Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w93 10/1 kur. 22-25
  • Uwe na Maoni Yafaayo Juu ya Rehema ya Mungu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Uwe na Maoni Yafaayo Juu ya Rehema ya Mungu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Je! Sisi Hupata Kusababu Hivyo?
  • Maoni Yafaayo Ni Yapi?
  • Maoni ya Yesu
  • Kuzoezwa kwa Uvumilivu
  • Uaminifu-Maadili Usio na Masharti
  • Je! Rehema ya Mungu Inafunika Dhambi Zako Zote?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • ‘Baba Yenu Ni Mwenye Rehema’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
  • Tunamtumikia Mungu Aliye “Tajiri Katika Rehema”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2021
  • Kukombolewa kwa “Damu Yenye Thamani”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
w93 10/1 kur. 22-25

Uwe na Maoni Yafaayo Juu ya Rehema ya Mungu

DAKTARI alikuwa mwenye fadhili na mwenye ufikirio sana. Kulingana na uamuzi wake mzuri kabisa, mgonjwa wake alihitaji upasuaji sana ili kuokoa uhai wake. Mgonjwa huyo aliposita na kutokeza suala la kutiwa damu mishipani, daktari alishangaa. Alipoeleza kwamba asingeweza kukubali kufanyiwa upasuaji uliohusisha kutiwa damu mishipani, kwa sababu za kidini, daktari aliduwazwa sana. Alijaribu sana kupata njia za kumsaidia mgonjwa huyo. Hatimaye, alifikiri kwamba alikuwa amepata suluhisho. Alisema: “Wajua, usipokubali kutiwa damu mishipani, utakufa. Hutaki hivyo, sivyo?”

“Bila shaka la,” mgonjwa wake akasema.

“Lakini, yaonekana, ukikubali [kutiwa damu mishipani], utaasi itikadi zako za kidini, ambazo ni za maana kwako pia. Basi, hili ndilo dokezo langu. Kwa nini usikubali kutiwa damu mishipani na hivyo uokoe uhai wako. Halafu ungama kwa Mungu kwamba umetenda dhambi, na kutubu. Kwa njia hiyo, utarudishwa katika dini yako pia.”

Daktari huyo mwenye nia njema alifikiri kwamba alikuwa amepata jibu kamilifu. Alifahamu kwamba mgonjwa wake alimwamini Mungu mwenye rehema. Kwa hakika, hiyo ilikuwa pindi ifaayo ya kujifaidi kutokana na rehema ya Mungu! Lakini, je, dokezo lake lilifaa jinsi lilivyosikika kuwa lenye kufaa?

Je! Sisi Hupata Kusababu Hivyo?

Nyakati nyingine huenda tukajipata wenyewe tukisababu kwa njia ambayo daktari huyo alisababu. Labda twaogopeshwa na mlipuko usiotazamiwa wa upinzani shuleni au kazini. Au huenda tukajipata wenyewe katika hali ya kuaibisha ambamo tumo chini ya msongo wa kufanya jambo linaloudhi dhamiri yetu. Tunaposhtuliwa, huenda tukawa na mwelekeo wa kufuata mwendo ulio rahisi zaidi na kufanya jambo tunalojua ni baya, tukiwa na nia ya kuomba msamaha baadaye.

Au huenda watu mmoja-mmoja wakashawishwa na mielekeo yao wenyewe mibaya. Kwa kielelezo, huenda kijana akajipata mwenyewe katika hali ambamo anashawishwa kwa nguvu kutenda ukosefu wa adili. Badala ya kupiga vita dhidi ya tamaa hiyo mbaya, huenda akashindwa, akiwa na nia ya kurekebisha mambo na Mungu baadaye. Wengine hata wamefikia hatua ya kufanya dhambi nzito ijapokuwa wanajua kwamba wangeweza kutengwa na ushirika wa kutaniko la Kikristo. Yaonekana wamesababu, ‘Nitangojea muda mfupi upite. Kisha nitatubu na kurudishwa.’

Hali hizo zote zina mambo mawili yanayofanana. Kwanza, watu mmoja-mmoja wanashindwa badala ya kung’ang’ana kufanya yaliyo mema. Pili, wanahisi kwamba baada ya kufanya lililo baya, Mungu atawasamehe moja kwa moja wakiomba tu.

Maoni Yafaayo Ni Yapi?

Je! hilo laonyesha uthamini ufaao kwa ajili ya rehema ya Mungu? Ebu fikiria kidogo rehema hiyo. Yesu alisema: “Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16) Mtume Yohana alieleza jinsi rehema hiyo inavyofanya kazi aliposema hivi: “Nawaandikia haya ili kwamba msitende dhambi. Na kama mtu akitenda dhambi tunaye Mwombezi kwa Baba, Yesu Kristo mwenye haki.” (1 Yohana 2:1) Kwa hiyo, tukitenda dhambi kwa sababu ya kutokukamilika, tunaweza kumwendea Mungu kwa sala na kuomba msamaha kwa msingi wa dhabihu ya Yesu.

Lakini, je, hilo lamaanisha kwamba haidhuru kama twatenda dhambi au la, maadamu twaomba msamaha baadaye? Hasha. Kumbuka maneno ya kwanza ya andiko hilo lililonukuliwa: “Nawaandikia haya ili kwamba msitende dhambi.” Maneno ya Yohana yanayofuata katika mstari huo yaonyesha mpango wa Yehova wenye upendo wa kushughulikia kutokukamilika kwetu. Hata hivyo, ni lazima tujaribu sana tuwezavyo kuepuka kutenda dhambi. Ama sivyo twaonyesha ukosefu wa staha wenye kusikitisha sana kuelekea upendo wa Mungu, sawa na wale wanaorejezewa na Yuda waliogeuza fadhili isiyostahiliwa ya Mungu iwe udhuru wa kuwa na mwenendo mlegevu.—Yuda 4.

Kuiona rehema ya Mungu kuwa namna ya kinga inayotulinda sikuzote yajapokuwa yale tunayofanya kunapunguza maana ya rehema ya Mungu na kuifanya ionekane kana kwamba dhambi si mbaya sana. Sivyo hata kidogo. Mtume Paulo alimwambia Tito hivi: “Neema [fadhili isiyostahiliwa, NW] ya Mungu iwaokoayo wanadamu wote imefunuliwa; nayo yatufundisha kukataa ubaya na tamaa za kidunia tupate kuishi kwa kiasi, na haki, na utauwa, katika ulimwengu huu wa sasa.”—Tito 2:11, 12.

Paulo alionyesha uthamini wake kwa ajili ya rehema ya Mungu kwa njia aliyong’ang’ana dhidi ya kutokukamilika kwake mwenyewe. Alisema hivi: “Nautesa mwili wangu na kuutumikisha; isiwe, nikiisha kuwahubiri wengine, mwenyewe niwe mtu wa kukataliwa.” (1 Wakorintho 9:27) Paulo hakuchukua mambo kizembe tu akiona kwamba ni lazima atende dhambi mara kwa mara. Je! twapaswa kufanya hivyo?

Maoni ya Yesu

Katika pindi moja, Yesu alionyesha jinsi alivyoona wazo la kuacha yaliyo mema na kufuata mwendo ulio rahisi zaidi ili kuepuka kuteseka. Alipoanza kuwaambia wanafunzi wake juu ya kifo chake cha kidhabihu kilichokuwa kikija, Petro alijaribu kumzuia, akisema: “Hasha [uwe mwenye fadhili kwako mwenyewe, NW], Bwana, hayo hayatakupata.” Yesu aliitikiaje? “Nenda nyuma yangu, Shetani; u kikwazo kwangu; maana huyawazi yaliyo ya Mungu, bali ya wanadamu.”—Mathayo 16:22, 23.

Karipio la Yesu lenye nguvu kwa Petro lilionyesha kwa njia ya kutokeza kwamba Yesu alikataa kufuata mwendo ulio rahisi uliohusisha kuasi dhidi ya mapenzi ya Mungu. Rekodi yaonyesha kwamba alifuata kijia kifaacho bila ugeugeu, akisumbuliwa daima mikononi mwa Shetani. Mwishowe alidhihakiwa, akapigwa vibaya, na kupatwa na kifo chenye maumivu makali. Hata hivyo, hakuridhiana, na kwa sababu hiyo aliweza kutoa uhai wake ukiwa fidia kwa ajili yetu. Kwa hakika hakuvumilia hayo yote ili tuweze ‘kuwa wenye fadhili kwetu wenyewe’ wakati magumu au vishawishi vinapotokea!

Inasemwa hivi kuhusu Yesu: “Umependa haki, umechukia maasi [uasi-sheria, NW].” (Waebrania 1:9) Kwa kawaida kufuata njia iliyo rahisi ili kuepuka magumu huhusisha uasi-sheria. Kwa hiyo, tukiuchukia kikweli—kama vile Yesu alivyouchukia—tutakataa kuridhiana sikuzote. Katika kitabu cha Mithali, Yehova asema hivi: “Mwanangu, uwe na hekima na kunifurahisha moyo wangu; ili nipate kumjibu anilaumuye.” (Mithali 27:11) Uadilifu wa Yesu wenye usawaziko lakini usio wenye kuridhiana uliletea moyo wa Yehova furaha nyingi. Tunaweza kumfurahisha Yehova vivyo hivyo tukifuata mwendo wa Yesu wa uaminifu-maadili.—1 Petro 2:23.

Kuzoezwa kwa Uvumilivu

Mtume Petro aliandika hivi: “Mnafurahi sana wakati huo, ijapokuwa sasa kwa kitambo kidogo, ikiwa ni lazima, mmehuzunishwa kwa majaribu ya namna mbalimbali; ili kwamba kujaribiwa kwa imani yenu, ambayo ina thamani kuu kuliko dhahabu ipoteayo, ijapokuwa hiyo hujaribiwa kwa moto, kuonekane kuwa kwenye sifa na utukufu na heshima, katika kufunuliwa kwake Yesu Kristo.” (1 Petro 1:6, 7) Kwa sababu sisi si wakamilifu na twaishi miongoni mwa ulimwengu wa Shetani, tutakabiliwa daima na mitihani na vishawishi. Kama vile Petro aonyeshavyo, hivyo vyaweza kutumikia kusudi zuri. Vinatahini imani yetu, kuonyesha kama ni dhaifu au yenye nguvu.

Pia vyatumika kutuzoeza. Yesu “alijifunza kutii kwa mateso hayo yaliyompata.” (Waebrania 5:8) Tukivumilia chini ya mtihani, sisi pia twaweza kujifunza kutii, pamoja na kumtegemea Yehova. Na utaratibu huo wa kujifunza utaendelea mpaka ukamilike, kama vile Petro alivyosema: “Mungu . . . mwenyewe atawatengeneza [atamaliza mazoezi yenu, NW], na kuwathibitisha, na kuwatia nguvu.”—1 Petro 5:10.

Lakini tukiridhiana chini ya mtihani, twajionyesha kuwa waoga au dhaifu, wenye kupungukiwa na upendo wenye nguvu kuelekea Yehova na uadilifu au wenye kupungukiwa na sifa ya kujidhibiti. Udhaifu wowote wa aina hiyo huhatarisha sana uhusiano wetu na Mungu. Kwa kweli, onyo la Paulo laweza kutimia katika hali yetu: “Tukifanya dhambi kusudi baada ya kuupokea ujuzi wa ile kweli, haibaki tena dhabihu kwa ajili ya dhambi.” (Waebrania 10:26) Ni bora zaidi kama nini kutokutenda dhambi hapo mwanzoni kuliko kushindwa na udhaifu na kupatwa na hatari ya kupoteza taraja lote la uhai!

Uaminifu-Maadili Usio na Masharti

Katika siku za nabii Danieli, Waebrania watatu walitishwa kwa kifo cha moto ikiwa wasingeabudu sanamu fulani. Itikio lao lilikuwa nini? “Kama ni hivyo, Mungu wetu tunayemtumikia aweza kutuokoa na tanuru ile iwakayo moto; naye atatuokoa na mkono wako, Ee Mfalme. Bali kama si hivyo, ujue Ee mfalme, ya kuwa sisi hatukubali kuitumikia miungu yako, wala kuisujudia hiyo sanamu ya dhahabu uliyoisimamisha.”—Danieli 3:17, 18.

Walichukua msimamo huo kwa sababu walitaka kufanya yaliyo mema. Kama ungeongoza kwenye kifo chao, basi na iwe hivyo. Walikuwa na uhakika katika ufufuo. Hata hivyo, ikiwa Mungu angewaokoa, hilo lingekuwa bora zaidi. Lakini msimamo wao imara haukuwa na masharti. Ndivyo ipaswavyo kuwa kwa watumishi wa Mungu sikuzote.

Katika siku yetu wengine ambao wamekataa kuridhiana wametiwa gerezani, kuteswa, hata kuuawa. Wengine wametoa dhabihu za kimwili, wakipendelea kuendelea wakiwa maskini kuliko kuwa tajiri kwa kugharimu kanuni zinazofaa. Ni nini kilichompata yule mwanamke Mkristo aliyetajwa mwanzoni mwa makala hii? Yeye alithamini nia ya yule daktari, yenye fadhili isipokuwa yenye kuongozwa vibaya, lakini hakuacha imani yake. Badala ya hivyo, kustahi kwake sheria ya Yehova kulimwongoza akatae ule upasuaji. Kwa furaha, alipona kwa vyovyote vile, akaendelea kumtumikia Yehova kwa bidii. Hata hivyo, alipochukua msimamo wake, hakujua tokeo lingekuwa nini, lakini alikuwa tayari kuacha mambo yote mikononi mwa Yehova.

Ni nini kilichomsaidia aendelee imara hivyo chini ya msongo? Yeye hakujaribu kutegemea nguvu zake mwenyewe, wala mtumishi yeyote wa Mungu hapaswi kufanya hivyo. Kumbuka kwamba, “Mungu kwetu sisi ni kimbilio na nguvu, msaada utakaoonekana tele wakati wa mateso.” (Zaburi 46:1) Ni bora zaidi kama nini kumgeukia Mungu ili kupata msaada ukiwa chini ya jaribu lolote kuliko kutenda dhambi kisha kulazimika kumgeukia ili kupata rehema!

Naam, acheni tusipuuze kamwe rehema kuu ya Mungu. Badala ya hivyo, acheni tukuze tamaa ya kweli ya kufanya yaliyo mema, hata tunapokabili magumu. Hilo litatia nguvu uhusiano wetu na Yehova, litatupa sisi mazoezi tunayohitaji kwa ajili ya uhai wa milele, na kuonyesha staha ifaayo kwa ajili ya rehema ya Mungu. Mwenendo huo wenye hekima utauletea shangwe moyo wa Baba yetu wa kimbingu.

[Picha katika ukurasa wa 24]

Uhakika kamili katika ufufuo uliwasaidia wale Waebrania watatu wadumishe uaminifu-maadili

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki