Katalia Mbali Fantasia za Kilimwengu, Fuatia Mambo Halisi ya Ufalme
“Utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa.”—MATHAYO 6:33.
1. Neno la Mungu hutoa onyo jipi kuhusu moyo wa ufananisho, na ni nini mojawapo ya njia kuu ambazo kwazo unatudanganya?
“LINDA moyo wako kuliko yote uyalindayo; maana ndiko zitokako chemchemi za uzima.” (Mithali 4:23) Ni kwa nini Mfalme Sulemani mwenye hekima alihitaji kutoa onyo hilo? Ni kwa sababu “moyo huwa mdanganyifu kuliko vitu vyote, una ugonjwa wa kufisha.” (Yeremia 17:9) Njia moja kuu ambayo kwayo moyo wetu wa ufananisho waweza kutudanganya ni kwa kutusababisha tujifurahishe na fantasia za kilimwengu. Lakini fantasia ni nini? Ni mawazio yasiyowezekana, ndoto za mchana, kuzurura-zurura kwa akili kusikofaa. Ndoto hizo za mchana zinapokuwa fantasia za kilimwengu, haziwi zenye kupoteza wakati tu bali pia zawa zenye kudhuru sana. Kwa hiyo, ni lazima tuzikatalie mbali kabisa. Kwa kweli, ikiwa tunachukia ukosefu wa kufuata sheria kama vile Yesu alivyochukia, tutaulinda moyo wetu dhidi ya kujifurahisha kwa fantasia za kilimwengu.—Waebrania 1:8, 9.
2. Fantasia za kilimwengu ni nini, na ni kwa nini twapaswa kuzikatalia mbali?
2 Lakini fantasia za kilimwengu ni nini? Ni fantasia zenye sifa ya ulimwengu huu ulio chini ya uwezo wa Shetani. Kuhusu ulimwengu huu, mtume Yohana aliandika hivi: “Maana kila kilichomo duniani, yaani, tamaa ya mwili, na tamaa ya macho, na kiburi cha uzima, havitokani na Baba, bali vyatokana na dunia.” (1 Yohana 2:16; 5:19) Kwa nini ni lazima Wakristo wakatalie mbali fantasia za kilimwengu? Kwa sababu fantasia za jinsi hiyo huchochea tamaa zenye ubinafsi akilini na moyoni. Kuota ndoto za mchana juu ya kufanya mabaya kwaweza kwa kweli kuwa mazoezi ya akilini ya yale ambayo mtu atafanya kihalisi. Mwanafunzi Yakobo atuonya hivi: “Kila mmoja hujaribiwa na tamaa yake mwenyewe huku akivutwa na kudanganywa. Halafu ile tamaa ikiisha kuchukua mimba huzaa dhambi, na ile dhambi ikiisha kukomaa huzaa mauti.”—Yakobo 1:14, 15.
Mifano Yenye Kuonya
3. Ni kisa cha nani kinachoandaa mfano mkuu wa kuonya juu ya madhara ya fantasia zenye ubinafsi?
3 Acheni tuchunguze mifano inayoonyesha sababu kwa nini ni lazima fantasia za kilimwengu zikataliwe mbali. Kisa cha Shetani Ibilisi huandaa mfano mkuu wa madhara yawezayo kutokana na kujifurahisha kwa fantasia zenye ubinafsi. Aliruhusu hisia za kujiona mkuu zisitawi moyoni mwake kufikia kadiri ambayo alionea wivu cheo cha Yehova kisicho na kifani akiwa Bwana Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote Mzima na akataka kuabudiwa. (Luka 4:5-8) Je! hiyo ilikuwa fantasia isiyowezekana? Kwa hakika ilikuwa hivyo! Hiyo itathibitishwa pasipo shaka wakati Shetani anapofungwa kwa miaka elfu na hasa wakati anaporushwa katika “ziwa la moto na kiberiti,” kifo cha pili.—Ufunuo 20:1-3, 10.
4. Shetani alimdanganyaje Hawa?
4 Tuna mfano mwingine wenye kuonya katika kisa cha mwanamke wa kwanza, Hawa. Katika juhudi za Shetani za kutimiza tamaa yake ya makubwa, alimshawishi Hawa kwa kuitolea akili yake fantasia ya kwamba ikiwa angelila lile tunda lililokatazwa, asingekufa bali angekuwa kama Mungu, akijua mema na mabaya. Je! fantasia hiyo ilikuwa isiyowezekana, yenye ubinafsi? Kwa kweli ilikuwa hivyo, kama vile tuwezavyo kuona kutokana na hukumu ya Mungu juu ya Hawa na mume wake, Adamu, walipobarizi. Likiwa tokeo, walijipotezea wenyewe na wazao wao wote wasio wakamilifu haki ya uhai katika Paradiso.—Mwanzo 3:1-19; Warumi 5:12.
5. Ni nini kilichosababisha anguko la baadhi ya wana wa Mungu wa kimalaika, na tokeo likawa nini kwao?
5 Tunao pia mfano wenye kuonya wa baadhi ya wana wa Mungu wa kimalaika. (Mwanzo 6:1-4) Badala ya kutosheka na baraka walizoonea shangwe mbele za Yehova mbinguni, walikuwa na fantasia juu ya wanawake duniani na jinsi ambavyo ingefurahisha kuwa na mahusiano ya kingono pamoja nao. Kwa sababu ya kutenda kulingana na fantasia hizo, wale malaika wasiotii wamo ndani ya giza la kiroho la Tartaro, wakingojea uangamizi wao kwenye mwisho wa Utawala wa Miaka Elfu wa Yesu Kristo.—2 Petro 2:4; Yuda 6; Ufunuo 20:10.
Katalia Mbali Fantasia za Kilimwengu
6, 7. Ni kwa nini fantasia za kilimwengu kuhusu utajiri wa kimwili ni zenye kudhuru na zenye udanganyifu?
6 Acheni sasa tuchunguze mojawapo ya fantasia za kawaida na zenye hatari zaidi zinazoendelezwa na Shetani. Kupitia kila namna ya usambazaji wa habari, tunashawishwa kujifurahisha kwa fantasia za kilimwengu. Hizo mara nyingi husababishwa na kutamani utajiri. Kuwa na mali nyingi si kubaya kwenyewe. Abrahamu, Ayubu, na Mfalme Daudi wenye kumcha Mungu walikuwa matajiri sana, lakini hawakutamani utajiri wa kimwili. Fantasia za kupenda vitu vya kimwili huchochea watu wafanye kazi kwa bidii nyingi kwa muda wa miaka kadhaa ili kupata mali nyingi. Fantasia hizo huwachochea pia wajifurahishe kwa aina zote za kucheza kamari, kama vile kubahatisha kwa farasi atakayeshinda na kununua tikiti za bahati-nasibu. Tusiwazie-wazie juu ya utajiri. Tukifikiri kwamba utajiri wa kimwili utaandaa usalama, angalia mithali hii iliyo jambo la hakika: “Mali hazifaidii kitu siku ya ghadhabu; bali haki huokoa na mauti.” (Mithali 11:4) Kwa kweli, utajiri wa kimwili hautafaidii kitu katika kuokoka “dhiki kubwa.”—Mathayo 24:21; Ufunuo 7:9, 14.
7 Utajiri wa kimwili waweza kutudanganya kwa urahisi. Ndiyo sababu tunaambiwa hivi: “Mali ya mtu tajiri ni mji wake wa nguvu; ni kama ukuta mrefu katika mawazo yake.” (Mithali 18:11) Naam, “katika mawazo yake” tu, kwani mali za kimwili hutoa ulinzi kidogo katika nyakati za mshuko mkubwa wa thamani ya pesa, kuporomoka kwa uchumi, msukosuko wa kisiasa, au ugonjwa wenye mwisho wa kifo. Yesu Kristo alionya dhidi ya upumbavu wa kuweka kwetu tumaini katika utajiri wa kimwili. (Luka 12:13-21) Tunayo pia maneno ya kuonya ya mtume Paulo: “Shina moja la mabaya ya kila namna ni kupenda fedha; ambayo wengine hali wakiitamani hiyo wamefarakana na Imani, na kujichoma kwa maumivu mengi.”—1 Timotheo 6:10.
8. Fantasia za kilimwengu zenye asili ya kingono zimeenea kadiri gani, na hizo zatokeza hatari zipi?
8 Fantasia nyinginezo zinahusu ngono haramu. Kadiri ambayo asili ya kibinadamu ya dhambi hupenda kufikiria fantasia za kingono yaweza kuonwa kutokana na umaarufu wa usemi mchafu unaopatikana kwa kupiga nambari fulani za simu na kusikiliza ujumbe mbalimbali wa kipornografia. Katika United States, nambari za simu ambazo hutoa ujumbe wa kipornografia ni biashara inayofanya mabilioni mengi ya dola. Ikiwa tungeruhusu akili zetu zifikirie juu ya ngono haramu, je, tusingekuwa wanafiki, tukionekana tu kuwa Wakristo safi? Na je, hakuna hatari ya kwamba fantasia za jinsi hiyo zaweza kuongoza kwenye mahusiano ya karibu sana yasiyo ya kiadili? Hilo limetukia na tokeo limekuwa kwamba wengine wametengwa na ushirika wa kundi la Kikristo kwa ajili ya kufanya uasherati au uzinzi. Kupatana na maneno ya Yesu kwenye Mathayo 5:27, 28, je, wote waendeleao kujifurahisha kwa fantasia za jinsi hiyo hawana hatia ya kufanya uzinzi mioyoni mwao?
9. Maandiko yana shauri gani zuri la kutuonya dhidi ya fantasia za kilimwengu?
9 Ili kuupinga mwelekeo wa mioyo yetu yenye dhambi wa kujifurahisha kwa fantasia za jinsi hiyo, twahitaji kuzingatia akilini onyo hili la Paulo: “Wala hakuna kiumbe kisichokuwa wazi mbele zake, lakini vitu vyote vi utupu na kufunuliwa machoni pake yeye aliye na mambo yetu.” (Waebrania 4:13) Twapaswa nyakati zote kutaka kuwa kama Musa, ambaye “alistahimili kama amwonaye yeye asiyeonekana.” (Waebrania 11:27) Naam, ni lazima tuendelee kujiambia wenyewe kwamba fantasia za kilimwengu hazimpendezi Yehova na zaweza tu kutokeza madhara kwetu. Ni lazima tuhangaikie juu ya kusitawisha matunda yote ya roho ya Mungu, hasa kujidhibiti, kwani hatuwezi kuepa ule ukweli wa kwamba tukipanda kwa mwili, tutavuna uharibifu katika mwili.—Wagalatia 5:22, 23; 6:7, 8.
Mambo Halisi ya Ufalme
10, 11. (a) Ni mambo gani ya hakika yanayotoa hoja juu ya uhalisi wa Muumba? (b) Kuna uthibitisho gani kwamba Biblia kwa hakika ni Neno la Mungu? (c) Kuna ushuhuda gani juu ya uhalisi wa Mfalme wa Ufalme wa Mungu?
10 Njia bora zaidi ya kukatalia mbali fantasia za kilimwengu ni kuendelea kufuatia mambo halisi ya Ufalme. Mambo halisi ya Ufalme yanayotokezwa na Mungu huwa tofauti kabisa na fantasia za kilimwengu. Je! Mungu ni halisi? Hakuna shaka yoyote juu ya kuwako kwake. Uumbaji uonekanao hushuhudia ukweli huo. (Warumi 1:20) Tunakumbushwa juu ya yale yaliyosemwa miaka zaidi ya mia moja iliyopita katika kitabu The Divine Plan of the Ages, kilichotangazwa na Watch Tower Society. Kilitaarifu hivi: “Mtu awezaye kutazama angani kwa darubini, au hata kwa jicho lake halisi peke yake, na kuona huko wingi wa uumbaji, upacha wao, uzuri, utaratibu, upatano na unamna-namna, na hata hivyo awe na shaka kwamba Muumba wa hivyo ni mkuu sana kuliko yeye katika hekima na uweza pia, au aweze kudhani kwa muda mfupi kwamba utaratibu wa jinsi hiyo ulikuja kwa nasibu tu, bila Muumba, amepoteza au kupuuza sana uwezo wa kusababu hivi kwamba aweza kwa kufaa kuonwa kuwa yule ambaye Biblia humwita, mpumbavu (mtu anayepuuza au ambaye hana usababu).”—Zaburi 14:1.
11 Twajifunza yote juu ya Ufalme katika Biblia Takatifu. Je! Biblia kwa hakika ni Neno la Mungu lililoandikwa? Kwa hakika ndivyo ilivyo, kama iwezavyo kuonwa kutokana na upatani wayo, usahihi wayo wa kisayansi, na uweza wayo wa kubadili maisha ya watu na hasa kwa utimizo wa unabii wayo mbalimbali.a Namna gani Mfalme wa Ufalme wa Mungu, Yesu Kristo? Je! yeye kwa kweli alikuwako? Masimulizi ya Gospeli na barua zilizopuliziwa kimungu za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo hushuhudia waziwazi na kwa ufasaha kuwako kwa Yesu Kristo. Kwa habari ya kuwako kwa Yesu, kunao pia ushuhuda wa Talmudi ya Kiyahudi, inayomrejezea kuwa mtu. Wanahistoria Wayahudi na Waroma wa karne ya kwanza W.K. humrejezea hivyo pia.
12, 13. Ni mambo gani ya hakika yanayoshuhudia uhalisi wa Ufalme wa Mungu?
12 Namna gani uhalisi wa Ufalme wenyewe? Unapuuzwa sana na Jumuiya ya Wakristo, kama ionyeshwavyo katika lalamiko hili la Mpresbiteria mmoja mashuhuri: “Kwa hakika imekuwa miaka zaidi ya thelathini tangu nilipomsikiliza padri akijaribu kuwaelezea watu wake uhalisi wa Ufalme kwao.” Hata hivyo, utakaso wa jina la Yehova kupitia Ufalme ndio kichwa kikuu cha Neno lake. Mungu mwenyewe ndiye aliyetoa ahadi ya kwanza ya Ufalme, akisema hivi: “Nitaweka uadui kati yako na huyo mwanamke, na kati ya uzao wako na uzao wake; huo utakuponda kichwa, na wewe utamponda kisigino.” (Mwanzo 3:15) Ufalme huo ulifananishwa na taifa la Israeli, hasa wakati wa utawala wa Mfalme Sulemani. (Zaburi 72) Zaidi ya hayo, Ufalme ndio uliokuwa kichwa kikuu cha mahubiri ya Yesu. (Mathayo 4:17) Aliukazia katika vingi vya vielezo vyake, kama vile katika Mathayo sura ya 13. Yesu alituambia tuombe Ufalme wa Mungu uje na kuendelea kuutafuta kwanza. (Mathayo 6:9, 10, 33) Kwa kweli, Ufalme wa Mungu unatajwa karibu mara 130 katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo.
13 Ufalme ni serikali halisi, yenye uweza na mamlaka, nao utatimiza matazamio yote ya haki. Una sheria fulani, zinazopatikana katika Biblia. Ufalme huo tayari umefanya mambo mengi kuwa ya hakika. Una raia waaminifu-washikamanifu—Mashahidi wa Yehova zaidi ya 4,000,000. Katika nchi 211 wao wanahubiri habari njema za Ufalme wa Mungu, katika kutimiza Mathayo 24:14. Wakati wa mwaka wao wa utumishi wa 1991, walitumia muda wa saa 951,870,021 kuhubiri ujumbe wa Ufalme. Utendaji huo una matokeo halisi, yenye kudumu wakati wengi wanapojifunza ile “lugha iliyo safi” ya kweli ya Biblia.—Sefania 3:9.
Kufuatia Mambo Halisi ya Ufalme
14. Tunaweza kuimarishaje uthamini wetu wa uhalisi wa Ufalme?
14 Basi, tunaweza kufuatiaje mambo halisi ya Ufalme? Ni lazima tumaini letu litegemezwe kabisa kwenye usadikisho wenye nguvu. Ni lazima ulimwengu mpya wa Mungu ulioahidiwa uwe halisi kwetu. (2 Petro 3:13) Na ni lazima tuwe na imani katika ahadi ya kwamba Mungu “atafuta kila chozi katika macho [yetu], wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena.” (Ufunuo 21:4) Twawezaje kuwa na uhakika kwamba hiyo si fantasia tu? Ni lazima itimizwe katika wakati wa Mungu ufaao, kwani hawezi kusema uwongo. (Tito 1:1, 2; Waebrania 6:18) Ni lazima tutafakari juu ya ahadi hizo. Kujiona wenyewe katika ulimwengu mpya wa Mungu na kuonea shangwe baraka zao si fantasia isiyowezekana bali kunatoa uthibitisho wa imani. Kama vile Paulo alivyoifafanua, “imani ni taraja lililohakikishwa la mambo yanayotumainiwa, wonyesho dhahiri wa mambo halisi ingawa hayaonwi.” (Waebrania 11:1, NW) Acheni tuimarishe imani yetu kwa kujilisha Neno la Mungu na vichapo vya Kikristo vinavyotusaidia tuielewe na kuitumia. Na kadiri tutoapo wakati mwingi zaidi kuwaambia wengine juu ya Ufalme, kirasmi na ki-vivi-hivi, ndivyo tuimarishapo imani yetu na kufanya tumaini letu katika Ufalme huo liwe jangavu zaidi.
15. Tuna wajibu gani kuhusu huduma ya Kikristo?
15 Tunahitaji pia kufanya kazi kwa kupatana na mambo halisi ya Ufalme kwa kufanyia maendeleo huduma yetu. Kwa kuwa kuna mengi zaidi ya kufanywa, twaweza kufanyaje hilo? (Mathayo 9:37, 38) Ule usemi ni wa kweli kwamba mtu hawi mzee sana kujifunza. Haidhuru ni miaka mingapi tumekuwa tukishiriki katika kazi ya kutoa ushahidi, twaweza kufanya maendeleo. Kwa kuwa wenye mafanikio zaidi katika kushughulikia Neno la Mungu, tunakuwa na uwezo zaidi wa kuwasaidia wengine kuisikia sauti ya Mfalme, Yesu Kristo. (Linganisha Yohana 10:16.) Tunapoona kwamba matokeo ya milele ya maisha ya watu yanahusika, twapaswa kutaka kulihubiri eneo letu kikamili ili tuwape nafasi ya mara kwa mara ya kuonyesha msimamo wao, ama wakiwa “kondoo” ama wakiwa “mbuzi.” (Mathayo 25:31-46) Bila shaka, hilo lamaanisha kuweka maandishi yenye uangalifu ya wale ambao hawako nyumbani na hasa ya wale wenye kupendezwa katika ujumbe ya Ufalme.
Endelea Kuufuatia Ufalme
16. Ni nani ambao wameweka mfano mzuri katika kufuatia mambo halisi ya Ufalme, nao ‘wanautekaje’ Ufalme?
16 Juhudi nyingi inahitajiwa ili kuendelea kufuatia mambo halisi ya Ufalme. Je! sisi hatutiwi moyo na mfano wenye bidii wa wale Wakristo wapakwa-mafuta wanaobaki? Wamekuwa wakifuatia mambo halisi ya Ufalme kwa miongo mingi. Ufuatiaji huo ulielezwa katika maneno haya ya Yesu: “Tangu siku za Yohana Mbatizaji hata sasa ufalme wa mbinguni hupatikana kwa nguvu, nao wenye nguvu wauteka.” (Mathayo 11:12) Hapo wazo si lile la maadui kuuteka Ufalme. Bali, hilo lahusu utendaji wa wale watakaoupata Ufalme huo. Mwanachuo mmoja wa Biblia alisema hivi: “Katika njia hiyo kunaelezwa kule kujitahidi kusikozuilika na kule kushindania ule ufalme wa Kimesiya unaokaribia.” Wapakwa-mafuta wamejitahidi sana kufanya Ufalme huo uwe mali yao wenyewe. Jitihada kama hizo zahitajiwa pia kutoka kwa wale “kondoo wengine” ili waweze kustahili kuwa raia wa kidunia wa Ufalme wa Mungu wa kimbingu.—Yohana 10:16.
17. Ni nini kitakachowapata wale wanaofuatia fantasia za kilimwengu?
17 Kwa kweli, tunaishi katika kipindi cha pekee cha nafasi kubwa. Wale wanaofuatia fantasia za kilimwengu wataamka siku moja na kuona hasa jinsi mambo yalivyo hakika. Yatakayowapata yanaelezwa vizuri katika maneno haya: “Tena itakuwa kama mtu mwenye njaa aotapo, kumbe, anakula; lakini aamkapo, nafsi yake haina kitu; na kama mtu mwenye kiu aotapo, kumbe, anakunywa; lakini aamkapo, kumbe, anazimia, na nafsi yake inatamani.” (Isaya 29:8) Kwa hakika, fantasia za ulimwengu hazitamfanya mtu yeyote atosheke wala kuwa na furaha.
18. Kwa kufikiria uhalisi wa Ufalme, twapaswa kufuatia mwendo gani, kukiwa na tarajio jipi la wakati ujao?
18 Ufalme wa Yehova ni jambo halisi. Unatawala kwa bidii, huku mfumo huu mbovu wa mambo ukikabili uharibifu wa karibuni, wenye kudumu. Kwa hiyo, zingatia moyoni shauri hili la Paulo: “Basi tusilale usingizi kama wengine, bali tukeshe, na kuwa na kiasi.” (1 Wathesalonike 5:6) Na tukaze mioyo na akili zetu juu ya mambo halisi ya Ufalme na hivyo kuonea shangwe baraka za milele. Na tupate kusikia Mfalme wa Ufalme akituambia hivi: “Njoni, mliobarikiwa na Baba yangu, urithini ufalme mliowekewa tayari tangu kuumbwa ulimwengu.”—Mathayo 25:34.
[Maelezo ya Chini]
a Ona kitabu Biblia—Neno la Mungu au la Binadamu? kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
Ungejibuje?
◻ Fantasia za kilimwengu ni nini, na ni kwa nini twapaswa kuzikatalia mbali?
◻ Ni mifano gani inayoonyesha upumbavu wa kujifurahisha kwa fantasia za kilimwengu?
◻ Ni mambo gani ya hakika yanayothibitisha uhalisi wa Muumba, wa Neno lake lililoandikwa, wa Yesu Kristo, na wa Ufalme?
◻ Tunaweza kuimarishaje imani yetu katika mambo halisi ya Ufalme?
[Picha katika ukurasa wa 15]
Mara nyingi fantasia za kilimwengu husababishwa na kutamani utajiri wa kimwili
[Picha katika ukurasa wa 16]
Kuhubiri habari njema ni njia moja ya kufuatia mambo halisi ya Ufalme
[Picha katika ukurasa wa 17]
Je! wewe unafuatia mambo halisi ya Ufalme kwa kujifunza Neno la Mungu kwa bidii-nyendelevu?