Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w92 5/1 kur. 26-29
  • Yehova Alitutunza Chini ya Marufuku-Sehemu ya 2

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Yehova Alitutunza Chini ya Marufuku-Sehemu ya 2
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kutwaa Madaraka
  • Kujitayarisha Kwa Ajili ya Kutengwa
  • Shule ya Kichini-Chini
  • Manufaa za Shule Hiyo
  • Wenye Kutenda Kazi Katika Huduma
  • Wenye Mamlaka Watufuatia Bado
  • Berlin—Wonyesho wa Jinsi Ulimwengu Wetu Ulivyo?
    Amkeni!—1991
  • Yehova Alitutunza Chini ya Marufuku—Sehemu ya 1
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Yehova Alitutunza Chini ya Marufuku-Sehemu ya 3
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Nilichochewa na Uaminifu-Mshikamanifu wa Familia Yangu kwa Mungu
    Amkeni!—1998
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
w92 5/1 kur. 26-29

Yehova Alitutunza Chini ya Marufuku-Sehemu ya 2

KATIKA Vita ya Ulimwengu 2, bizimu ya ukanda wangu wa mavazi ya askari-jeshi wa Nazi ilikuwa na maneno “Mungu Yu Pamoja Na Sisi.” Kwangu hilo lilikuwa mfano mwingine tu wa kujishughulisha kwa makanisa katika vita na umwagaji damu. Hilo lilikuwa limenichukiza. Kwa hiyo kufikia wakati ambao Mashahidi wa Yehova wawili waliponihusisha katika mazungumzo katika Limbach-Oberfrohna, Ujerumani Mashariki, nilichukia sana dini na nilikuwa nimekuwa asiyeamini kuwapo kwa Mungu na mwanamageuzi.

“Msidhani kwamba nitakuwa Mkristo,” nikawaambia Mashahidi hao walionitembelea. Lakini hoja zao zilinisadikisha kwamba kuna Mungu. Nikiwa na udadisi, nilinunua Biblia na baadaye nikaanza kujifunza pamoja nao. Hayo yalitukia katika masika ya 1953, wakati utendaji wa Mashahidi katika Ujerumani Mashariki ulipokuwa tayari umekuwa chini ya marufuku ya Kikomunisti kwa karibu muda wa miaka mitatu.

Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) la Agosti 15, 1953, lilieleza hali ya Mashahidi wa Yehova wakati huo, likisema hivi: “Ingawa wanapelelezwa na kutishwa daima, ingawa hawawezi kutembeleana bila kwanza kuhakikisha kwamba hawafuatwi, ingawa kupatikana kwa mtu akiwa na vichapo vya Watchtower kwamaanisha miaka miwili au mitatu gerezani kwa ajili ya ‘kueneza vichapo vya kuchochea uasi’, na ingawa mamia ya ndugu walio wakomavu zaidi, wale waliokuwa wameiongoza, wamo gerezani, hata hivyo watumishi wa Yehova katika Ujerumani Magharibi wanaendelea kuhubiri.”

Katika 1955 mke wangu, Regina, na mimi tulihudhuria mkusanyiko wa kimataifa wa Mashahidi wa Yehova katika Nuremberg, Ujerumani Mashariki, na mwaka uliofuata sote wawili tukabatizwa katika Berlin Magharibi. Hiyo ilikuwa, bila shaka, kabla ya ukuta wa Berlin kujengwa katika 1961, ukitenga Ujerumani Mashariki na Berlin Magharibi. Lakini hata kabla ya mimi kubatizwa, uaminifu-mshikamanifu wangu kwa Yehova Mungu ulijaribiwa.

Kutwaa Madaraka

Kundi la Mashahidi wa Yehova ambalo tulikuwa tumeanza kuhudhuria katika Limbach-Oberfrohna lilihitaji mtu ambaye angeweza kuchukua vichapo vya Biblia kutoka Berlin Magharibi. Tulikuwa na biashara ndogo na watoto wachanga wawili, lakini kumtumikia Yehova kulikuwa tayari kumekuwa kitovu cha maisha yetu. Tulirekebisha gari letu la zamani, jambo lililotuwezesha kuficha vitabu 60. Kuwa tarishi kulikuwa shughuli yenye hatari, lakini ilinifundisha kumtegemea Yehova.

Kuvuka kwa gari kutoka Berlin Mashariki hadi sehemu ya Magharibi hakukuwa rahisi, na mara nyingi mimi hushangaa jinsi tulivyoweza kufanya hivyo. Wakati tulipokuwa katika sehemu iliyo huru, tulikusanya vichapo na kuvificha vitabu katika gari kabla ya kuvuka mpaka kurudi Ujerumani Mashariki.

Pindi moja, tulikuwa tumemaliza tu kuvificha vitabu wakati mtu mgeni alipotoka katika nyumba moja. “Ninyi hapo,” akapaaza sauti. Niligutuka. Je! alikuwa amekuwa akituchungulia? “Ni afadhali mwende mahali penginepo wakati mwingine. Gari la redio la polisi wa Ujerumani Mashariki huegeshwa kwenye kona hapo, na huenda wakawashika.” Nilipumua kwa kufarijika. Tulipita mpaka vyema, na sote wanne tuliokuwa katika gari tukaimba mwendo wote kurudi nyumbani.

Kujitayarisha Kwa Ajili ya Kutengwa

Katika miaka ya 1950 akina ndugu katika Ujerumani Mashariki waliwategemea wale katika Magharibi ili kupata vichapo na mwongozo. Lakini katika 1960 marekebisho yalifanywa yaliyosaidia kila Shahidi katika Ujerumani Mashariki awe na ukaribu zaidi pamoja na Mashahidi katika eneo alimoishi. Halafu katika Juni 1961 darasa la kwanza la Shule ya Huduma ya Ufalme ya wazee lilifanywa katika Berlin. Nilihudhuria mtaala huo wa kwanza wa muda wa majuma manne. Baada ya muda usiozidi majuma sita, tulitengwa na Magharibi kwa ghafula wakati Ukuta wa Berlin ulipojengwa. Kazi yetu sasa haikuwa ya kichini-chini tu bali pia yenye kutengwa.

Wengine walihofu kwamba utendaji mbalimbali wa Mashahidi wa Yehova katika Ujerumani Mashariki ungepoa na kukoma kabisa. Hata hivyo, marekebisho ya kitengenezo yaliyoanzishwa katika muda usiozidi mwaka mmoja mapema zaidi yalitusaidia tudumishe umoja na imara ya kiroho. Kuongezea hilo, mazoezi yaliyopokewa na wazee waliohudhuria darasa la kwanza la Shule ya Huduma ya Ufalme yaliwawezesha kupitishia wazee wengine mazoezi hayo. Kwa hiyo Yehova alitutayarisha kwa ajili ya kutengwa kwetu, sawa na alivyokuwa ametutayarisha kwa ajili ya marufuku katika 1950 kwa mikusanyiko ya wilaya ya 1949.

Tukiwa tumetengwa na Magharibi, ilikuwa wazi kwamba tulihitaji kujianzishia mambo ili kuendeleza tengenezo katika hali ya kusonga mbele. Tuliwaandikia ndugu zetu Wakristo katika Berlin Magharibi na kudokeza tukutane pamoja nao kwenye barabara moja kuu katika Mashariki ambayo wasafiri kutoka Magharibi wangeweza kupitia. Tulijifanya kana kwamba gari letu limeharibika mahali tulipokuwa tumepanga. Dakika kadhaa baadaye ndugu hao walikuja kwa gari, wakituletea vichapo vya Biblia. Kwa furaha, walileta pia kitabu changu cha mafundisho cha Shule ya Huduma ya Ufalme, mambo niliyokuwa nimeandika, na Biblia ambayo nilikuwa nimeacha huko Berlin kwa sababu za usalama. Lilikuwa jambo la kusisimua kama nini kuvipata tena! Sikuwa nimejua jinsi ambavyo ningevihitaji vitu hivyo katika muda wa miaka kadhaa iliyofuata.

Shule ya Kichini-Chini

Siku chache baadaye, tuliagizwa tupange madarasa ya Shule ya Huduma ya Ufalme katika sehemu zote za Ujerumani Mashariki. Wafunzi wanne waliwekwa, kutia na mimi. Lakini kwangu, kuzoeza wazee wote huku kazi yetu ikiwa chini ya marufuku, kulionekana kuwa kazi isiyowezekana. Ili kuficha lile tulilokuwa tunafanya, niliamua kupanga madarasa hayo kuwa kama likizo la kupiga kambi.

Kila darasa lilifanyizwa kwa wanafunzi wanne na mimi nikiwa mfunzi, pamoja na ndugu wa sita aliyetumikia akiwa mpishi. Wake na watoto walikuwako pia. Kwa hiyo kwa ujumla tulikuwa na kikundi cha watu 15 hadi 20. Haikuwezekana kutumia mahali pa kambi pa kawaida, kwa hiyo familia yangu na mimi tukaenda kutafuta mahali mahali palipofaa.

Pindi moja, tulipokuwa tukisafiri kupitia kijiji kimoja, tuliona kijia chenye kuongoza hadi kwenye kichaka cha miti kilichokuwa mbali na barabara kuu. Palionekana kuwa mahali pa kufaa, kwa hiyo nilimwendea meya wa mji. “Tunatafuta mahali pa kutumia kwa majuma mawili ili kufanya kambi pamoja na familia nyingine kadhaa,” nikaeleza. “Twataka kuwa peke yetu ili watoto waweze kurukaruka huku na huku. Je! twaweza kuvitumia vichaka hivyo pale?” Alikubali, kwa hiyo tukafanya mipango.

Kwenye mahali hapo, tulipiga hema na kuweka gari-nyumba langu ili kuwe na mahali penye pembenne palipofichwa pasionekane nje. Gari-nyumba lilitumika kuwa darasa letu. Tulikutana ndani yalo kwa muda wa saa 8 zenye mafunzo mengi kila siku kwa siku 14. Katika mahali palipozungukwa palikuwako viti na meza, vilivyowekwa iwapo tu tulikuwa na wageni wasiotazamiwa. Na tulikuwa nao! Nyakati hizo tulithamini sana utegemezo wenye upendo wa familia zetu.

Tulipokuwa darasani, familia zetu zililinda. Katika pindi hii hasa, meya wa mji, aliyekuwa pia katibu wa Chama cha Kikomunisti cha mahali hapo, alionekana akija kwenye kijia kilichoelekea kichaka chetu. Mlinzi alifinya swichi iliyounganishwa kwa nyugwe hadi kwenye kengele iliyokuwa katika gari-nyumba. Papo hapo tulitoka kwenye gari-nyumba kwa haraka na kuchukua mahali petu palipopangwa mbeleni kuzunguka meza na kuanza kucheza karata. Kulikuwako hata chupa ya kileo au mvinyo ili kufanya hali ionekane halisi. Meya wa mji alitutembelea kirafiki na kurudi nyumbani bila shaka lolote juu ya lile lililokuwa likitukia hasa.

Madarasa ya Shule ya Huduma ya Ufalme yalifanywa kotekote nchini kutoka masika ya 1962 hadi mwisho mwisho wa 1965. Yale mazoezi mengi yaliyopokewa huko, yaliyotia ndani habari juu ya jinsi ya kukabiliana na hali yetu hasa katika Ujerumani Mashariki, yalitayarisha wazee kwa ajili ya uangalizi wa kazi ya kuhubiri. Ili wahudhurie madarasa hayo, wazee hawakudhabihu likizo zao tu bali pia walikuwa katika hatari ya kufungwa gerezani.

Manufaa za Shule Hiyo

Wenye mamlaka walikuwa wakichunguza utendaji wetu mbalimbali kwa uangalifu, na mwisho mwisho wa 1965, baada ya wazee walio wengi kuwa wamepitia shule hiyo, walijaribu kukomesha utendaji wa tengenezo letu. Walikamata Mashahidi 15 walioonwa kuwa ndio wenye kuongoza kazi. Hilo lilikuwa tendo lililotayarishwa vizuri, lenye kuenea kotekote nchini. Kwa mara nyingine tena, wengi walifikiria kwamba Mashahidi wangeacha kutenda. Lakini kwa msaada wa Yehova tulijirekebisha kwa hali hiyo na kuendelea na kazi yetu kama hapo mbeleni.

Jambo hasa lililowezesha hilo lilikuwa yale mazoezi ambayo wazee walikuwa wamepokea katika Shule ya Huduma ya Ufalme na vile vifungo vya kutumainiana vilivyofanyizwa visiweze kuvunjika kupitia ushirika walioonea shangwe wakati wa madarasa hayo. Hivyo, tengenezo lilionyesha nguvu yalo. Lilikuwa jambo la maana kama nini kwamba tulikuwa tumefuata kwa utiifu maagizo ya tengenezo kwa ukaribu!—Isaya 48:17.

Ikawa wazi katika miezi iliyofuata kwamba kule kukandamizwa kwingi kwa mamlaka za kiserikali hakukuathiri utendaji wetu vibaya sana. Baada ya muda mfupi, tuliweza kuanza tena madarasa yetu ya Shule ya Huduma ya Ufalme. Mara wenye mamlaka walipoona kurudi kwetu, walilazimika kubadili mbinu zao. Ulikuwa ushindi ulioje kwa Yehova!

Wenye Kutenda Kazi Katika Huduma

Katika wakati huo vikundi vyetu vya Funzo la Kitabu la Kundi vilikuwa na watu karibu watano. Kila mmoja wetu alipokea vichapo vya Biblia kupitia mpango huo wa funzo la kitabu, na kazi ya kuhubiri iliratibiwa kutoka vikundi vya mafunzo hivyo vidogo. Kutoka mwanzo Yehova alibariki Regina na mimi tuweze kupata watu wengi sana waliotaka kujifunza Biblia.

Utumishi wa nyumba kwa nyumba ulibadilishwa kwa njia fulani ili kutulinda tusigunduliwe na kukamatwa. Tungetembelea nyumba moja, halafu kuruka nyumba kadhaa kabla ya kubisha mlango mwingine. Katika nyumba moja mwanamke mmoja alitukaribisha Regina na mimi tuingie. Tulikuwa tukizungumza kichwa cha Kimaandiko pamoja naye wakati mwana wake alipoingia chumba hicho. Alikuwa mwenye kusema waziwazi.

“Je! mmepata kumwona Mungu wenu?” akauliza. “Ili tu mweze kujua kwamba mimi huamini yale nionayo tu. Kila kitu kinginecho chote ni upuzi.”

“Siwezi kuamini hilo,” nikajibu. “Je! umepata kuona ubongo wako? Kila ufanyacho chaonyesha kwamba unao ubongo.”

Regina na mimi tulitoa mifano ya vitu vingine ambavyo sisi hukubali bila kuviona, kama vile umeme. Kijana huyo alisikiza kwa makini, na funzo la Biblia nyumbani likaanzishwa pamoja na yeye na mama yake. Wote wawili wakawa Mashahidi. Kwa kweli, watu 14 ambao mke wangu na mimi tulijifunza nao walikuja kuwa Mashahidi. Nusu ya idadi hiyo tulikutana nao katika ziara zetu za nyumba kwa nyumba, na nusu ile nyingine tulikutana nao mara ya kwanza katika utoaji ushahidi wa vivi hivi.

Mara funzo la Biblia nyumbani lilipokuwa likiongozwa kwa ukawaida na tulimwona mtu huyo kuwa mwenye kustahili kutumainiwa, tulimwalika mtu huyo kwenye mikutano yetu. Hata hivyo, ufikirio wa maana ulikuwa kama mwanafunzi angeweza kuhatarisha usalama wa watu wa Mungu. Hivyo, ilichukua muda wa mwaka mmoja hivi kabla ya sisi kualika mwanafunzi wa Biblia mkutanoni, na pindi nyingine ilichukua muda mrefu zaidi. Nakumbuka mwanamume mmoja aliyekuwa na umashuhuri wa kadiri fulani; alikuwa na uhusiano wa karibu sana pamoja na maofisa wa juu katika Chama cha Kikomunisti. Alikuwa na funzo la Biblia kwa muda wa miaka tisa kabla ya kuruhusiwa kuhudhuria mikutano! Leo mwanamume huyo ni ndugu yetu wa Kikristo.

Wenye Mamlaka Watufuatia Bado

Baada ya 1965 hakukuwa kukamatwa-kamatwa kwa wingi tena, lakini hata hivyo hatukuachwa kwa amani. Wenye mamlaka waliendelea kutuchunguza kwa uangalifu. Wakati huo nilianza kuhusika kwa ukaribu na utendaji wa tengenezo letu, kwa hiyo nilipata uchunguzi wa kipekee kutoka kwa maofisa. Walinichukua mara nyingi sana ili kunihoji, wakinipeleka kwa gari hadi stesheni ya polisi na kuniuliza maswali. “Waweza kuaga uhuru wako sasa,” walikuwa wakiniambia. “Unaenda gerezani.” Lakini nyakati zote waliniachilia hatimaye.

Katika 1972 maofisa wawili walinizuru na kupongeza tengenezo letu bila kukusudia. Walikuwa wamesikiliza kisirisiri Funzo la Mnara wa Mlinzi letu la kundi. “Tulipata makala hiyo kuwa yenye kuudhisha sana,” wakagombeza. Kwa wazi walihangaikia vile watu huenda wakafikiria itikadi ya Kikomunisti ikiwa wangalisoma makala hiyo iliyokuwa ikizungumziwa. “Kwa vyovyote vile,” wakasema, “Mnara wa Mlinzi lina mweneo wa milioni tano au sita, nalo husomwa katika nchi zinazositawi. Hilo si gazeti duni tu.” Nilifikiria moyoni, ‘Wasema kwa usahihi kama nini!’

Kufikia 1972 tulikuwa tumekuwa chini ya marufuku kwa muda wa miaka 22, na Yehova alikuwa ametuongoza kwa upendo na kwa hekima. Tulikuwa tumefuata maagizo yake kwa uangalifu, lakini ingechukua muda wa miaka 18 zaidi kabla ya Mashahidi katika Ujerumani Mashariki kupewa utambuzi wa kisheria. Twashukuru kama nini kwa ajili ya uhuru mbalimbali mzuri ajabu tunaoonea shangwe sasa kumwabudu Mungu wetu, Yehova!—Kama ilivyosimuliwa na Helmut Martin.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki