Wapiga Mbiu ya Ufalme Waripoti
Kueneza Eneo Lililo Peke Yalo Katika Paraguai Kwazaa Tunda
TAWI la Paraguai la Watch Tower Society linajua kabisa uhitaji wa kuhubiri habari njema za Ufalme katika eneo lalo lote. (Matendo 1:8) Huu ndio wakati kwa wote kujifunza juu ya Ufalme na kutumikia Yehova kabla hajaleta mwisho wa mfumo huu mwovu katika ile “dhiki kubwa” inayokuja. (Mathayo 24:21, 22) Maono yafuatayo yaonyesha yale yanayofanywa kusaidia watu katika maeneo yasiyogawiwa kundi. Tawi laripoti hivi:
Mipango ilifanywa kueneza eneo lote lisilogawiwa mtu kwa njia ya mapainia wa pekee wa muda. Wakati wa miezi ya Novemba hadi Januari ya mwaka wa utumishi wa 1990, akini ndugu na dada 39 walieneza jumla ya majiji na miji midogo mia moja ambako kufikia wakati huo hakukuwa wahubiri wa Ufalme. Waliweza kugawanya vitabu 6,119, vijitabu 4,262, na magazeti 5,144. Likiwa tokeo la utendaji huo, vikundi vipya vya wahubiri vinafanyizwa.
◻Mwanamke mmoja alikubali kutoka kwa dada mmoja painia alipokuwa akifanya kazi katika eneo lisilogawiwa mtu kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani. Painia huyo alijitolea kuongoza funzo la Biblia pamoja naye, naye mwanamke huyo akakubali kwa furaha. Painia aliporudi, bibi huyo na pia mume wake na watoto wao kumi walikuwa wakimngoja. Katika ziara iliyofuata, familia hiyo pamoja na rafiki na jirani zao walikuwa tayari kwa funzo! Mwanamke huyo alikuwa amewaalika, akisema kwamba funzo lilikuwa zuri sana na kwamba tumaini na baraka ambazo Yehova hutoa zilikuwa nzuri ajabu. Hilo lilikuwa jambo ambalo hapana mtu aliyekuwa amepata kumwambia hapo mbele, kwa hiyo alihisi kwamba jirani na rafiki zake wapasa pia kusikia habari hizo njema.
Kila wakati painia huyo alipoongoza funzo, walikuwapo wengi sana waliohudhuria hivi kwamba ilionekana kama kundi dogo. Watu hao wenye kupendezwa waliuliza maswali mengi na kushiriki katika funzo. Wakati painia huyo alipoeleza kwamba mara eneo hilo likiisha fanyiwa kazi, yeye na waandamani wake wangelazimika kusonga mbele kwenye eneo jipya, bibi huyo akauliza kwa wasiwasi ingekuwaje kwao. Mipango ilifanywa pamoja na ndugu kutoka kundi lililo karibu zaidi ili funzo liendelezwe. Sasa mapainia wa pekee wamepewa mgawo wasaidie watu hao wenye kupendezwa, wa mfano wa kondoo.
◻Alipokuwa akienda nyumba kwa nyumba katika eneo jingine lisilogawiwa kundi, dada mmoja painia alimpata mwanamume mmoja ambaye miaka 10 iliyopita alikuwa amepata kitabu Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele. Tangu wakati huo alikuwa amepoteza mawasiliano na Mashahidi wa Yehova. Hata hivyo, yeye alijua kwamba Yehova, ambaye alimwita Yehova wa majeshi, ndiye Mungu pekee wa kweli na kwamba Yeye pekee apasa kuabudiwa. Kwa kuchukua hatua yeye mwenyewe, alikuwa akiongea juu ya Yehova na kila mtu ajuaye. Kwa kweli, kila juma alikuwa akienda kwa miguu kilometa tatu kutembelea mume na mke wenye kupendezwa ili kuongea nao juu ya Mungu kwa sababu, kama vile yeye mwenyewe alivyolisema jambo hilo, ‘Nikiacha kuwatembelea, watamsahau Yehova.’ Kuongezea mume na mke hao, walikuwako wengine wapatao kumi waliotaka funzo la Biblia—yote hayo kwa sababu mwanamume huyu mwenye kupendezwa aliwahubiria.
Kwa kutokeza, siku chache tu kabla ya painia huyo kumtembelea, mtu uyo huyo alikuwa amekataa kumruhusu padri wa mahali hapo na kundi lake lenye kuandamana wasiingie nyumba yake wakiwa na sanamu ya bikira, akieleza kwamba yeye hakuamini katika sanamu. Padri huyo akawa mwenye hasira kali. Usiku huo mwanamume huyo alisali kwa Yehova apate msaada. Hivyo wazia jinsi alivyosisimuka na kufurahi painia huyo alipomtembelea! Mipango ilifanywa mara moja kuwe na funzo la Biblia lenye kufanywa kwa utaratibu, naye mwanamume huyo azidi kufanya maendeleo akishirikiana na tengenezo la kitheokrasi.
Kweli kweli, Yehova anabariki kazi ya kukusanya ndani katika Paraguai huku akina ndugu wakijitahidi kutoa ushahidi kamili katika maeneo hayo yasiyogawiwa mtu.—Mathayo 24:14.