Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w92 4/1 kur. 9-14
  • Kukaribisha kwa Shangwe Ulimwengu Mpya wa Mungu Wenye Uhuru

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kukaribisha kwa Shangwe Ulimwengu Mpya wa Mungu Wenye Uhuru
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kuweka Huru Watu Wake
  • Uhuru wa Kweli Katika Ulimwengu Mpya wa Mungu
  • Elimu ya Tufeni Pote kwa Ajili ya Uhai
  • Uhuru Mkubwa Mbalimbali Hata Sasa
  • Kuweka Wengine Huru Na Dini Bandia
  • Mtafute-Tafute Yehova
  • Yatakayofanywa na Ufalme wa Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
  • Iko Wapi Ile Kweli Inayoweza Kutuweka Huru?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Uhuru wa Kweli Chini ya Utawala wa Ufalme
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Ulimwengu Usio na Vita U Karibu
    Amkeni!—1996
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
w92 4/1 kur. 9-14

Kukaribisha kwa Shangwe Ulimwengu Mpya wa Mungu Wenye Uhuru

“[Mungu] atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena.”—UFUNUO 21:4.

1, 2. Ni nani pekee awezaye kuleta uhuru wa kweli, nasi twaweza kujifunza nini juu Yake kutoka katika Biblia?

HISTORIA imethibitisha ukweli wa yale ambayo Nabii Yeremia alisema: “Njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.” Ni nani pekee awezaye kuelekeza hatua za mwanadamu? Yeremia aliendelea kusema: “Ee BWANA [Yehova, NW], unirudi.” (Yeremia 10:23, 24) Naam, ni Yehova pekee awezaye kuleta uhuru wa kweli kutoka katika matatizo yanayosumbua familia ya kibinadamu.

2 Biblia ina mifano mingi kuonyesha uwezo wa Yehova wa kuleta uhuru kwa wale wamtumikiao. “Yote yaliyotangulia kuandikwa yaliandikwa ili kutufundisha sisi; ili kwa saburi na faraja ya maandiko tupate kuwa na tumaini.” (Warumi 15:4) Hukumu za Yehova dhidi ya dini bandia ziliandikwa pia, nazo hutumika kuwa ‘onyo kwetu sisi, tuliofikiliwa na miisho ya zamani.’—1 Wakorintho 10:11.

Kuweka Huru Watu Wake

3. Yehova alionyeshaje uwezo wake wa kuweka huru watu wake katika Misri?

3 Mfano wa uwezo wa Mungu wa kutekeleza hukumu dhidi ya ibada bandia na kuweka huru wale ambao hufanya mapenzi yake ulitukia wakati watu wake wa nyakati za kale walipotiwa utumwani katika Misri. Kutoka 2:23-25 husema: “Kilio chao kikafika juu kwa sababu ya ule utumwa. Mungu akasikia kuugua kwao . . . na Mungu akawaangalia.” Katika wonyesho wenye kutia hofu wa ukuu wake upitao miungu bandia ya Misri, Mungu Mwenye Uweza Wote alileta mapigo kumi juu ya taifa hilo. Kila pigo lilikusudiwa kuaibisha mungu tofauti wa Misri, kuonyesha kwamba miungu hiyo ilikuwa bandia, isiyo na uwezo wa kusaidia Wamisri walioiabudu. Hivyo Mungu akaweka watu wake huru na kumwangamiza Farao na majeshi yake katika Bahari Nyekundu.—Kutoka, sura ya 7 hadi ya 14.

4. Kwa nini haikuwa ukosefu wa haki kwa upande wa Mungu kutekeleza hukumu zake dhidi ya Wakanaani?

4 Wakati Mungu alipowaleta Waisraeli katika Kanaani, wakaaji wayo wenye kuabudu mashetani waliangamizwa na nchi ikapewa kwa watu wa Mungu. Akiwa ndiye Mwenye Enzi Kuu wa Ulimwengu Wote Mzima, Yehova ana haki ya kutekeleza hukumu zake juu ya dini zenye upotovu. (Mwanzo 15:16) Na kuhusu dini ya Kikanaani, Bible Handbook cha Halley husema hivi: “Ibada ya . . . miungu ya Kikanaani ilitia ndani sherehe zilizopotoka zaidi; mahekalu yao yalikuwa vitovu vya uovu. . . . Wakanaani waliabudu mbele ya miungu yao, kwa kujitia sana katika ukosefu wa adili, ikiwa sherehe ya kidini; kisha, kwa kuua kimakusudi watoto wao wazaliwa wa kwanza, wawe dhabihu kwa miungu iyo hiyo. Yaonekana kwamba, kwa kadiri kubwa, nchi ya Kanaani ilikuwa imekuwa namna ya Sodoma na Gomora kwa kadiri ya taifa zima.” Mtungaji huyo huongeza: “Je! ustaarabu mchafu wenye kuchukiza na wa kinyama hivyo ulikuwa na haki ya kuendelea kuwako? . . . Waakiolojia ambao huchimbua kwenye magofu ya majiji ya Kikanaani hustaajabu kwa nini Mungu hakuwaangamiza mapema zaidi ya wakati alipofanya hivyo.”

5. Tendo la Mungu la kuweka huru watu wake wa kale linatumikaje kuwa kigezo kwa wakati wetu?

5 Masimulizi hayo ya Mungu akichukua hatua dhidi ya ibada bandia, akiwaweka huru watu wake wa agano, na kuwaandalia nchi ya ahadi hutumika kuwa kigezo cha mambo yajayo. Yalielekeza kwenye wakati ujao ulio karibu sana ambapo Mungu ataponda-ponda dini bandia za ulimwengu huu na waungaji-mkono wazo na kuongoza watu wake wa ki-siku-hizi waingie katika ulimwengu mpya wenye uadilifu. —Ufunuo 7:9, 10, 13, 14; 2 Petro 3:10-13.

Uhuru wa Kweli Katika Ulimwengu Mpya wa Mungu

6. Ni nini baadhi ya uhuru mbalimbali wa ajabu ambao Mungu ataandaa katika ulimwengu mpya?

6 Katika ulimwengu huo mpya, Mungu atabariki watu wake kwa zile pande nzuri ajabu za uhuru ambao amekusudia familia ya kibinadamu iwe nao. Kutakuwako kuwekwa huru na uonevu wa kisiasa, kiuchumi, na kidini bandia. Kutakuwako kuwekwa huru na dhambi na kifo, watu wakiwa na taraja la kuishi milele duniani. “Wenye haki watairithi nchi [dunia, NW], nao watakaa humo milele.”—Zaburi 37:29; Mathayo 5:5.

7, 8. Katika kupata afya kamili ni nini kitakachoonwa katika ulimwengu mpya?

7 Upesi baada ya ulimwengu huo mpya kuletwa, wakaaji wao watarudishwa kimwujiza kwenye afya kamilifu. Ayubu 33:25 husema: “Nyama ya mwili wake itakuwa laini kuliko ya mtoto; huzirudia siku za ujana wake.” Isaya 35:5, 6 huahidi hivi: “Ndipo macho ya vipofu yatafumbuliwa, na masikio ya viziwi yatazibuliwa. Ndipo mtu aliye kilema ataruka-ruka kama kulungu, na ulimi wake aliye bubu utaimba.”

8 Nyinyi wenye maradhi ya kimwili kwa sababu ya uzee au afya mbaya, jiwazieni mki-wa katika ulimwengu huo mpya, mkiamka kila siku mkiwa na afya na nguvu. Makunyanzi yametoweka kuachia nafasi ngozi laini, yenye afya—hakuna haja tena ya mafuta ya ngozi. Macho yako yenye kufifia au kupofuka yanarudishiwa uwezo kamili wa kuona—hakuna haja tena ya miwani. Uwezo kamili wa kusikia umerudishwa—tupilia mbali vidude hivyo vya kusaidia kusikia. Viungo vilivyolemaa vyarudishiwa afya na uzima—ondolea mbali hiyo mikwaju, mikongojo, na viti vyenye magurudumu. Hakuna magonjwa tena—tupilia mbali dawa hizo. Hivyo, Isaya 33:24 hutabiri hivi: “Hapana mwenyeji atakayesema, Mimi mgonjwa.” Yeye pia asema: “Watapata kicheko na furaha, huzuni na kuugua zitakimbia.”—Isaya 35:10.

9. Vita itakomeshwaje milele?

9 Hapana yeyote atakayekuwa dhabihu ya vita tena. “[Mungu] avikomesha vita hata mwisho wa dunia; avunja uta, akata mkuki, achoma moto magari.” (Zaburi 46:9) Silaha za vita hazitaruhusiwa tena kamwe na Mtawala wa Ufalme wa Mungu, Kristo Yesu, ambaye Isaya 9:6, NW, humwita “Mwana-Mfalme wa Amani.” Mstari wa 7, NW, huongeza hivi: “Kwa wingi wa utawala wa kimwana-mfalme na kwa amani kutakuwa hakuna mwisho.”

10, 11. Amani kamili itamaanisha nini kwa dunia?

10 Itakuwa baraka kama nini kwa wanadamu, na kwa dunia hii, kutokuwa na silaha za vita! Kwani, hadi leo hii, silaha zilizotumiwa kwenye vita vya wakati uliopita zingali zinaangamiza watu. Katika nchi moja, Ufaransa, jumla ya wataalamu zaidi ya 600 wa kutegua makombora wameuawa tangu 1945 walipokuwa wakijaribu kutegua baruti zilizobaki baada ya vita vya wakati uliopita. Kiongozi wa idara ya kutegua makombora katika Ufaransa alisema: “Sisi tungali twapata risasi za mviringo za mizinga ziwezazo kulipuka za tangu Vita ya 1870 kati ya Ufaransa na Prussia. Kuna maziwa ya maji ambayo yamejaa gruneti zenye sumu za tangu Vita ya Ulimwengu ya 1. Pindi kwa pindi, mkulima akiwa katika tingatinga hukanyaga baruti za tangu Vita ya Ulimwengu ya 2 naye alipuliwa pu! Vitu hivyo viko kila mahali.” Miaka miwili iliyopita gazeti The New York Times lilitoa maelezo haya: “Katika ile miaka 45 tangu mwisho wa Vita ya Ulimwengu ya 2 [idara za kutegua makombora] zimeondolea udongo wa [Ufaransa] risasi za mizinga milioni 16, makombora 490,000 na baruti za chini ya maji 600,000. . . . Mamilioni ya hekta yangali yamezungushiwa ua, yakiwa na silaha zenye kina cha kufika magotini na yakiwa yamezungukwa na ishara zenye kuonya hivi: ‘Usiguse. Inaua!’”

11 Ulimwengu mpya utakuwa tofauti kama nini! Kila mtu atakuwa na makao bora, chakula tele, na kazi yenye maana na yenye kuridhisha ya kugeuza dunia yote iwe paradiso. (Zaburi 72:16; Isaya 25:6; 65:17-25) Watu na dunia yenyewe hawatakumbwa-kumbwa tena kamwe na mamilioni ya vidude vyenye kulipuka. Ulimwengu mpya kama huo ndio Yesu alikuwa akifikiria alipomwambia mwanamume aliyeonyesha imani kwake yeye: “Utakuwa pamoja nami katika Paradiso.”—Lk. 23:43, ZSB.

Elimu ya Tufeni Pote kwa Ajili ya Uhai

12, 13. Ni kazi gani ya kielimu ya tufeni pote ambayo Yesu na Isaya walitabiri kwa wakati wetu?

12 Mtu ajifunzapo juu ya ulimwengu mpya wa Mungu, yeye hujifunza pia kwamba katika siku zetu, Yehova ametokeza kundi la ulimwenguni pote lililopangwa kitengenezo kwa ajili ya ibaada ya kweli. Litakuwa ndicho kiini cha ulimwengu mpya, naye Mungu analitumia sasa kufundisha wengine makusudi yake. Tengenezo hilo la Kikristo linafanya kazi ya kielimu ya tufeni pote ya namna na ukubwa ambao haujapata kuonwa tena katika historia. Yesu aliitabiri kwamba hiyo ingefanywa. Yeye alisema: “Na habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa kwa ajili ya ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo mwisho utakuja.”—Mathayo 24:14, NW.

13 Isaya pia alisema juu ya kazi hii ya kielimu ya tufeni pote. “Na itakuwa katika siku za mwisho [tunamoishi sasa], mlima wa nyumba ya BWANA [Yehova, NW; ibada yake safi iliyoinuliwa] utawekwa imara . . .; na mataifa yote watauendea makundi makundi. Na mataifa mengi watakwenda na kusema, Njoni, twende juu mlimani kwa BWANA [Yehova, NW], . . . naye atatufundisha njia zake, nasi tutakwenda katika mapito yake.”—Isaya 2:2, 3.

14. Twaweza kuwatambuaje watu wa Mungu leo?

14 Kwa hiyo, ile kazi ya tufeni pote ya kutoa ushahidi juu ya Ufalme wa Mungu ni ushuhuda wenye nguvu kwamba sisi tuko karibu na mwisho wa mfumo mbovu wa mambo, na kwamba uhuru wa kweli unakaribia. Wale wanaotembelea watu wakiwa na ujumbe huu wenye kujaa tumaini la ulimwengu mpya wa Mungu wanaelezwa kwenye Matendo 15:14 kuwa ‘watu kwa ajili ya jina la Mungu.’ Ni nani wanaolichukua jina la Yehova na kutoa ushuhuda wa tufeni pote juu ya Yehova na Ufalme wake? Maandishi ya Kihistoria ya karne hii ya 20 hujibu: ni Mashahidi wa Yehova pekee. Leo hesabu yao inazidi milioni nne katika makundi zaidi ya 66,000 kotekote ulimwenguni.—Isaya 43:10-12; Matendo 2:21.

15. Kwa habari ya mambo ya kisiasa, twaweza kutambuaje watumishi wa kweli wa Mungu?

15 Ushuhuda mwingine kwamba Mashahidi wa Yehova wanatimiza unabii wa Biblia juu ya kazi ya kuhubiri Ufalme waonyeshwa katika Isaya 2:4. “Nao watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu, taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe.” Kwa hiyo wale wanaofanya kazi ya tufeni pote ya kuhubiri juu ya utawala wa Ufalme wa Mungu lazima ‘wasijifunze vita tena.’ Yesu alisema kwamba lazima ‘wasiwe sehemu ya ulimwengu.’ (Yohana 17:16,) Hiyo yamaanisha kwamba lazima wasiwemo kabisa katika mambo ya kisiasa, wasijiunge na upande wowote katika mizozano na vita vya mataifa. Ni nani ambao si sehemu ya ulimwengu na hawajifunzi vita tena kamwe? Kwa mara nyingine tena, maandishi ya kihistoria ya karne ya 20 hushuhudia: ni Mashahidi wa Yehova pekee.

16. Kazi ya Mungu ya kielimu ya tufeni pote itakuwa kamili kadiri gani?

16 Kazi hii ya kielimu ya tufeni pote ya Mashahidi wa Yehova itaendelea hata baada ya Mungu kukomesha ulimwengu huu mwovu uliopo. Isaya 54:13 hutaarifu hivi: “Na watoto wako wote watafundishwa na BWANA [Yehova, NW].” Kazi hii ya kufundisha itakuwa kamilifu sana hivi kwamba Isaya 11:9 hutabiri hivi: “Dunia itajawa na kumjua BWANA [Yehova, NW], kama vile maji yanavyoifunika bahari.” Mafundisho yenye kuendelea yatahitajiwa si kwa wale tu watakaookoka mwisho wa ulimwengu huu wa kale na watoto ambao huenda watazaliwa katika ulimwengu huo mpya, kufundishwa bali pia mabilioni ambao watarudi kwenye uhai katika ufufuo. Hatimaye, kila mtu anayeishi duniani atafundishwa kutumia hiari yake ifaavyo ndani ya mipaka ya sheria za Mungu. Matokeo yatakuwaje? “Wenye upole watairithi nchi [dunia,NW], watajifurahisha kwa wingi wa amani.”—Zaburi 37:11.

Uhuru Mkubwa Mbalimbali Hata Sasa

17. Musa aliwaambia watu wa Mungu wa kale wafanye nini?

17 Waisraeli wa kale walipokuwa karibu sana kuingia katika Nchi ya Ahadi, Musa aliongea nao akawaambia hivi: “Angalieni nimewafundisha amri na hukumu, vile vile kama BWANA [Yehova, NW], Mungu wangu, alivyoniamuru, ili mzitende katika nchi mwingiayo ili kuimiliki. Zishikeni basi, mkazitende, maana hii ndiyo hekima yenu na akili zenu, machoni pa mataifa watakaozisikia amri hizi zote, nao watasema, Hakika taifa hili kubwa ni watu wenye hekima na akili. Kwa maana liko taifa gani kubwa, lililo na Mungu aliye karibu nao, kama BWANA [Yehova, NW], Mungu wetu, alivyo, kila tumwitapo? Tena liko taifa gani kubwa, lililo na amri na hukumu zenye haki kama torati hii yote, ninayoiweka mbele yenu leo.”—Kumbukumbu la Tolati 4:5-7.

18. Ni uhuru gani mkubwa mbalimbali ambao huwajia hata sasa wale wanaomtumikia Mungu?

18 Leo mamilioni ambao huabudu Yehova wako pia karibu sana kuingia katika nchi ya ahadi—ule ulimwengu mpya. Kwa sababu wao hutii sheria za Mungu, wako naye akiwa karibu nao nao wanatofautishwa na vikundi vingine vyote vya watu. Tayari Mungu amewaweka huru na mawazo bandia ya kidini, ubaguzi wa rangi, matumizi haramu ya dawa za kulevya, utukuzo wa taifa, vita, na mweneo mkubwa wa maradhi yenye kuambukizwa kingono. Zaidi ya hilo, yeye amewaunganisha katika udugu wenye upendo wa kimataifa usioweza kuvunjwa. (Yohana 13:35) Wao hawasumbukii wakati ujao bali ‘waimba kwa furaha ya moyo.’ (Isaya 65:14) Ni uhuru mkubwa kama nini wanaofurahia hata sasa kwa kutumikia Mungu akiwa Mtawala!—Matendo 5:29, 32; 2 Wakorintho 4:7; 1 Yohana 5:3.

Kuweka Wengine Huru Na Dini Bandia

19, 20. Watu wanawekwaje huru kwa njia ya mafundisho ya Biblia kuhusu hali ya wafu?

19 Wengi ambao Mashahidi wa Yehova huhubiria wanakuja pia kupata uhuru huo. Kwa mfano, katika nchi ambako ibada ya wazazi wa kale waliokufa huendelezwa, Mashahidi wa Yehova wanajulisha kwa wengine kwamba wafu hawako hai mahali popote na hawawezi kuumiza walio hai. Mashahidi huelekeza kwenye Mhubiri 9:5, ambalo hutaarifu kwamba “walio hai wajua kwamba watakufa; lakini wafu hawajui neno lo lote.” Wao huelekeza pia kwenye Zaburi 146:4, ambalo husema kwamba mtu afapo yeye “huurudia udongo wake, siku hiyo mawazo yake yapotea.” Kwa hiyo Biblia huonyesha kwamba hakuna roho ya namna ya kimzuka au nafsi isiyoweza kufa ya kufanya maponyo au kuogopesha sana walio hai. Hivyo, hakuna haja ya kupoteza pesa zilizochumwa kwa jasho ili kununua utumishi mbalimbali wa wachawi au wa padri apatanishe.

20 Maarifa hayo sahihi ya Biblia huweka watu huru na mafundisho bandia ya moto wa mateso na purgatori. Watu wajifunzapo kweli ya Biblia kwamba wafu hawana fahamu, ni kana kwamba wako katika usingizi mzito, hawawi na wasiwasi tena wakitaka kujua ni jambo gani limewapata wapendwa wao waliokufa. Badala ya hivyo, wao hutazamia ule wakati mzuri ajabu ambao mtume Paulo alinena juu yao aliposema: “Kutakuwa na ufufuo wa wafu, wenye haki na wasio haki pia.”—Matendo 24:15.

21. Ni nani ambao bila shaka watatiwa miongoni mwa wale watakaofufuliwa, na yaelekea itikio lao litakuwaje?

21 Katika ufufuo huo, wafu watarudi kwenye uhai katika dunia ambamo watakuwa wamewekwa huru milele na kifo kilichorithiwa kutoka kwa Adamu. Bila shaka wale watakaofufuliwa ni pamoja na watoto waliotolewa dhabihu kwa miungu ya Kikanaani, kama vile Moleki, vijana waliotolewa dhabihu kwa miungu ya Azteki, na mamilioni wasiohesabika waliotolewa kuwa dhabihu kwa mungu wa vita. Hao ambao hapo kwanza walikuwa mateka wa imani hizo bandia watashangaa na kufurahi kama nini! Ndipo wafufuliwa hao wataweza kujulisha wazi kwa furaha: ‘Ewe mauti, ya wapi mapigo yako? ewe kaburi ku wapi kuharibu kwako?’—Hosea 13:14.

Mtafute-Tafute Yehova

22. Tukitaka kuishi katika ulimwengu mpya wa Mungu, twahitaji kukumbuka nini?

22 Je! wewe wataka kuishi katika ulimwengu mpya wa Mungu wenye uadilifu, ambamo uhuru wa kweli utakuwa? Ikiwa ndivyo, basi zingatia maneno kwenye 2 Nyakati 15:2: ‘BWANA [Yehova, NW] yu pamoja nawe, ukiwa pamoja naye; nawe ukimtafuta ataonekana kwako; lakini ukimwacha atakuacha wewe.’ Na kumbuka kwamba jitihada zako za unyofu za kujifunza juu ya Mungu na za kumpendeza hazitakosa kuonwa. Waebrania 11:6 husema kwamba Mungu “huwapa thawabu wale wamtafutao.” Na Warumi 10:11 husema: “Kila amwaminiye hatatahayarika.”

23. Kwa nini yatupasa kukaribisha kwa shangwe ulimwengu mpya wa Mungu wenye uhuru?

23 Penye upeo wa macho tu pana ulimwengu mpya wa Mungu wenye uhuru wa kweli. Humo “viumbe vyenyewe navyo vitawekwa huru na kutolewa katika utumwa wa uharibifu, hata viingie katika uhuru wa utukufu wa watoto wa Mungu.” Naye “[Mungu] atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena.” (Warumi 8:21; Ufunuo 21:4) Ndipo, watumishi wote wa Yehova watakapoweza kuinua vichwa vyao na kukaribisha kwa shangwe ulimwengu mpya wa Mungu wenye uhuru kwa kupaaza sauti, ‘Asante, Yehova, kwa uhuru wa kweli hatimaye!’

Wewe Ungejibuje?

◻ Yehova alionyeshaje uwezo wake wa kuweka huru watu wake?

◻ Ni uhuru gani mbalimbali wa ajabu utakaokuwako katika ulimwengu mpya wa Mungu?

◻ Yehova anaelimishaje watu kwa ajili ya uhai?

◻ Ni baadhi ya uhuru gani mbalimbali ambao watu wa Mungu wanafurahia hata sasa kwa kutumikia Yehova?

[Picha katika ukurasa wa 10]

Yehova alionyesha ukuu wake juu ya miungu bandia ya Misri, akawakomboa waabudu wake

[Picha katika ukurasa wa 12, 13]

Leo, watumishi wa kweli wa Mungu wanatambuliwa kwa kutimiza kazi yake ya kielimu ya tufeni pote na kubeba jina lake

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki