Mtu Aitapo, Je! Wewe Huitikia?
KAMA ILIVYOSIMULIWA NA SHINICHI TOHARA
KWA sehemu ya kwanza ya maisha yangu, sikumwitia Mungu, wala sikutafuta mwelekezo kwake. Nyanya na babu yangu walikuwa wamehama Japani kwenda Hawaii, na wazazi wangu walikuwa wa Dini ya Buddha. Hawakuwa watendaji sana katika imani yao, kwa hiyo mawaza ya Mungu hayakutokeza sana akilini mwangu nilipokuwa nikikua.
Halafu nikajifunza juu ya mageuzi nikaanza kufikiri jinsi lilivyo jambo la kipumbavu kuamini katika Mungu. Hata hivyo, kadiri elimu yangu rasmi ilivyoendelea, masomo ya sayansi yaliniarifu juu ya astronomia, fizikia, na biolojia. Usiku nilikuwa nikikodoa macho angani na kutaka kujua jinsi nyota hizo zote zilivyotokea. Sauti hafifi ndani yangu ilianza kuuliza: ‘Je! kwaweza kuwako Mungu anayedhibiti mambo haya yote?’ Nikaja kuhisi kwamba ni lazima iwe kuna Mtu Fulani huko nje. Moyo wangu ukaanza kuita, ‘Mungu huyo ni nani?’
Baada ya kuhitimu shule ya upili, niliona nimeshikwa na kazi yangu nikiwa fundi wa mashine kwenye kiwanda cha kutengenezea kileo cha sake, na sikuwa na wakati wa kulitafakari swali kuhusu Mungu. Upesi nilikutana na Masako, aliyekuja kuwa mke wangu katika 1937, na hatimaye tulibarikiwa kuwa na watoto watatu. Masako amethibitika kuwa mwenzi na mama mwenye bidii kama nini!
Sasa kwa kuwa nilikuwa na familia, nilifikiria kwa uzito juu ya wakati ujao wetu. Nilianza tena kwenda nje na kukodoa macho kwenye nyota. Nilisadikishwa kwamba kulikuwako Mungu fulani. Sikujua Mungu huyo alikuwa nani, lakini haidhuru nilianza kumwitia. Niliomba kwa kurudia-rudia: ‘Ikiwa upo mahali fulani huko nje, tafadhali isaidie familia yangu ipate njia ya kutembea katika furaha.’
Mwito Wangu Ulijibiwa Hatimaye
Tulikuwa tumekuwa tukiishi na wazazi wangu tangu ndoa yetu, lakini katika 1941 tulianza kuishi peke yetu katika Hilo, Hawaii. Baada tu ya sisi kuanza kukaa katika makao yetu mapya, Wajapani walishambulia Bandari ya Pearl, katika Desemba 7, 1941. Huo ulikuwa wakati wenye wasiwasi, na kila mtu alihangaikia wakati ujao.
Mwezi mmoja baada ya shambulio la Bandari ya Pearl, nilikuwa niking’arisha gari langu wakati mwanamume mmoja aliponikaribia na kunitolea kitabu chenye kichwa Children. Alijijulisha mwenyewe kuwa Ralf Garut, mhudumu wa Mashahidi wa Yehova. Sikuelewa aliyokuwa akisema, lakini nilipendezwa na Mungu, kwa hiyo nilikikubali kitabu hicho. Juma lililofuata, Ralf alirudi na kunitolea funzo la Biblia nyumbani. Ingawa nilikuwa nimesikia juu ya Biblia, hiyo ilikuwa mara yangu ya kwanza hasa kuona moja. Nilikubali funzo la Biblia, na mke yangu na dada yake mchanga wakashiriki pia.
Ukweli wa kwamba Biblia ilikuwa Neno la Mungu ulinivutia sana. (2 Timotheo 3:16, 17) Jambo la kwamba Yehova alikuwa na kusudi lilikuwa la ajabu hata zaidi. Alikuwa ndiye Muumbaji ambaye nilikuwa nimekuwa nikitafuta! (Isaya 45:18) Tulisisimuka kujifunza kwamba Paradiso ya awali iliyokuwa imepotezwa ingerudishwa hapa hapa duniani, na tungeweza kuwa sehemu yayo. (Ufunuo 21:1-4) Hilo lilikuwa ndilo jibu la mwito wangu kwa Mungu!
Tulisema na kila mmoja juu ya kweli hizo mpya tulizopata. Wazazi wangu walifikiri tulikuwa na kichaa, lakini hilo halikutuvunja moyo. Baada ya miezi mitatu ya kujifunza Biblia sana, katika Aprili 19, 1942, mke wangu na mimi tulibatizwa katika kufananisha wakfu wetu kwa Mungu wetu, Yehova. Yoshi, dada mchanga zaidi wa Masako na mume wake, Jeri, ambao kufikia wakati huo walikuwa wamejiunga katika funzo letu la Biblia, walibatizwa pamoja nasi. Tulikuwa na maarifa machache tu ya Maandiko Matakatifu, lakini yalitosha kutusukuma tutake kumtumikia Mungu.
Vita ya ulimwengu ya pili ikiwa ingali inaendelea vikali, nilikisia kwamba mwisho wa mfumo huu ulikuwa karibu sana, na mke wangu na mimi tulihisi uhitaji wa kuwaonya watu juu ya hilo. Akina Garut walikuwa mfano wetu katika habari hiyo. Ralf na mke wake pia walikuwa wakitumikia wakiwa mapainia, wahudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova. Nililinganisha hali yetu na ya Ralf. Alikuwa na mke na watoto wanne. Nilikuwa na mke na watoto watatu tu. Ikiwa angeweza kufanya hivyo, mimi pia napaswa niweze kufanya hivyo. Kwa hiyo mwezi uliofuata ubatizo wetu, tulitoa maombi ya utumishi wa painia.
Hata kabla ya kukubaliwa kuwa painia, niliuza vitu vyote visivyohitajiwa, kutia na gambusihawaii yangu, saksafoni, na hamonika. Nilikuwa nimekuwa shabiki mkubwa wa muziki, lakini niliondolea mbali kila kitu ila hamonika yangu ndogo. Isitoshe, kazi yangu katika kiwanda cha kutengenezea sake haikuonekana yenye kuvutia tena. (Wafilipi 3:8) Nilijenga nyumba yenye kuburutwa na gari nikangojea kuona ikiwa Yehova angejibu maombi yangu ya bidii ya kutumiwa. Sikuhitaji kungojea sana. Tulikubaliwa kuwa mapainia kutoka Juni 1, 1942. Tulianza moja kwa moja kumtumikia Yehova wakati wote na hatujapata kamwe kujuta uamuzi huo.
Kupainia Katika Hawaii
Pamoja na akina Garut, tulieneza Hawaii, kile Kisiwa Kikubwa, kutia na Kona eneo mashuhuri la kahawa, na Kau. Katika siku hizo tulifanya kazi na kinanda. Kilikuwa kizito sana, lakini tulikuwa bado vijana na wenye nguvu. Kwa hiyo, tukiwa na kinanda katika mkono mmoja na mkoba mkubwa wenye vitabu katika ule mwingine, tulifuata vijia vyovyote vilivyoweza kutuongoza kwa watu ambao wangesikiliza katika mashamba ya kahawa, makonde, na kwingineko kote. Halafu, baada ya kueneza kisiwa chote, tulipewa mgawo kwenda Kohala kwenye kile Kisiwa Kikubwa. Kohala lilikuwa konde dogo la miwa, lenye wakazi Wakaukasia, Wafilipino, Wachina, Wahawaii, Wajapani, na Wareno. Kila kikundi kilikuwa na desturi, mawazo, mapendezi, na dini zacho chenyewe.
Mara nilipoanza kupainia, sikufanya kamwe tena kazi ya kuajiriwa ya kilimwengu. Kwa muda fulani tulitegemezwa na fedha zangu za akiba, na uhitaji ulipotokea, nilienda kuvua samaki kwa mkuki. Kwa kushangaza, sikuzote nilikuja nyumbani nikiwa na samaki. Tulichuna mboga na mimea ya mwituni iliyomea kando ya barabara, na hiyo ilipamba sahani zetu wakati wa mlo wa jioni. Nilitengeneza jiko kutoka kwa bati lililotiwa matiko, na Masako akajifunza kuoka mkate. Ulikuwa mkate mzuri zaidi ambao nimepata kula wakati wowote.
Tulipoenda Honolulu kwa ajili ya mkusanyiko wa Kikristo katika 1943, Donald Haslett, aliyekuwa wakati huo mwangalizi wa tawi katika Hawaii, alitualika tuhamie huko na kuishi katika chumba kidogo kilichojengwa juu ya nyumba ya kuwekea magari ya Watch Tower Society. Nilipewa mgawo wa kutumikia nikiwa mtunzaji wa tawi na nikafurahia miaka mitano iliyofuata ya kupainia huko.
Mwito Usiotazamiwa
Katika 1943 tulisikia kwamba Sosaiti ilikuwa imeanza shule ya kuwazoeza wamishonari kwa ajili ya utumishi wa kigeni. Tungalipenda kama nini kuihudhuria! Lakini, familia zenye watoto hazikualikwa, kwa hiyo hatukulifikiria hilo zaidi. Hata hivyo, katika 1947, Ndugu Haslett alituambia kwamba Sosaiti ilitaka kujua ikiwa kulikuwako Wahawaii wowote waliokuwa na nia ya kufanya utumishi wa kigeni katika Japani. Alituuliza vile tulivyofikiri juu ya hilo, na kama vile Isaya, nilisema: “Nitume.” (Isaya 6:8) Mke wangu alihisi vivyo hivyo. Hatukusita hata kidogo kujibu mwito wa Yehova.
Kwa hiyo tulialikwa kuhudhuria Watchtower Bible School of Gilead ili tuzoezwe kuwa wamishonari. Mwaliko huo ulitia ndani watoto wetu wachanga watatu. Wengine watano, Donald na Mabel Haslett, Jeri na Yoshi Toma, na Elsie Tanigawa, walialikwa pia, na pamoja tulifunga safari kwenda New York katika kipupwe cha 1948.
Tulivuka kontinenti kwa basi. Baada ya siku tatu tukiwa katika basi, sisi sote tulikuwa tumechoka, na Ndugu Haslett akadokeza kwamba tupumzike na kukaa katika hotel usiku kucha. Tuliposhuka kwenye basi, mtu mmoja alitukaribia na kupaaza sauti: “Tujapani! Naenda nyumbani nikailete bunduki yangu niwapige risasi!”
“Hawa si Wajapani,” akasema Ndugu Haslett. “Hawa ni Wahawaii. Je! huwezi kuona tofauti?” Tuliokolewa na maneno yake chapuchapu.
Je! kwa kweli sisi tulikuwa sehemu ya darasa la 11 la Gileadi? Hiyo ilionekana kama ndoto nzuri ajabu. Hata hivyo, upesi uhalisi wa hilo ulipenya. Katika darasa letu, wanafunzi walikuwa wamechaguliwa na msimamizi wa Watch Tower Society, Nathan H. Knorr, ili wazoezwe kwa ajili ya uwezekano wa kufanya utumishi wa mishonari katika Japani. Kwa kuwa nilikuwa wa nasaba ya Kijapani na nilisema kiasi fulani cha Kijapani, nilipewa mgawo wa kufundisha lugha hiyo kwa kikundi hicho cha wanafunzi. Kwa kuwa sikuwa mwenye ufasaha katika lugha hiyo, hilo halikuwa rahisi; lakini sote tuliweza kukabiliana na hilo kwa njia fulani!
Wakati huo, mwana wetu Loy, alikuwa na miaka kumi, na mabinti wetu, Thelma na Sally, walikuwa na miaka minane na sita. Tulipokuwa shuleni, ilitukiaje kwao? Walienda shuleni pia! Basi liliwachukua asubuhi na kuwarudisha nyumbani baadaye siku hiyo. Watoto waliporudi kutoka shule, Loy alifanya kazi pamoja na ndugu kwenye shamba la Sosaiti, na Thelma na Sally walifanya kazi katika mahali pa kufulia nguo wakikunja vitambaa vya mkono.
Kutayarisha Akili Kwa Ajili ya Mambo Yasiyojulikana
Tulipohitimu Gileadi katika Agosti 1, 1948, tulitamani sana kwenda kwenye mgawo wetu. Ndugu Haslett alienda mbele yetu kutafuta mahali pa wamishonari kuishi. Hatimaye, alipata nyumba yenye orofa mbili katika Tokyo, na katika Agosti 20, 1949, familia yetu iliondoka kwenda kwenye makao yetu ya wakati ujao.
Kabla ya kuwasili Japani, nilifikiria mara nyingi juu ya bara hilo la Mashariki. Nilifikiria ule uaminifu-mshikamanifu wa Wajapani kwa mabwana wao wa kibinadamu na kwa maliki wao. Wajapani wengi walitoa maisha yao kwa ajili ya watawala hao wa kibinadamu. Katika vita ya ulimwengu ya pili, marubani wa kamikaze walikufa kwa ajili ya maliki kwa kulenga ndege zao kwenye mabomba ya moshi ya meli za vita za maadui. Nakumbuka nikifikiri kwamba ikiwa Wajapani ni waaminifu sana kwa mabwana wao wa kibinadamu, wangefanya nini ikiwa wangempata Bwana wa kweli, Yehova?
Tulipowasili Japani, kulikuwako wamishonari saba tu na wahubiri wachache sana katika bara hilo lote. Sisi sote tulianza kufanya kazi, na nilijitahidi kufanyia maendeleo ujuzi wangu wa lugha hiyo na niliweza kuanzisha mafunzo ya Biblia na wengi waliokuwa wakimwitia Mungu katika mioyo yao. Idadi kadhaa ya wanafunzi wa Biblia hao wa mapema wameendelea kwa uaminifu hadi siku ya leo.
Utumishi wa Mishonari Pamoja na Watoto Wetu
Tungewezaje kufanya utumishi wa mishonari tukiwa na watoto wadogo watatu wa kutunza? Yehova alikuwa ndiye nguvu yenye kutegemeza. Tulipokea rudishio dogo kutoka kwa Sosaiti, na Masako aliwashonea watoto nguo. Kwa kuongezea tulipata msaada kutoka kwa wazazi wangu.
Baada ya Loy kuhitimu shule ya msingi, alitumikia kwenye tawi la Japani la Watch Tower Bible and Tract Society kwa muda fulani. Hata hivyo, kwa sababu ya matatizo ya afya, aliamua kurudi Hawaii kupata matibabu. Sasa yeye na mke wake wanamtumikia Yehova kwa uaminifu katika Kalifornia. Ndoa yake ilitokeza kubarikiwa kwetu na wajukuu waaminfu wanne. Wote wamebatizwa, na mmoja, pamoja na mke wake, wanatumikia kwenye Betheli ya Brooklyn, makao makuu ya Mashahidi wa Yehova.
Mabinti wangu, Thelma na Sally, walipewa cheo cha kuwa wamishonari walipokua. Thelma anatumikia sasa akiwa mishonari katika mji wa Toyama. Sally aliolewa na ndugu mishonari, Ron Trost, na wamekuwa wakitumikia Japani wakiwa wamishonari katika kazi ya kusafiri kwa zaidi ya miaka 25.
Kutoka Kaskazini Hadi Kusini
Baada ya kutumia miaka miwili katika Tokyo, tulitumwa Osaka kwa miaka miwili. Mgawo wetu uliofuata ulitupeleka kuelekea kaskazini hadi Sendai, ambako tulitumikia kwa miaka sita hivi. Miaka hiyo katika Sendai ilitutayarisha kwa ajili ya migawo kwenye kisiwa cha kaskazini kabisa cha Japani, Hokkaido. Huko Hokkaido ndiko mabinti wetu walipokea cheo cha kuwa wamishonari. Huko pia ndiko tulilazimika kuzoea halijoto za kipupwe ambazo nyakati nyingine zilikuwa chini ya sifuri. Baada ya kuishi Hawaii ya kitropiki hilo lilikuwa badiliko kubwa!
Halafu, siku moja nilisikia mwito mpya kwa namna ya barua kutoka Sosaiti. Iliniomba nifungue ofisi ya tawi katika Okinawa, iliyokuwa bado chini ya udhibiti wa U.S. Kuhama kutoka nchi ya kaskazini ya Japani yenye ubaridi hadi mahali ambapo sasa pamekuwa wilaya ya kusini zaidi ya Japani kungetokeza ugumu mkubwa. Ningefanya nini? Ingawa nilihisi kupungukiwa, niliwasili Okinawa katika Novemba 1965, nikiwa nime-ambatana kama sikuzote na mke wangu mwaminifu. Je! maisha katika Okinawa yangekuwa sawa na yale katika Japani? Namna gani utamaduni? Je! watu wangeitikia ujumbe wa Yehova wa wokovu?
Tulipowasili, kulikuwako wahubiri wasiozidi 200 katika Okinawa. Sasa kuna zaidi ya 2,000. Katika siku za mapema, nilikuwa mwangalizi wa mzunguko wa muda-muda na mwangalizi wa tawi wa muda-muda. Kusafiri kotekote visiwani kulinisaidia nijenge mahusiano ya karibu pamoja na ndugu wa huko, na naliona kuwa pendeleo kuwa niliweza kuwatumikia.
Bila Matatizo?
Kazi-maisha yetu ya mishonari haikuwa kamwe bila matatizo. Tulipokuwa likizoni United States katika 1968, Masako alikuwa mgonjwa akahitaji upasuaji. Aliondolewa tezi kutoka matumbo yake kisha akapata nafuu ya ajabu. Hatukuwa na bima ya kitiba, na tulikuwa na wasiwasi kwamba labda hatungeweza kurudi kwenye mgawo wetu. Hata hivyo, kwa mshangao wetu mkubwa, marafiki katika imani walishughulikia kila kitu.
Kwa habari yangu mwenyewe, sasa naishi na matatizo yaliyo ya kawaida kwa wale wenye ugonjwa wa sukari. Ingawa mimi si kipofu, uwezo wangu wa kuona umedhoofika sana. Lakini kupitia fadhili-upendo za Yehova, naweza kutwaa ndani ulaji wa kiroho wa kawaida kwa kusikiliza tepu zilizorekodiwa za Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Ndugu na dada katika imani husaidia pia kwa kunisomea habari mbalimbali.
Uwezo wangu wa kuona ukiwa umedhoofika, ningewezaje kuendelea kutoa hotuba za watu wote? Mwanzoni nilirekodi hotuba zangu ili ziweze kuchezwa kupitia mfumo wa sauti huku nikiigiza. Hata hivyo, kwa kudokezewa na binti yangu, nilifanyia maendeleo jambo hilo. Sasa mimi hurekodi hotuba zangu kwa tepurekoda ndogo na huzitoa hali nikisikiliza hotuba yangu niliyorekodi kimbele kupitia vyombo vya masikio.
Wakati wowote tulipokabili matatizo halisi, hatukukosa kamwe kumwitia Yehova. Hatimaye, baraka zilizotokana na kusuluhisha kwa Yehova matatizo hayo sikuzote zilionekana kuwa kubwa zaidi ya vile matatizo yenyewe yalivyokuwa yameonekana kuwa. Kuendelea katika utumishi wake ndiyo njia pekee ya kuonyesha shukrani yetu.
Baada ya miaka 23 katika Okinawa, tulipewa mgawo tena wa kwenda kwenye mahali palepale penyewe tulipokuwa tumetumikia tulipokuja Japani mara ya kwanza. Ofisi kuu ya Sosaiti na makao ya mishonari makubwa zaidi yako mahali pa awali pa lile jengo lenye orofa mbili katika Tokyo, lililonunuliwa na Ndugu Haslett miaka mingi sana iliyopita.
Licha ya Masako na mimi, watu wa jamaa yetu 11 wanatumikia sasa wakiwa wamishonari katika Japani. Wote huliona kuwa pendeleo kubwa ya kuwa waliweza kuona ukuzi ambao Yehova ameleta kwenye bara hilo la tamaduni za Dini ya Buddha na ya Shinto hasa. Kazi katika Japani ilikuwa na vyanzo vidogo, lakini uwezo wa Yehova umetokeza kwa kasi “taifa” la wahubiri wa habari njema zaidi ya 167,000.—Isaya 60:22.
Nilipomwitia Mungu, alinijibu. Aliponialika, nilijibu kwa kukubali. Mke wangu na mimi tunahisi kwamba tumefanya lile tu tulilopaswa kufanya. Namna gani wewe? Muumba wako aitapo, je, wewe huitikia?
[Picha katika ukurasa wa 28]
Akina Tohara pamoja na baadhi ya wale wa kikundi chao cha mapainia kiatika Hawaii, 1942
[Picha katika ukurasa wa 29]
Watoto wa Tohara kwenye Gileadi katika 1948
[Picha katika ukurasa wa 31]
Wakifurahi kwamba waliitikia mwito, Shinichi na Masako Tohara wamekamilisha miaka 43 katika kazi ya mishonari