Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w93 9/15 kur. 28-31
  • Dumu Katika Utumishi wa Painia

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Dumu Katika Utumishi wa Painia
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kutimiza Mahitaji ya Kifedha
  • Kupata Kazi ya Muda-Muda
  • Afya Mbaya na Kuvunjika Moyo
  • Hazini Pendeleo Lako la Utumishi
  • Baraka za Huduma ya Painia
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Kutoa Utegemezo kwa Mapainia
    Huduma Yetu ya Ufalme—1992
  • Mapainia Hutoa na Kupokea Baraka
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Baraka za Huduma ya Upainia
    Huduma Yetu ya Ufalme—2003
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
w93 9/15 kur. 28-31

Dumu Katika Utumishi wa Painia

MASHAHIDI WA YEHOVA wapatao 4,500,000 hujulisha habari njema ulimwenguni pote. Miongoni mwao kuna mapainia, au wapiga mbiu ya Ufalme wa wakati wote zaidi ya 600,000. Jeshi hilo la mapainia latia ndani wale wa miaka ya kuanzia kabla ya utineja hadi wale ambao wamestaafu walio katika miaka yao ya 90. Wanatoka katika malezi yote na tabaka zote za maisha.

Bila shaka, wahubiri hao wote wa wakati wote wanataka kufanikiwa katika huduma ya painia. Wengi hutamani kufanya hiyo iwe kazi ya maisha yao yote. Wengine hawawezi kufanya hivyo kwa sababu fulani. Lakini, wengine wameweza kuendelea kupainia yajapokuwa magumu ya kifedha, afya mbaya, kuvunjika moyo, na matatizo mengine. Kwa hiyo wahubiri wa wakati wote wanaweza kukabilianaje na matatizo hayo na bado wadumu katika utumishi wa painia?

Kutimiza Mahitaji ya Kifedha

Kwa ujumla, mapainia hufanya kazi ya kimwili ili kulipia gharama zao, kama vile mtume Paulo. (1 Wathesalonike 2:9) Katika sehemu nyingi za ulimwengu, wanakabili bei zinazozidi kupanda juu za chakula, mavazi, na usafiri. Mara nyingi ni vigumu kupata kazi ya kimwili ya muda-muda wanayohitaji. Zinapopatikana, mara nyingi kazi hizo hutoa mshahara mdogo tu, bila manufaa za bima ya afya.

‘Tukiendelea kuutafuta kwanza Ufalme wa Mungu na uadilifu wake,’ tunaweza kuwa na imani kwamba Yehova ataandaa mahitaji yetu ya kimwili. Kwa hiyo, wakiwa chini ya msongo wa kifedha, mapainia wanahitaji ‘kutohangaikia ya kesho.’ (Mathayo 6:25-34, NW) Wanapojitahidi sana kusuluhisha matatizo hayo, imani yenye nguvu katika Yehova itawazuia wasihangaike isivyofaa.

Mtu anapopatwa na magumu ya kifedha, labda gharama zaweza kupunguzwa. Kukiwa na mabadiliko fulani-fulani katika bajeti (makadirio ya matumizi), labda mahitaji yaweza kutimizwa, ingawa matakwa tu ya aina ya kimwili hayatatimizwa. Ili kupunguza gharama, mapainia fulani hushiriki nyumba moja pamoja na Wakristo wengine. Wakiwasaidia watoto wao kupainia, nyakati fulani wazazi huandaa makao ya bure au ya bei ya chini sana. Wengine huwasaidia mapainia kulipia chakula na usafiri. Lakini mapainia hawangetaka kuwa mzigo kwa wengine, kwani wana wajibu wa Kimaandiko wa kujitegemeza.—2 Wathesalonike 3:10-12.

Bei za usafiri zinaweza kupunguzwa kwa kugawanya gharama pamoja na mapainia wengine. Ikiwa mapainia wawili wana magari, wanaweza kushiriki pamoja katika kazi ya kuhubiri katika eneo moja, wakitumia gari moja na kuepuka gharama ya kuendesha magari mawili. Mapainia ambao hawana magari wanaweza kuungana na wale walio na magari na kushiriki katika kulipia gharama za usafiri. Gharama za kusafiri zinaweza kupunguzwa zaidi kwa kueneza maeneo ya karibu kwa kutembea hasa. Katika nchi nyingi mapainia hutumia usafiri wa umma wa bei ya chini.

Newton Cantwell na mke wake walikuwa miongoni mwa wale walioshinda matatizo ya kifedha na kudumu katika utumishi wa wakati wote. Waliuza shamba lao, wakaanza kupainia pamoja na watoto sita kati ya saba katika 1932, wakati wa Ule Mshuko Mkubwa wa Thamani ya Fedha. “Upesi tulikuwa tumetumia fedha zote tulizopokea baada ya kuuza shamba letu—hasa kwa gharama za daktari,” akaandika Ndugu Cantwell. “Twakumbuka kwamba tulipohamia mgawo wetu wa pili, tulikuwa na fedha za kutosha tu kulipia kodi ya majuma mawili kimbele, tukibaki na dola tano. Hata hivyo, tulijua kwamba Yehova angeandaa maadamu tungeendelea kutimiza utumishi wetu kwa bidii-nyendelevu. . . . Tulijifunza kupunguza gharama kwa njia mbalimbali. Kwa kielelezo, tulipohamia eneo jipya, nilikuwa nikisema na baadhi ya wenyeji wa vituo vya petroli na kueleza kwamba tulikuwa tukiendesha magari matatu kila siku kuhusiana na kazi yetu ya Kikristo. Kwa kawaida tokeo lilikuwa kwamba tulipunguziwa bei ya [petroli]. Upesi wana wetu walijifunza kurekebisha magari yetu, wakituokolea fedha nyingi za kulipia gharama za gereji.” Hivyo, akina Cantwell walikabiliana kwa mafanikio na magumu ya kifedha, wakadumu katika utumishi wa wakati wote. Ndugu Cantwell alikuwa bado kwenye orodha ya mapainia alipokufa akiwa na miaka 103.

Kupata Kazi ya Muda-Muda

Mapainia wengi hujitegemeza kifedha kwa kazi za muda-muda. Ili kujitegemeza katika huduma huko Korintho, Paulo alifanya kazi akiwa mfanyi-hema pamoja na waamini wenzake Akila na Prisila. (Matendo 18:1-11) Leo, mara nyingi ndugu wa kiroho wanafurahi kutolea mapainia kazi ya kimwili ya muda-muda. Mapainia wengine hupata kazi hiyo kupitia wakala mbalimbali wa kuajiri unaotoa kazi za muda. Imani katika Mungu ni muhimu, na pia sala yenye bidii ili kupata mwongozo wake katika kufanya maamuzi ya kuajiriwa.—Mithali 15:29.

“Baada ya kupata nguvu nyingi kutokana na kufikiria mambo kwa sala,” akasema painia mmoja, “nilimjulisha msimamizi wangu kwamba kazi yangu ya kihuduma ni daraka zito la kibinafsi na kwamba singeweza kukubali kazi ya wakati wote. Jumatano iliyofuata, niliombwa kama ningekubali kazi hiyo lakini ikiwa ya muda-muda. Nilikubali kwa furaha.” Usipunguze umaana wa nguvu za sala, na ufuatie sala zako kwa matendo.

Huenda mapainia wakaona inafaa kuwaambia wale watakaowaajiri kwamba kusudi la kutafuta kwao kazi ya muda-muda ni kujitegemeza katika huduma. Wanaweza kutaja siku ambazo wanapatikana na idadi ya saa kwa juma wanazoweza kutoa kwa kazi. Dada wawili wa kimwili waliweza kugawanya kazi ya wakati wote katika kampuni ya kisheria, ikiwezesha kila mmoja wao afanye kazi siku mbili na nusu kwa juma. Hilo liliwategemeza wakiwa mapainia mpaka walipohudhuria Watchtower Bible School of Gilead na kupokea migawo ya mishonari.

Aina mbalimbali za kazi zinazokubalika Kimaandiko zinaweza kupatikana kwa kuongea na waamini wenzetu na wengine au kwa kuchunguza matangazo ya gazeti la habari. Unyenyekevu ni wenye kusaidia, kwani unaweza kuwazuia mapainia wasiwe wateuzi mno juu ya aina ya kazi ambayo wangeweza kufanya. (Linganisha Yakobo 4:10.) Ili kuendelea kupainia huenda wakahitaji kufanya kazi ya kimwili ambayo watu fulani huona kuwa ya hali ya chini au yenye umaana mdogo. Kazi hiyo ikikubaliwa lakini kazi nyingine inatamaniwa, badiliko katika kazi ya kuajiriwa lawezekana hatimaye.

Afya Mbaya na Kuvunjika Moyo

Ni lazima wengine waache utumishi wao wa painia kwa sababu ya matatizo makubwa ya afya. Hata hivyo, ikiwa mapainia si wepesi katika kufanya uamuzi huo, huenda wakaona kwamba ugonjwa fulani unaweza kuponywa au afya inaweza kuwa bora vya kutosha ili waweze kuendelea kupainia. Wengi wanaweza kupainia yajapokuwa matatizo ya kiafya kwa sababu wanatibiwa, wanashikamana na ulaji unaowafaa, na kupata pumziko na mazoezi yanayohitajiwa. Mwangalizi mmoja asafiriye alimwona dada mmoja painia aliyeteseka sana na ugonjwa wa uyabisi na kuchochota kwa viungo hivi kwamba alihitaji msaada wa kutembea nyumba kwa nyumba katika huduma. (Matendo 20:20) Lakini, yeye na mume wake waliongoza mafunzo ya Biblia nyumbani 33 na walikuwa wamesaidia watu 83 kukubali kweli ya Mungu. Baada ya wakati fulani afya yake iliboreka, na miaka 11 baadaye alihudhuria Shule ya Utumishi wa Painia.

Kuvunjika moyo kwaweza kuwafanya wengine waache huduma ya painia. (Mithali 24:10) Painia mmoja alimwambia mwangalizi mmoja asafiriye hivi: “Mimi nitaacha kupainia. . . . Nina gharama za kulipa.” Alihitaji miwani iliyogharimu dola 20. “Je! utaacha kupainia kwa sababu ya uhitaji wa dola 20?” mwangalizi huyo akauliza. Ilidokezwa kwamba painia huyo afanye kazi kwa siku moja katika shamba lililopandwa kahawa, achume hizo dola 20, anunue miwani, na kuendelea kupainia. Mazungumzo zaidi yalifunua kwamba tatizo la msingi lilikuwa ni kuvunjika moyo juu ya gharama kubwa za kurekebisha gari. Ilidokezwa kwamba painia huyo apunguze gharama kwa kuendesha gari katika eneo la maili chache kila siku badala ya kuliendesha mbali sana. Pia alishauriwa adumishe hali yake ya kiroho. Painia huyo alitumia shauri hilo na miezi sita baadaye akapokea mwaliko wake wa kuhudhuria Shule ya Gileadi. Baada ya kuhitimu alipewa mgawo wa kwenda nchi ya kigeni, akatumikia huko kwa uaminifu kwa miaka mingi hadi kifo chake. Naam, mara nyingi, tusiposhindwa na hali ya kuvunjika moyo na tukikumbuka kwamba Yehova yuko nasi, baraka nyingi hutokea.

Hazini Pendeleo Lako la Utumishi

Yajapokuwa majaribu, kama vile hali za kuwa na uhitaji na nyakati bila chakula, Paulo aliiona huduma yake kuwa hazina. (2 Wakorintho 4:7; 6:3-6) Watumishi wengi wa Yehova katika Afrika, Esia, Ulaya ya Mashariki, na kwingineko wameendelea katika pendeleo lao la kupainia, wajapokabili magumu na mnyanyaso leo. Kwa hiyo, unapokabili majaribu, jitahidi sana kudumu katika utumishi huu wenye mapendeleo, kwa sifa ya Yehova.

Mapainia wengi waliweza kuingia kazi ya kuhubiri wakati wote kwa sababu tu walirahisisha mtindo-maisha wao. Kama vile Paulo, walikinza vishawishi vya kimwili, wakasitawisha kuridhika na “chakula na nguo.” Ili kudumu katika utumishi wa painia, wanahitaji kuendelea kuridhika na mambo ya lazima. (1 Timotheo 6:8) Shangwe hutokana na kuhazini mapendeleo yetu ya kupewa na Mungu, tukiyatanguliza kabla ya mali za kimwili.

Kwa kutoa kielezi: Anton Koerber alikuwa na pendeleo la kuwakilisha masilahi ya Ufalme kwa maofisa wa serikali katika Washington, D.C. Alitumikia akiwa painia kwa muda fulani na alikuwa mwangalizi wa mzunguko katika miaka ya 1950. Wakati mmoja baadhi ya wale waliokuwa washiriki wake wa biashara zamani walimjia wakimtolea kazi fulani ambayo ingemwezesha kujipatia dola milioni moja. Lakini, ili kufanya hivyo, angalilazimika kutoa wakati wake wote kwa shughuli za kibiashara kwa muda wa mwaka mmoja hivi. Baada ya kusali ili kupata mwongozo na roho ya akili timamu, alisema hivi: “Siwezi kuacha mapendeleo yangu mazuri ajabu ya kumtumikia Yehova nikiwa hapa hata kwa mwaka mmoja tu, la, hata nikipewa fedha zote ulimwenguni. Kuwatumikia ndugu zangu nikiwa humu Washington ni jambo lenye thamani kubwa zaidi kwangu, na nikiwa hapa najua nina baraka ya Yehova. Bila shaka ningechuma dola milioni moja, lakini mwishoni mwa mwaka mmoja wa aina hiyo ya maisha, ningekuwa namna gani kiroho, au hata kimwili?” Basi alikataa toleo hilo. Kuhazini mapendeleo yao kwa njia iyo hiyo huwasaidia wengi kudumu katika utumishi wa painia.

Mapainia hufurahia baraka tukufu kama nini! Ni baraka kutumia muda wa saa nyingi kusema juu ya umaliki mtukufu wa Yehova. (Zaburi 145:11-13) Kwa sababu ya kutoa wakati mwingi sana kwenye huduma, mapainia wana baraka ya kuleta faraja ya kiroho kwa walio maskini na wenye kuonewa, kwa wagonjwa au waliofiwa, na kwa wengine wanaosononeka sana na kuhitaji tumaini la hakika. Kwa hiyo, hali zikituruhusu kushiriki katika kazi ya kuhubiri wakati wote, kwa kweli tutafurahia baraka nyingi. ‘Baraka ya Yehova ndiyo hutajirisha.’ (Mithali 10:22, NW) Na ni kwa msaada wake na baraka yake kwamba wale wapiga mbiu ya Ufalme wengi hudumu kwa furaha katika utumishi wa painia.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki