Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w93 8/15 kur. 27-30
  • Jinsi Wakristo Wanavyoweza Kuwasaidia Wazee-Wazee

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jinsi Wakristo Wanavyoweza Kuwasaidia Wazee-Wazee
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Msaidizi Mwenye Kujitoa
  • Kupanga Mambo Ni Jambo la Thamani
  • Wakati Kifo Kinapoonekana Hakiwezi Kuepukika
  • Daraka Tunaloshiriki
  • Familia ya Kikristo Huwasaidia Wazee-Wazee
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • ‘Kuendelea Kuangalia’ Masilahi za Watu Wazee-Wazee
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
  • Yehova Huwakumbuka Wagonjwa na Wazee-Wazee
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Ni Daraka la Kikristo Kuwatunza Walio Wazee
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2004
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
w93 8/15 kur. 27-30

Jinsi Wakristo Wanavyoweza Kuwasaidia Wazee-Wazee

“HATULEGEI; bali ijapokuwa utu wetu wa nje unachakaa; lakini utu wetu wa ndani unafanywa upya siku kwa siku. . . . Tusiviangalie vinavyoonekana, bali visivyoonekana. Kwa maana vinavyoonekana ni vya muda tu; bali visivyoonekana ni vya milele.” Ndivyo mtume Paulo alivyosema katika barua yake ya pili kwa Wakorintho.—2 Wakorintho 4:16-18.

Katika nyakati za kale, wanaume na wanawake wa imani walikazia macho yao vitu visivyoonekana, vilivyotia ndani mambo yote ambayo Mungu wao, Yehova, alikuwa ameahidi kufanya kwa wakati wake. Katika kitabu cha Waebrania, Paulo asema kwa njia ya kuwasifu watu kama hao, walioidumisha imani yao hadi wakati wa kifo chao—na wengine wao waliishi wakawa wazee sana. Anawarejezea wakiwa kielelezo kwetu, akisema hivi: “Hawa wote wakafa katika imani, wasijazipokea zile ahadi, bali wakaziona tokea mbali na kuzishangilia.”—Waebrania 11:13.

Leo tuko karibu sana na utimizo wa ahadi hizo. Lakini miongoni mwetu tuna wagonjwa na wazee-wazee ambao hawana hakika kwamba wao binafsi watakuwa hai kuona mwisho wa mfumo huu mwovu. Labda baadhi yao pia watakufa katika imani bila kuona ahadi zote zikitimizwa wakiwa hai sasa. Kwa watu kama hao maneno ya Paulo kwenye 2 Wakorintho 4:16-18, yanaweza kuwa kitia-moyo kikubwa.

Yehova huwakumbuka waaminifu-washikamanifu wake wote, kutia ndani wagonjwa na wazee-wazee. (Waebrania 6:10) Wazee-wazee waaminifu wanatajwa kwa njia ya heshima mahali kadhaa katika Biblia, na katika Sheria ya Musa, kuna mtajo wa pekee juu ya heshima inayopasa kuonyeshwa kwa wazee-wazee. (Mambo ya Walawi 19:32; Zaburi 92:12-15; Mithali 16:31) Miongoni mwa Wakristo wa mapema, wazee-wazee walitendewa kwa njia ya staha. (1 Timotheo 5:1-3; 1 Petro 5:5) Kitabu kimoja cha Biblia kina simulizi lenye kupendeza la utunzaji wenye upendo na kujidhabihu kunakogusa moyo kulikoonyeshwa na mwanamke mchanga mmoja kuelekea mama-mkwe wake aliyezeeka. Kwa kufaa kitabu hicho kinaitwa jina la mwanamke huyo mchanga, Ruthu.

Msaidizi Mwenye Kujitoa

Maisha yalikuwa machungu kwa Naomi aliyezeeka. Njaa kubwa ilikuwa imemlazimisha yeye, pamoja na familia yake ndogo, kuacha nyuma marafiki na urithi katika Yuda na kuishi mashariki mwa Mto Yordani katika nchi ya Moabu. Mume wa Naomi alikufa huko, akimwacha na wavulana wao wawili. Baadaye, wao walikua na kuoa, lakini wao pia wakafa. Naomi aliachwa bila warithi wa kumtunza.

Alikuwa mzee sana asiweze kuanza familia mpya, na maisha yalionekana kutofaa kitu. Bila ubinafsi, alitaka kurudisha Ruthu na Orpa, wajane wa wana wake wawili, kwenye nyumba za mama zao ili wajitafutie waume. Angerudi nchi yake akiwa peke yake. Leo pia, baadhi ya wazee-wazee huhisi mshuko wa moyo, hasa ikiwa wamewapoteza wapendwa katika kifo. Kama vile Naomi, huenda wakahitaji mtu fulani awatunze, lakini hawataki kuwa mzigo.

Hata hivyo, Ruthu hakumwacha mama-mkwe wake. Yeye alimpenda mwanamke huyo mzee-mzee, na alimpenda Yehova, Mungu aliyeabudiwa na Naomi. (Ruthu 1:16) Kwa hiyo wakiwa pamoja walianza safari ya kurudi Yuda. Katika nchi hiyo, kulikuwa mpango wenye upendo chini ya Sheria ya Yehova kwamba watu maskini wangeweza kuokota, au kukusanya, chochote kilichoachwa mashambani baada ya mavuno kukusanywa. Ruthu, aliyekuwa mchanga zaidi, alijitoa kwa nia kufanya kazi hiyo, akisema: “Acha niende, tafadhali.” Alifanya kazi bila kuchoka kwa manufaa ya wote wawili.—Ruthu 2:2, 17, 18, NW.

Uaminifu wa Ruthu na upendo wake kwa Yehova ulikuwa kitia-moyo chenye nguvu kwa Naomi, aliyeanza kufikiri kwa njia chanya na yenye kujenga. Kujua kwake Sheria na desturi za nchi hiyo kulikuwa na mafaa sasa. Alitoa shauri lenye hekima kwa msaidizi wake mwenye kujitoa ili mwanamke huyo mchanga angeweza kupata tena urithi wa familia na kuwa na mwana wa kuendeleza nasaba ya familia, kupitia ndoa ya ndugu-mkwe. (Ruthu, sura 3) Ruthu ni kielelezo kizuri kwa wale wanaojidhabihu ili kuwatunza wagonjwa au wazee-wazee. (Ruthu 2:10-12) Ndani ya kutaniko leo, mengi vivyo hivyo yanaweza kufanywa ili kuwasaidia wagonjwa na wazee-wazee. Jinsi gani?

Kupanga Mambo Ni Jambo la Thamani

Katika kutaniko la Kikristo la mapema, orodha iliwekwa ya wajane waliohitaji utegemezo wa kimwili. (1 Timotheo 5:9, 10) Leo vilevile, katika hali fulani wazee wa kutaniko wanaweza kutayarisha orodha ya wagonjwa na wazee-wazee wanaohitaji ufikirio wa pekee. Katika baadhi ya makutaniko mzee mmoja ameombwa ashughulikie hilo likiwa daraka lake la pekee. Kwa kuwa wazee-wazee wengi, kama vile Naomi, hawataki kuomba msaada, ndugu huyo angehitaji kuwa na ustadi wa kuchanganua hali na—kwa njia ya busara na yenye utambuzi—hakikisha kwamba mambo ya lazima yanafanywa. Kwa kielelezo, angeweza kuona ikiwa Jumba la Ufalme lina maandalizi ya kutosha kwa ajili ya wagonjwa na wazee-wazee. Ikiwa yafaa, angeweza kufikiria mambo kama vile kijia chenye mteremko kwa ajili ya viti vyenye magurudumu, vyoo vyenye vifaa vinavyowafaa, vyombo vya masikio kwa wale wasiosikia vizuri, na mahali pa kuwekea viti vya pekee. Ndugu huyo angeweza pia kuhakikisha kwamba wote wasioweza kuja kwenye Jumba la Ufalme wanaweza kuazima ukanda ambao umerekodiwa mikutano au kuisikiliza kupitia simu.

Huenda pia kukawa uhitaji wa kupanga usafiri kwenye mikutano na mikusanyiko. Dada mmoja mzee-mzee alikuwa na tatizo kwa sababu yule aliyekuwa akimpeleka kwenye mikutano kwa ukawaida hakuwako. Alilazimika kuwapigia watu wengi simu kabla ya hatimaye kumpata mtu ambaye angeweza kumsafirisha na kwa sababu ya hiyo alikuja kuhisi kwamba alikuwa mzigo. Mpango fulani pamoja na mzee wa kutaniko ambaye angeweza kushughulikia mambo yote kama hayo ungalipunguza aibu yake.

Mzee huyo wa kutaniko angeweza pia kuomba familia mbalimbali kama zingechukua zamu ya kuwatembelea wazee-wazee. Kwa njia hiyo watoto wangejifunza kwamba kuwatunza wazee-wazee ni sehemu ya maisha ya Mkristo. Ni vema kwa watoto kujifunza kuchukua daraka hilo. (1 Timotheo 5:4) Mwangalizi mmoja wa mzunguko asema hivi: “Kwa yale ambayo nimeona, ni watoto au vijana wachache sana wanaowatembelea wazee-wazee au wagonjwa bila kuombwa.” Labda ni kwamba tu hawafikirii jambo hilo, au huenda ikawa hawajui kwa hakika lile la kufanya au la kusema; wazazi wanaweza kuwafundisha hilo.

Lakini, kumbuka kwamba wazee-wazee wengi wangethamini kujua kimbele kwamba rafiki fulani anakuja. Hilo huwapa shangwe zaidi ya kumtazamia mgeni. Wageni wakileta viburudisho, kama vile chai au maandazi, na kusafisha mahali upesi baadaye, hilo humwondolea mzee-mzee kazi ya ziada. Mume na mke wazee-wazee, walio na nguvu nyingi bado, wana siku moja ya kawaida kila juma ambayo wanapakia kikapu kidogo cha (kuwekea chakula cha) mandari na kuwatembelea wazee-wazee mbalimbali katika kutaniko. Ziara zao huthaminiwa sana.

Kwa manufaa ya wazee-wazee, makutaniko mengi yanafanya Funzo la Kitabu la Kutaniko katika saa za mchana. Katika sehemu fulani baadhi ya familia na wahubiri waseja waliombwa kama wangependa na kama wangeweza kuunga mkono kikundi kimoja kama hicho, na tokeo likawa kikundi cha funzo la kitabu ambamo wazee-wazee na wachanga zaidi wangeweza kutunzana.

Si wazee wa kutaniko peke yao wanaopaswa kuchukua hatua ya kwanza katika jambo hili. Sisi sote twapaswa kutambua mahitaji ya wagonjwa na ya wazee-wazee. Tunaweza kuwasalimu kwenye Jumba la Ufalme na kuchukua wakati wa kuongea nao. Wanaweza kufurahia kualikwa kwenye kikusanyiko kisichopangwa kimbele. Au tunaweza kuwaalika waandamane nasi kwenye mandari au hata likizo. Mara nyingi Shahidi mmoja aliwapeleka wahubiri wazee-wazee pamoja naye katika gari lake alipoenda nje ya mjini kufanya ziara za kibiashara. Ni jambo la maana kuwasaidia wazee-wazee waendelee kuhisi wanahusishwa katika mambo. Usiwaruhusu wajitenge wenyewe, kama vile Naomi alitaka kufanya, jambo ambalo lingeharakisha hatua ya kuzeeka au kupungukiwa akili.

Vijana walemavu au walio wagonjwa wanahitaji ufikirio pia. Shahidi mmoja aliyekuwa na wavulana watatu wenye magonjwa yasiyoponyeka, ambao wawili kati yao wamekufa tangu wakati huo, asema hivi: “Yaweza kuwa vigumu kwa kutaniko kuendelea kumtunza mtu ikiwa ana ugonjwa unaoendelea kwa kipindi kirefu cha wakati. Kwa nini wahubiri wachanga wenye kutegemeka wasipewe mgawo wa kuzungumzia andiko la siku na kusoma sura moja kutoka katika Biblia kila siku pamoja na rafiki yao asiyeweza kutoka kitandani? Vijana, kutia ndani mapainia, wanaweza kuchukua zamu ya kufanya hivyo.”

Wakati Kifo Kinapoonekana Hakiwezi Kuepukika

Sikuzote watumishi wa Yehova wamekabili kifo kwa ujasiri, iwe ni kwa sababu ya ugonjwa au mnyanyaso. Wagonjwa wanapoanza kuhisi kwamba huenda kifo kikawa karibu, ni jambo la asili kwao kupatwa na hisia tofauti za moyoni. Baada ya kifo chao, watu wa ukoo wao pia wangepitia kipindi cha marekebisho, huzuni, na kukubaliana na hali. Kwa hiyo mara nyingi ni vizuri kwa yule aliye mgonjwa kusema waziwazi juu ya kifo, kama vile Yakobo, Daudi, na Paulo.—Mwanzo, sura 48 na 49; 1 Wafalme 2:1-10; 2 Timotheo 4:6-8.

Shahidi mmoja aliye tabibu aandika hivi: “Ni lazima tuseme waziwazi juu ya habari hii. Sijapata kuona kamwe katika kazi-maisha yangu kwamba kumficha mgonjwa jambo la kwamba anakufa kunamsaidia kwa njia yoyote.” Hata hivyo, tunahitaji kuelewa lile ambalo mgonjwa mwenyewe ataka kujua, na wakati atakapo kujua jambo hilo. Wagonjwa wengine huelewesha wazi kwamba wanajua kwamba kifo chao kiko karibu, na wanahitaji kuzungumzia fikira na hisia zao juu ya jambo hilo. Wengine huonekana kusisitiza juu ya kutumaini, na rafiki zao hufanya vema kutumaini pamoja nao.—Linganisha Warumi 12:12-15.

Mtu aliye karibu kufa aweza kuwa amechoka sana au kufadhaika sana hivi kwamba ni vigumu kwake kusali. Labda mgonjwa kama huyo atafarijiwa kwa kujifunza kutoka Warumi 8:26, 27 kwamba Mungu aelewa “kuugua kusikoweza kutamkwa.” Yehova ajua kwamba chini ya mkazo wa jinsi hiyo huenda ikawa vigumu kwa mtu kupata maneno ya kusali.

Inapowezekana, ni jambo la maana kusali pamoja na mgonjwa. Ndugu mmoja asimulia hivi: “Mama yangu alipokuwa akifa na hakuwa na nguvu tena ya kusema, alitoa ishara kwa kuikunja mikono yake kwamba alitaka tusali pamoja naye. Baada ya sala yetu, tuliimba mmoja wa nyimbo za Ufalme, kwani sikuzote mama yangu alipenda muziki sana. Mwanzoni, tulikuwa tukiimba midomo yetu ikiwa imefumbwa, kisha tukaimba tukiyatamka maneno kwa sauti ya chini. Ilikuwa wazi kwamba alifurahia hilo. Bila shaka, nyimbo hizi tunazohusianisha na maisha yetu tukiwa Mashahidi wa Yehova hueleza hisia ambazo zingekuwa vigumu kuelezwa kwa njia nyingine.”

Kusema pamoja na mtu anayekufa kunahitaji upendo, busara, na ufikirio. Mgeni anaweza kutayarisha mambo ya kusema ambayo ni yenye kujenga na yenye kuimarisha imani, na anapaswa awe macho kuepuka maongezi yasiyofaa juu ya watu wengine na matatizo yao. Pia, muda wa ziara unapaswa urekebishwe ili uwe wa kiasi na unaofaa. Mgonjwa akionekana kutokuwa na fahamu, ni vema kukumbuka kwamba huenda bado akaweza kusikia yale yanayosemwa. Kwa hiyo uwe mwangalifu juu ya yale unayosema.

Daraka Tunaloshiriki

Kuwatunza wagonjwa na wazee-wazee ni daraka zito. Kwa wale walio karibu zaidi na mgonjwa, daraka hilo linahusisha mambo mengi sana, kimwili na katika hisia za moyoni pia. Wanahitaji na kustahili uelewevu na msaada kutoka kwa wengine katika kutaniko. Wale wanaowatunza washiriki wa familia au waamini wenzao walio wagonjwa wanafanya jambo linalofaa, hata ikimaanisha kwamba wanakosa baadhi ya mikutano au kwamba kushiriki kwao katika huduma ya shambani kunapungua kwa kipindi fulani. (Linganisha 1 Timotheo 5:8.) Wataimarishwa na mtazamo wa kutaniko wenye uelewevu. Nyakati nyingine huenda ndugu au dada fulani akaweza kumtunza mgonjwa kwa muda ili mtunzaji wa kawaida aweze kuhudhuria mkutano au kufurahia muda wa saa chache zenye kuburudisha katika kazi ya kuhubiri.

Bila shaka, ikiwa wewe mwenyewe ndiye mgonjwa, unaweza kufanya jambo fulani pia. Kuwa na hali ya kukosa tumaini na ya kuwa hoi kwa habari ya ugonjwa wako kungeweza kukufanya uwe na uchungu, lakini uchungu unamtenganisha mtu na kuwazuia wengine wasimkaribie. Badala ya hivyo ungeweza kujaribu kuonyesha uthamini na kuwa mwenye kushirikiana. (1 Wathesalonike 5:18) Sali kwa ajili ya wengine walio na maumivu. (Wakolosai 4:12) Tafakari juu ya zile kweli nzuri ajabu za Biblia, na kuzungumza juu yazo pamoja na wageni. (Zaburi 71:17, 18) Endelea kwenda sambamba kwa bidii na maendeleo ya watu wa Mungu yenye kuimarisha imani. (Zaburi 48:12-14) Mshukuru Yehova kwa matukio hayo ya furaha. Kutafakari juu ya mambo ya jinsi hiyo kunaweza kufanya miaka yetu ya mwisho iwe na uzuri wayo wenyewe, kama vile jua lenye kushuka linalotoa nuru nzito zaidi na yenye kuchangamsha zaidi ya jua la adhuhuri.

Sisi sote tunapaswa kujitahidi kudumisha lile tumaini linalolinda akili yetu kama kofia ya chuma, hasa katika nyakati za majaribu. (1 Wathesalonike 5:8) Ni vema kutafakari juu ya tumaini la ufufuo na msingi walo imara. Tunaweza kutazama mbele kwa uhakikishio na matazamio yenye hamu kwenye ile siku ambayo hakutakuwa tena ugonjwa wala udhaifu kwa sababu ya uzee. Wakati huo, kila mtu atakuwa na afya njema. Hata wafu watarudi. (Yohana 5:28, 29) Tunaviona vitu hivyo “visivyoonekana” kwa macho ya imani yetu na ya moyo wetu. Usikose kamwe kuviona.—Isaya 25:8; 33:24; Ufunuo 21:3, 4.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki