Maswali Kutoka kwa Wasomaji
Wakristo wana daraka gani katika kupunguza uchafuzi wa mazingira yetu—bara, bahari, na hewa?
Tukiwa Mashahidi wa Yehova, tunahangaikia sana yale matatizo mengi ya kiekolojia (mazingira) yanayoathiri makao yetu ya kidunia. Zaidi ya watu wengi, sisi tunathamini kwamba dunia iliumbwa iwe makao safi, yenye afya kwa ajili ya familia kamilifu ya kibinadamu. (Mwanzo 1:31; 2:15-17; Isaya 45:18) Pia tuna uhakikisho wa Mungu kwamba ‘atawaharibu hao waiharibuo dunia.’ (Ufunuo 11:18) Kwa hiyo inafaa kufanya jitihada zenye usawaziko, zinazofaa ili kuepuka kuongezea ule uharibifu wa mwanadamu wa dunia yetu unaoendelea sasa. Lakini, angalia lile neno “zinazofaa.” Inafaa Kimaandiko pia kujilinda dhidi ya kuruhusu masuala na mazoea ya kiekolojia yawe mahangaiko yenye kutulemea.
Hata kuishi kwa kibinadamu kwa kawaida hutokeza takataka. Kwa kielelezo, mara nyingi ukuzi, utayarishaji, na ulaji wa chakula hutokeza takataka, ingawa kadiri kubwa yayo yaweza kuoza. (Zaburi 1:4; Luka 3:17) Ule mlo wa samaki waliokaangwa ambao Yesu aliyefufuliwa aliwatengenezea wanafunzi wake yaelekea ulitokeza moshi, majivu, na taka za mifupa ya samaki. (Yohana 21:9-13) Lakini mifumo au kawaida za vitu vyenye uhai na visivyo na uhai vya dunia vimebuniwa ili kuozesha taka hizo.
Watu wa Mungu hawapaswi wawe wasahaulifu kuhusu mambo ya kiekolojia. Yehova aliwataka watu wake wa kale wachukue hatua za kuondolea mbali takataka, hatua zilizokuwa za muhimu kwa kiekolojia na kwa kiafya pia. (Kumbukumbu la Torati 23:9-14) Na kwa kuwa tunajua maoni yake juu ya wale wanaoiharibu dunia, kwa hakika hatupaswi kupuuza mambo tunayoweza kufanya ili kudumisha mazingira yakiwa safi. Twaweza kuonyesha hilo kwa kuondolea mbali takataka ifaavyo, hasa vitu vyenye sumu. Tunashirikiana kwa kudhamiria na jitihada za kutengeneza upya takataka fulani ili ziweze kutumiwa tena, tukiwa na sababu zaidi ya kufanya hivyo ikiwa hilo limeamriwa na Kaisari. (Warumi 13:1, 5) Na watu wengine mmoja mmoja hupata uradhi kutokana na kuchukua hatua za ziada, kama vile kutumia vitu viwezavyo kuoza badala ya vile ambavyo vingeongezea ile milima ya taka juu ya bara na chini ya bahari.
Hata hivyo, kadiri ambayo Mkristo angejitahidi katika hayo ni jambo la kibinafsi isipokuwa ikiwa inahitajiwa na sheria. Ni wazi kutokana na usambazaji habari kwamba wanadamu wasiokamilika hutumbukia kwa urahisi katika mtego wa kuwa bila kiasi. Shauri hili la Yesu lafaa kwa hakika: “Msihukumu, msije mkahukumiwa ninyi . . . Mbona wakitazama kibanzi kilicho ndani ya jicho la ndugu yako, na boriti iliyo ndani ya jicho lako mwenyewe huiangalii?” (Mathayo 7:1, 3) Kukumbuka hilo huenda kukatusaidia tusisahau mambo mengine ya muhimu.
Nabii Yeremia aliandika hivi: “BWANA [Yehova, NW] najua ya kuwa njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.” (Yeremia 10:23) Kupuuza kanuni hiyo kumeifanya ainabinadamu ikabili “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,” kama ilivyoandikwa kwenye 2 Timotheo 3:1-5, NW. Na yale ambayo Mungu alisababisha yaandikwe kwenye Ufunuo 11:18 yanathibitisha kwamba jitihada za kibinadamu za kuiondolea dunia matatizo yayo makubwa ya kiekolojia, kutia na uchafuzi, hazitafanikiwa kikamili. Huenda yakawa maendeleo huko na huko, lakini suluhisho pekee la kudumu lataka mwingilio wa Mungu.
Kwa sababu hiyo tunakaza jitihada na nyenzo zetu kwenye suluhisho la kimungu, kuliko kujaribu kusuluhisha dalili za kijuujuu tu. Katika hilo sisi hufuata mfano wa Yesu, aliyetumia sehemu kubwa zaidi ya huduma yake ‘akiishuhudia kweli.’ (Yohana 18:37) Badala ya kuulisha ulimwengu au kusuluhisha matatizo ya kadiri kubwa ya kijamii—kutia na uchafuzi—Yesu alielekezea suluhisho kamili la matatizo yanayoipata ainakibinadamu.—Yohana 6:10-15; 18:36.
Ingawa upendo kwa wanadamu wenzetu hutusukuma tuepuke kuchafua bara, angahewa, au ugavi wa maji isivyohitajiwa, sisi huendelea kuishuhudia kweli. Hiyo hutia ndani kuwafundisha watu kutumia kweli ya Biblia na kuepuka kuharibu miili yao kwa kuvuta sigareti, kunywa vileo kupita kiasi, au kwa dawa za kulevya zenye kudhuru. Mamilioni ya wapya wanapokuja kuwa wanafunzi, wamejifunza tabia za usafi na ufikirio kwa wengine. Kwa hiyo kazi ya kuhubiri imechangia kihalisi upungufu wa lile tatizo la ujumla la uchafuzi leo. Lakini la maana zaidi, wanafunzi Wakristo hujitahidi kubadili utu na tabia zao sasa ili waweze kufaana na ile dunia-Paradiso safi ambayo Mungu atawaandalia waabudu wake wa kweli hivi karibuni.