Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w92 8/15 kur. 10-15
  • Endeleeni Kujengana

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Endeleeni Kujengana
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kuepuka Usemi Uliooza
  • Fanyia Kazi Kuwajenga Wengine
  • Jenga Katika Njia ya Kimungu
  • Wazee Wanaojenga
  • Kuishi Kulingana na Sheria ya Kristo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Sema Lililo “Jema kwa Ajili ya Kujenga”
    “Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu”
  • Mavazi na Mapambo Yako—Je, Ni ya Maana kwa Mungu?
    Amkeni!—1998
  • Je, Mtindo Wako wa Mavazi Unamtukuza Mungu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2016
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
w92 8/15 kur. 10-15

Endeleeni Kujengana

“Neno lo lote lililo ovu lisitoke vinywani mwenu, bali lililo jema la kumfaa mwenye kuhitaji.”—WAEFESO 4:29.

1, 2. (a) Kwa nini yaweza kusemwa kwa kufaa kwamba usemi ni jambo la ajabu? (b) Ni onyo gani linalofaa kuhusu jinsi tunavyotumia ulimi wetu?

“USEMI ndio uzi wa ajabu unaounganisha pamoja marafiki, familia na jamii . . . Kutoka kwa akili ya kibinadamu na ile minyweo yenye kupatana ya vile vikundi-vikundi vya misuli [ya ulimi] sisi hutokeza sauti zinazochochea upendo, kijicho, staha—kwa kweli hisiamoyo yoyote ya kibinadamu.”—Hearing, Taste and Smell.

2 Ulimi wetu ni zaidi ya kuwa tu kiungo cha kumezea au kuonjea; ni sehemu ya uwezo wetu wa kushiriki lile tunalofikiri na kuhisi. “Ulimi nao ni kiungo kidogo,” akaandika Yakobo. “Kwa huo twamhimidi Mungu Baba yetu, na kwa huo twawalaani wanadamu waliofanywa kwa mfano wa Mungu.” (Yakobo 3:5, 9) Naam, twaweza kuzitumia ndimi zetu katika njia nzuri, kama vile kumsifu Yehova. Lakini tukiwa wasio wakamilifu, twaweza kwa urahisi kutumia ndimi zetu kusema mambo yenye kudhuru au yasiyofaa. Yakobo aliandika hivi: “Ndugu zangu, haifai mambo hayo kuwa hivyo.”—Yakobo 3:10.

3. Twapaswa kukazia fikira sehemu zipi mbili za usemi wetu?

3 Ingawa hakuna mwanadamu yeyote awezaye kudhibiti ulimi wake kikamilifu, twapaswa kwa hakika tujitahidi kufanya maendeleo. Mtume Paulo atushauri hivi: “Neno lo lote lililo ovu lisitoke vinywani mwenu, bali lililo jema la kumfaa mwenye kuhitaji, ili liwape neema [lile linalopendeleka, NW] wanaosikia.” (Waefeso 4:29) Ona kwamba agi-zo hilo lina sehemu mbili: lile tupaswalo tujitahidi kuepuka na lile tupaswalo tujaribu kufanya. Acheni tuchunguze sehemu zote mbili.

Kuepuka Usemi Uliooza

4, 5. (a) Wakristo wana pigano jipi kuhusu usemi mchafu? (b) Ni mfano gani uwezao kufaa yale maneno “neno lo lote lililo ovu”?

4 Waefeso 4:29 hutusihi hivi kwanza: “Neno lo lote lililo ovu lisitoke vinywani mwenu.” Hilo huenda lisiwe rahisi. Sababu moja ni kwamba unajisi umeenea sana katika ulimwengu unaotuzunguka. Wakristo wengi wachanga husikia matukano kila siku, kwani wanafunzi wenzao huenda wakafikiri kwamba hayo huongeza mkazo au huwafanya waonekane kuwa wenye nguvu zaidi. Huenda tusiweze kikamili kuepuka kusikia maneno machafu, lakini twaweza na twapaswa kujitahidi sana kutoweka hayo akilini. Hayana nafasi yoyote akilini wala vinywani mwetu.

5 Msingi wa onyo la Paulo ni neno la Kigiriki linalohusiana na samaki walioharibika au matunda yaliyooza. Ebu fikiria hili: ‘Wamtazama mtu anayeanza kukosa saburi na kisha kukasirika kabisa. Hatimaye alipuka kwa hasira, na kisha waona samaki aliyeharibika akitoka kinywani mwake. Halafu waona matunda yaliyooza, yenye harufu mbaya, yakianguka, na maji yayo yakiwarukiarukia wote walio karibu. Mtu huyo ni nani? Ingalikuwa vibaya kama nini ikiwa angalikuwa mmoja wetu! Hata hivyo, tungekuwa kama yeye ikiwa tungeruhusu ‘neno lolote lililooza litoke kinywani mwetu.’

6. Waefeso 4:29 hutumikaje kwa usemi wenye kuchambua, usiofaa?

6 Utumizi mwingine wa Waefeso 4:29 ni kwa sisi kuepuka kuwa wachambuzi sikuzote. Ni kweli, sisi sote tuna maoni na ladha mbalimbali kuhusu mambo ambayo hatupendi au kukubali, lakini je, umekuwa karibu na mtu anayeonekana kuwa na elezo (au maelezo mengi) lisilofaa juu ya kila mtu, mahali, au jambo linalotajwa? (Linganisha Warumi 12:9; Waebrania 1:9.) Usemi wake huvunja, hushusha moyo, au huharibu. (Zaburi 10:7; 64:2-4; Mithali 16:27; Yakobo 4:11, 12) Huenda asitambue jinsi anavyofanana na wale wachambuzi ambao Malaki alieleza juu yao. (Malaki 3:13-15) Angeweza kushangaa kama nini ikiwa mtu aliyekuwa akimtazama angemwambia kwamba samaki aliyeharibika au matunda yaliyooza yalikuwa yakitoka kinywani mwake!

7. Kila mmoja wetu apaswa kujichunguzaje kibinafsi?

7 Ingawa huenda ikawa rahisi kutambua wakati mtu mwingine anapotoa maelezo yasiyofaa au yenye kuchambua sikuzote, jiulize mwenyewe hivi, ‘Je! mimi nina mwelekeo wa kufanya hivyo? Je! kweli ninao?’ Lingekuwa jambo la hekima kuchunguza mwelekeo wa maneno yetu pindi kwa pindi. Je! sisi kwa msingi husema maneno yasiyofaa, yenye kuchambua? Je! sisi husikika kama wale wafariji watatu bandia wa Ayubu? (Ayubu 2:11; 13:4, 5; 16:2; 19:2) Kwa nini usipate jambo zuri la kutaja? Mazungumzo yakiwa yenye kuchambua hasa, kwa nini usiyageuze kuwa mambo ya kujenga?

8. Malaki 3:16 huandaa somo gani kuhusu usemi, na twaweza kuonyeshaje kwamba tunatumia somo hilo?

8 Malaki alionyesha tofauti hii: “Ndipo wale waliomcha BWANA [Yehova, NW] waliposemezana wao kwa wao. Naye BWANA [Yehova, NW] akasikiliza, akasikia; na kitabu cha ukumbusho kikaandikwa mbele zake, kwa ajili ya hao waliomcha BWANA [Yehova, NW], na kulitafakari jina lake.” (Malaki 3:16) Je! uliona jinsi Yehova alivyoitikia usemi wenye kujenga? Yaelekea mazungumzo hayo yalikuwa na matokeo gani kwa washirika wenzi? Twaweza kibinafsi kujifunza somo kuhusu usemi wetu wa kila siku. Inafaa zaidi kama nini kwetu na kwa wengine ikiwa mazungumzo yetu ya kawaida huonyesha ‘dhabihu yetu ya sifa kwa Mungu.’—Waebrania 13:15.

Fanyia Kazi Kuwajenga Wengine

9. Ni kwa nini mikutano ya Kikristo ni pindi nzuri za kujenga wengine?

9 Mikutano ya kundi ni pindi zilizo bora zaidi za kusema ‘maneno ya kufaa na ambayo hujenga na kuwasaidia wengine, ili yawaneemeshe wasikilizaji.’ (Waefeso 4:29, HNWW) Twaweza kufanya hivyo tunapotoa hotuba juu ya habari ya Kibiblia, tunaposhiriki katika wonyesho, au tunapotoa maelezo wakati wa sehemu za maswali na majibu. Hivyo tunahakikisha maneno ya Mithali 20:15: “Midomo ya maarifa ni kito cha thamani.” Ni nani ajuaye ni mioyo mingapi tunayogusa au kujenga?

10. Baada ya kufikiria juu ya wale ambao tumezungumza nao kwa ukawaida, ingefaa tufanye rekebisho gani? (2 Wakorintho 6:12, 13)

10 Wakati kabla na baada ya mikutano unafaa ili kuwajenga wengine kwa mazungumzo yanayowapa wasikiao lile linalopendeleka. Ingekuwa rahisi kutumia vipindi hivyo kwa maongezi yenye kupendeza pamoja na watu wa ukoo na marafiki wachache ambao tukiwa nao twahisi tumestareheka. (Yohana 13:23; 19:26) Hata hivyo, kulingana na Waefeso 4:29, kwa nini tusitafute wengineo kusema nao? (Linganisha Luka 14:12-14.) Tungeweza kuamua kimbele kusema zaidi ya salamu ya kidesturi tu au kusema hujambo ya kijuujuu kwa wapya fulani, watu wazee-wazee, au vijana, hata kuketi pamoja na wachanga ili tufikie urefu wao. Kupendezwa kwetu kikweli na vipindi vya usemi wenye kujenga vitawafanya wengine waweze hata zaidi kurudia maoni ya Daudi kwenye Zaburi 122:1.

11. (a) Wengi wamesitawisha zoea gani kuhusu mahali pa kuketia? (b) Ni kwa nini wengine hubadili mahali pao pa kuketia kimakusudi?

11 Msaada mwingine ili kuwe mazungumzo yenye kujenga ni kwa kubadilisha-badilisha mahali tunapoketia mikutanoni. Mama mwenye mtoto anayemnyonyesha huenda akahitaji kuketi karibu na choo, au mtu asiyejiweza huenda akahitaji kiti kilichopo mwisho wa safu, lakini namna gani sisi wengine? Mazoea tu huenda yakatuongoza turudi kwenye kiti au mahali palepale; hata ndege hurudia makao yake kisilika. (Isaya 1:3; Mathayo 8:20) Lakini, kwa kweli, kwa kuwa twaweza kuketi mahali popote, kwa nini tusibadilishe mahali petu pa kuketia—upande wa kulia, upande wa kushoto, karibu na mbele, na kadhalika—na hivyo tupate kufahamiana na watu tofauti-tofauti? Ingawa hakuna amri yoyote inayotutaka tufanye hivyo, wazee na wakomavu wengineo wanaobadilisha mahali wanapoketia wamepata kwamba ni rahisi kutoa lile linalopendeleka kwa wengi badala ya kwa marafiki wachache tu kwa kulinganisha.

Jenga Katika Njia ya Kimungu

12. Ni mwelekeo gani usiotamaniwa ambao umedhihirishwa muda wote wa historia?

12 Tamaa ya Mkristo ya kujenga wengine yapaswa imsukume amwige Mungu kwa habari hii badala ya kufuata ule mwelekeo wa kibinadamu wa kufanya amri nyingi sana.a Kwa muda mrefu wanadamu wasio wakamilifu wamekuwa na mwelekeo wa kutawala wale wanaowazunguka, na hata baadhi ya watumishi wa Mungu wamefuata mwelekeo huo. (Mwanzo 3:16; Mhubiri 8:9) Katika wakati wa Yesu viongozi Wayahudi ‘walifunga mizigo mizito na kuwatwika watu mabegani mwao; wasitake wenyewe kuigusa kwa kidole chao.’ (Mathayo 23:4) Waligeuza desturi zisizodhuru kuwa mapokeo ya lazima. Kwa kuhangaikia kwao mno amri za kibinadamu, walipuuza mambo ambayo Mungu alitambulisha kuwa yenye maana zaidi. Hakuna aliyejengwa na kufanya kwao amri nyingi zisizokuwa za kimaandiko; njia yao haikuwa njia ya Mungu hata kidogo.—Mathayo 23:23, 24; Marko 7:1-13.

13. Kwa nini haifai kuwatungia Wakristo wenzetu amri nyingi?

13 Wakristo wanataka kwa kweli kufuata sheria za kimungu. Hata hivyo, sisi pia tungeweza kuathiriwa na ule mwelekeo wa kufanya amri nyingi zenye kulemeza. Kwa nini? Kwanza, ladha au mapendeleo hutofautiana, kwa hiyo wengine huenda wakaona jambo fulani kuwa lenye kukubalika ambalo wengine huchukia na huona halifai. Wakri-sto hutofautiana pia, katika maendeleo yao kuelekea ukomavu wa kiroho. Lakini je, kufanya amri nyingi ndiyo njia ya kimungu ya kumsaidia mwingine afanye maendeleo kuelekea ukomavu? (Wafilipi 3:15; 1 Timotheo 1:19; Waebrania 5:14) Hata wakati ambapo mtu kwa kweli anafuatia mwendo unaoonekana kuwa wenye kupita kiasi mno au wenye hatari, je, amri ya kumzuia ndilo suluhisho lifaalo kabisa? Njia ya Mungu ni kwamba wale wanaostahili wajaribu kumrudisha mtu ambaye amekosea kwa kusababu pamoja na mtu huyo kwa upole.—Wagalatia 6:1.

14. Ni makusudi gani yaliyotimizwa na sheria ambazo Mungu alitolea Israeli?

14 Ni kweli, alipotumia Israeli kuwa watu wake, Mungu aliweka mamia ya sheria kuhusu ibada ya hekalu, dhabihu, hata usafi. Hilo lilifaa ili kuwe taifa lililo tofauti, na nyingine za sheria hizo zilikuwa na umaana wa kiunabii nazo zilisaidia kuwaongoza Wayahudi kwa Mesiya. Paulo aliandika hivi: “Torati imekuwa kiongozi kutuleta kwa Kristo, ili tuhesabiwe haki kwa imani. Lakini iwapo imani imekuja, hatupo tena chini ya kiongozi.” (Wagalatia 3:19, 23-25) Baada ya sheria kufutiliwa mbali kwenye mti wa mateso, Mungu hakuwapa Wakristo orodha ndefu ya amri kuhusu sehemu nyingi za maisha, kana kwamba hiyo ndiyo ilikuwa njia ya kuwajenga katika imani.

15. Mungu ameandaa mwongozo gani kwa ajili ya waabudu Wakristo?

15 Bila shaka, sisi hatuko bila sheria. Mungu hutuamuru tujiepushe na ibada ya sanamu, uasherati na uzinzi, na utumizi mbaya wa damu. Yeye hukataza kimahususi uuaji wa kimakusudi, kusema uwongo, uwasiliani-roho, na dhambi nyinginezo mbalimbali. (Matendo 15:28, 29; 1 Wakorintho 6:9, 10; Ufunuo 21:8) Na yeye hutoa katika Neno lake shauri la wazi kuhusu mambo mengi. Hata hivyo, kwa kadiri kubwa zaidi ya Waisraeli, tuna daraka la kujifunza na kutumia kanuni za Biblia. Wazee wanaweza kuwajenga wengine kwa kuwasaidia wapate na kuzichunguza kanuni hizo kuliko tu kutafuta au kufanya amri.

Wazee Wanaojenga

16, 17. Mitume walitoa mfano gani mzuri kuhusu kuwafanyia waabudu wenzi amri?

16 Paulo aliandika hivi: “Hapo tulipofika na tuenende katika lilo hilo.” (Wafilipi 3:16) Kulingana na maoni hayo ya kimungu, mtume alishughulika na wengine kwa njia iliyojenga. Kwa mfano, swali lilitokea kuhusu kama ingefaa kula nyama ambayo huenda ikawa ilitoka kwa hekalu la sanamu. Je! mzee huyo alitoa amri fulani kwa wote katika makundi ya mapema, labda kwa kusudi la kupatanisha mambo au kuyarahisisha? La. Alikiri kwamba tofauti katika maarifa na maendeleo kuelekea ukomavu ingeongoza Wakristo hao kwenye uchaguzi tofauti-tofauti. Kwa habari yake, aliazimia kuweka mfano mzuri.—Warumi 14:1-4; 1 Wakorintho 8:4-13.

17 Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo huonyesha kwamba mitume waliandaa shauri lenye msaada juu ya mambo fulani ya kibinafsi, kama vile kuhusu mavazi na mapambo, lakini hawakuamua kufanya amri za kufuatwa nyakati zote. Leo huo ni mfano mzuri kwa waangalizi Wakristo, wanaopendezwa na kulijenga kundi la kondoo. Nao kwa kweli huonyesha njia ya msingi ambayo Mungu alifuata hata kwa kushughulika na Israeli wa kale.

18. Yehova alitolea Israeli amri zipi kuhusu mavazi?

18 Mungu hakuwapa Waisraeli sheria nyingi kuhusu nguo. Yaonekana wanaume na wanawake walitumia mavazi ya nje yaliyofanana, ingawa ya mwanamke yangeweza kuwa yenye kutarizwa au yenye rangi-rangi. Jinsia zote mbili zilivaa pia sa·dhinʹ, au vazi la ndani. (Waamuzi 14:12; Mithali 31:24; Isaya 3:23) Mungu alitoa sheria zipi kuhusu mavazi? Wala wanaume wala wanawake wasingevaa mavazi ambayo yangewatambulisha na jinsia tofauti, wakiwa kwa wazi na nia ya kufanya ngono ya jinsia moja. (Kumbukumbu la Torati 22:5) Ili kuonyesha wao ni tofauti na mataifa yaliyowazunguka, Waisraeli walihitaji wajifanyie vishada katika ncha za mavazi yao, kukiwa na uzi wa buluu juu ya vishada hivyo, na labda vifundo kwenye pembe za mavazi hayo. (Hesabu 15:38-41) Huo kwa msingi ndio mwelekezo ambao Sheria ilitoa kuhusu mitindo ya mavazi.

19, 20. (a) Biblia huwapa Wakristo mwelekezo gani juu ya nguo na mapambo? (b) Wazee wanapaswa kuwa na maoni gani juu ya kufanya amri kuhusu sura ya kibinafsi?

19 Ingawa Wakristo hawako chini ya Sheria, je, tuna amri nyinginezo zenye kueleza mengi kuhusu nguo au mapambo zilizotolewa kwa ajili yetu katika Biblia? Sivyo kwa kweli. Mungu aliandaa kanuni zenye usawaziko ambazo twaweza kutumia. Paulo aliandika hivi: “Wanawake na wajipambe kwa mavazi ya kujisitiri, pamoja na adabu nzuri, na moyo wa kiasi; si kwa kusuka nywele, wala kwa dhahabu na lulu, wala kwa nguo za thamani.” (1 Timotheo 2:9) Petro alisihi kwamba badala ya kukazia fikira mapambo ya kimwili, wanawake Wakristo walipaswa wakazie fikira “utu wa moyoni usioonekana, katika mapambo yasiyoharibika; yaani; roho ya upole na utulivu.” (1 Petro 3:3, 4) Jambo la kwamba shauri hilo lilirekodiwa ladokeza kwamba baadhi ya Wakristo katika karne ya kwanza huenda ikawa walihitaji kuwa wenye kiasi na wenye kujizuia zaidi katika nguo zao na kujipamba kwao. Hata hivyo, badala ya kutaka—au kukataza—mitindo fulani, mitume waliandaa tu shauri lenye kujenga.

20 Mashahidi wa Yehova wanapaswa kustahiwa na kwa ujumla hustahiwa kwa ajili ya sura zao zenye kiasi. Hata hivyo, mitindo hutofautiana kutoka nchi moja hadi nyingine na hata katika eneo au kundi fulani. Bila shaka, mzee mwenye maoni yenye nguvu au mwenye ladha fulani kuhusu nguo na mapambo aweza kujiamulia yeye mwenyewe na familia yake kulingana na maoni yake. Lakini kwa habari ya kundi la kondoo, anahitaji kukumbuka jambo aliloonyesha Paulo: “Si kwamba tunatawala imani yenu; bali tu wasaidizi wa furaha yenu; maana kwa imani yenu mnasimama.” (2 Wakorintho 1:24) Naam, kwa kupinga mwelekeo wowote wa kuwekea kundi amri, wazee hujitahidi kujenga imani ya wengine.

21. Wazee wanaweza kuandaaje msaada ikiwa mtu fulani anapita kiasi kwa habari ya nguo?

21 Sawa na katika karne ya kwanza, nyakati nyingine mpya au aliye dhaifu kiroho huenda akafuata mwendo wenye kutiliwa shaka au usio wenye hekima kwa habari ya nguo au utumizi wa rangi za uso au wa vito. Namna gani kuhusu hilo? Tena, Wagalatia 6:1 hutoa mwongozo kwa wazee Wakristo wanaotaka kusaidia kwa unyoofu. Kabla ya mzee kuamua kutoa shauri, aweza kwa hekima kumwomba mzee mwenzake shauri, yafaa zaidi asimwendee mzee ambaye ajua hushiriki ladha au maoni yake. Ikiwa inaonekana kwamba mtindo wa nguo au mapambo ya kilimwengu huathiri wengi kundini, baraza la wazee laweza kuzungumzia jinsi ifaavyo zaidi kuandaa msaada, kama vile kupitia sehemu ya mkutano yenye fadhili, inayojenga au kwa kutoa msaada kwa mtu mmoja mmoja. (Mithali 24:6; 27:17) Lengo lao lingekuwa kutia moyo kuwe na maoni yanayoonyeshwa kwenye 2 Wakorintho 6:3: “Tusiwe kwazo la namna yo yote katika jambo lo lote, ili utumishi wetu usilaumiwe.”

22. (a) Kwa nini lisiwe jambo la kutatiza ikiwa kuna maoni tofauti-tofauti? (b) Paulo aliandaa mfano gani mzuri?

22 Wazee Wakristo ‘wanaolichunga kundi la Mungu lililo katika uangalizi wao’ wana-taka kufanya kama alivyoonyesha Petro, yaani, si “kupiga ubwana juu ya wale ambao ni urithi wa Mungu.” (1 Petro 5:2, 3, NW) Wanapofanya kazi yao yenye upendo, maswali huenda yakatokea juu ya mambo ambayo yangehusu mapendeleo tofauti-tofauti. Labda ni desturi ya mahali fulani kusimama ili kusoma mafungu wakati wa Funzo la Mnara wa Mlinzi. Mipango ya vikundi kwa ajili ya utumishi wa shambani na mambo mengi madogo-madogo kuhusu huduma yenyewe huenda yakafanywa kulingana na desturi za mahali fulani. Hata hivyo, je, ungekuwa msiba ikiwa mtu fulani angekuwa na njia iliyo tofauti kidogo? Waangalizi wenye upendo hutamani kwamba ‘mambo yote yatendeke kwa uzuri na kwa utaratibu,’ ambao ni usemi uliotumiwa na Paulo kuhusu zawadi za kimuujiza. Lakini muktadha huonyesha kwamba jambo lililompendeza Paulo hasa lilikuwa “ili kulijenga kanisa [kundi, NW].” (1 Wakorintho 14:12, 40) Yeye hakuonyesha mwelekeo wowote wa kufanya amri zisizo na mwisho, kana kwamba usawa mkamilifu au utendaji kazi wa kikamili ulikuwa ndilo kusudi lake kuu. Aliandika hivi: “[Mamlaka] tuliyopewa na Bwana, [ni ili] tupate kuwajenga wala si kuwaangusha.”—2 Wakorintho 10:8.

23. Ni baadhi gani za njia ambazo kwazo twaweza kuuiga mfano wa Paulo wa kuwajenga wengine?

23 Paulo bila shaka alifanya kazi ili kuwajenga wengine kwa usemi chanya na wenye kutia moyo. Badala ya kushirikiana na marafiki wachache tu, alijitahidi sana kuwatembelea ndugu na dada wengi, wale wenye nguvu kiroho na pia wale waliohitaji kujengwa hasa. Na yeye alikazia upendo—kuliko amri—kwani “upendo hujenga.”—1 Wakorintho 8:1.

[Maelezo ya Chini]

a Katika familia amri mbalimbali huenda zikafaa, kwa kutegemea hali. Biblia huwapa wazazi mamlaka ya kuwaamulia mambo watoto wao wachanga.—Kutoka 20:12; Mithali 6:20; Waefeso 6:1-3.

Mambo ya Kurudia

◻ Kwa nini badiliko lafaa ikiwa tuna mwelekeo wa usemi usiofaa au wenye kuchambua?

◻ Twaweza kufanya nini ili tuwe wenye kujenga zaidi kundini?

◻ Ni kigezo gani cha kimungu kinachohusu kuwafanyia wengine amri nyingi?

◻ Ni nini kitakachowasaidia wazee waepuke kulifanyia kundi la kondoo amri za kibinadamu?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki