Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w92 1/1 kur. 18-23
  • Hofuni Yehova na Kulitukuza Jina Lake Takatifu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Hofuni Yehova na Kulitukuza Jina Lake Takatifu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Hofu ya Kimungu Yashinda
  • Kutenda Katika Hofu ya Yehova
  • Penda Lililo Jema, Chukia Lililo Baya
  • Hofuni Yehova na Kumtukuza Yeye
  • Mtukuzeni Yehova Milele
  • Sitawisha Moyo wa Kumhofu Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
  • Kujifunza Kupata Furaha Katika Kumhofu Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Kwa Nini Tunapaswa Kuhofu Mungu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Kuogopa Mungu Je! Kunaweza Kukunufaisha Wewe?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
w92 1/1 kur. 18-23

Hofuni Yehova na Kulitukuza Jina Lake Takatifu

“Ni nani ambaye kwa kweli hatahofu wewe, Yehova, na kutukuza jina lako, kwa sababu wewe pekee ni mshikamanifu?”—UFUNUO 15:4, NW.

1, 2. (a) Yehova alifunguaje madirisha ya mbinguni muda wa 1991? (b) Ni ono gani la maishani lililomchochea misionari mwaminifu kutoa shauri: “Hofuni Yehova”? (Ona pia Kitabu-Mwaka 1991 (katika Kiingereza), kurasa 187-9.)

YEHOVA ‘alifungua madirisha ya mbinguni, na kumwaga baraka, hata isiwepo nafasi ya kutosha.’ Maneno hayo yangeweza kutumiwa tena na tena kwa Mashahidi wa Yehova katika nyakati za hivi karibuni. (Malaki 3:10) Kwa mfano, uchangamfu mwingi wa Mashahidi wanaotembelea na wahudhuriaji wa mahali hapo ulionyeshwa kwa kushirikiana pamoja kwenye mikusanyiko iliyofanywa duniani pote—kutoka São Paulo (Agosti 17-19, 1990) na Buenos Aires katika Amerika Kusini hadi Manila, Taipei, na Bangkok katika Mashariki na Budapest, Prague, na Zagreb (Agosti 16-18, 1991) katika Ulaya Mashariki. Katika mahali hapo panane peke yake, XXX,XXX walihudhuria na X,XXX wakabatizwa.

2 Ilikuwa shangwe kama nini kwa wahudhuriaji wa kutoka ng’ambo kukutana na Mashahidi waliokuwa waaminifu kwa muda mrefu katika mahali hapo mbalimbali! Kwa mfano, katika Bangkok, Frank Dewar—aliyekuwa wakati mmoja mhubiri wa Ufalme wa pekee katika Thailandi—alisimulia juu ya miaka yake 58 ya utumishi wa umisionari. Utendaji wake ulienea kutoka visiwa vya Pasifiki hadi Esia Kusini-Mashariki, na hata katika China. Alikuwa amekabili hatari mbalimbali kutoka kuvunjikiwa meli, wanyama wa porini katika misitu, magonjwa ya kitropiki, na utawala mkatili wa kamanda wa vita Wajapani. Alipoulizwa ni shauri gani angewapa wahudhuriaji, jibu lake lilikuwa rahisi: “Hofuni Yehova!”

3. Kwa nini twapaswa kuonyesha hofu ya kimungu?

3 “Hofuni Yehova!” Ni jambo la maana kama nini kwa sisi sote kusitawisha hofu hiyo inayofaa! “Kumcha [kumhofu, NW] BWANA [Yehova, NW] ndio mwanzo wa hekima.” (Zaburi 111:10) Hofu hiyo si kumwogopa Yehova kusivyofaa. Bali, ni staha nyingi kwa ajili ya utukufu wake wenye kutisha na sifa zake za kimungu, zenye msingi wa mwono-ndani tunaopokea kupitia funzo la Neno la Mungu. Kwenye Ufunuo 15:3, 4, NW, wimbo wa Musa na wa Mwana-Kondoo unatangaza rasmi hivi: “Kubwa na za ajabu ni kazi zako, Yehova Mungu, Mweza Yote. Za uadilifu na za kweli ni njia zako, Mfalme wa umilele. Ni nani ambaye kwa kweli hatahofu wewe, Yehova, na kutukuza jina lako, kwa sababu wewe pekee ni mshikamanifu?” Akiwa mwaminifu-mshikamanifu kwa waabudu wake, Yehova ana ‘kitabu cha ukumbusho kinachoandikwa mbele zake, kwa ajili ya hao wanaomhofu Yehova, na kulitafakari jina lake.’ Wanapewa thawabu ya uhai wa milele.—Malaki 3:16; Ufunuo 20:12, 15.

Hofu ya Kimungu Yashinda

4. Ni ukombozi gani wa kale unaopasa kututia moyo tumhofu Yehova?

4 Israeli walipoondoka Misri ya Farao, Musa alionyesha wazi kwamba alimhofu Yehova peke yake. Upesi, Waisraeli walifungwa kati ya Bahari Nyekundu na majeshi ya Misri yenye nguvu. Wangeweza kufanya nini? “Musa akawaambia watu, Msiogope, simameni tu, mkauone wokovu wa BWANA [Yehova, NW] atakaowafanyia leo; kwa maana hao Wamisri mliowaona leo hamtawaona tena milele. Bwana atawapigania ninyi, nanyi mtanyamaza kimya.” Yehova aliyagawanya maji kimuujiza. Waisraeli wakaenda ng’ambo ile nyingine kwenye bahari kavu. Kisha maji yakarudi tena kwa mshindo. Jeshi la Farao likafutiliwa mbali. Yehova aliliokoa taifa hilo lenye kumhofu Mungu, wakati ule ule akitekeleza hukumu kwenye Misri isiyomheshimu Mungu. Vilevile leo, yeye ataonyesha uaminifu-mshikamanifu wake kwa kuwakomboa Mashahidi wake wenye kumhofu Mungu kutoka ulimwengu wa Shetani.—Kutoka 14:13, 14; Warumi 15:4.

5, 6. Ni matukio gani katika wakati wa Yoshua yanayoonyesha kwamba tunapaswa kumhofu Yehova kuliko wanadamu?

5 Baada ya kule Kutoka Misri, Musa aliwatuma wapelelezi 12 katika Bara Lililoahidiwa. Kumi wao waliogopa sana walipowaona wakaaji huko waliokuwa kama majitu na wakajaribu kushawishi Waisraeli wasiingie bara hilo. Lakini wale wengine wawili, Yoshua na Kalebu, waliripoti hivi: “Ni nchi njema mno ya ajabu. Ikiwa BWANA [Yehova, NW] anatufurahia, atatuingiza katika nchi hii atupe iwe yetu, nayo ni nchi yenye wingi wa maziwa na asali. Lakini msimwasi BWANA [Yehova, NW], wala msiwaogope wale wenyeji wa nchi maana wao ni chakula kwetu; uvuli uliokuwa juu yao umeondolewa, naye BWANA [Yehova, NW] yu pamoja nasi; msiwaogope.—Hesabu 14:7-9.

6 Hata hivyo, Waisraeli hao walishindwa na hofu ya wanadamu. Tokeo likawa kwamba, hawakufika bara la ahadi. Lakini Yoshua na Kalebu, pamoja na kizazi kipya cha Waisraeli, walikuwa na pendeleo la kuingia bara hilo zuri na kulima mashamba yalo ya mizabibu na mizeituni. Katika hotuba yake ya kuwaaga watu wa Israeli waliokusanyika, Yoshua aliwapa shauri hili: “Mcheni [hofuni, NW] BWANA [Yehova, NW], mkamtumikia kwa unyofu wa moyo na kwa kweli.” Na Yoshua akaongeza hivi: “Lakini mimi na nyumba yangu tutamtumikia BWANA [Yehova, NW].” (Yoshua 24:14, 15) Hayo ni maneno yenye kutia moyo kama nini vichwa vya familia na wote wamhofu Yehova tunapojitayarisha kuingia ulimwengu mpya wa Mungu wenye uadilifu!

7. Daudi alikaziaje umaana wa hofu ya Mungu?

7 Mvulana mchungaji Daudi pia alionyesha mfano mzuri wa hofu ya Yehova wakati aliposhindana na Goliathi katika jina la Mungu. (1 Samweli 17:45, 47) Kwenye kitanda chake alipofia, Daudi aliweza kutangaza rasmi hivi: “Roho ya BWANA [Yehova, NW] ilinena ndani yangu, na neno lake likawa ulimini mwangu. Mungu wa Israeli alisema, Mwamba wa Israeli aliniambia, Atawalaye wanadamu kwa haki, akitawala katika kicho [hofu, NW] cha Mungu, atakuwa kama nuru ya asubuhi jua lichapo, ashubuhi isiyo na mawingu.” (2 Samweli 23:2-4) Hofu hiyo ya Mungu haipo miongoni mwa watawala wa ulimwengu, na tokeo ni lenye kuhuzunisha kama nini! Hali itakuwa tofauti kama nini wakati Yesu, “Mwana wa Daudi,” atakapotawala dunia katika hofu ya Yehova!—Mathayo 21:9.

Kutenda Katika Hofu ya Yehova

8. Kwa nini Yuda ilifanikiwa chini ya Yehoshafati, hilo likionyesha nini kwa leo?

8 Miaka mia moja hivi baada ya kifo cha Daudi, Yehoshafati alikuwa mfalme wa Yuda. Kulikuwako tena mfalme aliyetumikia katika hofu ya Yehova. Alirudisha utaratibu wa kitheokrasi katika Yuda, akaweka waamuzi kotekote nchini, na kuwapa maagizo haya: “Hammfanyii mwanadamu hukumu, ila BWANA [Yehova, NW]; naye yupo pamoja nanyi katika neno la hukumu; Basi sasa hofu ya BWANA [Yehova, NW] na iwe juu yenu; angalieni mkaifanye; kwa maana kwa BWANA [Yehova, NW] Mungu wetu, hapana uovu, wala kujali nafsi za watu, wala kupokea zawadi. . . . Ndivyo mtakavyotenda kwa hofu ya BWANA [Yehova, NW], kwa uaminifu, na kwa moyo kamili.” (2 Mambo ya Nyakati 19:6-9) Hivyo, Yuda ikasitawi katika hofu ya Yehova, kama vile watu wa Mungu hufaidika na utumishi wa waangalizi wenye hurumu leo.

9, 10. Yehoshafati alishindaje katika hofu ya Yehova?

9 Hata hivyo, Yuda ilikuwa na adui. Hao waliazimia kulifutilia mbali taifa la Mungu. Majeshi yaliyoungana ya Amoni, Moabu, na Mlima Seiri walijaza eneo la Yudea na kutisha Yerusalemu. Lilikuwa jeshi lenye nguvu nyingi. Yehoshafati alimgeukia Yehova katika sala “wakasimama Yuda wote mbele za BWANA [Yehova, NW], pamoja na wadogo wao, na wake zao, na watoto wao.” Kisha, kwa kujibu sala hiyo, roho ya Yehova ilimjia Mlawi Yahazieli, aliyesema hivi: “BWANA [Yehova, NW] awaambia hivi, Msiogope, wala msifadhaike kwa ajili ya jeshi kubwa hili; kwani vita si yenu bali ni ya Mungu. Kesho shukeni juu yao. . . . Hamtahitaji kupigana vita, jipangeni, simameni, mkauone wokovu wa BWANA [Yehova, NW] ulio pamoja nanyi, enyi Yuda na Yerusalemu; msiogope, wala msifadhaike; kesho tokeni juu yao kwa kuwa BWANA [Yehova, NW] yu pamoja nanyi.”—2 Mambo ya Nyakati 20:5-17.

10 Asubuhi iliyofuata, wanaume wa Yuda waliamka mapema. Walipoondoka kwa utiifu kukutana na adui, Yehoshafati alisimama na kusema hivi: “Nisikieni, enyi Yuda nanyi wenyeji wa Yerusalemu; mwaminini BWANA [Yehova, NW], Mungu wenu ndivyo mtakavyothibitika; waaminini manabii wake, ndivyo mtakavyofanikiwa.” Wakienda mbele ya wanaume wenye silaha, wenye kumwimbia Yehova waliimba kwa korasi: “Mshukuruni BWANA [Yehova, NW]; kwa maana fadhili [fadhili-upendo, NW] zake ni za milele.” Yehova alionyesha fadhili-upendo hizo kwa kufanya kuwe na mchafuko mwingi sana katika vikosi vya adui hivi kwamba waliangamizana wao kwa wao. Wanaume wa Yuda walipofika kwenye mnara wa mlinzi wa jangwani, maiti za adui tu ndizo zilizobaki.—2 Mambo ya Nyakati 20:20-24.

11. Kwa habari ya hofu, mataifa yanatofautianaje na watu wa Mungu?

11 Nchi za jirani ziliposikia juu ya ukombozi huo wa kimuujiza, “hofu ya Mungu” ikawajia. Kwa upande mwingine, taifa lililotii katika hofu ya Yehova sasa likawa na ‘starehe pande zote.’ (2 Mambo ya Nyakati 20:29, 30) Vivyo hivyo, Yehova atakapotekeleza hukumu kwenye Har–Magedoni, mataifa yatakuwa katika hofu ya Mungu na ya Mwana wake Mtekelezaji Hukumu, Yesu Kristo, na hawataweza kusimama katika siku kubwa ya ghadhabu ya kimungu.—Ufunuo 6:15-17.

12. Hofu ya Yehova imethawabishwaje katika nyakati za mapema?

12 Hofu ya Yehova inayofaa huleta thawabu nyingi. Noa “alivyomcha Mungu, aliunda safina, apate kuokoa nyumba yake.” (Waebrania 11:7) Na kwa habari ya Wakristo wa karne ya kwanza, imerekodiwa kwamba, kufuatia kipindi cha mnyanyaso, kundi “likapata raha katika Uyahudi wote na Galilaya na Samaria, likajengwa, likiendelea na kuongezeka katika kicho [hofu, NW] cha Bwana [Yehova, NW], na faraja ya Roho Mtakatifu [roho takatifu, NW].”—sawa na jinsi ilivyo katika Mashariki mwa Ulaya leo.—Matendo 9:31.

Penda Lililo Jema, Chukia Lililo Baya

13. Tunaweza kupata baraka ya Yehova kwa njia gani pekee?

13 Yehova ni mwema kikamili. Kwa hiyo, “Kumcha [kumhofu, NW] BWANA [Yehova, NW] ni kuchukia uovu [lililo baya, NW].” (Mithali 8:13) Imeandikwa kuhusu Yesu: “Umependa haki, umechukia maasi; kwa hivyo Mungu, Mungu wako, amekutia mafuta, mafuta ya shangwe.” (Waebrania 1:9) Ikiwa sisi, kama Yesu, tunatamani baraka ya Yehova, ni lazima tuchukie ubaya, ukosefu wa adili, jeuri, na pupa ya ulimwengu wa Shetani wenye kiburi. (Linganisha Mithali 6:16-19.) Ni lazima tupende lile ambalo Yehova hupenda na kuchukia lile analochukia. Ni lazima tuhofu kufanya lolote ambalo lisingempendeza Yehova. “Kwa kumcha BWANA [kumhofu Yehova, NW] watu hujiepusha na maovu [mabaya, NW].”—Mithali 16:6.

14. Yesu anatuandaliaje kielelezo?

14 Yesu alituachia kielelezo tufuate nyayo zake kwa ukaribu. “Yeye alipotukanwa, hakurudisha matukano; alipoteswa, hakuogofya; bali alijikabidhi kwake yeye ahukumuye kwa haki.” (1 Petro 2:21-23) Katika hofu ya Yehova, sisi pia twaweza kuvumilia masuto, dhihaka, minyanyaso, ambayo ulimwengu wa Shetani hutuwekea.

15. Kwa nini twapaswa kumhofu Yehova kuliko wale wawezao kuuua mwili?

15 Kwenye Mathayo 10:28, Yesu atuhimiza kwa upole: “Msiwaogope [msiwahofu, NW] wauuao mwili, wasiweze kuiua na roho [nafsi, NW]; afadhali mwogopeni [hofuni, NW] yule awezaye kuangamiza mwili na roho [nafsi, NW] pia katika jehanum.” Hata ikiwa mtu anayemhofu Yehova angeuawa na adui, uchungu wa kifo ni wa muda tu. (Hosea 13:14) Anapofufuliwa, yeye ataweza kusema: “Ku wapi, Ewe mauti, kushinda kwako? U wapi, Ewe mauti, uchungu wako?”—1 Wakorintho 15:55.

16. Yesu alionyeshaje hofu ya Yehova na kumtukuza?

16 Yesu mwenyewe aandaa mfano mzuri sana kwa wote wanaopenda uadilifu wa Yehova na kulichukia lililo baya. Hofu yake ya Yehova yaonyeshwa katika maneno yake ya mwisho kwa wanafunzi wake, kama yapatikanavyo kwenye Yohana 16:33: “Hayo nimewaambieni mpate kuwa na amani ndani yangu. Ulimwengu mnayo dhiki; lakini jipeni moyo; mimi nimeushinda ulimwengu.” Usimulizi wa Yohana waendelea hivi: “Maneno hayo aliyasema Yesu; akainua macho yake kuelekea mbinguni, akisema, Baba, saa imekwisha kufika. Mtukuze Mwanao, ili Mwana wako naye akutukuze wewe . . . Jina lako nimewadhihirishia watu wale ulionipa katika ulimwengu.”—Yohana 17:1-6.

Hofuni Yehova na Kumtukuza Yeye

17. Twaweza kuuiga mfano wa Yesu katika njia zipi?

17 Je! sisi leo twaweza kuuiga mfano wa Yesu wa moyo mkubwa? Hakika twaweza katika hofu ya Yehova! Yesu ametujulisha jina na sifa tukufu za Mungu. Kumhofu Yehova akiwa Bwana Mwenye Enzi Kuu yetu, tunamkweza juu zaidi ya miungu wengine wote, kutia ndani Utatu wa kifumbo wa Jumuiya ya Wakristo usio na jina. Yesu alimtumikia Yehova akiwa na hofu iliyofaa, akikataa kunaswa katika mtego wa hofu ya wanadamu wanaokufa. “Siku hizo za mwili wake, alimtolea yule, awezaye kumwokoa na kumtoa katika mauti, maombi na dua pamoja na kulia sana na machozi, akasikilizwa kwa jinsi alivyokuwa mcha Mungu [na hofu ya kimungu, NW].” Kama Yesu, na sisi pia tumhofu Yehova tunapoendelea kujifunza utii katika mateso yanayotupata—wokovu wa milele ukiwa mradi wetu sikuzote.—Waebrania 5:7-9.

18. Twaweza kumtoleaje Mungu utumishi mtakatifu tukiwa na hofu ya kimungu?

18 Baadaye katika barua hiyo kwa Wakristo Waebrania, Paulo ahimiza Wakristo wapakwa-mafuta hivi: “Kwa kuwa tunapokea ufalme usioweza kutetemeshwa, na tuwe na neema, ambayo kwa hiyo tumtolee Mungu ibada ya kumpendeza [utumishi mtakatifu, NW], pamoja na unyenyekevu [hofu ya kimungu, NW] na kicho.” Leo, “mkutano mkubwa” hushiriki katika utumishi huo mtakatifu. Na huo hutia ndani nini? Baada ya kuzungumzia fadhili za Yehova zisizostahiliwa katika kuandaa dhabihu ya Mwana Wake, Yesu Kristo, Paulo asema hivi: “Kwa njia yake yeye, na tumpe Mungu dhabihu ya sifa daima, yaani, tunda la midomo iliungamayo jina lake.” (Waebrania 12:28; 13:12, 15) Katika kuthamini fadhili za Yehova zisizostahiliwa, twapaswa kutaka kutoa kila saa tuwezayo kwa utumishi wake mtakatifu. Wakiwa waandamani waaminifu-washikamanifu wa Wakristo wapakwa-mafuta wanaobaki, wale wa umati mkubwa leo hutimiza kwa kadiri kubwa zaidi sehemu kuu ya utumishi huo. Hao humhesabia Mungu na Kristo wokovu, wanaposimama kitamathali mbele ya kiti cha enzi cha Mungu, ‘wakimtolea utumishi mtakatifu mchana na usiku.’—Ufunuo 7:9, 10, 15, NW.

Mtukuzeni Yehova Milele

19, 20. Ni aina gani mbili za hofu zitakazokuwa wazi katika ‘siku ya Yehova’?

19 Siku tukufu ya kutetewa kwa Yehova yakaribia kwa haraka! “Angalieni, siku ile inakuja, inawaka kama tanuru; na watu wote wenye kiburi, nao wote watendao uovu, watakuwa makapi; na siku ile inayokuja itawateketeza, asema BWANA [Yehova, NW] wa majeshi.” Huo wakati wa msiba mkuu ndio “siku ile ya BWANA [Yehova, NW], iliyo kuu na kuogofya.” (Malaki 4:1, 5) Italeta “kufadhaika” mioyoni mwa waovu, na hao “hawataokolewa.”—Yeremia 8:15; 1 Wathesalonike 5:3.

20 Hata hivyo, watu wa Yehova wanasukumwa na hofu ya aina tofauti. Malaika aliyekabidhiwa “Injili [habari njema, NW] ya milele” amewaalika kwa sauti kubwa, akisema: “Mcheni [hofuni, NW] Mungu, na kumtukuza, kwa maana saa ya hukumu yake imekuja.” (Ufunuo 14:6, 7) Tutaiona hukumu hiyo kwa kicho wakati moto wa Har–Magedoni wenye kuwaka unapoteketeza ulimwengu wa Shetani. Hofu ya Yehova inayofaa itaandikwa mioyoni mwetu isiweze kufutwa. Na tupendelewe basi kujipata wenyewe miongoni mwa wale ‘wenye kuokolewa ambao wameliitia jina la Yehova’!—Yoeli 2:31, 32; Warumi 10:13.

21. Hofu ya Yehova itaongoza kwenye mibaraka gani?

21 Mibaraka mizuri ajabu itafuata, kutia ndani “miaka ya maisha” hadi umilele wote! (Mithali 9:11; Zaburi 37:9-11, 29) Kwa hiyo, kama tumaini letu ni kuurithi Ufalme au kuutumikia katika milki yayo kwenye dunia, acheni tuendelee sasa kumtolea Mungu utumishi mtakatifu tukiwa na hofu ya kimungu na kicho. Acheni tuendelee kulitukuza jina lake takatifu. Kukiwa na tokeo gani lenye baraka? Shukrani ya milele kwamba tulizingatia moyoni shauri lenye hekima la kumhofu Yehova sikuzote!

Ungejibuje?

◻ Ni nini kinachomaanishwa na ‘hofu ya Yehova’?

◻ Hofu ya Mungu iliwanufaishaje watu wake wa kale?

◻ Yesu alituachia kielelezo gani cha hofu ya kimungu?

◻ Twaweza kudumishaje uaminifu wa kimaadili katika hofu ya Yehova?

[Picha katika ukurasa wa 18]

Katika kitabu cha Ufunuo, ndugu za Yesu wanaonwa wakiimba “wimbo wa Musa,” wimbo unaomsifu Yehova

[Picha katika ukurasa wa 20]

Jeshi la Yehoshafati linashinda katika hofu ya Yehova

[Picha katika ukurasa wa 23]

Miaka ya maisha inayoenea hadi umilele wote itakuwa thawabu ya wale wanaomhofu Yehova

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki