Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w94 2/1 kur. 8-13
  • Ufundishaji wa Kimungu Hushinda

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ufundishaji wa Kimungu Hushinda
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Jitihada ya Kutafuta Hekima
  • Kitabu Kikuu cha Mafundisho cha Yehova
  • Uelewevu wa Hatua kwa Hatua
  • Katika Nuru Nzuri Ajabu ya Mungu
  • Abudu Katika Roho na Kweli
  • Kushinda Majaribu na Ulimwengu
  • Furahia Manufaa za Ufundishaji wa Kimungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Ufundishaji wa Kimungu Watoa Uchocheo Wenye Nguvu
    Huduma Yetu ya Ufalme—1994
  • Mikusanyiko Yenye Kusisimua Yaendeleza Ufundishaji wa Kimungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • “Kufundisha kwa Kimungu” Mikusanyiko ya Wilaya
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
w94 2/1 kur. 8-13

Ufundishaji wa Kimungu Hushinda

“Macho yako yatawaona waalimu [Mfunzi Mtukufu, NW] wako; na masikio yako yatasikia neno nyuma yako, likisema, Njia ni hii, ifuateni.” —ISAYA 30:20, 21.

1. Kwa nini maagizo ya Yehova yaweza kuitwa ifaavyo ufundishaji wa kimungu?

YEHOVA MUNGU ndiye Chanzo cha ufundishaji bora zaidi ambao yeyote aweza kupokea. Tukisikiliza wakati asemapo, hasa kupitia Neno lake Takatifu, yeye atakuwa Mfunzi wetu Mtukufu. (Isaya 30:20) Maandiko ya Biblia ya Kiebrania humwita pia “Aliye wa Kimungu.” (Zaburi 50:1, NW) Kwa hiyo, maagizo ya Yehova ni ufundishaji wa kimungu.

2. Ni kweli katika maana gani kwamba Mungu pekee ndiye mwenye hekima?

2 Ulimwengu huonea fahari taasisi zayo nyingi za elimu, lakini hakuna mojayazo inayotoa ufundishaji wa kimungu. Kwani, hekima yote ya kilimwengu ya enzi zote ni duni ilinganishwapo na maagizo ya kimungu yanayotegemea hekima ya Yehova isiyo na kikomo. Warumi 16:27 lasema kwamba Mungu peke yake ndiye mwenye hekima, na hiyo ni kweli katika maana ya kwamba ni Yehova pekee aliye na hekima kamili.

3. Kwa nini Yesu Kristo ndiye mfundishaji mkuu zaidi aliyepata kutembea duniani?

3 Mwana wa Mungu, Yesu Kristo, ni kielelezo bora cha hekima na ndiye mfundishaji mkuu zaidi aliyepata kutembea duniani. Si ajabu! Kwa enzi nyingi Yehova alikuwa amekuwa Mfundishaji wake mbinguni. Kwa kweli, ufundishaji wa kimungu ulianza wakati Mungu alipoanza kufundisha kiumbe chake cha kwanza, M̃wana wake mzaliwa pekee. Kwa hiyo Yesu angeweza kusema hivi: “Kama Baba alivyonifundisha ndivyo ninenavyo.” (Yohana 8:28; Mithali 8:22, 30) Maneno ya Kristo mwenyewe yaliyorekodiwa katika Biblia huongezea ujuzi wetu wa ufundishaji wa kimungu. Kwa kufundisha yale ambayo Yesu alifundisha, Wakristo wapakwa humtii Mfunzi wao Mtukufu, ambaye mapenzi yake ni kwamba “hekima ya Mungu iliyo ya namna nyingi” ijulishwe kupitia kutaniko.—Waefeso 3:10, 11; 5:1; Luka 6:40.

Jitihada ya Kutafuta Hekima

4. Ni nini imesemwa kuhusu uwezo wa ubongo?

4 Kupata hekima inayotokana na ufundishaji wa kimungu hutaka kutumia kwa bidii uwezo wetu wa kufikiri tuliopewa na Mungu. Hilo lawezekana kwa sababu ubongo wa kibinadamu una uwezo mkubwa sana. Kitabu The Incredible Machine chasema hivi: “Hata kompyuta za hali ya juu zaidi tuwezazo kuwazia ni duni zikilinganishwa na ubongo wa kibinadamu ambao ni wenye kutatanika na wenye kuweza kupokea mambo mapya kwa kadiri ambayo karibu haina kikomo—sifa hizo zikiwezeshwa na mfumo wao wa viishara vya kielektroni-kemia uliotatana, uliopangwa kwa sehemu-sehemu zenye utaratibu mzuri. . . . Mamilioni ya viishara vinavyopita kasi akilini mwako wakati wowote ule hupeleka habari nyingi ajabu. Huleta habari kuhusu mazingira ya ndani na ya nje ya mwili wako: juu ya kukazika kwa misuli ya kidole chako cha mguu, au harufu nzuri ya kahawa, au maelezo yenye kuchekesha ya rafiki. Kadiri ambavyo viishara vingine vinashughulikia na kuchanganua habari, hivyo hutokeza hisiamoyo, kumbukumbu, fikira, au mipango fulani inayoongoza kwenye uamuzi fulani. Karibu mara iyo hiyo, viishara kutoka katika ubongo wako huambia sehemu nyinginezo za mwili wako mambo ya kufanya: kukinyosha-nyosha kidole chako cha mguu, kunywa ile kahawa, kucheka, au labda kutoa jibu lenye kuchekesha. Wakati uo huo ubongo wako unaongoza pia kupumua kwako, utendaji wa damu yako, hali-joto ya mwili wako, na shughuli nyinginezo za maana sana ambazo wewe huna habari nazo. Huo hupeleka amri zinazofanya mwili wako uendelee kusawazika na kufanya kazi kwa utaratibu yajapokuwa mabadiliko ya mara kwa mara katika mazingira yako. Huo pia hujitayarisha kwa ajili ya mahitaji ya wakati ujao.”—Ukurasa 326.

5. Hekima ni nini, katika maana ya Kimaandiko?

5 Ingawa bila shaka ubongo wa kibinadamu una uwezo mzuri ajabu, tunaweza kutumiaje ubongo katika njia bora zaidi? Si kwa kujitia wenyewe kipekee katika funzo la bidii la lugha, historia, sayansi, au dini ya ulinganisho. Twapaswa kutumia uwezo wetu wa kufikiri hasa ili tupokee ufundishaji wa kimungu. Huo pekee ndio hutokeza hekima ya kweli. Lakini hekima ya kweli ni nini? Katika maana ya Kimaandiko, neno hekima hukazia uamuzi mzuri unaotegemea ujuzi sahihi na uelewevu halisi. Hekima hutuwezesha kutumia ujuzi na uelewevu kwa mafanikio katika kusuluhisha matatizo, kuepuka au kuondolea mbali hatari, kusaidia wengine, na kutimiza miradi. Kwa kupendeza, Biblia hutofautisha hekima na upumbavu na ujinga—tabia ambazo kwa kweli tungependa kuepuka.—Kumbukumbu la Torati 32:6; Mithali 11:29; Mhubiri 6:8.

Kitabu Kikuu cha Mafundisho cha Yehova

6. Ikiwa tutaonyesha hekima ya kweli, ni lazima nini kitumiwe vizuri?

6 Tumezungukwa na hekima nyingi ya kilimwengu. (1 Wakorintho 3:18, 19) Kwani, ulimwengu huu umejaa shule na maktaba zenye mamilioni ya vitabu! Vitabu vingi kati ya hivyo ni vya mafundisho vinavyotoa maagizo katika lugha, hisabati, sayansi, na nyanja nyinginezo za ujuzi. Lakini yule Mfunzi Mtukufu ameandaa kitabu cha mafundisho kinachopita vitabu vingine vyote—Neno lake lililopuliziwa, yaani Biblia. (2 Timotheo 3:16, 17) Hiyo ni sahihi si wakati inapotaja tu mambo kama vile historia, jiografia, na botania bali pia wakati inapotabiri wakati ujao. Zaidi ya hayo, hiyo hutusaidia tuishi maisha yaliyo ya kufurahisha zaidi na yenye matokeo zaidi sasa hivi. Bila shaka, kama vile wanafunzi wanavyohitaji kutumia vitabu vyao katika shule ya kilimwengu, ni lazima tufahamu vizuri Kitabu kikuu cha Mafundisho cha Mungu ikiwa tutaonyesha hekima ya kweli kama wale ambao “wamefundishwa na Yehova.”—Yohana 6:45.

7. Kwa nini ungesema kwamba kujua kiakili yale yaliyomo katika Biblia hakutoshi?

7 Lakini, kufahamu Biblia kiakili si sawa na kuwa na hekima ya kweli na kufuata ufundishaji wa kimungu. Ili kutoa kielezi: Katika karne ya 17 W.K., mwanamume Mkatoliki aitwaye Cornelius van der Steen alitaka kuwa Myesuiti lakini hakukubaliwa kwa sababu alikuwa mfupi mno. Manfred Barthel asema hivi katika kitabu chake The Jesuits—History and Legend of the Society of Jesus: “Kamati ilimfahamisha van der Steen kwamba ilikuwa tayari kutoshikilia takwa la kimo, lakini kwa sharti tu la kwamba yeye angejifunza kukariri Biblia nzima kwa moyo. Kisa hicho kisingalistahili kusimuliwa ikiwa van der Steen asingalifuata ombi hilo la kupita kiasi.” Ilikuwa jitihada iliyoje kukariri Biblia yote! Kwa hakika, hata hivyo, ni jambo la maana zaidi kuelewa Neno la Mungu kuliko kulikariri.

8. Ni nini kitatusaidia tunufaike na ufundishaji wa kimungu na kuonyesha hekima ya kweli?

8 Ikiwa tutanufaika kikamili na ufundishaji wa kimungu na kuonyesha hekima ya kweli, tunahitaji ujuzi sahihi wa Maandiko. Ni lazima pia tuongozwe na roho takatifu ya Yehova, au kani ya utendaji. Hiyo itatuwezesha tujifunze kweli za kina kirefu, “mambo ya ndani kabisa ya Mungu.” (1 Wakorintho 2:10, Habari Njema kwa Watu Wote) Kwa hiyo, acheni tujifunze kwa bidii Kitabu kikuu cha Mafundisho cha Yehova na kusali ili kupata mwongozo wake kwa roho takatifu. Kwa kupatana na Mithali 2:1-6 NW, acheni tutoe uangalifu kwenye hekima, mioyo yetu ielekezwe kupata utambuzi, na tupaze wito wa kuomba uelewevu. Tunahitaji kufanya hivyo kana kwamba tulikuwa tukitafuta hazina zilizofichwa, kwani ndipo tu ‘tutaelewa hofu ya Yehova na kupata ujuzi wenyewe wa Mungu.’ Kufikiria baadhi ya ushindi na manufaa za ufundishaji wa kimungu kutaongeza uthamini wetu kuelekea hekima ya kupewa na Mungu.

Uelewevu wa Hatua kwa Hatua

9, 10. Mungu alisema nini, kama ilivyorekodiwa kwenye Mwanzo 3:15, na nini ndio uelewevu ufaao wa maneno hayo?

9 Ufundishaji wa kimungu hushinda kwa kutolea watu wa Yehova uelewevu wa hatua kwa hatua wa Maandiko. Mathalani, tumejifunza kwamba ni Shetani Ibilisi aliyesema kupitia nyoka katika Edeni na kushtaki kwa uwongo kwamba wakati Mungu aliposema kifo kingekuwa adhabu ya kula tunda lililokatazwa, Yeye alikuwa akisema uwongo. Hata hivyo, twaona kwamba kutotii Yehova Mungu kulileta kifo kwa jamii ya kibinadamu. (Mwanzo 3:1-6; Warumi 5:12) Lakini, Mungu aliipa ainabinadamu tumaini alipomwambia nyoka, na hivyo akimwambia Shetani: “Nitaweka uadui kati yako na huyo mwanamke, na kati ya [mbegu yako na mbegu yake, NW]; huo utakuponda kichwa, na wewe utamponda kisigino.”—Mwanzo 3:15.

10 Maneno hayo yalikuwa na siri ambayo imefunuliwa hatua kwa hatua kupitia ufundishaji wa kimungu. Yehova amewafundisha watu wake kwamba kichwa kikuu cha Biblia ni kutetewa kwa enzi kuu yake kupitia ile Mbegu, mzao wa Abrahamu na Daudi akiwa na haki halali ya utawala wa Ufalme. (Mwanzo 22:15-18; 2 Samweli 7:12, 13; Ezekieli 21:25-27) Mfunzi wetu Mtukufu ametufundisha pia kwamba Yesu Kristo ndiye Mbegu ya msingi ya “mwanamke,” tengenezo la Mungu la ulimwengu wote mzima. (Wagalatia 3:16) Ujapokuwa kila mtihani ambao Shetani alimletea, Yesu alidumisha uaminifu-maadili—hata hadi kifo, kule kupondwa kwa Mbegu kwenye kisigino. Tumejifunza pia kwamba warithi-washirika wa Ufalme 144,000 kutoka katika ainabinadamu watashiriki pamoja na Kristo katika kuponda kichwa cha Shetani, “yule nyoka wa zamani.” (Ufunuo 14:1-4; 20:2; Warumi 16:20; Wagalatia 3:29; Waefeso 3:4-6) Jinsi tunavyothamini ujuzi huo wa Neno la Mungu!

Katika Nuru Nzuri Ajabu ya Mungu

11. Kwa nini yaweza kusemwa kwamba ufundishaji wa kimungu hushinda kwa kuleta watu katika nuru ya kiroho?

11 Ufundishaji wa kimungu hushinda kwa kuleta watu katika nuru ya kiroho. Wakristo wapakwa wamekuwa na ono hilo kwa utimizo wa 1 Petro 2:9: “Ninyi ni mzao mteule, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu wa milki ya Mungu, mpate kuzitangaza fadhili zake yeye aliyewaita mtoke gizani mkaingie katika nuru yake ya ajabu.” Leo nuru ya kupewa na Mungu hufurahiwa pia na “umati mkubwa” utakaoishi milele katika dunia-paradiso. (Ufunuo 7:9; Luka 23:43, NW) Kadiri Mungu anavyowafunza watu wake, Mithali 4:18 huthibitika kuwa kweli: “Njia ya wenye haki ni kama nuru ing’aayo, ikizidi kung’aa hata mchana mkamilifu.” Utaratibu huo wa kujifunza hatua kwa hatua huongeza uelewevu wetu wa ufundishaji wa kimungu, kama vile wanafunzi wafanyavyo maendeleo kwa sababu ya msaada mzuri wa mfundishaji wanapojifunza fasihi, historia, au somo jinginelo.

12, 13. Ufundishaji wa kimungu umewasaidia watu wa Yehova dhidi ya hatari zipi za kimafundisho?

12 Ushindi mwingine zaidi wa ufundishaji wa kimungu ni kwamba huo huwalinda wapokezi wao wanyenyekevu dhidi ya “mafundisho ya mashetani.” (1 Timotheo 4:1) Kwa upande mwingine, ebu tazama Jumuiya ya Wakristo! Huko nyuma katika 1878, kasisi wa Roma Katoliki John Henry Newman aliandika hivi: “Wakati huo wakitegemea uwezo wa Ukristo ili kukinza ambukizo la uovu, na kubadili vyombo na mazoea yenyewe ya ibada ya mashetani kuwa ya utumizi wa kievanjeli . . . kuanzia nyakati za zamani viongozi wa Kanisa walikuwa tayari, iwapo fursa inatokea, kutumia, au kuiga, au kuzuia sherehe na desturi zilizopo za jumuiya, kutia na falsafa ya jamii iliyoelimika.” Newman aliongeza kwamba vitu kama vile maji matakatifu, mavazi ya makasisi, na mifano “vyote vilikuwa na chanzo cha kipagani, na vikatakaswa kwa kukubaliwa katika Kanisa.” Watu wa Mungu wanashukuru kwelikweli kwamba ufundishaji wa kimungu huwalinda dhidi ya uasi-imani kama huo. Huo hushinda kila aina ya ibada ya mashetani.—Matendo 19:20.

13 Ufundishaji wa kimungu hushinda makosa ya kidini katika kila njia. Mathalani, tukiwa watu wanaofundishwa na Mungu, hatuamini katika Utatu bali tunakiri kwamba Yehova ndiye Aliye Juu Zaidi, Yesu ni Mwanae, na roho takatifu ni kani ya utendaji ya Mungu. Sisi hatuhofu moto wa helo, kwani twang’amua kwamba helo ya Biblia ni kaburi la kawaida la ainabinadamu. Na ingawa wanadini bandia husema kwamba nafsi ya kibinadamu haiwezi kufa, twajua kwamba wafu hawajui neno lolote. Orodha ya kweli tulizopata kupitia ufundishaji wa kimungu haina kikomo. Ni baraka kama nini kuwa huru na utumwa wa kiroho wa Babuloni Mkubwa, milki ya ulimwengu ya dini bandia!—Yohana 8:31, 32; Ufunuo 18:2, 4, 5.

14. Kwa nini watumishi wa Mungu wanaweza kuendelea kutembea katika nuru ya kiroho?

14 Kwa sababu ufundishaji wa kimungu hushinda makosa ya kidini, huo huwezesha watumishi wa Mungu watembee katika nuru ya kiroho. Kwa kweli, wao wasikia neno nyuma yao likisema: “Njia ni hii, ifuateni.” (Isaya 30:21) Mafundisho ya Mungu hulinda watumishi wake pia dhidi ya mawazo bandia. Wakati “manabii bandia” walipokuwa wakisababisha taabu katika kutaniko la Korintho, mtume Paulo aliandika hivi: “Silaha za vita vyetu si za mwili, bali zina uwezo katika Mungu hata kuangusha ngome; tukiangusha mawazo na kila kitu kilichoinuka, kijiinuacho juu ya elimu ya Mungu; na tukiteka nyara kila fikira ipate kumtii Kristo.” (2 Wakorintho 10:4, 5; 11:13-15) Mawazo yaliyo kinyume cha ufundishaji wa kimungu huangushwa na maagizo yanayotolewa kwa upole kutanikoni na kwa kuhubiri habari njema kwa wale walio nje.—2 Timotheo 2:24-26.

Abudu Katika Roho na Kweli

15, 16. Ni nini maana ya kumwabudu Yehova katika roho na kweli?

15 Kazi ya kuhubiri Ufalme isongapo mbele, ufundishaji wa kimungu hushinda katika kuonyesha wapole jinsi ya kumwabudu Mungu “katika roho na kweli.” Kwenye kisima cha Yakobo karibu na jiji la Sikari, Yesu alimwambia mwanamke Msamaria kwamba yeye angeweza kuandaa maji yanayotoa uhai wa milele. Akirejezea Wasamaria, yeye aliongeza hivi: “Ninyi mnaabudu msichokijua . . . Saa inakuja, nayo sasa ipo, ambayo waabuduo halisi watamwabudu Baba katika roho na kweli. Kwa maana Baba awatafuta watu kama hao wamwabudu.” (Yohana 4:7-15, 21-23) Ndipo Yesu akajitambulisha kuwa Mesiya.

16 Lakini sisi twaweza kumwabuduje Mungu katika roho? Kwa kutoa ibada safi kutoka kwa mioyo yenye shukrani iliyojaa upendo kwa Mungu kwa msingi wa ujuzi sahihi wa Neno lake. Twaweza kumwabudu katika kweli kwa kukataa uwongo wa kidini na kwa kufanya mapenzi ya kimungu, kama yanavyofunuliwa katika Kitabu kikuu cha Mafundisho cha Yehova.

Kushinda Majaribu na Ulimwengu

17. Ungeweza kuthibitishaje kwamba ufundishaji wa kimungu umesaidia watumishi wa Yehova wakabili majaribu?

17 Watu wa Mungu wanapokabili majaribu, ufundishaji wa kimungu hushinda tena na tena. Fikiria hili: Kwenye mwanzo wa Vita ya Ulimwengu 2, katika Septemba wa 1939, watumishi wa Yehova walihitaji mwono-ndani wa kipekee katika Kitabu chake kikuu cha Mafundisho. Makala katika Mnara wa Mlinzi la Novemba 1, 1939, ilikuwa yenye msaada mkubwa, ikiandaa waziwazi ufundishaji wa kimungu kwa habari ya kutokuwamo kwa Kikristo. (Yohana 17:16) Vivyo hivyo, katika miaka ya mapema ya 1960, makala za Mnara wa Mlinzi juu ya ujitiisho wa kadiri kwa ‘wenye mamlaka wakuu’ wa kiserikali zilisaidia watu wa Mungu wafuate ufundishaji wa kimungu walipokabili msukosuko wa kijamii.—Warumi 13:1-7; Matendo 5:29.

18. Wale waliodai kuwa Wakristo katika karne ya pili na ya tatu W.K. walionaje vitumbuizo vyenye kushusha tabia, na ufundishaji wa kimungu huandaa msaada gani kwa habari hiyo leo?

18 Ufundishaji wa kimungu hutusaidia tushinde vishawishi, kama vile kushawishwa kutafuta vitumbuizo vinavyoshusha tabia. Ona yale yaliyosemwa na wale waliodai kuwa Wakristo wa karne ya pili na ya tatu ya Wakati wa Kawaida wetu. Tertullian aliandika hivi: “Sisi hatuhusiki, katika kusema, kuona au kusikia, kile kichaa cha sarakasi, yale mambo ya aibu katika majumba ya michezo ya kuigiza, ule ukatili wa uwanja wa michezo.” Mwandikaji mwingine wa kipindi hicho aliuliza hivi: “Mkristo mwaminifu anafanya nini akiwa kati ya vitumbuizo hivyo, kwa kuwa hata hapaswi kufikiri juu ya uovu? Kwa nini yeye apate furaha katika viwakilisho vya uchu?” Hata ingawa waandikaji hao waliishi miaka fulani baada ya Wakristo wa karne ya kwanza, wao waliepuka vitumbuizo vinavyoshusha tabia. Leo, ufundishaji wa kimungu hutupa sisi hekima tuepuke vitumbuizo vilivyo vichafu, visivyo na adili, na vyenye jeuri.

19. Ufundishaji wa kimungu hutusaidiaje tuushinde ulimwengu?

19 Kutii ufundishaji wa kimungu hutuwezesha tuushinde ulimwengu wenyewe. Naam, kutumia mafundisho ya Mfunzi wetu Mtukufu hutufanya tushinde mavutano maovu ya ulimwengu huu ambao umo katika uwezo wa Shetani. (2 Wakorintho 4:4; 1 Yohana 5:19) Waefeso 2:1-3 lasema kwamba Mungu ametuhuisha ingawa tulikuwa tumekufa katika makosa na dhambi tulipokuwa tukitembea kulingana na mtawala wa mamlaka ya hewa. Twamshukuru Yehova kwamba ufundishaji wa kimungu hutusaidia tushinde tamaa za kilimwengu na roho inayotoka kwa adui wake na wetu—mdanganyi-mkuu, Shetani Ibilisi!

20. Ni maswali gani yastahiliyo ufikirio zaidi?

20 Basi, kwa wazi, ufundishaji wa kimungu hushinda katika njia nyingi. Kwa kweli, inaonekana haiwezekani kutaja ushindi wao wote. Huo huathiri watu kotekote ulimwenguni. Lakini huo unakufanyia nini? Ufundishaji wa kimungu unaathirije maisha yako?

Umejifunza Nini?

◻ Hekima ya kweli yaweza kufasiliwaje?

◻ Mungu amefunua nini hatua kwa hatua kuhusu Mwanzo 3:15?

◻ Ufundishaji wa kimungu umeshindaje katika mambo ya kiroho?

◻ Ni nini maana ya kumwabudu Mungu katika roho na kweli?

◻ Ufundishaji wa kimungu umesaidiaje watumishi wa Yehova washinde majaribu na ulimwengu?

[Picha katika ukurasa wa 10]

Yesu alidumisha uaminifu-maadili hadi kifo—kule kupondwa kwa Mbegu kwenye kisigino

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki