sana muda wote wa miaka ambayo imepita.
Utumishi wa Betheli
Nilipopeleka maombi ya kuwa painia, nilipeleka maombi pia ya kutumikia katika makao makuu ya Mashahidi wa Yehova katika New York, yaitwayo Betheli. Katika masika ya 1935, nilijulishwa kwamba ombi langu lilikuwa limekubaliwa na kwamba nilitakiwa niende Kingdom Farm ya Watchtower Society katika South Lansing, New York, kuanza utumishi wangu wa Betheli. Mara moja nikafanya mipango ili Shahidi mwenzangu aweze kulichukua gari-nyumba langu la kupainia.
Niliendesha gari langu la Fodi Modeli A kwenda New York, na nikawasili saa nne na nusu hivi asubuhi ya Mei 3, 1935. Karibu na saa saba alasiri hiyo, nilipewa kazi ya kupasua kuni. Keshoye niliambiwa niende kwenye nyumba ya kukama ng’ombe ili nisaidie. Nilifanya kazi ya ng’ombe wa maziwa kwa miaka mingi, nyakati nyingine nikikama asubuhi na jioni na kufanya kazi pamoja na wafanyakazi wa shambani na wa mimea ya shambani wakati wa mchana. Niliwatunza nyuki pia na kuvuna asali kwa ajili ya familia ya Betheli. Katika 1953, nilihamishwa kwenda kwenye idara ya kutengeneza jibini.
Mmoja wa wale waliokuwa na uvutano maishani mwangu kwa sababu ya mfano wake mzuri wa unyenyekevu, uaminifu-mshikamanifu, na utii kwa Yehova alikuwa Walter John “Papi” (Baba) Thorn. Yeye alikuwa mmoja wa Wanafunzi wa Biblia 21 waliowekwa rasmi katika 1894 kuwa pilgrimu wa kwanza—wanaume waliofanya kazi sawa na ile ya waangalizi wa mzunguko wa leo—kutembelea makundi kadhaa ili kuyatia moyo. Baada ya miaka zaidi ya 30 katika kazi ya kusafiri, Ndugu Thorn akaja Kingdom Farm na kufanya kazi katika nyumba ya kuku. Katika vipindi vingi nilimsikia akisema: “Wakati wowote nianzapo kujifikiria sana, mimi husubiri kidogo na kusema: ‘Ewe kavumbi katiti. Una nini cha kujivunia?’”
Mwanamume mwingine mwenye kiasi aliyepata kuwa kwangu kielelezo cha kuigwa alikuwa John Booth, ambaye sasa ni mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova. Amenukuliwa kwa muda wa miaka mingi kuwa akisema: “Jambo lenye maana si mahali unapotumikia bali ni nani unayemtumikia.” Hiyo ni taarifa sahili lakini ni yenye ukweli kama nini! Kumtumikia Yehova ndilo pendeleo kubwa kuliko mapendeleo yote!
Mojawapo ya mambo makuu katika utumi-shi wangu wa Betheli lilikuwa kufunguliwa kwa shule ya misionari ya Gileadi huko Kingdom Farm katika 1943. Kushiriki pamoja na mapainia kutoka sehemu nyingi za ulimwengu kulikuwa jambo lenye kusisimua sana. Katika siku hizo kulikuwako wanafunzi mia moja hivi katika kila darasa, kwa hiyo kila miezi sita watu mia moja wapya walikuja Kingdom Farm. Kuhitimu kungevutia maelfu ya watu kwa kifaa hiki cha elimu kilicho katika eneo la mashambani ya wilaya iliyo nje ya New York.
Kubadilisha Kazi
Shule ya Gileadi ilipohamishwa Brooklyn na jengo kuu la chumba cha kulala na la darasa huko South Lansing lilipouzwa, nyumba ya kukama ng’ombe ilihamishwa Watchtower Farms huko Wallkill, New York. Kwa hiyo katika vuli ya 1969, nilihamishwa kwenda shamba la Wallkill na kuendelea kutengeneza jibini mpaka 1983. Kisha nikabadilishwa kazi, na nikaanza kufanya kazi katika kutengeneza sura ya nchi iwe yenye kupendeza.
Nilipokuwa nikihojiwa wakati fulani uliopita, niliulizwa jinsi nilivyohisi juu ya kubadilishwa kazi baada ya miaka 30 ya kutengeneza jibini. “Hilo halikunisumbua,” nilisema kwa unyofu, “kwa sababu kwa vyovyote sikuwa napenda kutengeneza jibini.” Lililomaanisha ni kwamba twaweza kuwa na furaha tukimtumikia Yehova katika mgawo wowote ikiwa tunaona mambo kwa usawaziko na kujitiisha kwa unyenyekevu kwenye mwelekezo wa kitheokrasi. Kwa hiyo ingawa kwa kweli sikuwa napenda kutengeneza jibini, niliuonea shangwe mgawo wangu kwa sababu ulisaidia familia ya Betheli. Tukimtumikia Mungu wetu mtukufu, Yehova, kwa uaminifu na bila kulalamika, twaweza kuwa na furaha haidhuru mgawo wetu uwe ni gani.
Katika miaka yangu ya kudhoofika, sidhani ningekuwa katika hali bora kuliko kutumikia Betheli. Ninatunzwa vema na nimeweza kuendelea kufanya migawo yangu ya kazi hata ingawa mimi ni mwenye umri wa miaka 90. Kwa miaka mingi sasa, nimekuwa na pendeleo la kufanya zamu yangu ya kuongoza programu ya ibada ya asubuhi ya familia ya Betheli huku Watchtower Farms. Jinsi nilivyo na fursa, mimi huwatia moyo wapya katika Betheli wafaidike na mapendeleo yote ya utumishi wanayopewa na wajifunze kuridhika na kufurahi nayo.
Muda wa miaka ambayo imepita, nyakati kadhaa nimeweza kutembelea sehemu mbalimbali za kigeni—India, Nepali, Mashariki ya Mbali, na Ulaya. Shauri lifuatalo huenda likawa lenye msaada kwa wale walio katika makundi mbalimbali ya watu wa Yehova kuzunguka ulimwengu: Iweni wenye furaha na wenye kuridhika katika hali zenu za sasa na kusitawi katika njia ya kiroho ndani ya udongo mlimopandwa.
Nimechagua kubaki mseja, kwa kuwa kumeniwezesha kuendelea bila kukengeushwa fikira katika utumishi wangu kwa Mungu. Kama thawabu ya uaminifu, Mungu wetu mkuu ametoa tazamio la uhai wa milele. Kwa wengi, hilo litamaanisha uhai usio na mwisho katika makao ya paradiso hapa duniani. Wengine wetu wanatazamia uhai usio na mwisho mbinguni, kushughulikia mgawo wowote tunaopewa.
Wengine wangefikiri kwamba miaka yangu 90 imekuwa maisha marefu, yenye hali ya juu. Maisha yangu yamekuwa yenye hali ya juu lakini si ya muda mrefu wa kutosha. Kwa kubaki karibu na tengenezo la Mungu na maneno yake ya kweli, twaweza kurefusha maisha zetu milele.a
[Maelezo ya Chini]
a Wakati Roy Ryan alipokuwa akirekodi mambo aliyoona maishani mwake, afya yake ikawa mbaya kwa ghafula. Alimaliza mwendo wake wa kidunia katika Julai 5, 1991, si muda mrefu baada ya kufanya zamu yake ya kawaida ya kuongoza ibada ya asubuhi huko Watchtower Farms.
[Picha of Roy A. Ryan katika ukurasa wa 24]
[Picha katika ukurasa wa 26]
Ndugu Ryan katika miaka yake ya mapema akiwa kando ya gari la Fodi Modeli T