Gospeli Kwa Kweli Ni Nini?
KATIKA majira ya Krismasi, watu katika mabara mengi husikia na hata husema juu ya, Gospeli. Neno hilo ni la kawaida sana, lakini je, lina maana zaidi ya vile watu huwazia? Je! Gospeli ingeweza kumaanisha jambo zuri sana kwako na kwa wapendwa wako?
“Gospeli” humaanisha “habari njema,” na kwa hakika, habari njema hupokewa kwa furaha si wakati wa Krismasi tu bali kila wakati. Hata hivyo, “ile Gospeli” si habari njema zozote tu. Ni habari njema maalumu kutoka chanzo mahususi kuhusu habari fulani hasa. Kwa kweli, huo ni ujumbe ambao Mungu ameamuru utangazwe kwa ainabinadamu yote.
Eugênio Salles, askofu mkuu wa Rio de Janeiro, Brazili, alisema juu ya habari njema alipohimiza hivi: “Tunapaswa kutenda kulingana na Gospeli si kulingana na itikadi mbalimbali.” Askofu mkuu huyo alisema kweli. Hata hivyo, kutenda kulingana na Gospeli, kunataka tujue Gospeli ni nini. Tunaweza kujifunzaje hilo? Na kutenda kulingana na Gospeli kutatusaidiaje?
Gospeli Ni Nini?
Mara nyingi asili ya Gospeli hueleweka vibaya. Katika 1918 Baraza la Muungano la Makanisa ya Kristo katika Amerika liliupongeza Ushirika wa Mataifa ambao hauko sasa kuwa ndio wonyesho wa kisiasa wa Ufalme wa Mungu duniani na lilijulisha wazi kwamba “una mizizi katika Gospeli.” Shirika hilo lilishindwa vibaya sana katika mradi walo wa kuhifadhi amani. Kwa wazi, baraza hilo halikusema kweli. Ushirika wa Mataifa haukuhusika hata kidogo na Gospeli.
Katika miaka ya hivi karibuni waenezaji theolojia ya ukombozi wameitokeza Gospeli kwa huru wakati wanapoongea juu ya mawazo yao ya mapinduzi makubwa ya kisiasa na ya kijamii. Kwa kufanya hivyo wamepuuza Gospeli ya kweli. Gazeti la Kibrazili Veja lilieleza hivi: “Kanisa la Katoliki lilianza kupendelea ufalme wa kijamii, likipuuza mahitaji ya kiroho ya washiriki walo. Wale waliotafuta neno Mungu katika mahubiri walipata mara nyingi mabishano ya kifasaha dhidi ya udhalimu mbalimbali wa kijamii.”
Maendeleo katika hali za maisha au badiliko katika mifumo ya kisiasa huenda zikawa habari njema kwa wengine. Hata hivyo, hizo sizo zile habari njema, ile Gospeli. Akikiri kushindwa kwa kanisa lake kuihubiri Gospeli ya kweli, askofu mmoja alisema hivi: “Tulipuuza fundisho la kiroho la washiriki wetu tangu miaka ya 60 kwa sababu ya mwingilio wa ufuatiaji vitu vya kimwili katika fundisho letu.”
Ripoti moja katika gazeti la habari la U.S., Time inadokeza kwamba Waprotestanti pia wamekengeushwa kutoka Gospeli. Gazeti hilo linaonelea hivi: “Madhehebu ya kimapokeo hayashindwi tu kuwasilisha ujumbe wao ili ueleweke; bali yanazidi kutokuwa na uhakika juu ya ujumbe huo ni nini hasa.” Ujumbe wao unapaswa uwe nini? Gospeli ni nini?
Kuitambulisha Gospeli
Webster’s Ninth New Collegiate Dictionary huifasili “Gospeli” kuwa “ule ujumbe kuhusu Kristo, ufalme wa Mungu, na wokovu.” Neno “gospeli” hufasiliwa pia kuwa “ufasiri wa ujumbe wa Kikristo (gospeli ya kijamii)”; “ujumbe au mafundisho ya mwalimu wa kidini.” Je! fasili hizo zote zaweza kutumiwa? La, si kama tunasema juu ya ile Gospeli. Gospeli ya kweli inategemea Biblia; kwa hiyo, ni fasili ya kwanza tu kati ya hizo tatu ambayo ni sahihi. Za mwisho mbili huonyesha tu njia ambayo neno “gospeli” limekuja kutumiwa leo.
Kupatana na wazo hilo, Vine’s Expository Dictionary of New Testament Words husema kwamba katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo (“Agano Jipya”), Gospeli “humaanisha habari njema za Ufalme wa Mungu na za wokovu kupitia Kristo, utakaopokewa kwa imani, kwenye msingi wa kifo Chake cha kupatanisha.” Ni jambo la maana kuelewa hilo kwa sababu uelewevu sahihi wa habari njema za kweli unahusu sana hali njema yetu ya sasa na furaha yetu ya wakati ujao.
Ujumbe wa Wazi
Kama vile kile kitabu cha marejezo kilichotangulia kutajwa kionyeshavyo, Gospeli inalinganika kwa ukaribu na Yesu Kristo—sana sana hivi kwamba yale masimulizi manne ya Biblia kuhusu maisha yake duniani yanaitwa Gospeli nne. Tangu mwanzo kabisa wa uhai wake wa kibinadamu, habari juu ya Yesu zilikuwa habari njema. Alipokuwa akitangaza juu ya kuzaliwa kwa Yesu kulikokuwa kukija, malaika mmoja alisema hivi: “Mimi ninawaletea habari njema ya furaha kuu itakayokuwa kwa watu wote; maana leo katika mji wa Daudi amezaliwa, kwa ajili yenu, Mwokozi, ndiye Kristo Bwana.”—Luka 2:10, 11.
Yesu aliyetoka kuzaliwa angekua akawe Kristo, Mesiya aliyeahidiwa. Angefunua kusudi la Mungu la wokovu, kusalimisha uhai wake mkamilifu wa kibinadamu kwa ajili ya ainabinadamu, kufufuliwa, na kisha kuja kuwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu. Habari njema kwelikweli! Hiyo ndiyo sababu ujumbe juu yake unaitwa Gospeli.
Katika huduma yake fupi ya kidunia, Yesu alikuwa na bidii sana katika kuhubiri habari njema. Tunasoma katika Gospeli ya Mathayo hivi: “Yesu alikuwa akizunguka katika miji yote na vijiji, akifundisha katika masinagogi yao, na kuihubiri habari njema ya ufalme.” (Mathayo 9:35) Kuhubiri kwake hakukuwa tu ili kufanya watu wahisi vizuri zaidi. Marko arekodi Yesu kuwa akisema: “Wakati umetimia, na ufalme wa Mungu umekaribia; tubuni, na kuiamini injili [habari njema, New World Translation].” (Marko 1:15) Naam, wale walioitikia na kutii habari njema waliona kwamba zilibadili maisha zao.
Baada ya kifo cha Yesu, wafuasi wake waliendelea kuihubiri Gospeli. Hawakusema juu ya Ufalme tu bali waliongeza zile habari zenye furaha kwamba Yesu alikuwa amefufuliwa kwenye mkono wa kuume wa Mungu mbinguni na alikuwa ametoa thamani ya uhai wake mkamilifu wa kibinadamu kwa ajili ya ainabinadamu. Akiwa yule aliyechaguliwa na Mungu kutawala juu ya dunia akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu, angekuwa Wakili wa Mungu katika kuharibu maadui wa Mungu na katika kurudisha dunia kuwa paradiso.—Matendo 2:32-36; 2 Wathesalonike 1:6-10; Waebrania 9:24-28; Ufunuo 22:1-5.
Leo, habari njema zinatia ndani jambo jingine zaidi. Kulingana na ushuhuda wote wa utimizo wa unabii, Yesu ametawazwa sasa, na tunaishi katika siku za mwisho wa mfumo huu wa mambo. (2 Timotheo 3:1-5; Ufunuo 12:7-12) Wakati Ufalme utakapotenda dhidi ya maadui wa Mungu unakaribia kwa kasi. Kungeweza kuwa na habari njema zipi bora zaidi?
Tutaona katika makala ifuatayo jinsi Gospeli ilivyo na nguvu. Ilimsaidia mwanamke mmoja aliyekuwa amenaswa na uchawi apate uhuru. Ilimsaidia mwanamume mmoja aliyekuwa gerezani kwa ajili ya unyang’anyi apate furaha. Nayo itakunufaisha sana pia—ukisikiliza na kutii habari njema.