Muumba Wetu Mtukufu na Kazi Zake
NI ZENYE utukufu kama nini! Maporomoko ya maji yenye kunguruma ya Iguaçú au Niagara, mabondi makuu ya Arizona au Hawaii, vizingiti vizuri ajabu vyenye miamba mirefu kando kando vya Norwei au New Zealand—maajabu hayo ya asili yanavutia vilio vilivyoje vya kusifu! Lakini je, hayo ni mazao tu ya Nguvu za Kiasili? La, ni zaidi ya hilo! Hayo ni kazi zenye kuchochea hofu za Muumba Mtukufu, Baba wa kimbingu mwenye upendo ambaye Mfalme Sulemani mwenye hekima aliandika hivi juu yake: “Kila kitu amekifanya kizuri kwa wakati wake; tena ameiweka hiyo milele ndani ya mioyo yao; ila kwa jinsi mwanadamu asivyoweza kuivumbua kazi ya Mungu anayoifanya, tangu mwanzo hata mwisho.” (Mhubiri 3:11) Kwa kweli, ingechukua umilele wa wakati kwa wanadamu kujaribu kupata ufahamu wa kazi zote tukufu ambazo Muumba wetu ameujaza ulimwengu wote mzima nazo.
Tuna Muumba Mtukufu kama nini! Na tunafurahi kama nini kwamba Mungu huyo mweza yote ‘amesema na sisi mwisho wa siku hizi kupitia Mwana, aliyemweka kuwa mrithi wa yote, tena kwa yeye aliufanya ulimwengu.’ (Waebrania 1:2) Mwana huyo, Yesu Kristo, alithamini vitu vya kupendeza vya uumbaji wa Baba yake. Alivirejezea mara nyingi katika kutolea kielezi makusudi ya Baba yake na katika kuwaambia wasikilizaji wake maneno ya kitia-moyo. (Mathayo 6:28-30; Yohana 4:35, 36) “Kwa imani” wengi wametambua kwamba maajabu ya uumbaji ‘yaliumbwa kwa neno la Mungu.’ (Waebrania 11:3) Maisha zetu za kila siku zapasa kuonyesha imani hiyo.—Yakobo 2:14, 26.
Kwa kweli, uumbaji wa Mungu wetu ni wenye utukufu. Unaonyesha vizuri ajabu hekima yake, nguvu zake, uadilifu wake, na upendo wake. Kwa kielelezo, aliiegemeza dunia kidogo na kuifanya izunguke jua ili uumbaji wake wa wakati ujao, mwanadamu, uweze kufurahia ule mwandamano wenye kupendeza wa majira. Mungu alitaarifu hivi: “Muda nchi idumupo, majira ya kupanda, na mavuno, wakati wa baridi na wakati wa hari, wakati wa kaskazi na wakati wa kusi, mchana na usiku, havitakoma.” (Mwanzo 8:22) Zaidi ya hayo, Mungu aliiwekea dunia yetu akiba kubwa ya madini yenye thamani. Hasa, aliandaa maji mengi sana, ambayo baadaye yangekuja kuwa sehemu ya maana na yenye kutegemeza uhai wote duniani.
Katika mfuatano wenye utaratibu wa ‘siku sita za uumbaji,’ kila moja ikiwa muda wa maelfu ya miaka, “kani ya utendaji ya Mungu” iliendelea kuitayarisha dunia ili mwanadamu aikalie. Nuru tunayoona kwayo, hewa tunayopumua, bara kavu tunakoishi, mimea, mfuatano wa mchana na usiku, samaki, ndege, wanyama—vyote hivyo vilitokezwa kwa mfuatano na Muumba wetu Mtukufu kwa ajili ya utumishi na furaha ya mwanadamu. (Mwanzo 1:2-25, New World Translation) Kwa hakika, twaweza kuungana na mtunga zaburi katika kusema kwa mshangao: “Ee BWANA [Yehova, NW], jinsi yalivyo mengi matendo yako! Kwa hekima umevifanya vyote pia. Dunia imejaa mali zako.”—Zaburi 104:24.
Uumbaji wa Mungu Wenye Ustadi
“Siku” ya sita ya uumbaji ulipokaribia mwisho, Mungu alimfanya mwanamume kisha msaidizi wake, mwanamke. Huo ulikuwa upeo wenye ustadi kama nini kwa uumbaji wa kidunia, wenye ajabu zaidi ya uumbaji wowote wa kimwili uliokuwa umetukia mapema! Zaburi 115:16 hutujulisha hivi: “Mbingu ni mbingu za BWANA [Yehova, NW], bali nchi amewapa wanadamu.” Kwa hiyo, Yehova alitubuni sisi nafsi za kibinadamu ili tuweze kufurahia na pia kutumia uumbaji wake wa mapema zaidi duniani. Twapaswa kushukuru kama nini kwa ajili ya macho yetu—ambayo yametatanika zaidi ya kamera bora zaidi—yawezayo kuona ulimwengu wenye rangi-rangi unaotuzunguka! Tuna masikio—yaliyo bora zaidi ya mfumo wowote wa sauti uliofanyizwa na mwanadamu—ili yatusaidie kufurahia mazungumzo, muziki, na wimbo mtamu wa ndege. Tuna mtambo wa kusema wa ndani, kutia na ulimi wenye matumizi mbalimbali. Vionjio vya ulimi, pamoja na hisia yetu ya kunusa, huandaa pia uwezo wa kufurahia kuonja unamna-namna wa vyakula usio na mwisho. Na tunathamini kama nini ule mguso wa mkono wenye upendo! Kwa hakika twaweza kumshukuru Muumba wetu, kama vile yule mtunga zaburi aliyesema: “Nitakushukuru kwa kuwa nimeumbwa kwa jinsi ya ajabu ya kutisha. Matendo yako ni ya ajabu, na nafsi yangu yajua sana.”—Zaburi 139:14.
Fadhili-Upendo za Muumba Wetu
Mtunga zaburi aliandika hivi: “Mshukuruni BWANA [Yehova, NW] kwa kuwa ni mwema; . . . Yeye peke yake afanya maajabu makuu; kwa maana fadhili [fadhili-upendo, NW] zake ni za milele.” (Zaburi 136:1-4) Fadhili-upendo hizo zinamsukuma sasa afanye mambo ya ajabu yenye utukufu zaidi ya uumbaji wote ambao tumetoka tu kusimulia. Naam, hata anapopumzika baada ya kuumba vitu vya kimwili, yeye anaumba kwenye kiwango cha kiroho. Anafanya hivyo katika kujibu upinzani mwovu ulioelekezwa kwake kwa majivuno. Jinsi gani?
Mwanamume na mwanamke wa kwanza waliwekwa katika paradiso tukufu, Edeni. Hata hivyo, malaika mwasi, Shetani, alijitukuza kuwa kijimungu na akawaongoza wenzi hao wawili wa kibinadamu katika uasi dhidi ya Yehova. Kwa haki, Mungu aliwapa hukumu ya kifo, kukiwa na tokeo la kwamba watoto wao, jamii nzima ya kibinadamu, wametokezwa katika hali yenye dhambi, ya kufa. (Zaburi 51:5) Usimulizi wa Biblia kuhusu Ayubu huonyesha kwamba Shetani alimpinga Mungu, akidai kwamba hakuna mwanadamu anayeweza kushika uaminifu-maadili Kwake chini ya mtihani. Lakini Ayubu alimthibitisha Shetani kuwa mwongo mbaya sana, kama vile watumishi wa Mungu wengine wengi katika nyakati za Biblia na hadi siku yetu wamefanya. (Ayubu 1:7-12; 2:2-5, 9, 10; 27:5) Yesu, akiwa mwanadamu mkamilifu, alitoa kielelezo cha ushikaji uaminifu-maadili usio na kifani.—1 Petro 2:21-23.
Hivyo, Yesu angeweza kusema hivi, “Mtawala wa ulimwengu [Shetani] hana uvutano juu yangu mimi.” (Yohana 14:30, NW) Hata hivyo, hadi siku ya leo “ulimwengu mzima uko katika uwezo wa yule mwovu.” (1 Yohana 5:19, NW) Akiwa amebisha haki ya enzi kuu ya Yehova, Shetani tayari amepewa miaka 6,000 hivi ili aonyeshe kama utawala wake mwenyewe wa ainabinadamu waweza kufanikiwa. Ameshindwa vibaya kama nini, kama vile hali za ulimwengu zenye kuharibika zinavyoendelea kushuhudiza! Mungu wetu mwenye upendo, Yehova, hivi karibuni ataondoa hii jamii ya ulimwengu yenye ufisadi, akisimamisha enzi kuu yake yenye haki juu ya dunia. Hilo litaleta kitulizo chenye furaha kama nini kwa wanadamu wanaotamani utawala wenye amani na uadilifu!—Zaburi 37:9-11; 83:17, 18.
Hata hivyo, si hayo tu! Fadhili-upendo za Mungu zitaonyeshwa zaidi kwa msingi wa maneno ya Yesu kwenye Yohana 3:16: “Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima [uhai, NW] wa milele.” Kurudishwa huko kwa ainabinadamu kwa lile taraja la uhai wa milele duniani kunatia ndani uumbaji wa vitu vipya. Hivyo vitu ni nini? Vinanufaishaje wanadamu wenye kuugua? Makala yetu inayofuata itaonyesha.