Wapiga Mbiu ya Ufalme Waripoti
Kondoo wa Yesu Husikiliza Sauti Yake
KAZI ya kuhubiri ipanukapo kwenye sehemu zote za dunia, Yehova kupitia malaika wake huwaelekeza watumishi wake kwa wale wenye mfano wa kondoo. Wanasikia sauti ya Yesu na kujifunza kumtumikia wakiwa na tumaini la uhai wa milele. Yesu alisema hivi kwenye Yohana 10:27, 28: “Kondoo wangu waisikia sauti yangu; nami nawajua, nao wanifuata. Nami nawapa uzima wa milele.” Ona jinsi wale wenye mioyo minyoofu katika Madagaska wanavyosikiliza sauti ya Yesu.
Mmoja wa Mashahidi wa Yehova alimpa tabibu mmoja aliyekuja kumwangalia baba yake mgonjwa, nakala za vitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani na Kupata Faida Zote za Ujana Wako.
Huyo daktari alikuwa Mprotestanti na mwenye kupinga sana Mashahidi, lakini alisoma kitabu hicho na kuchunguza maandiko katika Biblia yake mwenyewe. Mke wake, aliyekuwa Mkatoliki na daktari pia, alisoma kitabu Ujana mara kadhaa kwa sababu alisema kilionekana kana kwamba kiliandikwa kwa ajili yake hasa. Elezo la Sosaiti lenye msingi wa Biblia kuhusu umaana wa 1914 liliwavutia wote wawili. Mume aliwasiliana na Shahidi aliyempa vitabu hivyo. Huyo Shahidi alimpa kitabu Life—How Did It Get Here? By Evolution or by Creation? akafanya mipango ya kumtembelea yeye na mke wake ili kujibu maswali yao. Alipowatembelea, alianza funzo la Biblia la kawaida pamoja na wenzi hao wa ndoa na watoto wao watatu. Maendeleo katika uelewevu wa Biblia yalikuwa ya haraka.
Baada ya funzo la kwanza, familia nzima ilianza kuhudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme na upesi baada ya hapo walijiandikisha katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Mwenendo wa watoto uliendelea kuwa bora sana. Kutokana na funzo lao la Biblia, walijifunza kwamba kusherehekea siku za kuzaliwa na sikukuu nyinginezo za kidini hakukuwa jambo la Kikristo; kwa hiyo, waliacha kuziadhimisha. Mume alikataa kumtolea mtu wa ukoo damu yake, hata ingawa habari hiyo haikuwa imezungumziwa katika funzo la Biblia. Upesi mavazi yake ya karate yakatoweka kutoka katika kabati yake; aliyapeleka kwa fundi wake wa nguo ili awatengenezee watoto wake nguo. Alichoma magazeti na vitabu vyake vyote kuhusu falaki. Miezi mitatu tu baada ya wao kuanza kujifunza, huyo mume na mke wake pia walijiuzulu kila mmoja kutoka kwa kanisa lake wakaonyesha tamaa yao ya kushiriki katika kazi ya kuhubiri. Sasa wamebatizwa.
Mwanamke mmoja katika Thailandi alikuwa akitafuta kweli. Ingawa alikuwa katika dini ya Kibuddha, hakuwa kamwe amejitolea dini yake kwa sababu alikuwa ameona unafiki na pupa nyingi mno. Isitoshe, kulikuwako desturi mbalimbali alizoona kuwa zenye kuudhi. Alikuwa amechoka na hayo yote.
Kisha, jirani mmoja alipendekeza kwamba huyo mwanamke ajaribu Wakristo, basi akampeleka kwenye kanisa la Kipentekoste. Hata hivyo, wakati wa mahubiri, huyo mwanamke alitamani sana kuondoka na kwenda nyumbani kwa sababu ya kelele, kwani wote waliokuwapo walikuwa wakisali kwa sauti kubwa. Hiyo ilikuwa mara ya mwisho alipohudhuria kanisa hilo.
Baadaye, akajaribu kanisa la Katoliki ya Kiroma. Hata hivyo, baada ya kuhudhuria mara kadhaa, alianza tena kuona unafiki na pupa, pamoja na mtindo-maisha wa anasa wa padri. Alichukizwa na kuacha kwenda huko. Padri alitaka kujua ni kwa nini huyo mwanamke aliondoka. Baada ya kupata kujua sababu, alisema katika njia ya kudhihaki: “Ukitaka kujiunga na watu wenye kufuata sana kanuni, enda kwa Mashahidi wa Yehova.” Akauliza: “Wako wapi?” Padri akajibu: “Wako karibu na jengo la shirika la maji.” Siku iliyofuata aliwatafuta bila kufanikiwa. Akiwa ametamauka, yeye bado aliendelea kuwafikiria Mashahidi wa Yehova.
Siku moja alimsikia mmoja wa majirani wake akimwambia mwingine kwa kudhihaki: “Hivi karibuni utakuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova!” Aliposikia hilo, huyo mwanamke alimwendea huyo jirani kwa haraka na kuuliza: “Je! kuna Mashahidi wa Yehova huku?” Jibu lilikuwa, “Ndiyo.” “Baadhi yao watakuja kwenye ujirani huu wakihubiri nyumba kwa nyumba. Utawatambua kwa njia yao ya kuvalia iliyo safi na nadhifu.” Baada ya hayo huyo mwanamke alikimbia nje ili awatafute. Mwanzoni hakuwapata, lakini alipokuwa akitembea kurudi nyumbani kwake, aliona wanawake wawili waliovalia kinadhifu wakizungumza na mtu fulani. Alikaribia na kuuliza ikiwa walikuwa Mashahidi wa Yehova. Waliposema ndiyo, alisihi hivi: “Tafadhali njooni nyumbani kwangu. Ninataka kuongea nanyi.”
Funzo la Biblia lilianzishwa, na ijapokuwa upinzani na dhihaka kutoka kwa washiriki wa familia, huyo mwanamke ameanza kuhudhuria mikutano na kuwatolea ushahidi watu wake wa ukoo.
Yesu kwa kweli anawajua kondoo wake na anawakusanya ndani ya tengenezo lake ili waokoke kuingia ulimwengu wake mpya wenye uadilifu.