“Kufundisha kwa Kimungu” Mikusanyiko ya Wilaya
WOTE wanaotamani kufundishwa na Yehova wanatazamia kwa hamu “Kufundishwa kwa Kimungu” Mikusanyiko ya Wilaya. Programu hiyo ya siku nne itakazia sehemu za maana za kufundishwa kwa Maandiko kunakolinda Wakristo katika nyakati hizi za matatizo ya kibinafsi na msukosuko wa ulimwengu wenye kuongezeka. Programu hiyo itawasaidia wakinze kwa imara ‘neno lo lote lisilopatana na mafundisho yenye uzima’ na kuwa walimu bora zaidi wa neno la Mungu.—1 Timotheo 1:10.
Tuna vielelezo vizuri kama nini vya kuiga! Mwalimu Mkuu Zaidi siye mwingine ila Yehova Mungu mwenyewe! Hivyo, Elihu alimwambia Ayubu ifaavyo kwamba Yehova ndiye “atufundishaye zaidi ya hayawani wa nchi, na kutufanya wenye hekima kuliko ndege za angani.” Aliuliza hivi pia kuhusu Yehova: “Ni nani afundishaye kama yeye?” (Ayubu 35:11; 36:22) Mungu anarejezewa kwenye Isaya 30:20, NW, kuwa “Mfunzi Mtukufu.”
Wa pili tu baada ya Yehova akiwa mwalimu ni Yesu Kristo. Aliitwa “Mwalimu” na “Mfunzi,” akirejezewa hivyo mara 50 hivi katika Gospeli. Kujapokuwa kuponya kwake kwingi kwa ajabu na miujiza mingine, Yesu hakujulikana kuwa Tabibu bali kuwa Mwalimu, Mfunzi.—Mathayo 8:19; Luka 5:5, NW; Yohana 13:13.
Kwa kufaa sana, Yesu aliwafundisha wanafunzi na mitume wake kuwa walimu kama alivyokuwa. Twaweza kuona hilo kutokana na Mathayo 10:5 hadi 11:1 na Luka 10:1-11. Muda mfupi kabla ya kupaa mbinguni, Yesu aliwapa wanafunzi wake utume wa kufundisha unaojulikana sana uliorekodiwa kwenye Mathayo 28:19, 20. Kitabu cha Matendo, pamoja na barua zilizopuliziwa zinazofuata kitabu hicho katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, zinasimulia jinsi wafuasi wa Yesu wa mapema walivyoutekeleza utume huo wa kufundisha kwa bidii nyingi, kwa ustadi, na kwa uaminifu.
Kazi hiyo ya kufundisha ni ya haraka leo kuliko wakati mwingine wowote ule. Tunaishi katika siku za mwisho za mfumo huu wa mambo, na kwa sababu hiyo, uhai unahusika. Ili watu wasishiriki katika dhambi za Babuloni Mkubwa na kupokea sehemu za mapigo yake, ni lazima wafundishwe na kusaidiwa kutoka katika Babuloni na kuamua kumtumikia Yehova na Ufalme wake.—Ufunuo 18:4.
Ili kuwasaidia Mashahidi wa Yehova wote katika jitihada zao za kutekeleza utume wao wa kufundisha, Yehova kupitia tengenezo lake ameandaa “Kufundishwa kwa Kimungu” Mikusanyiko ya Wilaya. Mikusanyiko hiyo ya siku nne itaanza katika Kizio cha Kaskazini katika kiangazi cha mapema. Kila mtumishi wa Yehova aliyejiweka wakfu na ahakikishe kwamba ahudhuria angalau mmojawapo mikusanyiko hiyo, akiwepo na kusikiliza kwa uangalifu kutoka wimbo na sala ya kufungua Alhamisi alasiri hadi sala ya kufunga Jumapili alasiri.