Yehova Alitutunza Chini ya Marufuku—Sehemu ya 1
Kwa miongo kadhaa Mashahidi wa Yehova wametaka kujua kuhusu ndugu zao katika nchi ambako utendaji wao wa Kikristo ulikuwa umezuiwa. Tunafurahi kutoa ya kwanza kati ya makala tatu zinazofunua baadhi ya mambo yaliyotukia. Haya ni masimulizi ya kibinafsi ya Wakristo waaminifu katika ile iliyoitwa wakati huo Ujerumani Mashariki.
KATIKA 1944, nilikuwa mfungwa wa vita Mjerumani katika gereza, nikifanya kazi nikiwa mtumishi wa hospitali katika kambi la Kemnak, karibu na Ayr, Uskochi. Niliruhusiwa kutoka kambini, ingawa kufanya urafiki na watu wa huko kulizuiliwa. Nilipokuwa nikitembea polepole Jumapili moja, nilikutana na mtu aliyejitahidi sana kunieleza mambo kutoka kwa Biblia. Baadaye tulikuwa tukitembea pamoja mara nyingi.
Baadaye alinialika kwenye mkutano katika nyumba fulani. Hilo lilikuwa jambo la hatari kwa upande wake, kwa kuwa nilikuwa mshiriki wa taifa la adui. Wakati huo sikutambua ya kwamba alikuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova—mkutano huo kwa wazi ulikuwa kimojawapo vikundi vyao vidogo vya funzo la Biblia. Ingawa sikuwa naelewa mengi sana, nakumbuka kwa wazi picha ya mtoto mwenye vazi refu jeupe, pamoja na simba na kondoo. Picha hiyo ya ulimwengu mpya, kama ilivyoelezwa katika kitabu cha Biblia cha Isaya, ilinivutia sana.
Katika Desemba 1947, niliachiliwa kutoka kambi ya gereza. Niliporudi nyumbani Ujerumani, nilimwoa Margit, ambaye nilikuwa nimemjua kabla ya vita. Tulifanya makao yetu katika Zittau, karibu na mipaka ya Polandi na Chekoslovakia. Katika siku chache, mmoja wa Mashahidi wa Yehova alibisha mlangoni petu. “Ikiwa kikundi hiki ndicho kile kile nilichokutana nacho katika Uskochi,” nikamwambia mke wangu, “basi ni lazima tuungane nao.” Juma hilo hilo, tulihudhuria mkutano wetu wa kwanza pamoja na Mashahidi.
Katika Biblia, tulijifunza upesi uhitaji wa kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida na kushiriki katika kazi ya kuhubiri. Kwa kweli, yale ambayo Mashahidi walifundisha kutoka kwa Biblia yakawa upesi jambo la maana zaidi maishani mwetu. Baadaye nilianza kuongoza kikundi cha funzo la Biblia. Kisha, katika Februari 1950, waangalizi wasafirio wawili waliuliza: “Je! hamtaki kuzamishwa wakati wowote?” Alasiri hiyo hiyo Margit na mimi tukaonyesha wakfu wetu kwa Mungu kwa ubatizo.
Mwanzo wa Taabu
Zittau ilikuwa katika eneo la Ujerumani la Sovieti, na jitihada za kuwaletea Mashahidi wa Yehova taabu zilikuwa zimeanza katika 1949. Ni baada tu ya ugumu mwingi ndipo vifaa vilipoweza kupatikana kwa ajili ya kusanyiko dogo katika Bautzen. Halafu, wakati wa kiangazi, mpango wa kupata magari-moshi ya pekee kwa ajili ya mkusanyiko wa wilaya mkubwa zaidi katika Berlin ulifutwa kwa ghafula. Hata hivyo maelfu walihudhuria.
Mikutano ya kundi ilisumbuliwa pia. Watu wasumbufu wangehudhuria ili tu kupaaza sauti na kupiga mbinja. Kwenye pindi moja tulikuwa karibu tulazimike kukomesha hotuba ya mwangalizi asafiriye. Vyombo vya habari vilituita manabii wa mambo mabaya. Makala za magazeti ya habari zilidai kwamba tulikuwa tumekusanyika kwenye vilele vya vilima tukingojea kuchukuliwa katika mawingu. Magazeti pia yalinukuu wasichana fulani wakisema kwamba Mashahidi walijaribu kufanya uasherati pamoja nao. Lile elezo kwamba ‘wale wafanyao wakfu kwa Yehova wangepokea uhai wa milele’ uligeuzwa kusema kwamba wale waliofanya ngono pamoja na Mashahidi wangepata uhai wa milele.
Baadaye tulishtakiwa kuwa wachochezi wa vita. Yale tuliyosema kuhusu vita ya Mungu ya Har–Magedoni yalifasiriwa vibaya kumaanisha kwamba tulitia moyo kule kushindania kuunda silaha na vita. Upuzi ulioje! Hata hivyo, katika Agosti 1950, nilipowasili ili kufanya zamu ya usiku katika kampuni ya gazeti la habari la mji huo nilikofanyia kazi nikiwa mchapishaji, nilisimamishwa langoni. “Umefutwa kazi,” akasema mlinzi, ambaye polisi aliandamana naye. “Ninyi watu mnaunga mkono vita.”
Huko nyumbani, Margit alitulizika. “Hakuna tena kazi ya usiku,” akasema. Hatukuwa na wasiwasi. Upesi nilipata kazi nyingine. Tulimtumaini Mungu atuandalie, na alifanya hivyo.
Kazi Yetu Yapigwa Marufuku
Agosti 31, 1950, utendaji wa Mashahidi wa Yehova katika Jamhuri ya Kidemokrasi ya Ujerumani ulipigwa marufuku. Wimbi la kukamatwa likafuata. Mashahidi walijaribiwa, wengine wakipata vifungo vya maisha. Wawili kutoka Zittau, waliokuwa wameteseka katika kambi za mateso chini ya Wanazi, walitiwa kifungoni na Wakomunisti.
Yule aliyekuwa mwangalizi wa kundi letu alikamatwa pamoja na mke wake. Wale waliowakamata waliwaacha watoto wao wachanga wawili peke yao nyumbani wajitunze wenyewe. Babu na nyanya kutoka kwa upande wa mama waliwachukua watoto hao, na leo wasichana hao wawili ni wenye bidii katika kuambia wengine juu ya Ufalme wa Mungu.
Wajumbe kutoka makundi katika Ujerumani Mashariki walisafiri kwenda hadi Berlin na kurudi ili kuchukua vichapo kutoka mahali pa kuchukulia katika sehemu huru ya magharibi. Wengi wa wajumbe hao wenye moyo mkubwa walikamatwa, wakaletwa mahakamani, na kupewa hukumu za vifungo.
Wenye mamlaka waliwasili mapema asubuhi moja ili kupekuapekua nyumba yetu. Tulikuwa tumetazamia kuja kwao, kwa hiyo nilikuwa nimeweka rekodi zote za kundi, nilizokuwa ninaweka, katika ghala letu la nafaka, karibu na kiota cha duduvule. Wadudu hao hawakunisumbua mimi, lakini wanaume hao walipoanza kupekuapekua mahali hapo, kwa ghafula walifunikwa na wingu la waduduvule. Lile tu ambalo wanaume hao wangeweza kufanya ni kukimbia ili kupata usalama!
Yehova alikuwa ametutayarisha kwa ajili ya marufuku kwa njia ya mikusanyiko iliyofanywa katika 1949. Programu ilikuwa imetusihi tuzidishe funzo la kibinafsi, kuhudhuria mikutano, na utendaji wetu wa kuhubiri, pamoja na kutegemeana kwa ajili ya utegemezo na kitia-moyo. Hilo lilitusaidia kweli kweli kubaki waaminifu-washikamanifu. Hivyo, hata ingawa watu mara nyingi walituchambua na kutulaani, hatukuruhusu hilo lituathiri vibaya.
Kufanya Mikutano Chini ya Marufuku
Baada ya tangazo la marufuku, nilikutana na Mashahidi wenzangu wawili ili kuzungumza jinsi ya kuendeleza mikutano yetu ya kundi. Kuhudhuria kulikuwa hatari, kwa kuwa kukamatwa ukiwapo kungeweza kumaanisha hukumu ya kifungo. Tuliwatembelea Mashahidi katika eneo letu. Wengine wao walikuwa na wasiwasi, lakini ilitia moyo kwamba kila mmoja alitambua uhitaji wa kuhudhuria mikutano.
Mtu mwenye kupendezwa aliyekuwa na ghala ya nafaka aliitoa ili itumiwe kuwa mahali pa kukutania. Ingawa ilikuwa katika uwanja, mahali ambapo wote wangeweza kuona, ghala hiyo ilikuwa na mlango wa nyuma uliofunguka kwenye kijia kilichofichwa na vichaka. Kwa hiyo kuja na kwenda kwetu hakukuonekana. Muda wote wa kipupwe ghala hiyo ya zamani iliandaa mahali pa mikutano yetu iliyofanywa kwa nuru ya mishumaa, watu karibu 20 wakihudhuria. Tulikutana kila juma kwa ajili ya funzo letu la gazeti la Mnara wa Mlinzi na kwa ajili ya Mkutano wa Utumishi. Programu ilibadilishwa kulingana na hali zetu, ikikazia kwamba tulipaswa kuendelea kuwa wenye kutenda kiroho. Upesi tulisisimuka kumkaribisha mtu uyo huyo mwenye kupendezwa akiwa ndugu yetu mpya katika kweli.
Katika miaka ya katikati ya 1950, hukumu za mahakama zikawa afadhali zaidi, na ndugu wengine waliachiliwa kutoka gerezani. Wengi walihamishiwa Ujerumani Magharibi. Kwa habari yangu, mambo yalibadilika kwa ghafula baada ya ziara ya ndugu kutoka Ujerumani Mashariki.
Mgawo Wangu Mkubwa wa Kwanza
Ndugu huyo alijiita mwenyewe Hans. Baada ya mazungumzo yetu, niliombwa nifike mahali fulani katika Berlin. Nilipoweza kutoa jina la fumbo kwenye kengele ya mlango, nilikaribishwa ndani. Watu wawili walijiunga nami na wakashiriki pamoja na mimi katika mazungumzo yenye kupendeza lakini ya kawaida sana. Kisha likaja lile ambalo walikuwa wanaelekea: “Ikiwa ungepewa mgawo wa pekee, je, ungeukubali?”
“Bila shaka,” likawa jibu langu.
“vyema,” wakasema, “hilo tu ndilo tulilotaka kujua. Uwe na safari njema hadi nyumbani.”
Majuma matatu baadaye niliombwa nirudi Berlin na tena nikawa katika chumba hicho. Wakinipa ramani ya eneo linalozunguka Zittau, ndugu hao wakasema kusudi hasa la mkutano huo. “Hatuwasiliani na Mashahidi katika eneo hilo. Je! waweza kutusaidia tuweze kuwasiliana nao tena?”
“Bila shaka nitafanya hivyo,” likawa jibu langu la mara moja. Eneo hilo lilikuwa kubwa sana, zaidi ya kilometa 100 kwa urefu, kutoka Riesa hadi Zittau, na kufikia upana wa kilometa 50. Na nilikuwa na baiskeli tu. Wakati uwasiliano pamoja na Mashahidi mmoja mmoja ulipowezekana, kila mmoja aliunganishwa na kundi lake mwenyewe, lililotuma mjumbe Berlin kwa kawaida ili kupata vichapo na maagizo. Njia hiyo ya kutenda ilizuia uwezekano wa kuhatarisha makundi yale mengine wakati wenye mamlaka walikuwa wakinyanyasa kundi lolote moja.
Mtumaini Yehova
Ujapokuwa mnyanyaso huo, kwa kutii maagizo ya Biblia, hatukukoma kamwe kwenda nyumba kwa nyumba tukiwa na ujumbe wetu wa Ufalme wa Mungu. (Mathayo 24:14; 28:19, 20; Matendo 20:20) Tulitembelea anwani zilizopendekezwa na watu mmoja mmoja tuliowajua, na tulionea shangwe maono mazuri ajabu. Nyakati nyingine hata makosa yetu yaligeuka yakawa mibaraka, kama yafuatayo yanavyoonyesha.
Mke wangu na mimi tulipewa anwani ya kuzuru, lakini tulitembelea nyumba nyingine kwa makosa. Mlango ulipofunguliwa, tuliona mavazi ya polisi kwenye chombo cha kuwekea makoti. Uso wa Margit ukawa mweupe-mweupe; moyo wangu ulipigapiga. Hilo lingeweza kumaanisha kufungwa gerezani. Kulikuwako tu wakati wa kutoa sala ya haraka.
“Ninyi ni akina nani?” akauliza mtu huyo kwa maneno machache. Tuliendelea kuwa watulivu.
“Nina uhakika nakujua kutoka mahali fulani,” Margit akasema, “lakini siwezi kukumbu-ka ni wapi. Ndiyo, wewe ni polisi. Ni lazima niwe nilikuona ukiwa kazini.”
Hilo lilituliza hali, na yeye akasema katika sauti ya urafiki. “Je! ninyi ni wale Yehova?”
“Ndiyo,” nikajiunga, “sisi ni hao, na ni lazima ukubali kwamba moyo mkubwa unahitajiwa ili tuweze kubisha mlango wako. Tunapendezwa na wewe binafsi.”
Alitukaribisha ndani ya nyumba yake. Tulimzuru mara kadhaa na kuanza funzo la Biblia. Baadaye mtu huyo akawa ndugu yetu Mkristo. Ono hilo liliimarisha tumaini letu katika Yehova kama nini!
Mara nyingi akina dada walitenda wakiwa wajumbe, jambo lililowataka waweke imani yao kabisa katika Yehova. Ndivyo hali ilivyokuwa wakati Margit aliposafiri pindi moja kutoka Berlin ili kuchukua vichapo. Kulikuwako vitu vingi zaidi ya vile vilivyotazamiwa. Kamba ya kuanikia nguo ndiyo iliyotumiwa kufunga sanduku hilo zito, lililojazwa kupita kiasi. Mambo yalienda sawa mpaka wakati Margit alipokuwa katika gari-moshi. Kisha akaja ofisa wa mpakani.
“Hii ni ya nani, na ni nini kilichomo ndani?” akataka kujua kwa lazima, akielekezea kidole sanduku hilo.
“Ni nguo zangu zilizofuliwa,” Margit akajibu.
Akishuku, alimwamuru Margit alifungue. Polepole na kwa makusudi, akitoa kila kifundo kimoja baada ya kingine, Margit alianza kufungua ile kamba ya kuanikia nguo iliyolizunguka sanduku hilo. Kwa kuwa kazi ya ofisa wa mpaka humtaka asafiri kwa gari-moshi mwendo fulani tu na kisha ashuke na kuchukua gari-moshi jingine ili arudi, alizidi kukosa saburi. Hatimaye wakati vifundo vitatu vilipobaki, alichoka na kuacha. “Ondoka hapa, na uchukue nguo zako zilizofuliwa!” akapiga kelele.
Utunzi wa Yehova
Mara nyingi niliweza kuwa na saa zisizozidi nne za kulala kwa usiku mmoja, kwa kuwa nilikuwa kwa kawaida nikishughulikia mambo ya kundi gizani. Ilikuwa baada ya usiku wa utendaji kama huo wakati maofisa walipogongagonga mlangoni petu asubuhi moja. Walikuwa wamekuja kupekuapekua. Ilikuwa kuchelewa mno kuweza kuficha chochote.
Maofisa hao walitumia asubuhi yote wakipekuapekua mahali hapo kwa uangalifu sana, hata wakichunguza chooni iwapo kitu fulani kilikuwa kimefichwa ndani yacho. Hakuna yeyote aliyefikiria kulichunguza koti langu lililokuwa kwenye chombo cha kuwekea makoti. Nilikuwa nimeingiza kwa haraka ndani ya mifuko yalo mingi hati kadhaa. Mifuko hiyo ilikuwa ikitokeza ikiwa na mambo yale yale ambayo maofisa hao walikuwa wakitafuta, lakini waliondoa mikono mitupu.
Pindi nyingine, katika Agosti 1961, nilikuwa Berlin. Hiyo ilithibitika kuwa mara yangu ya mwisho kuchukua vichapo kabla ya Ukuta wa Berlin kusimamishwa. Stesheni ya gari-moshi ya Berlin ilikuwa imejaa watu nilipojitayarisha kurudi Zittau. Gari-moshi liliwasili, na kila mtu akakimbia jukwaani ili kuingia. Nikisukumwa miongoni mwa umati huo, kwa ghafula nilijipata nikiwa katika sehemu ya gari-moshi isiyo na watu. Mara tu nilipoingia ndipo mlinzi akaifunga milango kutoka nje. Nilisimama peke yangu katika sehemu moja ya gari-moshi, huku maabiria wengine wakisongamana katika sehemu ile nyingine ya gari-moshi.
Tuliondoka kuelekea Zittau. Kwa muda fulani nilikuwa peke yangu katika gari hilo. Kisha gari-moshi likasimama, na milango ya sehemu yangu ikafunguliwa. Askari-jeshi wengi wa kutoka Sovieti wakaingia. Ndipo tu nikatambua kwamba nilikuwa nimesafiri katika sehemu iliyowekewa jeshi la Sovieti. Nilitamani ardhi ifunguke, inimeze. Hata hivyo, askari-jeshi hao hawakuonekana kana kwamba waliona kasoro yoyote.
Tuliendelea na safari yetu hadi Zittau, ambapo milango ya sehemu yetu ilifunguliwa, na askari-jeshi hao wakaruka nje. Walianza kuwapekuapekua maabiria wote stesheni. Ni mimi peke yangu niliyeweza kuondoka bila kuzuiwa. Askari-jeshi wengi hata walinipigia saluti, wakifikiria nilikuwa ofisa wa cheo cha juu.
Ni baadaye tu nilipotambua jinsi vichapo hivyo vilivyokuwa vya thamani, kwani kusimamishwa kwa Ukuta wa Berlin kulizuia kwa muda njia yetu ya kupokea vichapo. Hata hivyo, vichapo hivyo vilitosheleza uhitaji wetu kwa miezi kadhaa. Wakati ule ule, mipango ya kuwasiliana nasi ingeweza kufanywa.
Kusimamishwa kwa Ukuta wa Berlin katika 1961 kulituletea mabadiliko katika Ujerumani Mashariki. Lakini Yehova, kama afanyavyo sikuzote, aliyatangulia matukio hayo. Aliendelea kututunza chini ya marufuku.—Kama ilivyosimuliwa na Hermann Laube.
[Picha katika ukurasa wa 27]
Tulionea shangwe kusanyiko dogo katika Bautzen