Yehova Huwakumbuka Wagonjwa na Wazee-Wazee
KULAZIMIKA kukabili “wakati wa ubaya [msiba, NW]” kwaweza kuwa jambo gumu sana. (Zaburi 37:18, 19) Wakati kama huo waweza kuja kwa namna ya kuzeeka pamoja na ule udhaifu mbalimbali unaohusika nako. Wengine huingia wakati wa msiba wanapopatwa na ugonjwa mahututi, wa muda mrefu. Huenda wakahisi kana kwamba ugonjwa wao unaongoza maisha yao, ukitawala mawazo na matendo yao yote.
Lakini ni uhakikishio kukumbuka kwamba Yehova hukaza macho yake juu ya watumishi wake wote. Moyo wake hushangilia wakati watumishi wake wenye kujitoa wanapoendelea kuonyesha uaminifu-mshikamanifu na hekima ijapokuwa uzee, ugonjwa, au hali nyingine zenye kujaribu. (2 Mambo ya Nyakati 16:9a; Mithali 27:11) Mfalme Daudi atuhakikishia hivi: “BWANA [Yehova, NW] yu karibu na wote wamwitao, . . . naye atakisikia kilio chao.” Naam, yeye ajua kushindana kwao; yeye huwaimarisha kwa roho yake. “Na kuwaokoa.” Yeye huwakumbuka na kuwasaidia wavumilie. (Zaburi 145:18, 19) Lakini namna gani sisi? Je! sisi huwakumbuka wagonjwa na wazee-wazee kama vile Yehova?
Udhaifu mbalimbali kwa sababu ya ugonjwa au uzee ni mambo halisi ya maisha katika mfumo huu uliopo. Ni mambo ya hakika ambayo ni lazima tuvumilie mpaka Yehova anapotimiza kusudi lake kwa dunia na ainabinadamu. Leo, watu wengi zaidi wanaishi hadi umri wa uzee sana, kwa hiyo wengi sana wanafahamu udhaifu mbalimbali wa watu hao. Kwa kuongezea, wakiwa wangali wachanga, wengi hupatwa na aksidenti au magonjwa yenye kutisha uhai au yenye kulemaza. Mpaka ulimwengu huu wa zamani upitie mbali, ugonjwa na uzee utaendelea kuwa ugumu mkubwa.
Tunathamini kama nini wale kati yetu walio wagonjwa na wazee-wazee wanaoendelea wakiwa mfano wa “kustahimili mabaya, na wa uvumilivu”! Naam, “twawaita heri [wenye furaha, NW] wao waliosubiri.” (Yakobo 5:10, 11) Wengi walio wazee-wazee ambao nguvu zao zimepungua sasa wameshiriki kwa miongo mingi katika kufundisha, kuzoeza, na kuwafinyanga wale ambao sasa huongoza katika kutaniko. Wazee-wazee kadhaa wanashangilia pia kuona kwamba watoto wao wameshiriki katika huduma ya wakati wote.—Zaburi 71:17, 18; 3 Yohana 4.
Kwa njia iyo hiyo, tunawathamini wale miongoni mwetu ambao ni wagonjwa mahututi na bado, ijapokuwa kuteseka kwao, huweza kututia moyo kupitia uaminifu wao. Hao wanapoonyesha uthibitisho wa tumaini lao bila ugeugeu, tokeo linachochea sana na kuimarisha imani. Amani yao ya akili na uradhi unafunua imani ambayo kwa kweli yastahili kuigwa.
Inastusha wakati mtu anapopatwa kwa ghafula na kansa, ugonjwa wa ghafula, au hali nyingine inayobadili maisha yake kabisa. Pia ni mtihani mgumu kwa wazazi kuona watoto wao wakipatwa na ugonjwa au kuteseka kwa sababu ya aksidenti. Wengine wanaweza kufanya nini ili kusaidia? Wakati wowote kama huo wa msiba ni mtihani kwa udugu wote wa Kikristo. Ni fursa ya kuonyesha kwamba ‘rafiki wa kweli ni ndugu ambaye amezaliwa kwa siku ya taabu.’ (Mithali 17:17) Kwa asili, si wagonjwa na wazee-wazee wote wawezao kutazamia msaada wa kibinafsi kutoka kwa kila mshiriki wa kutaniko. Lakini Yehova atahakikisha kwamba kupitia roho yake wengi watahisi kusukumwa kusaidia katika njia mbalimbali. Na wazee wanaweza kuwa macho ili kuhakikisha kwamba hakuna anayepuuzwa.—Ona Kutoka 18:17, 18.
Jaribu Kuelewa
Unapojaribu kumsaidia mtu fulani, ni jambo la maana kuwa na uwasiliano mzuri, na huo wahitaji wakati, subira, na hisia-mwenzi. Ukiwa msaidizi, kwa asili unatamani ‘kutia nguvu kwa kinywa chako’; lakini sikiliza kwa uangalifu kabla ya kusema au kutenda, ama huenda mwishoni ukawa ‘mfariji mwenye kutaabisha.’—Ayubu 16:2, 5.
Nyakati nyingine ni vigumu kwa wagonjwa na wazee-wazee kuficha kufadhaika kwao. Wengi wamethamini sana tumaini lao la kuokoka dhiki kubwa, na sasa wanahofu kwamba watakufa kabla ya wakati huo. Pia, mara nyingi hali yao huwachosha na kuwatia wasiwasi. Kudumisha imani ikiwa hai na yenye nguvu ni shindano gumu, hasa wakati mtu hawezi tena kufuata tamaa ya moyo ya kushiriki kikamili katika huduma ya Kikristo. Mzee mmoja Mkristo alimtembelea dada mmoja mzee-mzee; aliposali pamoja naye, mzee huyo alimwomba Yehova asamehe dhambi zetu. Baada ya sala hiyo aliona kwamba dada huyo alikuwa akilia machozi. Alieleza kwamba alihisi alihitaji msamaha wa Yehova wa pekee kwa sababu ya kutoweza kushiriki tena katika kuhubiri nyumba kwa nyumba. Naam, ingawa mara nyingi hisia ya kutoweza au ya kutofaa haistahili, inaweza kumhuzunisha mtu sana moyoni.
Ujue kwamba hangaiko na uchovu unaweza kuathiri usawaziko wa akilini. Kwa sababu ya udhaifu mbalimbali wa uzee au mkazo wa ugonjwa wenye kudhoofisha, mtu aweza kuhisi ameachwa na Yehova, labda akisema hivi: “Nimefanya nini? Kwa nini niteseke?” Kumbuka maneno ya Mithali 12:25: “Uzito katika moyo wa mtu huuinamisha; bali neno jema huufurahisha.” Jaribu kupata maneno mazuri yatakayofariji. Wazee-wazee walio na maumivu huenda hata wakaonyesha tamaa ya kufa, kama vile Ayubu. Hilo halipasi litustushe; jaribu kuelewa. Si lazima malalamiko kama hayo yawe uthibitisho wa ukosefu wa imani au kutumaini. Ayubu alisali ‘kufichwa Sheoli,’ na bado maneno yake mara tu baada ya maneno hayo yalifunua imani yake thabiti kwamba Yehova angemfufua baadaye. Imani imara inamwezesha mtu apitie vipindi vya uchungu mkubwa na mshuko wa moyo na bado kubaki karibu na Yehova.—Ayubu 14:13-15, NW.
Kuonyesha Heshima kwa Wagonjwa na Wazee-Wazee
Ni jambo la maana sana kuwatendea wagonjwa na wazee-wazee kwa heshima na fahari. (Warumi 12:10) Wasipoitikia upesi kama zamani au ikiwa hawawezi kufanya mengi kama zamani, usipoteze subira yako. Usiingilie upesi na kuwafanyia maamuzi. Hata tuwe na nia njema kadiri gani, tukienenda kwa njia ya kutawala au ya kimamlaka, sikuzote hiyo itamnyima yule mtu mwingine kujistahi kwake. Katika insha ya utafiti ya kidaktari iliyochapishwa katika 1988, mtafiti mmoja, Jette Ingerslev, alieleza jambo ambalo kikundi cha watu wa miaka 85 waliloona wenyewe kuwa la maana zaidi kwa ubora wa maisha yao: “Walitaja sehemu za kutangulizwa zaidi: kuwa na watu wa ukoo; afya njema; ya mwisho lakini yenye maana vilevile, kuweza kujiamulia wenyewe.” Ona kwamba mzee wa ukoo Yakobo hakutendewa na wana wake kwa njia ya kumshusha alipokuwa amezeeka; mambo aliyotamani yalistahiwa.—Mwanzo 47:29, 30; 48:17-20.
Ni lazima wagonjwa watendewe kwa fahari pia. Mzee mmoja alipoteza uwezo wake wa kusema, kusoma, na kuandika kwa sababu ya kosa lililofanywa wakati wa upasuaji. Hilo lilikuwa pigo kali, lakini wazee wenzake waliamua kufanya lolote wawezalo ili asiwe na hisia za kutofaa. Sasa wanamsomea barua zote za kutaniko wakimtia ndani katika kufanya mipango ya mambo mengine ya kikundi. Kwenye mikutano ya wazee, wanajaribu kupata maoni yake. Wanamsaidia ajue kwamba bado wanamwona kuwa mzee mwenzao na wanathamini kuwa pamoja naye. Katika kutaniko la Kikristo, sisi sote twaweza kujitahidi ili kusiwe mgonjwa wala mzee-mzee anayehisi ‘ametupwa’ au kuachwa.—Zaburi 71:9.
Msaada Ili Kupata Nguvu za Kiroho
Sisi sote twahitaji chakula cha kiroho ili tudumishe imani yetu ikiwa hai na imara. Ndiyo sababu tunatiwa moyo tusome Biblia na vichapo vya Biblia kila siku na kushiriki kwa bidii katika mikutano ya Kikristo na utendaji wa kuhubiri. Mara nyingi, wagonjwa na wazee-wazee wanahitaji msaada ili kutimiza hilo, na ni jambo la maana kufanya lile linalofaa hali yao hasa. Kwa furaha, wengi waweza kuhudhuria mikutano ikiwa wanasafirishwa na kupewa msaada mdogo katika Jumba la Ufalme. Kuhudhuria kwao mikutano kama hiyo ni kitia-moyo kikubwa kwa kutaniko. Uvumilivu wao unachochea na kuimarisha imani.
Katika visa vingi wagonjwa na wazee-wazee wanaweza pia kuwa na ushirika wa maana katika huduma ya Kikristo. Wengine wanaweza kutiwa ndani katika kikundi cha gari ili kutoa ushahidi, na bila shaka watahisi kuburudishwa kwa kuweza kufanya ziara chache. Hilo lisipowezekana tena, wanaweza kupata shangwe katika kutoa ushahidi vivi hivi kwa watu mmoja mmoja wanaokutana nao. Dada mmoja aliyepatwa na kansa aliamua kutumia maisha yake yaliyobaki kwa jitihada ya pekee ya kueneza habari njema. Kuhubiri kwake kwa ujasiri kulikuwa kitia-moyo kwa wote. Hata alipanga maziko yake mwenyewe ili ushahidi mzuri uweze kutolewa kwa watu wa ukoo wasioamini, wafanyakazi, na majirani. Hivyo hali zake zenye kutia uchungu ‘zilikuwa na tokeo la kuieneza habari njema,’ na azimio lake la kuonyesha imani na uhakika lilizifanya siku zake za mwisho ziwe na maana ya pekee.—Wafilipi 1:12-14, NW.
Ni vizuri kusaidia wagonjwa na wazee-wazee waimarishwe kiroho. Familia zinaweza kuwaalika washiriki jioni pamoja nao, au mara kwa mara sehemu ya funzo lao la familia linaweza kuhamishwa kwenye nyumba ya mtu ambaye hawezi kutoka nje. Mama mmoja aliwaleta watoto wake wawili wachanga zaidi kwenye nyumba ya dada mwenye umri mkubwa zaidi ili waweze kusoma Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia pamoja. Hilo lilimfurahisha dada huyo mzee-mzee, na watoto walifurahia uangalifu aliowapa.
Hata hivyo, kuna nyakati ambapo mtu mgonjwa hapaswi kusumbuliwa sana, na huenda ikafaa zaidi kuwasomea habari fulani kwa sauti mara kwa mara tu. Lakini, kumbuka kwamba ikiwa mtu ni mdhaifu sana kimwili kushiriki katika mazungumzo, huenda huyo akahitaji na kutamani bado ushirika wa kiroho. Tunaweza kusali pamoja na hao, kuwasomea vitabu, au kusimulia maono; lakini ni lazima tuwe waangalifu tusije tukakaa muda mrefu kuliko wawezavyo kuvumilia.
Kuna utumishi mmoja mtakatifu ambao wagonjwa na wazee-wazee wengi waweza bado kufanya: kusali kwa ajili ya wengine. Wanafunzi wa mapema walitolea huduma hiyo umaana mkubwa. Katika pindi moja waligawanya kazi katika kutaniko kwa njia ambayo mitume wangeweza kukaza fikira juu ya sala. Epafra mwaminifu anatajwa kuwa ‘mwenye kufanya bidii sikuzote kwa ajili ya wengine katika maombi yake.’ (Wakolosai 4:12; Matendo 6:4) Sala kama hiyo ni ya maana na yenye mafaa sana.—Luka 2:36-38; Yakobo 5:16.
Yehova huwakumbuka wagonjwa na wazee-wazee na kuwatunza katika wakati wao wa msiba. Yeye hutazamia ifaavyo kwamba sisi pia tuonyeshe lile tuwezalo kufanya kuwasaidia na kuwategemeza. Hangaiko tunaloonyesha laangaza azimio letu kudumisha uaminifu-maadili wetu wenyewe. Na tunafurahi kufikiria juu ya maneno haya ya Mfalme Daudi: “BWANA [Yehova, NW] anazijua siku za wakamilifu, na urithi wao utakuwa milele.”—Zaburi 37:18.
[Sanduku katika kurasa za 28 na 29]
KUTOA MSAADA UFAAO kwa uelewevu
RAFIKI na watu wa ukoo wanapaswa kupata ujuzi wa msingi lakini ulio sahihi juu ya jinsi ya kuwatunza wagonjwa na wazee-wazee. Zaidi ya yote, wanaweza kutiwa moyo wadumishe mtazamo ufaao kuelekea maisha, kuhisi kuhitajiwa na kuthaminiwa, na kujihisi kuwa wanafaa. Hivyo ubora wa maisha yao utabaki kwenye hali ya kuhifadhi shangwe yao katika Yehova, ijapokuwa maumivu na uchungu wao mbalimbali. Imeonwa kwamba Mashahidi wa Yehova wengi huishi kufikia umri mkubwa sana. Jambo moja lenye nguvu linalochangia hilo bila shaka ni kupendezwa kwao kwa uchangamfu na tumaini lililo mbele, nia yao nyangavu ya akilini, na kushiriki kwao katika utendaji wa Ufalme kadiri wawezavyo. Msimamizi wa Watch Tower Society Frederick W. Franz, aliyekufa kwa amani katika mwaka wake wa 100 baada ya maisha ya shangwe yenye matokeo, alikuwa kielelezo kizuri sana cha hilo.—Linganisha 1 Mambo ya Nyakati 29:28.
Kwa ujumla, kukazia fikira mambo ya msingi ya utunzaji wa kila siku kwaweza kumaanisha mengi: usafi, chakula kifaacho, vinywaji na chumvi ya kutosha, mazoezi yafaayo, hewa safi, kusuguliwa kwa uanana, na mazungumzo yenye kuchochea. Chakula kifaacho kinaweza kuchangia kusikia vizuri zaidi, kuona vizuri zaidi, akili kufanya kazi vizuri zaidi, na hali-njema ya kimwili nzuri zaidi, pamoja na hali ya juu zaidi ya kukinza magonjwa. Kwa wazee-wazee jambo sahili la chakula kifaacho na vinwaji vingi linaweza kumaanisha tofauti kati ya hali njema na kupungukiwa na akili. Huenda ikahitaji kufikiria kwa kadiri fulani ili kupata namna ya mazoezi ya kimwili yanayomfaa mtu fulani. Dada mmoja anayekuja kumsomea vitabu dada mzee-mzee na ambaye karibu ni kipofu huanza na kumaliza kila ziara ya kila juma kwa kucheza dansi kwa uanana na dada huyo huku na huku chumbani. Sikuzote tepu-rekoda iko tayari na muziki uliochaguliwa, na wote wawili hufurahia “mazoezi” hayo.
Katika nchi nyingi, mashirika ya kusaidia yanaweza kuandaa msaada ufaao wenye thamani na kutoa maarifa na shauri kuhusu hali hususa na jinsi ya kukabiliana nazo. (Bila shaka, sikuzote Mkristo anapaswa ajiangalie asije akakengeushwa na utendaji mbalimbali unaogeuza fikira kutoka huduma yetu ya kweli ya Kikristo.) Nyakati nyingine msaada unatolewa kwa namna ya mpango wa kukopa kitanda cha hospitali, mikongojo, kanda, kiti cha magurudumu, chombo cha kusaidia kusikia, na kadhalika. Kwa kuwa wazee-wazee wengi huhisi kwamba hawahitaji chochote au kwamba si lazima kupata vitu vipya kama hivyo, mara nyingi ni lazima watu wa ukoo watoe shauri lifaalo au hata kutumia uvutio wa kusadikisha. Mpini ufaao kwa mlango wa chumba cha kuogea unaweza kuleta shangwe zaidi ya kweli kuliko shada la maua.
Kuwatunza wazee-wazee kwaweza kusababisha mkazo mwingi wa akilini, hasa ikiwa mtu huyo anakuja kupungukiwa na akili. Mara nyingi kupungukiwa na akili huja kwa njia yenye hila. Mtu anaweza kutangua hali hiyo kwa kumzuia mgonjwa asijikalie kitako bila sababu. Mtu aliyepungukiwa na akili kwa sababu ya uzee anaweza kuudhika kwa ghafula na mtu aliyekuwa anampenda sana zamani. Ni lazima watu wa ukoo watambue kwamba mtu anayezeeka anaweza hata kusahau kila kitu kinachohusu kweli—tokeo lenye kuhuzunisha la kudhoofika kwa mwili, si uthibitisho wa kupoteza imani.
Mgonjwa akiwa hospitalini au katika makao ya uguzi, mawasiliano mazuri na wafanyakazi ni ya lazima ili wafanyakazi wajue jambo la kufanya kuhusiana na siku za kuzaliwa, Krismasi, au sikukuu nyingine za kilimwengu. Ikiwa upasuaji ni wa lazima, watu wa ukoo wanaweza kueleza na kuandika maoni ambayo mgonjwa huyo amekuwa nayo kuhusu utiaji damu mishipani.