Vijana Wanauliza...
Je! Ni Vibaya Kuwa na Ndoto za Mchana?
Jambo la mwisho unalokumbuka ni sauti ya kivivu ya mwalimu akiongea juu ya hesabu za aljebra, lakini haupo tena darasani; akili zako zimeenda kwenye ufuko ambao familia yenu ilizuru kiangazi kilichopita. Unaweza kuhisi mchanga moto na ujoto wa jua. Unaweza kusikia sauti ya mawimbi yakiangukia ufuko, sauti ya watoto wanaocheza, sauti ya . . . vicheko vya wanadarasa wenzi? Naam, ndoto zako nzuri zimekwisha na mahali pazo panachukuliwa na mwalimu mwenye hasira, mkono ukiwa nyongani, anataka ujibu swali lake ambalo hukusikia.
NDOTO ZA MCHANA—ni za kawaida sana miongoni mwa watu wa kila aina, vijana kwa wazee, hivi kwamba mtafiti mmoja mashuhuri alizitaja kuwa “mojapo mambo makuu zaidi katika maisha ya kibinadamu.” Wengine huamini kwamba muda wapata theluthi moja ya saa ambao tuko macho huchukuliwa na ndoto za mchana kwa njia moja au nyingine. Wanasayansi hawana uhakika kabisa jinsi mawazo hayo ya muda mfupi hufanyizwa na kwa nini yanafanyizwa, wala hawakubaliani ulimwenguni pote juu ya fasili ya ndoto za mchana. Kamusi moja inafasili ndoto ya mchana kuwa “mwono wenye kufurahisha . . . uumbaji wa mawazo.” Hata hivyo, watafiti wengi huifasili kuwa inatia ndani aina yoyote ya mawazo ya mtu anapokuwa macho au mawazo yanayokuja yenyewe—yawe yanafurahisha au yasifurahishe. Katika makala hii tutatumia neno hilo katika maana yalo kubwa zaidi, kutia ndani mawazo yanayokuja yenyewe na vilevile yanayoletwa na mtu mwenyewe.
Basi, si ndoto zote za mchana ni mawazo yenye kupendeza na ya ajabu. Mengi huwa tu mawazo mafupi yenye kupendeza ya mambo yaliyopita. Katika makala moja katika gazeti Parents, Dakt. James Comer anataja ono lake mwenyewe la ndoto za mchana—kama vile anapoendesha gari kurudi nyumbani baada ya siku yenye kazi nyingi ofisini, mawazo yake yanaweza kuchukuliwa akumbuke jinsi alivyofunga bao vizuri kwenye uwanja wa mpira wa vikapu alipokuwa kijana. “Labda, ni mambo yasiyo na maana, lakini bado yananisaidia kuhisi vizuri,” yeye asema. Hata hivyo, watu wengine hutumia ndoto za mchana kupangia mambo yao ya wakati ujao. “Nilikuwa na ndoto nyingi za mchana za kuwa mwanamuziki anayetambuliwa kimataifa,” akumbuka mtu mmoja, ambaye kwa kweli alikuja kuwa mwanamuziki na mtungaji wa muziki wa jazi.
Ingawa hivyo, ndoto nyingi za mchana huonekana kukazia mambo ya kawaida—shule, vitumbuizo vya kijamii, kazi za shule zinazofanywa nyumbani. Nyakati nyingine watu wanaweza kufanyiza mambo hayo kimakusudi ili kuondoa uchovu wa hotuba isiyofurahisha shuleni au kazi ya nyumbani yenye kuleta uchovu. Ndoto nyinginezo za mchana huja tu zenyewe. Neno, sauti, au kitu fulani akilini kwa ghafula huwakumbusha juu ya uhitaji fulani wa wakati huo, hali fulani ya kufurahisha ya wakati uliopita, au kitu fulani cha kufanywa wakati ujao, na akili zao zaanza kutangatanga. Biblia inasema hivi: “Kwa maana ndoto huja kwa sababu ya shughuli nyingi.” (Mhubiri 5:3) Kwa kweli, mtu ambaye anajishughulisha na mambo na tamaa za kibinafsi anaweza kumezwa katika ndoto za mchana za mambo ya kimwili.
Hata hivyo, hata ndoto za mchana ziwe nzuri kama nini, zinaweza pia kuathiri jinsi unavyokaza akili kwenye mikutano ya Kikristo, shuleni, au kazini. Ndoto nyinginezo za mchana hata zaweza kuwa zisizofaa—au zenye kudhuru. Basi, je, ndoto za mchana ni tabia unayohitaji kuacha?
Je! Inadhuru Afya ya Akili Yako?
Katika nyakati zilizopita, ndoto za mchana zilidharauliwa na wafanyakazi wa afya ya akili, madaktari, na walimu. Basi kijana mmoja aliambiwa na tabibu wa akili hivi: “Ni lazima tukusaidie uache kuwa na ndoto za mchana.” Kulingana na mtafiti Dakt. Eric Klinger, shauri kama hilo kwa kawaida lilitegemea nadharia za wale wanaoitwa eti mwanzilishi wa utibabu wa akili, Sigmund Freud, aliyeona ndoto za mchana kuwa kitu cha kitoto na isiyoweza kuzuiliwa. Kwa hiyo, kitabu kimoja cha saikolojia ilidai hivi: “Ndoto za mchana mara nyingi ni tokeo la mtu kukosa kupendezwa kwa mazingira yake ya sasa, na kwa hakika ni kutoka kwa mambo halisi.” Kizazi cha walimu, na wafanyakazi wa afya ya akili walifundishwa kwamba ndoto zote za mchana zapaswa zizuiliwe. Madai yalifanywa kwamba ndoto za mchana za kupita kiasi zinaweza kutokeza ugonjwa wa kurukwa na akili.
Hata hivyo, nadharia za Freud zimeshindwa na mambo hakika ya utafiti mwingi. Katika kitabu chake Daydreaming, Dakt. Eric Klinger anasema kwamba miongoni mwa mambo mengine, watafiti wanadai kwamba:
Ndoto ya mchana ni utendaji unaotukia sana na ni wa kawaida.
Kwa kawaida, watu wenye ndoto za mchana mara nyingi wako sawasawa akilini kama vile wale ambao hawapati ndoto za mchana.
Ndoto za mchana haziongozi kwenye kupotewa na akili.
Ndoto za mchana haziongozi kwenye kurukwa na akili. Watu ambao wamerukwa akili hawana uwezekano wa kupata ndoto za mchana kuliko watu wengine.
Kutumia Mawazo kwa Njia Yenye Matokeo
Basi, haishangazi kwamba hakuna mahali popote ambapo Biblia inashutumu kutumia mawazo kwa njia inayofaa. Kwa kweli, uwezo wa akili zetu kuweza kuona vitu na kuwaza mambo ni uthibitisho kwamba sisi, katika maneno ya mtunga Zaburi, ‘tumeumbwa kwa jinsi ya ajabu.’ (Zaburi 139:14) Uwezo huo ukitumiwa kwa njia yenye matokeo, unaweza kuwa kitu cha thamani sana. Wakristo wanaambiwa ‘wasiviangalie vinavyoonekana, bali visivyoonekana.’ (2 Wakorintho 4:18) Hilo laweza kutia ndani kujaribu kufanyiza picha ya ulimwengu mpya wenye uadilifu wa Mungu akilini. Maelezo ya Biblia ya Paradiso hiyo ya duniani pote ya wakati ujao yatachochea mawazo yetu kwa habari hiyo!—Isaya 35:5-7; 65:21-25; Ufunuo 21:3, 4.
Mawazo yako pia yanaweza kukusaidia ikiwa una jambo gumu la kufanya. Kwa mfano, vijana miongoni mwa Mashahidi wa Yehova mara nyingi hupewa migawo ya kutoa hotuba katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Mbali na kufanya mazoezi kwa sauti, jaribu kurudia-rudia hotuba yako akilini. Jaribu kuwa na picha ya wasikilizaji wako wakiitikia habari unazotoa na jinsi unavyoitoa hotuba hiyo. Jambo hilo laweza kukusaidia ufanye marekebisho yanayohitajika katika hotuba yako na kukupa uhakika zaidi.
Unaweza pia kufanya mazoezi akilini ya jinsi ya kushughulikia hali ngumu. Labda unatambua kwamba Mkristo mwenzi ana jambo fulani dhidi yako, na unataka kuzungumzia tatizo hilo. (Mathayo 5:23, 24) Badala ya kumwendea mtu huyo bila kujitayarisha, unaweza kurudia hali hiyo akilini, ukijaribu njia tofauti za kutatua tatizo hilo. Jambo hilo lingepatana na kanuni hii ya Biblia: “Moyo wa mwenye haki hufikiri jinsi atakavyojibu.”—Mithali 15:28.
Je! mtu amekuchokoza au kukukasirisha? Tazama shauri linalotolewa katika Zaburi 4:4: “Mwe na hofu wala msitende dhambi, tafakarini vitandani mwenu na kutulia.” Jambo hilo halimaanishi kurudia-rudia hali zenye kuumiza akilini mwako, wala halimaanishi kuwa na picha akilini ya jinsi unavyochapa mtu kwa majibu makali. Iwayo yote, Yesu alionya kwamba “kila amwoneaye ndugu yake hasira itampasa hukumu,” kama vile “mtu akimfyolea ndugu yake.” (Mathayo 5:22) Lakini kupitia mambo unayoweza kufanya akilini—ambayo yanaweza kutia ndani kumsamehe tu mkosaji—kwaweza kukusaidia kusuluhisha matatizo naye kwa njia ya utulivu, na inayofaa.
Ndoto za mchana pia zinaweza kuwa na fungu zuri la kusuluhisha matatizo. Dakt. Klinger asema hivi: “Ndoto za mchana zenyewe ni njia ya kuvumbua masuluhisho yanayotumika kwa matatizo. Watu ambao huwa na ndoto za mchana nyakati nyingine wanaweza kupata masuluhisho ambayo hawangefikiria kama wangejaribu tu kuyatatua matatizo hayo kihususa.”
Kuna uthibitisho kwamba ndoto za mchana zinaweza kukusaidia kufanyia maendeleo njia yako ya kufanya kazi zako. Kwa mfano, mwalimu mmoja wa mchezo wa kutelezea juu ya theluji huambia wanafunzi wafanyize picha akilini ya uwanja ambao uko mbele wa kutelezea juu ya theluji na wajione wakipiga kila kona na kuingia ndani ya kila shimo katika uwanja huo. Watafiti wanaamini kwamba kufanya hivyo hasa huchochea ile sehemu ya ubongo unaodhibiti misuli, kukiichochea kwa ajili ya utendaji. Bila shaka, hakuna kitu kinachoweza kutumiwa kama badala ya mazoezi halisi, lakini kurudia-rudia jambo akilini kwaweza kukusaidia kufanya uwezo wako wa kucheza kinanda cha muziki au wa kuchapa maneno kuwa bora zaidi. “Kwa ufupi,” asema Dakt. James Comer, “ndoto ya mchana si kupoteza wakati bali ni kitulizo kinachohitajika cha kutusaidia kufanya kazi vizuri zaidi.”
Hatari za Ndoto za Mchana
Hata hivyo, “kwa kila jambo kuna majira yake.” (Mhubiri 3:1) Ingawa ndoto za mchana zaweza kufaa wakati unapostarehe chumbani mwako, kuna nyakati ambazo kufanya hivyo hakungefaa au hata kuwa hatari. Je! wewe huendesha gari? Basi unahitaji kuwa mwangalifu zaidi na kuwa macho kwa ajili ya hatari. Vipi wakati unapofanya mtihani fulani au unaposikiliza hotuba ya Biblia? Basi unahitaji kuwa na “fikira safi akilini.”—2 Petro 3:1, Habari Njema kwa Watu Wote.
Biblia pia inatutahadharisha dhidi ya kufikiria mno mambo yasiyofaa. Ni kawaida kuhangaika kidogo mtu anapokabili mtihani muhimu au mahoji ya kazi, lakini hutimizi kitu kwa kuweka akilini picha zenye kuhofisha za kushindwa na kukataliwa. (Linganisha Mhubiri 11:4.) “Uzito katika moyo wa mtu huuinamisha,” Mithali 12:25 inaonya. Yesu Kristo alishauri wasikilizaji wake hivi: “Msisumbukie ya kesho; kwa kuwa kesho itajisumbukia yenyewe. Yatosha kwa siku maovu yake.”—Mathayo 6:34.
Isitoshe, ndoto za mchana za kupita kiasi au zisizofaa zinaweza kutokeza hatari nyinginezo zaidi. Kwa mfano, vijana wengine hukuza mawazo ya kingono. Wengine hupata kwamba ndoto za mchana huharibu kukazia kwao akili kwa mambo. Makala yetu inayofuata katika mfululizo huu itatoa madokezo fulani ya kukusaidia kushughulikia matatizo kama hayo.
[Picha katika ukurasa wa 24]
Mazoezi ya akilini yanaweza kufanya utendaji halisi wa mtu kuwa bora