Vijana Wanauliza...
Naweza Kuachaje Ndoto Nyingi za Mchana?
“NINA tatizo kubwa,” akakiri kijana aitwaye Jonathan. “Mimi huota ndoto za mchana ninapokuwa kazini, ninapotembea, kabla ya kulala, na hata katika Jumba la Ufalme. Kwa kawaida ni juu ya wasichana, ngono, au kuwa bingwa au shujaa maarufu.”
Kuota ndoto za mchana ni kawaida miongoni mwa watu wachanga na wenye umri mkubwa. Kukifanywa kwa kiasi, kwaweza kuwa tendo la kawaida, lifaalo.a Hata hivyo, kitu kizuri kikipita kiasi chaweza kudhuru. (Linganisha Mithali 25:16.) Ndivyo ilivyo hasa ikiwa hizo ndoto za mchana ni za aina mbaya.
Kwa mfano, tuseme kwamba wakati mwingine unajifikiria ukiwa mwimbaji unayempenda. Mara ya kwanza unaweza kutumia dakika chache kila siku ukijifikiria mwenyewe kuwa kwenye jukwaa ukisifiwa na watu. Lakini majuma yanapopita, unaanza kutumia wakati mwingi zaidi katika ulimwengu wako wa ndoto kwenye maonyesho ya muziki, mahojiano, na vipindi vya kurekodi. Ndoto hizo zinakuletea raha, na huwezi kuzikomesha.
‘Kwa hivyo, kuna madhara gani katika kuigiza?’ unauliza. Sababu moja ni kwamba, wataalamu wanasema kwamba wanaoota ndoto za mchana bila kujizuia mara nyingi “hawawezi . . . kufanikiwa katika ulimwengu halisi.” (The Parents’ Guide to Teenagers) Kuishi katika ulimwengu wa ndoto za mchana huzuia kukua; unashikilia vitabia vya utoto, badala ya kuviachilia mbali. (1 Wakorintho 13:11) Unasitawisha mahaba, badala ya maoni halisi ya maisha. Badala ya kusitawisha ‘akili zako za kufikiri’ yaani tatizo moja, unazisonga kwa kujiingiza katika ulimwengu wa ndoto. (Waebrania 5:14) Hivyo kuota ndoto za mchana kwatawala maisha yako, na kudhuru mahusiano na mambo yanayotangulizwa katika maisha halisi.
Kitabu Daydreaming, cha Dakt. Eric Klinger, chaonyesha kinachoweza kuwa hatari kubwa zaidi, kwa kuitaja, “kudumu katika jambo unalotaka lakini hupaswi kuwa nalo kunaweza kufanya iwe vigumu kwako kuacha kulifuatia.” Biblia husema hivi: “Kila mmoja hujaribiwa na tamaa yake mwenyewe huku akivutwa na kudanganywa.” (Yakobo 1:14) Tendo linatanguliwa na mawazo. Na ijapokuwa yaelekea hutakuwa mwanamuziki mzoefu wa dawa za kulevya kwa sababu tu ya ndoto za mchana, huenda ukasitawisha hamu mbaya ya “tamaa ya mwili, na tamaa ya macho.”—1 Yohana 2:16.
Kuzikomesha Ndoto za Mchana
Basi, unaweza kuvunjaje ndoto hizo? Kwanza, ingeweza kuwa msaada ukijiuliza ni kwa nini ndoto hii inakuvutia sana.b Je! ni kwa sababu unataka wengine wakupende? Je! unapata raha kwa kufikiria kwamba una urembo au kipawa ambacho kilimfanya mtu huyo maarufu ajulikane hivyo? Au labda unaonea wivu tu mtindo wa maisha wa kutojali wa mtu huyo. Mstadi mmoja wa akili alisema jambo hili kuhusu mwimbaji mashuhuri Madonna: “Katika akili za mashabiki wake, yeye hana wasiwasi wa pesa, kazi ya shule, na upweke.” Wengine basi wanaweza kuota kuwa kama yeye.
Ingawa hivyo, mambo halisi yaweza kukomesha ndoto kama hiyo. Tumia kanuni iliyo kwenye Wafilipi 4:8, ambamo tunaambiwa tudumu katika mambo yaliyo ya kweli na yenye kusifika. Je! ni kweli kwamba watu mashuhuri huwa na maisha mazuri? Je! maadili yao ni yenye kusifika? Kwa kweli, mtindo-maisha usiofaa unaotia ndani utendaji hatari, umewaacha wengi wakiwa wameumizwa kimwili na kihisia-moyo. Mbali na kuwa na mali, watu wengi mashuhuri wanaumia kifedha. Ni wachache wanaofurahia ndoa zenye kudumu. Je! unataka kuweka moyo wako kwenye maisha ya namna hiyo?
Bila shaka, ni jambo la asili kutaka kupendwa na kutamaniwa. Olivia mwenye umri wa miaka kumi na sita ana ndoto ya mchana ambayo humrudia ambayo hujifikiria kuwa “mtu aliye wa pekee ambaye kila mtu anampenda.” Lakini ndoto ya mchana—haidhuru kama ni kweli au halisi—haiwezi kutosheleza hizo tamaa kama vile kuota kwamba unakula hakuwezi kujaza tumbo lako. (Isaya 29:8) Zaidi ya hilo, Biblia huonya: “Mwenye kuuangalia upepo hatapanda.” (Mhubiri 11:4) Kwa hivyo badala ya kuota juu ya kupendwa, jitahidi kufanya upendeke.—Ona makala “Vijana Wanauliza . . . Naweza Kuwafanyaje Watu Wanipende?” katika toleo letu la Oktoba 8, 1989.
Ndoto za Ngono
Wakati wa miaka yake ya utineja, Alan (siyo jina lake hasa) alikuwa na ndoto za mchana za aina nyingine. “Alijifunza kubuni mawazo ya ashiki” na angetumia wakati wake mwingi akifanya hivyo. Baadaye, aliamua kuweka wakfu maisha yake kwa Mungu akiwa Mkristo. “Hilo halikubadili chochote,” akubali Alan. “Ndoto za mchana juu ya ngono ziliendelea kuwa njia yangu ya maisha.”
Je! wewe pia una tatizo la ndoto za mchana za kuamsha kingono?c Hilo laweza kuwa jambo la kawaida kama upo katika “uzuri wa ujana,” wakati tamaa za ngono zinapokuwa na nguvu. (1 Wakorintho 7:36) Hata hivyo, unajidhuru mwenyewe ikiwa unakuza kimakusudi mawazo ya ngono. Biblia katika Wakolosai 3:5 husema: “Basi, vifisheni viungo vyenu vya mwili vilivyo katika nchi, uasherati, uchafu, tamaa mbaya, na kutamani.” Kudumu katika ndoto za ngono huongeza tamaa mbaya. Kunaweza kuongoza kwenye kupiga punyeto—au kwenye uasherati hasa.
Unaweza kukomeshaje ndoto za ukosefu wa adili? Alan akumbuka: “Niliamua kushughulika nazo kwa kutafuta jambo jingine la badala. Singeweza kukazia akili ngono nilipokuwa nikikazia akili jambo jingine.” Alan alijifunza nidhamu. (1 Wakorintho 9:27) Alitafakari mambo yafaayo na akajifunza kuondoa mawazo yoyote ya ukosefu wa adili mara moja. (Zaburi 77:12) “Nilifanikiwa!” akumbuka Alan.
Kwa kupendeza, watafiti wameona kwamba sisi huota ndoto za mchana tunapokuwa hatuna mengi ya kufanya. Kwa hivyo kuwa na mengi ya kufanya, hasa “katika kazi ya Bwana,” ni njia nyingine ambayo inazuia kufikiri kubaya.—1 Wakorintho 15:58.
Usiruhusu Akili Yako Kutangatanga
Kwa vijana wengi, tatizo si yaliyomo katika ndoto zao za mchana, bali jinsi hizo zinaingilia kazi yao ya shule na masomo. “Siwezi kukaza fikira,” alalamika Karine mwenye umri wa miaka 16. “Siwezi kuweka akili yangu kwa jambo moja.” Unaweza kutoaje uangalifu kwa yale unayosikia? (Linganisha Marko 4:24.) Watafiti wengine wanaamini huenda ikasaidia ikiwa unajua unaota ndoto za mchana kwa kiwango gani. Labda ungeweza tu kuweka alama katika karatasi kila wakati unapopata akili ikitangatanga darasani. Wanafunzi walipofanya hivyo katika uchunguzi mmoja, ndoto za mchana zilipungua sana.
Pia jaribu kusitawisha kupendezwa kwa yale unayojifunza. Ikiwa umeamua kwamba hesabu inakera au historia inachosha akili, itakuwa vigumu kwako kukaza fikira. Ingawa hivyo, masomo yako yatakuwa yenye kupendeza ikiwa utajikumbusha jinsi unavyoweza kufaidika kutokana na habari hizo. Angalau kujifunza kutakusaidia ukuze “uwezo wa kufikiri.” (Mithali 1:4, NW) Unaweza pia kujifunza stadi za maana. Kwa mfano, hesabu itakusaidia katika kazi ya kuajiriwa, katika kupanga mambo ya nyumba, na katika kushughulikia madaraka fulani ya kundi. Ujuzi wa historia unaweza kukusaidia kuelewa watu na matukio ya karibuni. Daniel mwenye umri wa miaka 14, mmoja wa Mashahidi wa Yehova, anasema: “Sikuzote ninajaribu kuona jinsi masomo yangu ya nyumbani yanavyohusiana na Biblia na jinsi ninavyoweza kutumia habari hiyo katika kazi ya kuhubiri. Hilo hufanya akili yangu isifikirie kucheza mpira, na siwi na haraka ya kumaliza mgawo wangu.” Ndiyo, kadiri unavyothamini yale unayojifunza, ndivyo utakavyochochewa kutafuta ujuzi.—Linganisha Mithali 2:4.
Ni jambo gumu hasa kukaza fikira unapofanya jambo fulani la kawaida, kama vile kupika, kusafisha, au kupanga faili. Jinsi ilivyo rahisi kurudia ndoto! Hata hivyo, Biblia huonyesha kwamba uradhi mkubwa huja kutokana na kufanya kazi vizuri. (Mhubiri 2:24) Inatutia moyo kwamba ‘yoyote ufanyayo uyafanye kama kwa Yehova.’ (Wakolosai 3:23) Mwelekeo unaofaa kama huo unaweza kukusaidia ukaze fikira. “Ninapoweka akili yangu kwa yale ninayofanya,” akasema Samuel mwenye umri wa miaka 12, “kazi inafanywa upesi.”
Ndoto za mchana huenda zikaleta raha, lakini hayaondoi mambo halisi. Usiziruhusu zitawale maisha yako. Tia akili yako nidhamu. Kazia fikira mambo yanayofaa. Katika njia hii, hutaacha tu kuota ndoto za mchana sana bali utapata “uzima ulio kweli kweli.”—1 Timotheo 6:19.
[Maelezo ya Chini]
a Ona makala “Vijana Wanauliza . . . Je! Ni Vibaya Kuwa na Ndoto za Mchana?” katika toleo letu la Julai 8, 1993.
b Wakati mwingine kuwa na ndoto za mchana huonyesha kwamba kuna tatizo kubwa. Uchunguzi wa watu wazima walio na mwelekeo wa ndoto za mchana unaonyesha kwamba baadhi yao walikuwa wametendwa vibaya kimwili au kingono wakiwa watoto. Ndoto ilitumika kuwa chombo cha kukabiliana na hali. Kijana aliye katika hali ya kutendwa vibaya anahitaji kumwendea mtu mzima mwenye kutumainiwa ili apate msaada.
c Uchunguzi umeonyesha kwamba ndoto za ngono hufanyiza asilimia ndogo tu ya mawazo ya kuamka ya mtu wa kawaida. Lakini kitabu Daydreaming, cha Dakt. Eric Klinger chasema hivi: “Sisi huelekea kukumbuka haraka vitu ambavyo hutuamsha kihisia-moyo. Kwa sababu ndoto za mchana za kingono kwa ujumla ni zenye kuamsha sana, labda sisi huzikumbuka sana kuliko ndoto nyingine za mchana.”
[Picha katika ukurasa wa 21]
Badala ya kuota tu kuwa unapendwa, jitahidi kufanya upendeke