Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w92 10/15 kur. 30-31
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Habari Zinazolingana
  • Maswali Kutoka Kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Kubali Mwongozo wa Mungu Aliye Hai
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2004
  • Damu—Ni Muhimu kwa Uhai
    Damu Yaweza Kuokoaje Uhai Wako?
  • Damu
    Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
w92 10/15 kur. 30-31

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Wakristo wanapaswa wahangaike kadiri gani kwamba sehemu za damu, kama vile plazima iliyokaushwa, huenda zikawa zimeongezwa katika vyakula?

Ikiwa kuna msingi wa hakika wa kuamini kwamba damu ya mnyama (au sehemu yayo) kwa wazi inatumiwa katika vyakula mahali fulani, Mkristo apaswa ajihadhari ifaavyo. Hata hivyo, lisingekuwa jambo la hekima kuhangaishwa na shuku tu au kuishi na wasiwasi usio na msingi.

Mapema katika historia ya mwanadamu, Muumba wetu aliamuru kwamba wanadamu hawapaswi kula damu. (Mwanzo 9:3, 4) Alitaarifu kwamba damu huwakilisha uhai, ambao ni zawadi kutoka kwake. Damu iliyoondolewa kutoka kiumbe ingeweza kutumiwa tu katika dhabihu, kama vile kwenye madhabahu. La sivyo, damu kutoka kiumbe ilipaswa imwagwe kwenye ardhi, kwa maana fulani ya kuirudisha kwa Mungu. Watu wake walipaswa waepuke kutegemeza uhai kwa kula damu. Aliamuru hivi: “Msile damu ya mnyama wa aina yo yote; kwa kuwa uhai wa wanyama wote ni katika hiyo damu yake; atakayeila awaye yote atakatiliwa mbali.” (Mambo ya Walawi 17:11-14) Katazo la Mungu juu ya kula damu lilirudiwa kwa Wakristo. (Matendo 15:28, 29) Kwa hiyo Wakristo wa mapema walihitaji kuepuka chakula chenye damu, kama vile nyama kutoka kwa wanyama wa kunyongwa au soseji zenye damu.

Lakini, Wakristo hao wangetendaje katika njia zifaazo kulingana na azimio lao la ‘kujilinda nafsi zao na damu’? (Matendo 21:25) Je! watumie tu maneno ya Paulo kwamba: “Kila kitu kiuzwacho sokoni kuleni, bila kuuliza-uliza, kwa ajili ya dhamiri”?

La. Yale maneno kwenye 1 Wakorintho 10:25 hurejezea nyama ambayo huenda ikawa imetoka kwa mnyama aliyetolewa dhabihu kwenye hekalu la sanamu. Wakati huo, nyama ya ziada kutoka mahekalu iliondolea mbali kwa kuuzwa kwa wafanyi biashara, ambao huenda ikawa waliitia miongoni mwa ugavi wao wa nyama ya kuuzwa madukani mwao. Jambo kuu la Paulo lilikuwa kwamba nyama kutoka kwa hekalu haikuwa mbaya au chafu yenyewe. Yaonekana lilikuwa jambo la kidesturi kuondoa na kutumia kwenye madhabahu ya kipagani damu ya wanyama waliotolewa dhabihu huko. Kwa hiyo ikiwa sehemu fulani ya nyama ya ziada iliuzwa sokoni, bila kuwa na jambo lolote la kuihusianisha na hekalu au na mawazo yasiyofaa ya wapagani, Wakristo wangeweza tu kuinunua kuwa nyama ya kuuzwa iliyokuwa safi na iliyokuwa imeondolewa damu ifaavyo.

Hata hivyo, hali ingepaswa kuwa tofauti ikiwa Wakristo hao wangejua kwamba nyama kutoka kwa wanyama walionyongwa (au soseji yenye damu) imo miongoni mwa vitu bora kabisa kwenye maduka ya mahali fulani. Wangehitaji kujihadhari katika kuchagua nyama ya kununua. Huenda ikawa wangeweza kutambua vitu vyenye kufanyizwa kwa nyama vilivyokuwa na damu ikiwa vingekuwa na rangi tofauti (sawa na vile leo soseji yenye damu yaweza nyakati zote kutambuliwa katika zile nchi ambako ni ya kawaida). Au huenda Wakristo wakamwuliza mchinja nyama au muuza nyama mwenye sifa njema. Ikiwa wasingekuwa na sababu ya kuamini kwamba nyama fulani ilikuwa na damu, wangeweza tu kununua na kula.

Paulo aliandika hivi pia: “Acheni kiasi chenu kijulikane kwa watu wote.” (Wafilipi 4:5, NW) Hilo lingeweza kuhusu kununua nyama. Wala Sheria ya Israeli wala ile amri ya baraza linaloongoza la Kikristo la karne ya kwanza haikuonyesha kwamba watu wa Mungu walipaswa watumie wakati na juhudi nyingi wakiuliza-uliza juu ya nyama, hata kufikia kiasi cha kuwa walaji mboga tu ikiwa kungekuwako shaka lolote juu ya kuwako kwa damu katika nyama inayopatikana.

Mwindaji Mwisraeli aliyeua mnyama angeondoa damu yake. (Linganisha Kumbukumbu la Torati 12:15, 16.) Ikiwa familia yake isingeweza kula nyama hiyo yote, angeweza kuiuza. Hata katika mzoga ulioondolewa damu ifaavyo, kiasi kidogo cha damu kingebaki katika nyama, lakini hakuna lolote katika Biblia linalodokeza kwamba Myahudi aliyenunua nyama alihitaji kupita kiasi hata kutaka kujua zilipita dakika ngapi kati ya kuua na kuondoa damu, ni ateri au vena (mshipa) gani iliyokatwa ili kuruhusu damu itiririke, na jinsi mnyama alivyotundikwa na alitundikwa muda gani. Zaidi ya hayo, baraza linaloongoza halikuandika kwamba Wakristo walihitaji kujihadhari isivyo kawaida kwa habari hiyo, kana kwamba walihitaji majibu mkataa yenye kutia ndani mambo mengi madogomadogo kabla ya kula nyama yoyote.

Katika nchi nyingi leo, sheria, desturi, au zoea la kidini ni kwamba vitu vinavyofanyizwa kwa nyama (isipokuwa vitu visivyo vya kawaida, kama vile soseji yenye damu) hutoka kwa wanyama ambao ni lazima waondolewe damu wanapochinjwa. Hivyo, Wakristo katika maeneo hayo kwa kawaida hawahitaji kuhanga-ikia sana njia za kuchinja na kutayarisha viwandani. Kwa maana ya urefusho, huenda ‘wakaendelea kula tu nyama inayouzwa, bila kuuliza-uliza,’ nao wanaweza kuwa na dhamiri safi kwamba wanaepukana na damu.

Lakini mara kwa mara kumekuwako ripoti juu ya utumizi wa damu kibiashara ambao umesumbua Wakristo fulani. Wafanyi biashara wengine katika kiwanda cha kutayarishia nyama hutoa hoja kwamba kiasi kikubwa cha damu kutoka kwa wanyama waliochinjwa chaweza kukusanywa ili itumiwe kwa njia ifaayo na kupata faida, kama vile katika mbolea au chakula cha wanyama. Watafiti wamechunguza kama damu (au sehemu zayo) yaweza kutumiwa katika nyama zilizotayarishwa kiwandani. Viwanda vichache vya kibiashara hata vimetokeza kiasi kidogo kidogo cha plazima (au sehemu ya chembe nyekundu iliyoondolewa rangi) ya umajimaji, iliyogandishwa, au ya ungaunga ambayo yaweza kutumiwa badala ya asilimia ndogo ya nyama katika vyakula vilivyo kama soseji au nyama iliyosagwa kabisa. Utafiti mwingineo umekazia kutumia sehemu za damu za ungaunga kuwa kijazio, au cha kuunganishia maji na mafuta katika kima, vyakula kuokwa, au katika vyakula na vinwaji vinginevyo ili kuongeza protini au chuma.

Hata hivyo, inastahili kuangaliwa kwamba utafiti huo umekuwa ukiendelea kwa miongo kadhaa. Hata hivyo, inaonekana kwamba utumizi wa vitu hivyo umekuwa mdogo sana, au hauko, katika nchi nyingi. Baadhi ya ripoti za kawaida zasaidia kuonyesha ni kwa sababu gani:

“Damu ndiyo chanzo cha protini za chakula na za utendaji kazi. Hata hivyo, ni kiasi kidogokidogo tu cha damu ya nyama ya ng’ombe ambacho kimetumiwa ili kuwa chakula cha moja kwa moja cha binadamu kwa sababu ya rangi yayo nyangavu na ladha yayo isiyo ya kawaida.”—Journal of Food Science, Buku 55, Nambari 2, 1990.

“Protini za plazima ya damu zina sifa zifaazo kama vile umumunyifu wa juu, utendaji wa emalshani na kuepa maji . . . na utumizi wazo katika utayarishaji wa chakula hutoa faida nyingi. Hata hivyo, hakuna njia yoyote ambayo imeanzishwa Japani ya kusafisha plazima, hasa baada ya kuikausha.”—Journal of Food Science, Buku 56, Nambari 1, 1991.

Wakristo fulani mara kwa mara wamechunguza vibandiko kwenye vyakula vilivyotiwa ndani ya pakiti, kwa kuwa serikali nyingi hutaka viambato viorodheshwe. Na huenda wakachagua kufanya hivyo kikawaida na vyakula vyovyote ambavyo wana sababu za kuamini kwamba vyaweza kuwa na damu. Bila shaka, lingekuwa jambo lifaalo kuepuka bidhaa zilizoorodhesha vitu kama vile damu, plazima ya damu, plazima, globini (au globulini) protini, au chuma ya hemoglobini (au globini). Habari ya mauzaji kutoka kwa kampuni moja ya Ulaya inayoshughulika na mambo hayo ilikiri hivi: “Habari kuhusu utumizi wa globini ikiwa kiambato ni lazima iandikwe kwenye pakiti ya chakula kwa njia ambayo mnunuzi hataongozwa vibaya juu ya vitu vinavyofanyiza chakula hicho au thamani yacho.”

Hata hivyo, hata kwa habari ya kuchunguza vibandiko au kuuliza wachinja nyama, kiasi kinahitajiwa. Si kwamba kila Mkristo ulimwenguni pote apaswa kuanza kuchunguza kwa makini vibandiko na viambato kwenye vyakula vyote vilivyotiwa ndani ya pakiti au kwamba apaswa kuwahoji-hoji waajiriwa kazi kwenye mikahawa au maduka ya chakula. Mkristo aweza kwanza kujiuliza mwenyewe hivi, ‘Je! kuna uthibitisho wowote wa kweli kwamba damu na sehemu zayo zinatumiwa katika vyakula vya kawaida katika eneo au nchi hiyo?’ Katika mahali pengi jibu ni la. Kwa hiyo, Wakristo wengi wamekata maneno kwamba wao binafsi hawatatumia wakati na uangalifu mwingi kuchunguza uwezekano wa jambo hilo lisilo la kawaida. Mtu asiyehisi hivyo apaswa kutenda kulingana na dhamiri yake, bila kuwahukumu wengine ambao huenda wakaamua jambo hilo kwa njia nyingine lakini wakiwa na dhamiri safi mbele za Mungu.—Warumi 14:2-4, 12.

Hata kama vyakula vilivyo na damu vyaweza kufanyizwa, huenda kwa kadiri kubwa ikawa kwamba hilo halifanywi sana kwa sababu ya gharama, sheria, au sababu nyinginezo. Kwa mfano, Food Processing (Septemba 1991) ilionyesha hivi: “Kwa wale watayarishaji chakula walio na matatizo yoyote kwa kutumia chini ya asilimia 1 (katika andazi lenye nyama lililokwisha tayarishwa) ya plazima ya nyama ng’ombe iliyoyeyushwa kwa maji katika mchanganyiko wa nyama, mchanganyiko badala hutumia protini ya mtindi iliyokolezwa mahali pa plazima hiyo na hiyo yaweza kufaa kuliwa.”

Inastahili kukaziwa kwamba sheria, desturi, au ladha katika nchi nyingi ni kwamba kwa kawaida damu huondolewa kutoka kwa wanyama waliochinjwa na kwamba damu hiyo haitumiwi katika vyakula vingine. Ikiwa hakuna msingi wa kutosha wa kufikiri kwamba hali iko tofauti mahali fulani au kwamba badiliko kubwa limefanywa hivi karibuni, Wakristo wapaswa wajilinde dhidi ya kusumbuliwa na jambo linalowezekana kuwa au uvumi tu. Lakini, inapokuwa hakika au yaelekea sana kwamba damu inatumiwa sana—iwe ni katika chakula au katika matibabu—twapaswa kuazimia kutii amri ya Mungu ya kuepukana na damu.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki