Paradiso au Mahali pa Kutupia Takataka—Wewe Wapendelea Jambo Gani?
HAKUNA yeyote ambaye angalimdhania kuwa mwingine ila kuwa: mtalii kutoka Ulaya aliyehitaji pumziko na aliyekuwa na hamu ya kufurahia jua kwenye kisiwa kilicho kama paradiso. Akiivuka miinuko ya mchanga iliyopakana na ukingo wa bahari, alienda kwa uangalifu katikati ya takataka za chupa, mikebe, mifuko ya plastiki, vikaratasi vya kufungia peremende, magazeti ya habari, na magazeti mengine yaliyotupwa. Akiwa ameudhika kwa wazi, alistaajabu kama hiyo ndiyo paradiso aliyokuwa amesafiri kuifikia.
Je! umepata kuwa na ono kama hilo? Kwa nini watu huota juu ya kuwa na likizo katika paradiso fulani, lakini wanapokuwa huko, hawasiti kuigeuza kuwa mahali hasa pa kutupia takataka?
Si Katika “Paradiso” Tu
Kupuuza huko kwa wazi uzuri, unadhifu, na usafi hakutukii tu katika mahali palipo kama “paradiso” ambako watalii wengi humiminikia. Jamii ya ki-siku-hizi imekumbwa sana na uchafuzi karibu kila mahali. Biashara nyingi husababisha kadiri kubwa ya uchafuzi kwa kutokeza tani nyingi za takataka. Takataka zenye sumu zisizoondoshwa ifaavyo na aksidenti za mivujo ya mafuta inatisha kuharibu maeneo makubwa-makubwa ya dunia yetu, ikiyafanya yasifae kwa uhai.
Vita pia huchafua. Ulimwengu ulipotazama kwa hofu, ile vita ya Ghuba ya Uajemi ya 1991 ilitokeza mambo mengine. Majeshi ya Iraq yaliwasha moto kwa makusudi visima 600 hivi vya mafuta, vikigeuza Kuwait “kuwa njozi ya kiapokalipsi ya helo,” kama vile gazeti la habari la Ulaya lilivyosimulia hali hiyo. Gazeti la Ujerumani Geo liliuita moto huo “msiba mkuu zaidi wa kimazingira ambao ulipata kusababishwa na wanadamu.”
Vita hiyo ilipoisha, kazi ya usafishaji ilianza mara hiyo. Kuzima tu visima hivyo vyenye kuwaka moto kulihusisha miezi mingi ya kazi ngumu. Shirika la Afya Ulimwenguni liliripoti kwamba uchafuzi uliongezeka katika Kuwait huenda ukasababisha hesabu ya watu wanaokufa huko ikue kwa asilimia 10.
Wenye Hatari Kidogo Lakini Wenye Kuudhi Sana
Kwa kila kielelezo mashuhuri na kibaya sana cha uharibifu mkubwa wa kimazingira, kuna maelfu ya vielelezo vidogo. Wenye kutupa-tupa takataka na “wasanii” wa kuchora katika sehemu za umma huenda wakawa wachafuzi wenye hatari kidogo zaidi, lakini hata hivyo wanainyang’anya Dunia uwezo wayo wa kuwa paradiso.
Katika sehemu fulani michoro katika sehemu za umma ni ya kawaida sana hivi kwamba raia wanakuwa “vipofu kwa michoro ya sehemu za umma,” hata wasiione michoro hiyo. Michoro hiyo iko kwenye mabehewa ya reli ya chini, kwenye kuta za majengo, na kwenye vibanda vya simu. Michoro hiyo haimo tu kwenye kuta za vyoo vya umma.
Majiji mengine yamejaa majengo yaliyoharibika na kuachwa. Maeneo ya makazi yameharibiwa na makao na bustani zisizo nadhifu. Magari yaliyoharibika, mashine zilizoachwa, na takataka zinachafua mashamba ambayo yangeweza kuwa yenye kuvutia kwa njia yenye kupendeza.
Katika hali nyingine watu huonekana kutohangaika juu ya kuwa na miili isiyo safi na nadhifu. Kutembea-tembea katika mavazi na mapambo ovyoovyo huenda kukawa si jambo linalokubalika tu bali pia kuwa jambo la kimtindo. Wale wanaothamini unadhifu na usafi huonwa kuwa washamba kabisa.
Kazi Kubwa Kama Nini!
Ni kampeni kubwa kama nini ya usafishaji ambayo ingehitajiwa ili kugeuza fuko, misitu, na milima ya makao yetu ya kidunia kuwa paradiso zinazoonyeshwa katika picha za majalada yenye kung’aa ya magazeti ya kiutalii—zaidi ya hayo ni usafishaji wa kadiri kubwa kama nini ambao ungehitaji kufanyiwa majiji, miji, na mashamba na watu wenyewe!
Mtalii aliyetajwa hapo mbeleni alifurahia kuona kikundi cha wasafishaji kikipitia eneo hilo baadaye siku hiyo kikiondoa vile vipande vikubwa-vikubwa vya takataka. Hata hivyo, waliacha nyuma vipande vya gilasi zilizovunjika, vifuniko vya chupa, vifuniko vya mikebe, na vigutu vingi sana vya sigareti visiweze kuhesabiwa. Kwa hiyo hata baada ya usafishaji, bado kulikuwako ushuhuda mwingi wa kwamba mandhari hiyo ilifanana sana na mahali pa kutupia takataka kuliko paradiso.
Usafishaji wa duniani pote ili kuiokoa Dunia sayari kutoka kuwa mahali pa kutupia takataka pa duniani pote ungehitaji kuondolewa mbali kwa alama zote za mkumbo huo. Je! kuna matarajio yoyote kwamba usafishaji huo utatukia? Ikiwa ndivyo, kwa jinsi gani? Ni nani atakayeutekeleza? Wakati gani?