Wapiga Mbiu ya Ufalme Waripoti
Walibadili Njia Yao ya Maisha
BILA shaka umewaona wakiongea na wengine barabarani, wakifanya ziara kutoka nyumba hadi nyumba, au wakihudhuria mikutano ya Kikristo katika Majumba ya Ufalme yao. Tunasema juu ya vijana wenye kujipamba vizuri wa Mashahidi wa Yehova. Huenda ikawa umekata maneno kwamba wao ni Mashahidi kwa sababu wazazi wao waliwafundisha wawe hivyo, na ndivyo ilivyo na wengi wao. Kwa upande mwingine, kuna wengine kati ya vijana hao walio na malezi tofauti sana na ambao njia yao ya maisha ya kwanza ilikuwa tofauti na maisha wanayoishi sasa. Kwa kweli, wale wanaoonyeshwa kwenye ukurasa ufuatao walikuwa wakishirikiana na vikundi ambamo uhalifu na utumizi mbaya wa dawa za kulevya ulikuwa matukio ya kila siku. Ni nini kilichowafanya wabadili maisha zao kabisa? Acheni tuzuru mji mmoja katika Norwei na kukutana na baadhi ya vijana ambao wamefanya mabadiliko hayo.
Msingi wa Badiliko
Mashahidi wawili walipokutana na Annette katika kazi ya nyumba kwa nyumba, alikuwa na miaka 19. “Mara nyingi nilikuwa nimeambiwa nisiongee kamwe na Mashahidi wa Yehova, lakini nilikuwa na udadisi nikawaalika waingie,” yeye akumbuka. Alikuwa amekuwa mtumizi wa dawa za kulevya tangu alipokuwa na miaka 11 na alikuwa amehusika katika uvunjaji nyumba na wizi wa magari.
Habari njema za Ufalme zilimvutia. Alitiwa moyo hasa na tumaini la ufufuo, akiwa amepoteza mama yake katika kifo akiwa na miaka mitano. Kwa hiyo alikubali funzo la Biblia bila malipo akaanza kuja kwenye mikutano kwenye Jumba la Ufalme. Alimwambia rafiki mvulana wake na wengine yale aliyokuwa akijifunza. Itikio likawa nini? Hawakutaka kuhusika hata kidogo na hayo na wakamshtaki Annette kwamba alikuwa amepigwa msasa. Hata hivyo, baadaye wale waliopinga zaidi wakaanza kujifunza Biblia.
Kama kielelezo, chukua Espen, kijana mwenye miaka 20. Alisikia kuhusu habari njema za Ufalme kutoka kwa rafiki mvulana wa Annette na mara hiyo akataka funzo la Biblia. Hata hivyo, alikuwa akingojea kufungwa gerezani kwa muda wa miezi minne, kwa kuwa alikuwa amehusika katika kusafirisha kimagendo dawa za kulevya na, kama vile Annette, alikuwa amehusika mara kadhaa katika uvunjaji nyumba. Yeye pia alikuwa mtumizi wa tumbaku, marijuana, na dawa nyinginezo za kulevya. Sasa, ni nini ambacho kingeweza kumfanya mtu aliyekuwa amehusika katika mambo hayo atake kuanza kujifunza Biblia? Espen alianza kutambua utupu na ukosefu wa kusudi katika njia yake ya maisha. Yeye asimulia hivi: “Nilivutiwa na ahadi za Biblia za wakati ujao ulionipa kusudi katika maisha. Kwa hiyo nilianza kujifunza ili nipate kujua ikiwa nilikuwa nimeambiwa ile kweli.”
Wengine Wataka Kujifunza Biblia
Karibu wakati huo, kijana mmoja kutoka kikundi icho hicho cha vijana akapata kusikia habari njema, naye pia akaanza kujifunza na kuhudhuria mikutano. Tena, funzo likaanzishwa na mwingine wa vijana hao, naye akaanza kuhudhuria mikutano. Muda mfupi baadaye, hata kijana mwingine akajiunga na marafiki wake katika kujifunza Biblia na kufanya maendeleo ya kiroho. Ndipo bado kijana mwingine katika kikundi icho hicho akavutiwa na mabadiliko chanya ambayo marafiki wake walikuwa wakifanya, na katika muda mfupi, yeye alitaka kujifunza Biblia.
Gilbert, mwanamuziki mchanga kutoka kikundi icho hicho, sasa alianza kujifunza Biblia. Wazazi wake wote wawili walikuwa wamekufa kwa kansa, kwa hiyo alifarijiwa na tumaini la Biblia la ufufuo. (Yohana 5:28, 29) Yeye pia alikuwa akitumia marijuana na kuishi maisha ya ufasiki, na alikuwa akijitakia makuu ya kuwa bingwa wa muziki wa roki. Hata hivyo, wakati ulipopita, alifanya maendeleo mazuri ya kiroho na upesi akaamua kuwa Shahidi wa Yehova. Hatimaye, ndugu mchanga zaidi wa Espen akaanza kuichunguza Biblia na kushirikiana na Mashahidi.
Kweli ya Biblia Inabadili Maisha
Badiliko kubwa lilitukia katika vijana hao waliokuwa wakivalia ovyoovyo, kuwa na nywele zisizochanwa, na kujihusisha na dawa za kulevya, wivi, na uhalifu mwingine mwingi. Annette ni mhubiri mzuri wa Ufalme na ametumikia akiwa painia kwa karibu mwaka mmoja. Espen na Gilbert wametumikia wakiwa mapainia wasaidizi, na wao ni watumishi wa huduma pia. Wote wawili wamefunga ndoa katika kundi la Kikristo. Wanne wengine wa hicho kikundi cha kwanza pia ni wapiga mbiu ya Ufalme wenye bidii!
Namna gani kile kifungo cha miezi minne ambacho Espen alipaswa atimize? Kwa sababu ya mabadiliko aliyokuwa amefanya maishani mwake, Kifungo chake kilibadilishwa kuwa saa 80 za kazi za jumuiya. Kwa kibali cha Polisi na wengine, alitumia saa hizo akifanya kazi kwenye Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova la huko. Polisi walipendezwa sana na mpango huo.
Naam, vijana wengine wengi kotekote ulimwenguni wana historia ya kihalifu. Lakini kweli ya Neno la Mungu imewapa majibu kwa maswali muhimu na tumaini hakika kwa ajili ya wakati ujao. Kwa hiyo, wao si wahalifu au watumizi wa dawa za kulevya tena, na hawaendi mahali-mahali wakiwa wamevalia ovyoovyo. Wakiwa wamebadili njia yao ya maisha, wako sawasawa kabisa na wale watu waliotajwa juu—Mashahidi wa Yehova wachanga, wenye kujipamba vizuri, na watendaji. Wanataka kuwajulisha wengine masuluhisho ya Biblia yenye kudumu kwa matatizo ambayo vijana wengi sana wanayo leo.—Ona 1 Wakorintho 6:9-11.
[Picha katika ukurasa wa 8]
Espen, Annette, na Gilberty