Shangilia Katika Dunia Safi Iliyoko Mbele!
TWAWEZA kufurahi kama nini kwamba Yehova, Mungu wa utaratibu na usafi, atatimiza kusudi lake la kwanza la kufanya dunia kuwa paradiso ya duniani pote! (Isaya 11:6-9) Yeye anaahidi hivi: “Neno langu, litokalo katika kinywa changu; halitanirudia bure, bali litatimiza mapenzi yangu.” “Mungu hawezi kusema uongo,” kwa hiyo hayo si maneno matupu tu.—Isaya 55:11; Waebrania 6:18.
Twaweza kuwa na kitulizo kwamba Yehova ataingilia mambo kwa upendo kabla ya wanadamu kusababisha uchafuzi mwingi sana, hivi kwamba uharibifu kamili wa kimazingira usiweze kukomeshwa!—Ufunuo 11:18.
Yehova ataondolea mbali wachafuzi wa kimakusudi wasiotubu na watu wanaopuuza kanuni zake za utaratibu na usafi. Hakuna atakayeruhusiwa ahatarishe Paradiso itakayorudishwa.—Mithali 2:20-22.
Wakati wa utawala wa Ufalme wa Mungu, chini ya mwelekezo wa Kristo Yesu, wanadamu watafundishwa jinsi ya kung’olea mbali visababishi vyovyote vinavyobaki vya uchafuzi wa kimwili. Wakati huo—si sasa—ndipo itakapokuwa lazima watumishi wote wa Mungu wahusike kwa bidii katika hatua za binafsi na za pamoja zitakazochangia usafishaji wa duniani pote usio na kifani.—Linganisha Ezekieli 39:8-16.
Waokokaji wa mwisho wa mfumo mbovu wa mambo uliopo wataunga mkono programu hiyo ya usafishaji wa kimwili kwa ujitoaji na idili ileile waliyonayo wanaposhiriki katika kampeni ya leo ya usafishaji wa kiroho.—Zaburi 110:3.
Kwa hakika dunia safi itakuja, ikitanguliwa na kampeni kubwa zaidi ya usafishaji ya wakati wote, yenye kutimizwa na Ufalme wa Mungu. Alama zote za uchafuzi zitaondolewa mbali. Hakutakuwa tena mahali popote pa umma palipochorwa-chorwa. Hakutakuwa tena chupa, mikebe, mifuko ya plastiki, vikaratasi vya kufungia peremende, magazeti ya habari, na magazeti mengine yaliyotupwa yakichafua ufuko au mahali popote pa kiparadiso.
Shangilia katika dunia safi iliyoko mbele!
[Picha katika ukurasa wa 7]
Je! wewe utashiriki katika usafishaji wa duniani pote unaokuja?