Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w91 12/15 kur. 28-29
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Habari Zinazolingana
  • Vyeo vya Kuchaguliwa kwa Kura
    Shule na Mashahidi wa Yehova
  • Kutumia Neno la Mungu Katika Jamaa Zetu Wenyewe
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Vijana Waigeukia Dini—kwa Sababu Gani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
  • Tembea Kama Ufundishwavyo na Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
w91 12/15 kur. 28-29

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

◼ Familia ya Kikristo yapaswa kufanya nini ikiwa mtoto wao analazimika kuhudhuria shule ambapo maagizo ya kidini ni ya lazima?

Wazazi Wakristo hawataki watoto wao wafundishwe mafundisho ya dini bandia. Lakini huenda kukawa hali ambazo watoto hawawezi kukataa kuwa darasani ambapo dini inafundishwa, ingawa hawangeshiriki katika vitendo au sherehe za dini bandia.

Abrahamu rafiki ya Mungu aliweka kiolezo kizuri kuhusu maagizo ya kidini kwa watoto. Aliwalea wazao wake Kanaani, ambapo walizungukwa na makosa ya kidini na mazoea “matakatifu” yenye kuchukiza mno. (Linganisha Kutoka 34:11-15; Mambo ya Walawi 18:21-30; Kumbukumbu la Torati 7:1-5, 25, 26; 18:9-14, NW.) Hata hivyo, yeye alikuwa chanzo cha maagizo ya kidini kwa familia yake. Mungu alikuwa na uhakika kwamba Abrahamu ‘angewaamuru wanawe, na nyumba yake baada yake waishike njia ya Yehova, wafanye haki.’—Mwanzo 18:19.

Akiwa kijana, Yesu pia alinufaika kutokana na maagizo ya familia na ya kikundi katika ibada ya kweli. Hivyo, “akazidi kuendelea katika hekima na kimo, akimpendeza Mungu na wanadamu.”—Luka 2:52.

Katika sehemu zilizo nyingi za dunia, vijana Wakristo hupokea elimu ya kilimwengu katika shule za umma. Si mambo yote yanayofundishwa ambayo hupatana kabisa na kweli ya Kibiblia na hakika iliyothibitishwa. Kwa mfano, vizazi vingi vya vijana Wakristo vimehudhuria masomo ya sayansi au bayolojia yakiwa sehemu ya kawaida ya mtaala wao wa elimu. Hivyo wengi wao wamefunuliwa wazi kwa nadharia zenye kuenea za mageuzi na maoni yenye kushirikiana nazo juu ya vyanzo “asili” vya uhai duniani.

Hata hivyo, kufunuliwa wazi huko hakukuwageuza vijana hao Wakristo kuwa wafuasi wa mageuzi ya kumkana Mungu. Kwa nini? Kwa sababu nyumbani na kwenye mikutano ya Kikristo, walikuwa wamepokea kimbele habari sahihi yenye msingi wa Neno la Mungu lililopuliziwa roho, ambalo limesaidia kuzoeza ‘akili zao, kupambanua mema na mabaya.’ (Waebrania 5:14) Wazazi wengi walikuwa wamejifunza na watoto wao habari yenye usawaziko juu ya mageuzi katika lile buku linaloimarisha imani Life—How Did It Get Here? By Evolution or by Creation?a Wakiwa wametayarishwa hivyo, watoto hao wa shule hawakukubali maagizo ya darasani juu ya mageuzi kuwa habari yenye kuaminika. Hata hivyo waliweza kuonyesha katika maitikio yao ya darasani na katika mitihani kwamba walikuwa wakisikiliza kwa makini na wangeweza kujifunza maelezo yaliyotolewa. Wengine waliweza hata kuwa na nafasi ya kuandaa maelezo ya badala yenye kupatana na mambo ya hakika yaliyotolewa katika Biblia na Muumba wa mwanadamu.—1 Petro 3:15.

Lakini, vipi kuhusu vipindi vya masomo vilivyotolewa kwa maagizo juu ya dini kuu ya mahali au hata juu ya dini kwa ujumla?

Haielekei kwamba maagizo ya jinsi hiyo yatatolewa bila upendeleo, kuwa habari ya kuarifu tu. Mwalimu huenda hata akawa mshiriki wa dini hiyo na hivyo huenda akajaribu kuwa na uvutano juu ya akili na mioyo ya wanafunzi. Kwa hiyo Mashahidi wa Yehova hupendelea kwamba watoto wao wasishirikishwe katika masomo ya maagizo ya kidini. Hiyo huenda ikawawezesha watoto wao watumie wakati wa shule kwa faida zaidi kukamilisha migawo ya masomo mengine au kujifunza katika maktaba ya shule.

Hata hivyo, katika mahali fulani-fulani, maombi ya jinsi hiyo yamekatazwa; shule au mamlaka za umma huenda hata zikataka kwamba watoto wote wahudhurie na kukamilisha mtaala wa dini ili kuhitimu. Kila familia yapasa iamue kibinafsi jambo la kufanya katika hali hiyo.

Watumishi wengine wa Yehova wa wakati uliopita wamelazimika kuwa katika hali ambazo walihitaji kuvumilia kufunuliwa wazi kwa mafundisho au vitendo vya kidini huku wakibaki waaminifu-washikamanifu kwa Mungu wa kweli. Yaelekea ilikuwa hivyo na Musa. Alilelewa akiwa mjukuu wa Farao wa Misri, naye “akafundishwa hekima yote ya Wamisri.” (Matendo 7:20-22) Hiyo huenda ikawa ilitia ndani kwa kadiri fulani imani na mazoea ya kidini yaliyokuwa kawaida katika Misri. Lakini Musa alilindwa na maagizo yenye ubora wa juu zaidi ambayo kwa wazi alipokea kutoka kwa familia yake na labda kwa Waebrania wengine.—Kutoka 2:6-15; Waebrania 11:23-26.

Ebu fikiria pia mfano wa wale vijana Waebrania watatu, washirika wa Danieli, waliopewa maagizo ya pekee katika Babuloni na kufanywa wafanyakazi wa serikali. (Danieli 1:6, 7) Hawakuwa huru kufanya au kukataa kufanya lolote walilotaka. Katika pindi moja Mfalme Nebukadreza aliamuru wakusanyike pamoja na maofisa wengine kwenye sanamu ya dhahabu aliyoweka juu ya uwanda wa Dura, ambapo vitendo vya uchaji wa kitaifa vingefanywa. Wale Waebrania watatu waliitikiaje? Twaweza kuwa na hakika kwamba wangalipendelea kutokuwa huko, lakini hilo halikuwezekana.b Hata hivyo walibaki waaminifu kwa imani zao na kwa Mungu Mweza Yote. Dhamiri zao za kimungu ziliwaruhusu wawe huko, huku wakikataa katakata kushiriki au kushughulika kibinafsi katika kitendo chochote cha dini bandia.—Danieli 3:1-18.

Inapokuwa jambo la lazima kwa wanafunzi wote kuwako kwenye somo la dini na labda kujifunza kwa kadiri ya kuweza kupita mitihani ya kiwango fulani, watoto kutoka kwa familia za Wakristo wa kweli waweza kuwako, kama wale watatu walivyokuwako kwa amri ya Nebukadreza. Lakini vijana Wakristo wangemtanguliza Mungu. Kusingekuwa uhitaji wowote kwao kupinga kila taarifa isiyo sahihi inayotolewa au kila zoea lisilo la kimaandiko ambalo katika hilo wengine hushiriki, kama vile wale Waebrania watatu hawakujaribu kuingilia wakati wengine walipoinamia ile sanamu ya dhahabu. Hata hivyo, vijana Wakristo wenyewe hawangeshiriki katika vitendo vya ibada, sala za muungano, nyimbo za kidini, na mambo kama hayo.

Vijana hao wanapaswa wajitahidi wenyewe sana katika nyakati nyingine kutwaa maarifa yenye kujenga kutoka kwa ‘maandiko matakatifu, ambao yaweza kuwahekimisha hata wapate wokovu kwa imani iliyo katika Kristo Yesu.’ (2 Timotheo 3:15) Kupitia mawasiliano pamoja na watoto wao, wazazi wapaswa daima kuchunguza yaliyomo katika maagizo ya darasani. Hilo litasaidia watu wazima Wakristo waone yale yanayohitaji kurekebishwa au kueleweshwa wazi kutoka kwa Biblia ili watoto wao wasije wakafadhaika au kuongozwa vibaya.

[Maelezo ya Chini]

a Lililochapwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

b Biblia haimtaji Danieli kuwa kwenye uwanda wa Dura. Labda cheo chake cha juu zaidi katika serikali kilimwezesha asishirikishwe kwenda huko.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki