Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w92 3/15 kur. 28-31
  • Justin-Mwanafalsafa, Mteteaji, na Shahidi Mfia-Imani

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Justin-Mwanafalsafa, Mteteaji, na Shahidi Mfia-Imani
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mazoezi na Maisha ya Mapema
  • Uchunguzi wa Karibu Zaidi wa Vitabu Vyake
  • Kifo Chake
  • Hadithi Moja ya Uwongo Inatokeza Nyingine
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2009
  • Sehemu ya 3-Je! Wateteaji-Ukristo Walifundisha Fundisho la Utatu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Watetezi wa Imani—Je, Walikuwa Watetezi wa Imani au Wanafalsafa?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2010
  • Nifanye Nini Ikiwa Nina Tatizo la Afya? (Sehemu ya 3)
    Vijana Huuliza
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
w92 3/15 kur. 28-31

Justin-Mwanafalsafa, Mteteaji, na Shahidi Mfia-Imani

“TWAOMBA kwamba mashtaka dhidi ya Wakristo yachunguzwe, na kwamba, ikiwa yaweza kuthibitishwa, wapewe adhabu jinsi wastahilivyo . . . Lakini ikiwa hakuna yeyote awezaye kuwatia hatiani juu ya lolote, kusababu kwa kweli kunawakataza, kwa ajili ya uvumi mbovu, kuwatendea vibaya watu wasio na hatia . . . Kwani, ikiwa mwapata kuijua kweli, kisha hamfanyi lililo haki, mtamtolea Mungu hesabu bila udhuru.”

Kwa maneno hayo, Justin Martyr, aliyedai kuwa Mkristo wa karne ya pili W.K., alitaka rufani kwa maliki Mroma Antoninus Pius. Justin aliomba baraza la kihukumu lenye busara lichunguze maisha na imani za wale waliodai kuwa Wakristo. Ombi hilo la haki lilitoka kwa mtu aliyekuwa na malezi na falsafa yenye kupendeza sana.

Mazoezi na Maisha ya Mapema

Justin alikuwa asiye Myahudi, aliyezaliwa Samaria yapata 110 W.K. katika mji wa Falvia Neapolis, ambao ni Nablus wa siku hizi. Alijiita mwenyewe Msamaria, ingawa yaelekea baba na babu yake walikuwa Waroma au Wagiriki. Malezi yake katika desturi za kipagani, pamoja na kiu yake ya kupata kweli, zilimwongoza kwenye kujifunza falsafa kwa bidii-nyendelevu. Kutotosheka na utafutaji-tafutaji wake miongoni mwa Wastoiko, Waperipatetiki, na Wapithagorea, alifuatia mawazo ya Plato.

Katika kitabu chake kimoja, Justin asema juu ya tamaa yake ya kuongea pamoja na wanafalsafa na asema hivi: “Nilijisalimisha kwa Mstoiko fulani; na nikiwa nimetumia wakati mwingi pamoja naye, nilipokuwa sijatwaa ndani maarifa zaidi juu ya Mungu (kwani yeye mwenyewe hakujua), . . . Nilimwacha na kumwendea mwingine.”—Dialogue of Justin, Philosopher and Martyr, With Trypho, a Jew.

Kisha Justin akamwendea Mperipatekiki aliyependezwa zaidi na pesa kuliko kweli. “Mwanamume huyo, baada ya kunitumbuiza kwa siku chache za kwanza,” asema Justin, “aliniomba nimlipe ada, ili uhusiano wetu usiwe bila faida. Nilimwacha yeye pia kwa sababu hiyo, nikiamini kwamba hakuwa mwanafalsafa hata kidogo.”

Akitamani sana kusikia ile “falsafa bora,” Justin “alimjia Mpithagorea, mashuhuri sana—mwanamume aliyejivunia hekima yake mwenyewe.” Justin asema: “Nilipokuwa na mahoji pamoja naye, nikiwa na nia kuwa msikiaji na mwanafunzi wake, alisema, ‘Nini basi? Una ufahamu wa muziki, astronomia, an jiometria? Je! watazamia kuelewa yoyote ya mambo hayo [ya kimungu] yanayoongoza kwenye maisha yenye furaha, ikiwa hujapata kuarifiwa kwanza mambo [haya]?’ . . . Alinifukuza nilipomwambia siyajui.”

Ingawa alikuwa amevunjika moyo, Justin aliendelea kutafuta-tafuta kweli kwa kuwageukia wale Waplato mashuhuri. Yeye ataarifu hivi: “Kisha nilitumia wakati wangu mwingi iwezekanavyo pamoja na mmoja aliyekuwa amehamia kukaa katika mji wetu—mtu mwenye hekima nyingi, alikuwa na cheo cha juu miongoni mwa Waplato,—na nilifanya maendeleo, na kufanya marekebisho mengi sana kila siku . . . , hivi kwamba katika muda mfupi nilidhani kwamba nilikuwa nimekuwa mwenye hekima; na kumbe huo,” amalizia Justin, “ndio uliokuwa upumbavu wangu.”

Utafutaji-tafutaji wa kweli wa Justin kupitia mikutano pamoja na wanafalsafa ulikuwa wa bure. Lakini alipokuwa akitafakari kwenye ukingo wa bahari, alikutana na Mkristo mmoja mwenye umri mkubwa, “mwanamume mzee fulani, asiyekuwa kwa vyovyote mwenye sura ya kuchukiza, aliyeonyesha upole na tabia zenye kicho.” Mazungumzo yaliyofuata yalielekeza fikira zake kwenye mafundisho ya Biblia ya msingi yaliyokazia uhitaji wa kuwa na maarifa sahihi kuhusu Mungu.—Warumi 10:2, 3.

Yule Mkristo asiyetajwa jina alimwambia Justin: “Muda mrefu kabla ya wakati huu, kulikuwako wanaume fulani wa kale zaidi ya wale wanafalsafa wote wanaostahiwa, ambao . . . walitabiri mambo ambayo yangetukia, na yanayotukia sasa. Waliitwa manabii. Hao peke yao ndio walioona na pia kutangaza kweli kwa watu, . . . wakiwa wamejawa na Roho Takatifu.” Akizidi kumtamanisha Justin, Mkristo huyo alisema hivi: “Maandishi yao yangali yako, na mtu ambaye ameyasoma husaidiwa sana katika maarifa yake kuhusu mwanzo na mwisho wa mambo.” (Mathayo 5:6; Matendo 3:18) Mwanamume huyo mwenye fadhili alipomsihi, Justin aliyachunguza Maandiko kwa bidii-nyendelevu na yaonekana alipata kadiri fulani ya uthamini wayo na wa unabii wa Biblia, kama ionekanavyo katika maandishi yake.

Uchunguzi wa Karibu Zaidi wa Vitabu Vyake

Justin alivutiwa na kutohofu kwa Wakristo walipokabili kifo. Alithamini pia mafundisho ya kweli ya Maandiko ya Kiebrania. Ili kutegemeza hoja zake katika kitabu chake Dialogue With Trypho, Justin alinukuu kutoka Mwanzo, Kutoka, Mambo ya Walawi, Kumbukumbu la Torati, 2 Samweli, 1 Wafalme, Zaburi, Isaya, Yeremia, Ezekieli, Danieli, Hosea, Yoeli, Amosi, Yona, Mika, Zekaria, na Malaki, pamoja na Gospeli. Uthamini wake wa vitabu hivyo vya Biblia waonekana katika mazungumzo yake pamoja na Trypho, ambayo katika hayo Justin alishughulikia na Dini ya Kiyahudi iliyoamini katika Mesiya.

Inaripotiwa kwamba Justin alikuwa mweneza evanjeli, akitangaza rasmi habari njema kwa kila nafasi. Yaelekea, alisafiri sana. Sehemu ya wakati wake ulitumiwa katika Efeso, na yaonekana alikaa katika Roma kwa kipindi kirefu.

Vitabu vya Justin vinatia ndani utetezi mbalimbali ulioandikwa kuutetea Ukristo. Katika kitabu chake First Apology, yeye ajaribu kuondolea mbali ile giza nzito ya falsafa ya kipagani kupitia nuru kutoka kwa Maandiko. Atangaza rasmi kwamba hekima ya wanafalsafa ni bandia na si halisi kwa kutofautisha na maneno na vitendo vya Kristo vyenye nguvu nyingi. (Linganisha Wakolosai 2:8.) Justin atetea Wakristo waliodharauliwa ambao ajitambulisha nao. Baada ya kuongoka kwake, aliendelea kuvaa mavazi ya mwanafalsafa, akisema kwamba alikuwa amepata ile falsafa iliyo ya kweli peke yake.

Kwa ajili ya kukataa kuabudu miungu wa kipagani, Wakristo wa karne ya pili walionwa kuwa wasioamini kuwako kwa Mungu. “Sisi si wasioamini kuwako kwa Mungu,” akapinga Justin, “Tukiwa twamwabudu Mfanyi wa ulimwengu wote mzima . . . mwalimu wetu wa mambo hayo ni Yesu Kristo . . . Yeye ni Mwana wa Mungu wa kweli.” Kuhusu ibada ya sanamu, Justin alisema: “Wao hufanyiza kile waitacho mungu; ambacho sisi huona kuwa si upumbavu tu, bali hata kuwa kumtusi Mungu . . . Ni upumbaziko ulioje! kwamba watu waovu waweze kubuni na kufanyiza miungu kwa ajili ya ibada yenu.”—Isaya 44:14-20.

Kwa kutumia marejezeo kadhaa kutoka kwa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, Justin aonyesha imani yake katika ufufuo, adili za Kikristo, ubatizo, unabii wa Biblia (hasa kuhusu Kristo), na mafundisho ya Yesu. Kuhusu Ufalme wa Mungu, Justin anukuu Isaya, akitaarifu hivi: “Serikali hiyo itakuwa mabegani mwa [Kristo].” Justin aongeza hivi: “Tukitafuta ufalme wa kibinadamu, twapaswa pia kumkana Kristo wetu.” Azungumzia majaribu na wajibu wa Wakristo, ashikilia kwamba utumishi unaofaa kwa Mungu hutaka mtu awe mwenye kufanya mapenzi Yake, na aendelea kusema kwamba “watu wapaswa kutumwa na Yeye katika kila taifa ili kuhubiri mambo hayo.”

Kitabu The Second Apology of Justin (kinachoonwa kuwa mwendelezo tu wa kitabu cha kwanza) kinaelekezwa kwa Bunge la Roma. Justin awasihi Waroma kwa kuwasimulia maono ya Wakristo, walionyanyaswa baada ya kupata maarifa sahihi kuhusu Yesu Kristo. Ubora wa kiadili wa mafundisho ya Yesu, ulioonekana katika mwenendo wa raia Wakristo, ulionekana kutokuwa na thamani yoyote kwa wenye mamlaka ya Kiroma. Badala yake, kudai tu uanafunzi kungaliweza kuwa na matokeo ya kifo. Kuhusu mmoja aliyekuwa mwalimu wa mafundisho ya Kikristo, Justin alinukuu mtu aliyeitwa Lucius, aliyeuliza: “Ni kwa nini umempa mtu huyo adhabu, akiwa si mzinzi, wala mwasherati, wala muuaji, wala mwizi, wala mnyang’anyi, wala mwenye kutiwa hatiani juu ya uhalifu wowote, bali ambaye amedai kwamba aitwa kwa jina Mkristo?”

Kadiri ya chuki isiyo na msingi dhidi ya waliodai kuwa Wakristo kwa wakati huo inaonyeshwa na taarifa hii ya Justin: “Kwa hiyo, mimi pia, hutazamia kufanyiwa njama na kuwekwa kwenye mti, na baadhi ya wale ambao nimetaja, au labda na Crescens, yule mpenda kiburi na kujivuna; kwani mtu ambaye hutoa ushahidi peupe dhidi yetu katika mambo ambayo haelewi, hastahili kupewa jina mwanafalsafa, akisema kwamba Wakristo ni wasioamini kuwako kwa Mungu na hawamheshimu Mungu, na kufanya hivyo ili apate upendeleo wa umati uliodanganywa, na kuwapendeza. Kwani akitufanyia jeuri bila kusoma mafundisho ya Kristo, yeye ni mwovu kabisa, na ni mbaya zaidi ya wasioweza kusoma wala kuandika, ambao huepuka kuzungumza au huendelea kutoa ushahidi bandia kuhusu mambo wasioelewa.”

Kifo Chake

Iwe mikononi mwa Crescens au ya Wasiniki wengine, Justin alishtakiwa kwa mamlaka ya Roma kuwa mwenye kupotosha na akahukumiwa kufa. Katika yapata 165 W.K., alikatwa kichwa katika Roma na akawa “shahidi mfia-imani” (martyr). Kwa hiyo, yeye aitwa Justin Martyr (Justin Shahidi Mfia-Imani).

Mtindo wa kuandika wa Justin huenda ukakosa ule ulaini na busara wa wanaume wengine wasomi wa siku yake, lakini bidii yake kwa ajili ya kweli na uadilifu yaonekana kuwa ya kweli. Kadiri alivyoishi kupatana na Maandiko na mafundisho ya Yesu haiwezi kusemwa kwa uhakika. Hata hivyo, vitabu vya Justin ni vyenye thamani kwa ajili ya mambo ya kihistoria yaliyomo na marejezeo mengi ya Kimaandiko. Vinaandaa mwono-ndani katika maisha na maono ya waliodai kuwa Wakristo wa karne ya pili.

Zenye kutokeza ni jitihada za Justin za kuonyesha maliki ukosefu wa haki wa mnyanyaso ulioelekezwa dhidi ya Wakristo. Kukataa kwake dini na falsafa ya kipagani kwa kupendelea maarifa sahihi ya Neno la Mungu kwatukumbusha kwamba katika Athene mtume Paulo alisema kwa ujasiri kwa wanafalsafa Waepikureo na Wastoiko kuhusu Mungu wa kweli na Yesu Kristo aliyefufuliwa.—Matendo 17:18-34.

Justin mwenyewe alikuwa na sehemu fulani ya maarifa juu ya ufufuo wa wafu wakati wa Mileani. Na lile tumaini la Biblia la ufufuo la kweli ni lenye kuimarisha imani kama nini! Limewategemeza Wakristo wa-napokabili mnyanyaso na limewawezesha wavumilie majaribu makubwa, hata hadi kifo.—Yohana 5:28, 29; 1 Wakorintho 15:16-19; Ufunuo 2:10; 20:4, 12, 13; 21:2-4.

Kwa hiyo, basi, Justin alitafuta kweli na kukataa falsafa ya Kigiriki. Akiwa mteteaji, alitetea mafundisho na mazoea ya waliodai kuwa Wakristo. Na kwa ajili ya kudai kuwa Mkristo mwenyewe, alipata kuwa shahidi mfia-imani. Wenye kutokeza hasa ni ule uthamini wa Justin wa kweli na kutoa kwake ushahidi kwa ujasiri alipokabili mnyanyaso, kwani sifa hizo zinapatikana katika maisha ya wafuasi wa Yesu wa kweli leo.—Mithali 2:4-6; Yohana 10:1-4; Matendo 4:29; 3 Yohana 4.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki