Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w93 9/1 kur. 15-20
  • Familia ya Kikristo Hufanya Mambo Pamoja

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Familia ya Kikristo Hufanya Mambo Pamoja
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kwa Nini Mfanye Mambo Pamoja?
  • Kuwa Pamoja Katika Funzo la Familia
  • Kuwa Pamoja Katika Kueneza Evanjeli
  • Kuwa Pamoja Katika Kushughulikia Matatizo
  • Kuwa Pamoja Katika Kufanya Tafrija
  • Baraka za Kuwa Pamoja
  • Familia—Binadamu Wanaihitaji!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Kutumia Neno la Mungu Katika Jamaa Zetu Wenyewe
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Je, Kuna Siri ya Kupata Furaha ya Familia?
    Siri ya Furaha ya Familia
  • Jifunzeni Neno la Mungu kwa Ukawaida Mkiwa Familia
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
w93 9/1 kur. 15-20

Familia ya Kikristo Hufanya Mambo Pamoja

“Basi ndugu, nawasihi, . . . mhitimu katika nia moja na shauri moja.”—1 WAKORINTHO 1:10.

1. Hali ikoje kwa habari ya kuungana katika familia nyingi?

JE! FAMILIA yako ni moja iliyoungana? Au kila mtu aonekana akifanya mambo kivyake? Je! mnafanya mambo pamoja? Au mnakuwa pamoja mara haba? Neno lenyewe “familia” hudokeza nyumba iliyounganishwa.a Lakini, si familia zote zilizoungana. Mhadhiri mmoja Mwingereza alifikia hatua ya kusema hivi: “Badala ya kuwa msingi wa jamii njema, familia . . . ndiyo chanzo cha manung’uniko yetu yote.” Je! ni hivyo kuhusu familia yako? Ikiwa ndivyo, je, ni lazima iwe hivyo?

2. Ni watu gani katika Biblia wanaotoa uthibitisho wa kutoka katika familia nzuri?

2 Kwa kawaida kuungana au kutoungana kwa familia hutegemea uongozi wayo, iwe kutoka kwa wazazi wawili au kwa mzazi asiye na mwenzi. Katika nyakati za Biblia, familia zilizoungana ambazo ziliabudu pamoja zilipata baraka ya Yehova. Ndivyo ilivyokuwa katika Israeli la kale, ambako binti Yeftha, Samsoni, na Samweli, kila mmoja alionyesha, katika njia tofauti, uthibitisho wa kutoka katika familia iliyomwogopa Mungu. (Waamuzi 11:30-40; 13:2-25; 1 Samweli 1:21-23; 2:18-21) Katika nyakati za Ukristo wa mapema, Timotheo, mshiriki mwaminifu wa Paulo kwenye baadhi ya safari za Paulo za umishonari, alilelewa na nyanya yake Loisi na mama yake Eunike, akiwa na ujuzi wa Maandiko ya Kiebrania. Alikuja kuwa mwanafunzi na mishonari mwenye kutokeza kama nini!—Matendo 16:1, 2; 2 Timotheo 1:5; 3:14, 15; ona pia Matendo 21:8, 9.

Kwa Nini Mfanye Mambo Pamoja?

3, 4. (a) Ni sifa zipi zinazopaswa kuonekana wazi katika familia iliyoungana? (b) Makao yanaweza kufanywaje yasiwe nyumba tu?

3 Kwa nini yafaa kwa familia kufanya mambo pamoja? Kwa sababu hilo hujenga kuelewana na kustahiana. Badala ya kuwa na uhusiano wa mbali, tunaendelea kuwa na ukaribu na kutoa utegemezo. Makala ya karibuni katika jarida Family Relations ilisema hivi: “Wazo lililo wazi kwa kadiri fulani limetokea likisimulia sifa hususa za ‘familia imara.’ Sifa hizo zatia ndani kujitia katika wajibu kwa mmoja na mwenzake na kuthaminiana, kuwa pamoja, uwasiliano mzuri, uwezo wa kusuluhisha matatizo, na kuwa na hali ya kiroho yenye nguvu.”

4 Sifa hizo zikiwa katika familia, makao hayawi tena kama mahali pa kwenda tu kujaza gari mafuta na kuondoka. Si nyumba tu. Ni mahali panapowavutia washiriki wa familia. Ni mahali salama penye uchangamfu na shauku, huruma, na ufahamu. (Mithali 4:3, 4) Ni kiota ambamo kuungana kwa familia kwapatikana, si tundu la nge lenye mzozano na mgawanyiko. Lakini hilo hutimizwaje?

Kuwa Pamoja Katika Funzo la Familia

5. Tunatumia nini ili kujifunza ibada ya kweli?

5 Tunapata kujifunza ibada ya kweli ya Yehova kwa kutumia uwezo wetu wa kufikiri au “nguvu za kusababu.” (Warumi 12:1, NW) Mwenendo wetu haupaswi kuongozwa na hisia za moyoni za muda tu kama zile zinazochochewa na mahubiri yenye hotuba za msisimuko na ujanja zitolewazo na mashirika ya kidini. Badala ya hivyo, tunachochewa na funzo letu na kutafakari kwa kawaida juu ya Biblia na vichapo vya funzo la Biblia vinavyoandaliwa na “mtumwa mwaminifu mwenye akili.” (Mathayo 24:45) Matendo yetu ya Kikristo yanatokana na kupata kwetu akili ya Kristo juu ya hali yoyote au kishawishi chochote ambacho huenda kikatokea. Kwa habari hiyo, Yehova ndiye Mwelimishaji wetu Mkuu.—Zaburi 25:9; Isaya 54:13; 1 Wakorintho 2:16.

6. Tuna kielelezo kipi cha ulimwenguni pote cha funzo la familia?

6 Funzo la Biblia la familia huchangia sehemu muhimu katika hali ya kiroho ya kila familia ya Kikristo. Nyinyi hufanya funzo lenu la familia lini? Ikiwa halijapangwa au linaamuliwa kwa ghafula, basi yaelekea linafanywa mara haba ikiwa hata lapata kufanywa. Kuwa pamoja katika funzo la familia kwataka ratiba ya kawaida, iliyowekwa. Ndipo wote watajua ni siku gani na saa gani wanatazamiwa kuwapo ili kufurahia kikusanyiko cha familia cha kiroho. Wale washiriki zaidi ya 12,000 wa familia ya Betheli ulimwenguni pote wanajua kwamba funzo lao la familia ni Jumatatu jioni. Inavutia kama nini kwa wajitoleaji hawa wa Betheli kukumbuka kwamba wote wanashiriki funzo lilo hilo mwishoni mwa siku, kuanzia visiwa vya Pasifiki na New Zealand, kisha hatua kwa hatua katika Australia, Japani, Taiwani, Hong Kong, halafu kupitia Esia, Afrika, na Ulaya, na mwishoni katika mabara makuu ya Amerika. Ingawa limetenganishwa na maelfu ya maili na lugha nyingi, funzo hilo la familia huchochea katika washiriki wa familia ya Betheli hisia ya kuwa pamoja. Mwaweza kusitawisha hisia iyo hiyo kupitia funzo lenu la familia, kwa kiwango kidogo zaidi.—1 Petro 2:17; 5:9.

7. Kulingana na Petro, tunapaswa kulionaje neno la kweli?

7 Mtume Petro atushauri hivi: “Kama watoto wachanga waliozaliwa sasa yatamanini maziwa ya akili [yaliyo ya neno, NW] yasiyoghoshiwa, ili kwa hayo mpate kuukulia wokovu; ikiwa mmeonja ya kwamba Bwana ni mwenye fadhili.” (1 Petro 2:2, 3) Petro atoa kielezi kizuri kama nini kwa maneno hayo! Alitumia kitenzi cha Kigiriki e·pi·po·theʹsa·te, ambacho, kulingana na kitabu Linguistic Key to the Greek New Testament, hutokana na neno linalomaanisha “kuwa na hamu nyingi, kutamani, kuwa na uchu.” Linadokeza tamaa nyingi sana. Je! umeona jinsi mnyama mchanga anavyotafuta kwa hamu titi la mama yake na jinsi mtoto mchanga wa kibinadamu anavyoridhika anaponyonya titini pa mama yake? Twapaswa kuwa na tamaa iyo hiyo kwa ajili ya neno la kweli. Msomi Mgiriki William Barclay alisema hivi: “Kwa Mkristo mwenye moyo mweupe, kujifunza neno la Mungu si kazi ngumu bali kunafurahisha, kwani ajua kwamba humo moyo wake utapata chakula unachotamani sana.”

8. Ni ugumu gani humkabili kichwa cha familia katika kuongoza funzo la familia?

8 Funzo la familia humwekea kichwa cha familia daraka kubwa. Anapaswa kuhakikisha kwamba funzo linawapendeza wote na kwamba wote wanaweza kushiriki. Watoto hawapaswi kuhisi kwamba kwa kweli funzo ni kwa ajili ya watu wazima tu. Ubora wa funzo ni wa maana sana kuliko kiasi cha habari kinachopitiwa. Fanya Biblia iwe hai. Inapofaa, wasaidie watoto wako wajionee akilini maeneo na sura za nchi ya Palestina ambako matukio yanayozungumziwa yalitukia. Wote wanapaswa kutiwa moyo kufanya utafiti wao wa kibinafsi na kuushiriki pamoja na familia. Kwa njia hiyo watoto pia wanaweza ‘kukua pamoja na Yehova.’—1 Samweli 2:20, 21, NW.

Kuwa Pamoja Katika Kueneza Evanjeli

9. Kazi ya kuhubiri yaweza kufanywaje kuwa ono la familia lenye furaha?

9 Yesu alisema hivi: “Sharti Injili ihubiriwe kwanza katika mataifa yote.” (Marko 13:10) Maneno hayo yanatolea kila Mkristo mwenye kudhamiria mgawo—wa kueneza evanjeli, kushiriki na wengine habari njema za utawala wa Ufalme wa Mungu. Kufanya hivyo pamoja mkiwa familia kwaweza kuwa ono la kutia moyo na lenye shangwe. Akina mama na akina baba huonea fahari utoaji wa habari njema wa watoto wao. Mume na mke fulani wenye wana watatu kati ya miaka 15 na 21 wanasimulia kwamba sikuzote wamekuwa na zoea la kuandamana pamoja na watoto wao katika kazi ya kuhubiri hadharani kila Jumatano baada ya shule na kila Jumamosi asubuhi. Baba alisema hivi: “Tunawafundisha jambo fulani kila mara. Na tunahakikisha kwamba ni ono la kufurahisha, lenye kutia moyo.”

10. Wazazi wanaweza kuwanufaishaje watoto wao katika huduma?

10 Kufanya kazi pamoja mkiwa familia katika kuhubiri na kufundisha kwaweza kuwa na matokeo mengi. Nyakati fulani watu huitikia vizuri zaidi utoaji wa mtoto ulio sahili na wa moyo mweupe. Kisha, Mama au Baba yupo hapo kusaidia inapohitajiwa. Wazazi wanaweza kuhakikisha kwamba watoto wao wanapata mazoezi ya kuendelea na hivyo kuwa wahudumu ‘wasio na sababu ya kutahayari, wakitumia kwa halali neno la kweli.’ Kuhubiri pamoja katika njia hiyo kwawawezesha wazazi watazame mwelekeo wa mtoto wao, matokeo yake, na tabia zake nzuri katika huduma. Kwa kuwa na utaratibu wa kawaida, wanaona maendeleo ya mtoto na kutoa mazoezi na kitia-moyo cha daima ili kuimarisha imani yake. Wakati uo huo, watoto wanaona kwamba wazazi wao ni vielelezo vyema katika huduma. Katika nyakati hizi za hatari na zenye jeuri, kufanya kazi mkiwa familia iliyoungana na inayojali kwaweza hata kuandaa kadiri fulani ya usalama katika ujirani ambamo uhalifu ni mwingi.—2 Timotheo 2:15; Wafilipi 3:16.

11. Ni nini kiwezacho kwa urahisi kumpunguzia mtoto bidii yake kwa ajili ya kweli?

11 Ni rahisi kwa watoto kuona ikiwa watu wazima wanafuata viwango viwili vya mwenendo. Ikiwa wazazi hawaonyeshi upendo wa moyo mweupe kuelekea kweli na huduma ya nyumba kwa nyumba, watoto hawawezi kutazamiwa hata kidogo kuwa wenye bidii. Hivyo, mzazi mwenye afya njema ambaye utumishi wake pekee wa shambani ni lile funzo la Biblia la kila juma pamoja na watoto aweza kupata hasara kubwa watakapokuwa na umri mkubwa zaidi.—Mithali 22:6; Waefeso 6:4.

12. Familia fulani zinaweza kupataje baraka ya pekee kutoka kwa Yehova?

12 Faida moja ya kuwa “katika nia moja” ni kwamba labda familia yaweza kushirikiana pamoja ili angalau mshiriki mmoja aweze kutumikia akiwa mhudumu painia wa wakati wote katika kutaniko. Familia nyingi kotekote ulimwenguni hufanya hivyo, na wote hupokea baraka kutokana na maono na matokeo yenye kuongezeka ya mshiriki wa familia yao aliye painia.—2 Wakorintho 13:11; Wafilipi 2:1-4.

Kuwa Pamoja Katika Kushughulikia Matatizo

13, 14. (a) Ni hali zipi zinazoweza kuathiri upatano wa familia? (b) Matatizo mengi ya familia yanaweza kuzuiwaje?

13 Katika nyakati hizi ngumu za “mkazo” na “hatari,” sisi sote hupatwa na msongo. (2 Timotheo 3:1, Revised Standard Version; Phillips) Kuna matatizo kazini, shuleni, mtaani, na hata nyumbani kwenyewe. Watu fulani wana afya mbaya au matatizo ya kihisiamoyo yenye kuendelea muda mrefu, ambayo nyakati fulani husababisha mikazo na kutoelewana katika familia. Hali hizo zaweza kushughulikiwaje? Je! ni kwa kila mmoja kunyamaa? Je! ni kwa kujitenga mwenyewe hata ingawa unashiriki makao ayo hayo? La. Badala ya hivyo, tunahitaji kuwasilisha mahangaiko yetu na kuomba msaada. Na ni wapi pengine palipo bora kuliko katika familia yenye upendo?—1 Wakorintho 16:14; 1 Petro 4:8.

14 Kama vile daktari yeyote ajuavyo, kuzuia ugonjwa ni bora kuliko kuutibu. Ndivyo ilivyo kwa habari ya matatizo ya familia. Mara nyingi mazungumzo ya wazi na ya moyo mweupe yaweza kuzuia matatizo yasiwe makubwa. Hata matatizo makubwa yakitokea, yanaweza kushughulikiwa na hata kusuluhishwa ikiwa familia inapitia pamoja kanuni za Biblia zinazohusika. Mara nyingi mzozano unaweza kugeuzwa uwe uhusiano laini kwa kutumia maneno ya Paulo kwenye Wakolosai 3:12-14: “Jivikeni moyo wa rehema, utu wema, unyenyekevu, upole, uvumilivu, mkichukuliana, na kusameheana, mtu akiwa na sababu ya kumlaumu mwenzake. . . . Jivikeni upendo, ndio kifungo cha ukamilifu.”

Kuwa Pamoja Katika Kufanya Tafrija

15, 16. (a) Ni sifa ipi ipaswayo kutofautisha familia za Kikristo? (b) Dini fulani hutokeza watu wa aina gani, na kwa nini?

15 Yehova ni Mungu mwenye furaha, na ile kweli ni ujumbe wa furaha—wenye tumaini kwa ainabinadamu. Zaidi ya hayo, mojawapo matunda ya roho ni shangwe. Shangwe hiyo ni tofauti sana na ile furaha nyingi mno ya muda tu ya mwanariadha anayeshinda katika mchezo fulani wa kushindana. Ni ile hisia ya uradhi yenye kina na ya kuendelea inayofurika moyoni kwa sababu ya kusitawisha uhusiano wa karibu sana na Yehova. Ni shangwe ambayo msingi wayo ni Mungu. Ni shangwe inayotegemea kanuni za kiroho na mahusiano yenye kujenga.—Wagalatia 5:22; 1 Timotheo 1:11.

16 Kwa hiyo, sisi Mashahidi wa Yehova Wakristo, hatuna sababu yoyote ya kuwa wanunaji au ya kuwa bila ucheshi. Dini fulani hutokeza watu kama hao kwa sababu aina yazo ya imani hukazia mambo yasiyofaa. Mafundisho yazo yanatokeza aina ya ibada yenye huzuni, isiyo na shangwe, ambayo si ya Kibiblia wala usawaziko. Hazitokezi familia zenye furaha katika utumishi wa Mungu. Yesu aliona uhitaji wa tafrija na pumziko. Kwa kielelezo, katika pindi moja aliwaalika wanafunzi wake waende ‘kwa faragha, mahali pasipokuwa na watu, wakapumzike kidogo.’—Marko 6:30-32; Zaburi 126:1-3; Yeremia 30:18, 19.

17, 18. Familia za Kikristo zinaweza kufurahia tafrija katika njia zipi zifaazo?

17 Familia vilevile zinahitaji wakati wa kufurahia tafrija. Mzazi mmoja alisema hivi juu ya watoto wake: “Sisi hufanya mambo mengi ya kujifurahisha tukiwa pamoja—kwenda ufukoni, kucheza mpira katika bustani, kupanga mandari milimani. Pindi kwa pindi, tunakuwa na ‘siku ya upainia’ pamoja katika huduma; halafu tunasherehekea kwa kuwa na mlo wa pekee, na hata twaweza kupeana zawadi.”

18 Madokezo mengine ambayo wazazi wanaweza kufikiria ni kufanya safari ndogo-ndogo za kwenda kwenye hifadhi za wanyama, kwenye tamasha ya maonyesho, kwenye majumba ya ukumbusho, na kwingineko kunakovutia. Kutembea msituni, kuwatazama nyuni, na kutunza bustani ni utendaji unaoweza kushirikiwa kwa furaha. Wazazi wanaweza pia kuwatia watoto wao moyo kujifunza kucheza ala fulani ya muziki au kushiriki katika jambo fulani la kujifurahisha lenye mafaa. Kwa hakika, wazazi wenye usawaziko wataweka kando wakati wa kucheza pamoja na watoto wao. Familia zikicheza pamoja, zinaelekea zaidi kukaa pamoja!

19. Ni mwelekeo gani wa kisasa uwezao kuidhuru familia?

19 Mwelekeo wa kisasa ni kwa vijana kutaka kujitenga na familia na kufanya mambo kivyao kwa habari ya tafrija. Ingawa hakuna hatari yoyote kwa kijana kuwa na jambo fulani la kujifurahisha au shughuli fulani analopenda kufanya kibinafsi, lisingekuwa jambo la hekima kuruhusu mapendezi hayo yasababishe ajitenge daima na wengine katika familia. Badala ya hivyo, tunataka kutumia ile kanuni ambayo Paulo alitaarifu: “Kila mtu asiangalie mambo yake mwenyewe, bali kila mtu aangalie mambo ya wengine.”—Wafilipi 2:4.

20. Makusanyiko na mikusanyiko inawezaje kuwa nyakati zenye shangwe?

20 Ni shangwe iliyoje kwetu sote kuona familia zikiketi pamoja kwenye mikusanyiko na makusanyiko! Hivyo, mara nyingi watoto wenye umri mkubwa zaidi wanaweza kusaidia kuwatunza wale wenye umri mdogo zaidi. Mpango kama huo huzuia pia mwelekeo wa wabaleghe fulani wa kujitenga katika vikundi-vikundi kwenye safu za nyuma na kutokutoa uangalifu mwingi kwenye programu ya mkusanyiko. Hata kusafiri hadi na kutoka makusanyiko kwaweza kuleta shangwe wakati familia inapoombwa maoni juu ya njia ya kufuata, mahali-mahali pa kuona njiani, na mahali pa kukaa. Ebu wazia jinsi ambavyo ni lazima iwe ilisisimua familia kusafiri pamoja hadi Yerusalemu katika siku ya Yesu!—Luka 2:41, 42.

Baraka za Kuwa Pamoja

21. (a) Tunaweza kujitahidije kuwa na mafanikio katika ndoa? (b) Ni madokezo gani manne kwa ajili ya ndoa yenye kudumu?

21 Ndoa zenye mafanikio na familia zilizoungana hazijawa kamwe mambo rahisi kutimiza, na hazitokei zenyewe tu. Yaonekana watu fulani huona ni rahisi zaidi kuacha kujitahidi, kuvunja ndoa kwa kutaliki, na kujaribu kuanza upya. Lakini, mara nyingi matatizo ayo hayo hujitokeza katika ndoa ya pili au ya tatu. Jibu lililo bora zaidi ni lile la Kikristo: Jitahidi kufanikiwa kwa kutumia kanuni za Biblia za upendo na staha. Familia zilizoungana hutegemea roho ya kila mtu kumpa mwenzake, isiyo na ubinafsi. Mshauri mmoja wa ndoa alitoa kanuni sahili ya kufanya ndoa zidumu. Aliandika hivi: “Mambo manne ya muhimu yanayopatikana katika karibu ndoa zote nzuri ni nia ya kusikiliza, uwezo wa kuomba msamaha, kuweza kuandaa utegemezo wa daima wa kihisiamoyo, na tamaa ya kugusana kwa shauku.” Mambo hayo kwa kweli yanaweza kusaidia kufanya ndoa idumu kwa sababu yanategemea pia kanuni za Biblia zinazofaa.—1 Wakorintho 13:1-8; Waefeso 5:33; Yakobo 1:19.

22. Ni manufaa gani kadhaa za kuwa na familia iliyoungana?

22 Tukifuata shauri la Biblia, tutakuwa na msingi imara kwa familia iliyoungana, na familia zilizoungana ndio msingi wa kutaniko lililoungana na lenye nguvu kiroho. Hivyo, tutapokea baraka nyingi kutoka kwa Yehova tunapomtolea tukiwa pamoja, sifa zilizoongezeka.

[Maelezo ya Chini]

a “Neno family hutokana na neno la [Kilatini] familia, hapo awali [ikitia ndani] watumishi na watumwa wa nyumba kubwa, kisha nyumba yenyewe pamoja na bwana mkubwa, bibi, watoto—na wafanyakazi.”—Origins—A Short Etymological Dictionary of Modern English, ya Eric Partridge.

Je! Wakumbuka?

◻ Kwa nini yafaa kwa familia kufanya mambo pamoja?

◻ Kwa nini funzo la Biblia la kawaida la familia ni muhimu?

◻ Kwa nini ni vizuri kwa wazazi kushiriki katika huduma ya shambani pamoja na watoto wao?

◻ Kwa nini yasaidia kuzungumzia matatizo ndani ya familia?

◻ Kwa nini familia za Kikristo hazipaswi kuwa zenye majonzi na bila shangwe?

[Picha katika ukurasa wa 17]

Je! familia yako hufurahia ikiwa pamoja angalau mlo mmoja kwa siku?

[Picha katika ukurasa wa 18]

Safari ndogo-ndogo za familia zinapaswa kuwa zenye kupumzisha na zenye kufurahisha

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki