Yehova Alitutunza Chini ya Marufuku-Sehemu ya 3
ILIKUWA Machi 14, 1990. Siku hiyo yenye matukio ya maana, nilikuwa miongoni mwa wale waliokuwapo wakati ofisa wa cheo cha juu wa serikali katika Wizara ya Mambo ya Kidini ya Berlin Mashariki alipotukabidhi hati iliyohalalisha kisheria Mashahidi wa Yehova katika ile iliyoitwa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Ujerumani, au Ujerumani Mashariki. Wakati wa matukio ya siku hiyo, nilikumbuka wakati nilipopata kuwa Shahidi na kufikiria zile nyakati ngumu tulizokuwa tumepitia.
Katika miaka ya katikati ya 1950, Margarete, mfanyakazi mwenzangu aliyekuwa Shahidi, alisema na mimi kwa mara ya kwanza kuhusu imani zake zenye msingi wa Biblia, mnyanyaso wa Mashahidi wa Yehova katika Ujerumani Mashariki ulikuwa mbaya sana. Upesi baada ya hapo aliondoka kufanya kazi kwingineko, na mimi nikaanza kujifunza Biblia pamoja na Shahidi mwingine. Nilibatizwa katika 1956, na Margarete na mimi tukafunga ndoa mwaka uo huo. Tulishirikiana na kundi la Lichtenberg katika Berlin. Lilikuwa na wahubiri wa Ufalme karibu 60 wakishiriki katika kazi ya kuhubiri.
Miaka miwili baada ya ubatizo wangu, maofisa wa serikali walitembelea nyumba ya yule aliyekuwa akiongoza katika kundi letu. Walitaka kumkamata, lakini alikuwa kazini katika Berlin Magharibi. Familia yake iliweza kumwarifu aendelee kukaa huko, na miezi kadhaa baadaye ilijiunga naye huko Magharibi. Hata ingawa nilikuwa na umri wa miaka 24, wakati huo nilipewa madaraka mazito kundini. Ninashukuru kwamba Yehova huandaa hekima na imara inayohitajika ili kushughulikia wajibu huo mbalimbali.—2 Wakorintho 4:7.
Kuandaa Chakula cha Kiroho
Ukuta wa Berlin ilipojengwa katika Agosti 1961, Mashahidi wa Yehova katika Mashariki wakatengwa kwa ghafula na ndugu zao katika Magharibi. Hivyo kikaanza kipindi ambacho tulinakili vichapo vyetu, kwanza kwa taipureta, halafu kwa mfululizo wa mashine za kunakili. Kuanzia 1963, nilitumia siku mbili kujenga mahali pa kujifichia nyumbani mwetu ili kufanya uchapaji huo. Baada ya kufanya kazi siku nzima nikiwa mtengenezaji wa vifaa vya kufanyia kazi, nilitumia usiku kuchapa nakala za Mnara wa Mlinzi nikisaidiwa na ndugu wengine wawili. Wenye mamlaka walitaka sana kufumania mpango wetu wa uchapaji, lakini Yehova alitusaidia ili kwamba chakula chetu, kama tulivyokiita, kilitokea kwa wakati wacho.
Kuchapa nakala za kutosha za magazeti yetu kulitaka karatasi nyingi sana, na haikuwa rahisi kupata kiasi kikubwa cha karatasi. Kama tungalinunua kwa kawaida karatasi kwa wingi, hilo lingalivuta uangalifu wa wenye mamlaka. Kwa hiyo tuliwaagiza Mashahidi mmoja mmoja wanunue kiasi kidogo cha karatasi na kukileta kwenye kikundi chetu cha funzo la Biblia. Kutoka hapo zilipelekwa mahali tulipochapa magazeti. Mashahidi wengine waligawanya magazeti yaliyomalizika kuchapishwa.
Kwa kuwa maofisa walishuku kwamba nilihusika katika kuchapa vichapo, walinichunguza kwa ukaribu. Mwisho-mwisho mwa 1965, niliwaona wakinifuata zaidi ya kawaida nikahisi kwamba walikuwa wakipanga jambo fulani. Kwa ghafula, walikuja mapema asubuhi moja.
Karibu Nishikwe
Nilikuwa njiani kwenda kazini asubuhi hiyo ya kipupwe. Ilikuwa kabla ya kupambazuka, nami nilikuwa nimejikaza dhidi ya baridi kali. Nilipokuwa nikitembea, niliona vichwa vinne juu ya nyua. Wanaume hao walipiga kona na kunielekea katika kijia. Kwa hofu yangu kuu nikawatambua kuwa maofisa wa serikali. Ningefanya nini?
Theluji yenye kina ilikuwa imesukumwa upande moja kwa kijiko cha mchanga ikiacha kijia chembamba. Niliendelea kutembea. Nikiinamisha kichwa changu, nilisonga mbele macho yangu yakiwa yamekazwa kuelekea chini. Nilisali kimya-kimya kwa haraka. Wanaume hao wakakaribia zaidi na zaidi. Je! walikuwa wamenitambua? Tulipotembea karibu-karibu tukipitana katika kijia hicho chembamba, ilikuwa vigumu kuamini lililokuwa likitukia. Nilizidi kukaza mwendo. “We,” mmoja wao akapaaza sauti, “ndiye huyo. Simama!”
Nilikimbia upesi kadiri niwezavyo. Nilipiga kona kwa kasi, nikaruka ua wa jirani yangu na kuingia uwanja wangu wa nyuma. Nikiruka ndani ya nyumba, nikafunga mlango na kuuweka kufuli. “Kila mtu tokeni kitandani!” nikapaaza sauti. “Wanakuja kunikamata.”
Margarete alishuka ngazi upesi sana na kusimama mlangoni. Kwa wakati mfupi nilikuwa katika chumba cha chini nikiwasha jiko moto. Nilichukua rekodi zote za kundi nilizokuwa nazo na kuzitupa motoni.
“Fungueni!” wanaume hao wakasema kwa sauti. “Fungueni mlango! Huyu ni wakili wa mashtaka.”
Margarete alikataa kufungua nilipokuwa nikichoma kila kitu kisiweze kutambulika. Halafu nikajiunga na Margarete na kuinamisha kichwa ili aufungue mlango. Wanaume hao wakaingia nyumba kwa kishindo.
“Ni kwa nini ulikimbia?” wakauliza.
Upesi maofisi wa serikali wengine zaidi wakafika, na nyumba yote ikapekuliwa. Hangaiko langu hasa lilikuwa mahali pale pa kufichia vifaa palipokuwa mashine yetu ya kuchapia na kurasa 40,000 za karatasi. Lakini mwingilio uliofichwa ulibaki bila kugunduliwa. Ingawa mahoji yaliendelea kwa muda wa saa nyingi, Yehova alinisaidia kuendelea nikiwa mtulivu. Ono hilo lilituvuta karibu zaidi na Baba yetu wa kimbingu mwenye upendo na likatuimarisha tuvumilie.
Gerezani Lakini Huru
Katika mwisho-mwisho wa miaka ya 1960, niliarifiwa niripoti kwa ajili ya kazi ya kijeshi. Kwa kuwa nisingeweza kutumikia kwa kudhamiria, nililazimika kutumia miezi saba gerezani na katika kambi ya kazi. Walikuwamo Mashahidi 15 kambini huko Cottbus, kusini-mashariki mwa Berlin. Sisi sote tulikuwa humo kwa ajili ya kutokuwamo kwa Kikristo. (Isaya 2:2-4; Yohana 17:16) Siku zetu za kufanya kazi zilikuwa ndefu na kazi ilikuwa ngumu. Tuliamka saa 10:15 za asubuhi na kuchukuliwa nje ya kambi kufanya kazi kwenye reli. Hata hivyo tulipokuwa gerezani, tulikuwa na nafasi za kuambia wengine juu ya Ufalme wa Yehova.
Kwa mfano, wabashiri-matukio wawili walikuwa pamoja nasi katika Cottbus. Siku moja nilisikia kwamba yule aliyekuwa mchanga zaidi alitaka sana kusema na mimi. Angetaka nini? Aliniambia kila kitu. Nyanya yake kwa upande wa mama yake alikuwa amekuwa mbashiri, na mwanamume huyo alikuwa amekuza nguvu izo hizo baada ya kusoma vitabu vya nyanya yake. Ingawa mwanamume huyo alitaka sana kuwa huru na nguvu hizo zilizomtawala, aliogopa kisasi. Alilia sana. Lakini hayo yote yalinihusuje?
Katika mazungumzo yetu, alieleza kwamba uwezo wake wa kutabiri wakati ujao ulidhoofishwa alipokuwa miongoni mwa Mashahidi wa Yehova. Nilieleza kwamba kuna roho wabaya, au mashetani, na roho wazuri, au malaika waadilifu. Nikitumia mfano wa wale waliokuwa Wakristo katika Efeso ya kale, nilikazia uhitaji wa kuondolea mbali vifaa vyote vinavyohusiana na ubashiri au zoea jingine lolote la uwasiliani-roho. (Matendo 19:17-20) “Kwa hiyo wasiliana na Mashahidi,” nikamwambia. “Kuna Mashahidi wanaoishi kila mahali.”
Kijana huyo aliondoka kambini siku chache baadaye, nami sikusikia lolote zaidi juu yake. Lakini ono hilo la mwanamume huyo mwenye hofu kuu na asiyeweza kufarijiwa aliyetamani uhuru liliongeza sana upendo wangu kwa Yehova. Sisi Mashahidi 15 tulikuwa kambini kwa sababu ya imani yetu, lakini tulikuwa huru katika njia ya kiroho. Yule kijana alikuwa amewekwa huru kutoka gerezani, lakini alikuwa bado mtumwa wa “mungu” aliyemhofisha sana. (2 Wakorintho 4:4) Sisi Mashahidi twapasa kuthamini kama nini uhuru wetu wa kiroho!
Watoto Wetu Wajaribiwa
Si watu wazima tu waliohitajiwa wasimame imara kwa ajili ya masadikisho yao bali pia watoto. Walibanwa waridhiane shuleni na kazini pia. Watoto wetu wote wanne walihitaji kuchukua msimamo kwa ajili ya imani zao.
Sherehe ya kusalimu bendera ilifanywa shuleni kila Jumatatu. Watoto walipanga mstari kuingia uwanjani, wakiimba wimbo, na kupiga ile saluti iliyoitwa eti Thälmann wakati bendera ilipopandishwa. Ernst Thälmann alikuwa Mkomunisti Mjerumani aliyeuawa kimakusudi na Wanazi wa SS (kikosi cha polisi cha upelelezi) katika 1944. Baada ya vita ya ulimwengu ya pili, Thälmann akawa shujaa katika Ujerumani Mashariki. Kwa sababu ya sadikisho letu lenye msingi wa Biblia kwamba utumishi mtakatifu wapasa kuelekezwa kwa Yehova Mungu tu, mke wangu na mimi tuliwafunza watoto wetu kusimama kwa staha wakati wa sherehe hizo bila kushiriki.
Watoto wa shule walifundishwa pia nyimbo za Kikomunisti. Margarete na mimi tulienda kwenye shule ya watoto wetu na kueleza ni kwa nini wasingeimba nyimbo hizo za kisiasa. Lakini, tulisema kwamba wangekuwa na nia ya kuimba nyimbo za aina nyingine. Hivyo, kuanzia umri wa mapema, watoto wetu walijifunza kusimama imara na kuwa tofauti na marika wao.
Kuelekea mwisho wa miaka ya 1970, binti yetu mkubwa zaidi alitaka kuwa mwanafunzi wa kazi katika ofisi moja. Hata hivyo, kila mwanafunzi wa kazi alihitaji kwanza apate mazoezi ya kijeshi kwa muda wa siku 14. Kwa kuwa dhamiri ya Renate isingemruhusu ashiriki katika hayo, alichukua msimamo wa ujasiri na hatimaye akaondolewa daraka la kupokea mazoezi hayo.
Wakati wa uanafunzi wake wa kazi, Renate alienda kwenye darasa ambalo katika hilo aliitwa ahudhurie mazoezi ya kupiga risasi. “Renate, utakuja pia kwenye mazoezi ya kupiga risasi,” akasema mwalimu. Mwalimu hakujali kukataa kwake. “Si lazima upige risasi,” akaahidi. “Waweza kushughulikia viburudisho.”
Jioni hiyo, tulizungumza mambo hayo tukiwa familia. Tulihisi kwamba kuwako kwa Renate kwenye mazoezi hayo ya kupiga risasi hakukufaa, hata ikiwa hangeshiriki moja kwa moja. Akiwa ameimarishwa na mazungumzo yetu na sala, hakujiruhusu atishwe. Ni kitia-moyo kama nini kwetu kuona binti yetu mchanga akichukua msimamo kwa ajili ya kanuni zenye uadilifu!
Kuongeza Utendaji Wetu wa Kuhubiri Peupe
Wakati upinzani kwa kazi yetu ulipopungua katika mwisho-mwisho wa miaka ya 1970, kiasi kikubwa cha ugavi wa vichapo vyetu vya Kikristo kilianza kuletwa kutoka Magharibi. Ingawa hiyo ilikuwa kazi ya hatari, ndugu wenye ujasiri walijitolea kuifanya. Tulithamini sana ugavi huo wa vichapo wenye kuongezeka na jitihada za wale waliofanya uwezekane. Mnyanyaso ulipokuwa mkali zaidi katika miaka ya mapema ya marufuku, utendaji wa kuhubiri nyumba kwa nyumba ulikuwa mgumu kweli kweli. Kwa kweli, hofu ya kuadhibiwa na wenye mamlaka ilifanya wengine wauepuke. Lakini baadaye kazi yetu ya kuhubiri peupe iliongezeka kwa kutazamisha. Katika miaka ya 1960, ni karibu asilimia 25 tu ya wahubiri wa Ufalme waliokuwa wakishiriki katika utumishi wa nyumba kwa nyumba kwa ukawaida. Hata hivyo, idadi ya wale waliokuwa wakishiriki kwa kawaida katika sehemu hiyo ya huduma ilikuwa imepanda hadi asilimia 66 kufikia mwisho-mwisho wa miaka ya 1980! Kufikia wakati huo wenye mamlaka hawakuhangaikia sana utendaji wetu wa kuhubiri peupe.
Katika pindi moja ndugu mmoja ambaye nilikuwa nikifanya kazi pamoja naye katika huduma alimleta binti yake mchanga pamoja naye. Akichangamshwa na kuwako kwa msichana huyo, mwanamke mzee-mzee tuliyesema naye alitualika ndani ya nyumba yake. Alithamini utoaji wetu wa Kimaandiko na kukubali kwamba tumtembelee tena. Baadaye nilimpa mke wangu rudio hilo, ambaye alianzisha funzo la Biblia nyumbani pamoja na mwanamke huyo. Ijapokuwa umri mkubwa sana na afya mbaya, mwanamke huyo akawa dada yetu naye anaendelea akiwa mwenye bidii katika utumishi wa Yehova.
Marekebisho Wakati Uhuru Ulipokaribia
Yehova alitutayarisha kwa ajili ya wakati ambao tungeonea shangwe uhuru zaidi. Kutoa mfano: Muda mfupi kabla ya marufuku kuondolewa, tulishauriwa tubadili jinsi tulivyoitana mikutanoni. Kwa sababu za usalama, tulikuwa tumeitana kwa majina ya kwanza tu. Wengi waliojuana kwa muda wa miaka mingi hawakujua jina la mwisho la waamini wenzao. Hata hivyo, kwa kujitayarisha ili kukaribisha kwenye mikutano yetu wengi zaidi waliopendezwa, tulitiwa moyo tuitane kwa majina ya familia. Kwa wengine hilo lilionekana kutokuonyesha ukaribu, lakini wale waliofuata shauri hilo waliweza baadaye kujirekebisha kwa urahisi zaidi tulipopata uhuru wetu.
Tulitiwa moyo pia tuanze mikutano yetu kwa wimbo. Kwa njia hiyo tulizidi kuzoeleana na utaratibu uliofuatwa na makundi kwingineko. Rekebisho jingine lilikuwa katika ukubwa wa vikundi vyetu vya mafunzo. Ukubwa wavyo uliongekeza polepole kutoka watu wanne katika miaka ya 1950 hadi wanane. Baadaye ukubwa ukaongezeka hadi 10 na hatimaye hadi 12. Kwa kuongezea, uchunguzi ulifanywa ili kuhakikisha kwamba mahali pa kukutania pa kila kundi palikuwa mahali pa katikati kwa Mashahidi wengi.
Nyakati nyingine tuliweza kuona hekima ya rekebisho lililodokezwa baada tu ya hilo kufanywa. Ni mara nyingi kama nini Yehova alijionyesha kuwa Baba mwenye hekima na ufikirio! Polepole, alitupatanisha na sehemu ile nyingine ya tengenezo lake la kidunia, na tulijihisi zaidi na zaidi tukiwa sehemu ya udugu wa watu wake wa ulimwenguni pote. Kwa hakika Yehova Mungu alikuwa amelinda watu wake kwa upendo muda wote wa karibu miaka 40 ambayo walifanya kazi chini ya marufuku katika Ujerumani Mashariki. Tunashukuru kama nini sasa kuwa na hali ya kuwa halali kisheria!
Leo, kuna Mashahidi wa Yehova 22,000 au zaidi katika ile iliyoitwa Ujerumani Mashariki. Wao ni ushuhuda wa ule uongozi wenye hekima na utunzi wenye upendo wa Yehova Mungu. Utegemezo wake katika ile miaka ambayo tulikuwa chini ya marufuku huonyesha kwamba yeye aweza kushinda hali yoyote. Kila silaha itakayofanyika dhidi ya watu wake, haitafanikiwa. Sikuzote Yehova hutunza vizuri wale wanaomtumaini. (Isaya 54:17; Yeremia 17:7, 8)—Kama ilivyosimuliwa na Horst Schleussner.
[Picha katika ukurasa wa 31]
Horst na Margarete Schleussner kwenye makao ya Society katika Berlin Mashariki