Ulimwengu Bila Wezi
ILITUKIA upesi sana. Mtu mmoja mwenye mavazi mazuri alielekeza bastola kichwani pa Antônioa akiwa mbele ya nyumba yake katika São Paulo, Brazili, akaamuru apewe funguo na hati za wenyeji wa gari lake, akatoroka upesi kwa gari hilo.
Katika Rio de Janeiro, wanaume wanne wenye silaha nyingi walimweza mtu aitwaye Paulo, machoni pa binti yake wa miaka kumi. Halafu, baada ya kuendesha gari hadi kwenye nyumba yake, wanyang’anyi hao waliingia wakaiba walichotaka, wakiyajaza magari mawili ya Paulo. Wakitisha kumuua mke wa Paulo, walimpeleka yeye na mwajiriwa mmoja wakiwa watekwa hadi kwenye duka la Paulo mjini la kuuzia vito, ambalo walipora kila kitu chenye thamani. Lakini, bila kutazamiwa, wezi hao walipiga simu baadaye, wakisema walikoyaacha magari.
Kwafadhaisha kama nini kunyang’anywa fedha na mali zilizochumwa kwa kazi ngumu! Ingawa wala Antônio wala Paulo hawakuchukua hatua wenyewe, wengine hufanya hivyo bila kutumia njia za kisheria. Huenda wakamlipiza mwizi vikali, au huenda wakapoteza uhai wao wenyewe. Kwa kielelezo, mwanamke mmoja Mbrazili aliponyang’anywa saa yake na kijana mmoja, mwanamke huyo mwenye hasira alitoa bastola mkobani mwake akampiga mwizi huyo risasi, akamwua. Tokeo lilikuwa nini? O Estado de S. Paulo laripoti: “Watu waliojionea tukio hilo walisifu sana mtazamo wa mwanamke huyo asiyejulikana, na hakuna mmoja aliyetaka kuwasaidia polisi kumtambulisha.” Ingawa wanatamani ulimwengu bila wezi, Wakristo hawalipizi kisasi kama mwanamke huyo alivyofanya. Kwa kuwa kisasi ni cha Mungu, wao hutii maneno haya kwenye Mithali 24:19, 20: “Usikasirike kwa sababu ya watenda mabaya; wala usiwahusudu wabaya; kwa maana mtu mbaya hapati thawabu.”
Lakini, waweza kufanya nini ukishambuliwa? Tukio moja katika Rio de Janeiro laonyesha jinsi ilivyo muhimu kubaki ukiwa mtulivu. Mkristo mmoja, Heloísa alikuwa njiani akienda kwa basi kuongoza funzo la Biblia. Wanaume wawili wakaanza kuwaibia abiria. Alipofika kituo cha basi alikopaswa kushuka, Heloísa aliwaambia kwamba alikuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova na kwamba alikuwa akienda kuongoza funzo la Biblia. Alionyesha Biblia yake na kitabu cha funzo. Bila kumwibia, hao wezi walimruhusu ashuke. Lakini, abiria mwingine hakuruhusiwa kushuka. Dereva alisema baadaye kwamba hakuwa ameona kamwe jambo lolote kama hilo.
Regina pia alibaki akiwa mtulivu alipoamriwa na watu wawili wenye silaha, aingie ndani ya gari lake. Regina alitoa ushahidi, akionyesha nakala yake binafsi ya gazeti Amkeni! Kwa kuwa wanyang’anyi hao walikuwa na wasiwasi, aliwaomba wafungue kile kikabati kwenye sehemu ya mbele ya gari alimokuwa ameweka peremende. Lakini walipoona kaseti za Kingdom Melodies, walianza kuusikiliza muziki huo. Kwa kuwa hali ilikuwa yenye urafiki zaidi, wanyang’anyi hao waliamua kumwacha Regina kwenye barabara kuu bila kumdhuru, wakimhakikishia kwamba angepata mtu mwenye fadhili wa kumsaidia. Baada ya kutembea kwa muda wa dakika kumi, alipata nyumba, lakini mwenye-nyumba huyo hakuweza kuamini simulizi lake, akisema: “Huonekani kana kwamba umeshambuliwa; wewe ni mtulivu sana.”
Ingawa huenda ikawa mtu aliyeibiwa hakudhuriwa kimwili, ono hilo lenye kutia wasiwasi mwingi laweza kuwa na matokeo mazito ya baadaye. ‘Huenda mtu huyo akawa mwenye kutohisi usalama, mwenye chuki kuelekea washiriki wa familia au wale wanaojaribu kumsaidia, asiweze kuwatumaini wengine, akitaka kupanga mambo madogomadogo kupita kiasi, huenda akahisi kwamba ulimwengu si wenye haki,’ laripoti O Estado de S. Paulo. Kinyume cha hilo, mtu mwenye kuibiwa amtumainiye Yehova Mungu aelekea zaidi kupona ono hilo bila madhara ya kimwili na ya kihisiamoyo. Hata hivyo, je, usingekubali kwamba ingekuwa baraka ikiwa kusingekuwako uhalifu tena wala lolote lenye kusababisha hofu?
“Mwibaji Asiibe Tena”
Ingawa wengi hupendelea mtindo-maisha wao wenye pupa, Neno la Mungu limewasaidia wezi wabadili tamaa zao na nyutu zao. (Waefeso 4:23) Wakiwa na kusudi la kweli, lenye msingi wa Biblia maishani, wanatia maanani maneno haya: “Afadhali mali kidogo pamoja na haki, kuliko mapato mengi pamoja na udhalimu.” (Mithali 16:8) Cláudio asimulia hivi: “Karibu wote katika familia yangu walikuwa Mashahidi, lakini sikusikiliza kamwe yale waliyosema juu ya Yehova na makusudi yake. Niliporudi kutoka safari ya karibu kilometa 2,000 katika lori dogo lililoibwa, nililazimika kupita vizuizi vingi vya uchunguzi wa polisi. Nilipofanya hivyo niling’amua kwamba nilipaswa kubadili maisha yangu. Nilikuwa nimejaribu kufanya hivyo kabla ya hapo lakini bila kufanikiwa. Wakati huu nilianza kufikiri juu ya watu wangu wa ukoo walio Mashahidi wa Yehova na jinsi walivyo tofauti, wakiwa na shangwe, furaha, na amani.” Likiwa tokeo, Cláudio alianza kujifunza Neno la Mungu, akaacha dawa za kulevya na wale waliokuwa marafiki wake, akawa mhudumu Mkristo.
Sasa wengine pia hutii maneno haya: “Msitumainie dhuluma, wala msijivune kwa unyang’anyi.” (Zaburi 62:10) Baada ya kifungo cha gerezani kwa sababu ya kujaribu kumwua mtu wakati wa unyang’anyi, José, mzoelevu wa dawa za kulevya na mlanguzi wa dawa hizo, alinufaika kutokana na funzo la Biblia pamoja na ndugu-mkwe wake. Aliacha kutumia na kuuza dawa za kulevya na sasa yeye ni Shahidi mwenye bidii.
Hata hivyo, utu mpya haupatikani mara moja au kimuujiza. Oscar, aliyekuwa amehusika sana na dawa za kulevya na kuiba, asimulia hivi: “Nilisali kwa Yehova kwa bidii sana hivi kwamba mara nyingi sakafu ilionekana kama ziwa dogo kwa sababu ya machozi yangu mengi.” Naam, zaidi ya funzo la Neno la Mungu lenye bidii-nyendelevu, sala ya kudumu, yenye kuhisiwa moyoni yahitajiwa. Ebu ona hekima iliyomo katika maoni haya ya sala: “Usinipe umaskini wala utajiri; unilishe chakula kilicho kadiri yangu. Nisije nikashiba nikakukana, nikasema, BWANA [Yehova, New World Translation] ni nani? Wala nisiwe maskini sana nikaiba, na kulitaja bure jina la Mungu wangu.”—Mithali 30:8, 9.
Upendo wa kweli wapaswa kuchukua mahali pa kujipendeza mwenyewe: “Mwibaji asiibe tena; bali afadhali afanye juhudi, akitenda kazi iliyo nzuri kwa mikono yake mwenyewe, apate kuwa na kitu cha kumgawia mhitaji.” (Waefeso 4:28) Kama vile katika hali ya Wakristo wa karne ya kwanza waliokuwa wamekuwa ‘wezi au wenye pupa,’ Yehova huwasamehe kwa rehema wale wanaotubu, kupitia fidia ya Yesu Kristo. (1 Wakorintho 6:9-11, NW) Inafariji kama nini kwamba twaweza kuubadili mtindo-maisha wetu na kupata upendeleo wa Mungu, haidhuru jinsi tulivyokuwa zamani!—Yohana 3:16.
Usalama Katika Ulimwengu Mpya wa Mungu
Ebu wazia dunia bila wezi. Usingehitaji mfumo wa kutekeleza sheria wenye kugharimu wa mahakimu, mawakili, polisi, na magereza! Ungekuwa ulimwengu wenye ufanisi ambao kila mtu ndani yao angestahi wengine na mali zao! Je! hilo laonekana kutoaminika? Je! kweli Mungu ataingilia shughuli za mwanadamu na kukomesha uhalifu wa sheria? Twakualika uchunguze uthibitisho kwamba Biblia ni Neno la Mungu na kwamba unabii wayo mwingi wategemeka. Utapata msingi thabiti wa kuwa na uhakika kwamba badiliko liko mbele. Hakuna awezaye kumzuia Mungu asilete kitulizo kilichoahidiwa kwa wote wapendao uadilifu: “Usikasirike kwa sababu ya watenda mabaya, usiwahusudu wafanyao ubatili. Maana kama majani watakatika mara, kama miche mibichi watanyauka.” (Zaburi 37:1, 2) Maneno hayo yaliyoandikwa zamani za kale yatatimizwa kikamili hivi karibuni.
Ufalme wa Mungu utakomesha huzuni na ukosefu wa uadilifu, ambao husababisha ukosefu mwingi wa tumaini na uhakika. Hakuna atakayekuwa na uhitaji, akijihisi kuwa chini ya msongo wa kuiba. Tunahakikishiwa hivi katika unabii: “Na uwepo wingi wa nafaka katika ardhi juu ya milima; matunda yake na yawaye-waye kama Lebanoni [ya kale], na watu wa mjini wasitawi kama majani ya nchi.” (Zaburi 72:16) Kwa kweli, katika ile Paradiso itakayorudishwa, hakuna litakalosumbua amani ya wanadamu wanaomjua na kumwabudu Mungu wa kweli.—Isaya 32:18.
Hiyo itakuwa thawabu iliyoje kwa ajili ya kukinza njia za ulimwengu huu wenye pupa! Mithali 11:19 yasema hivi: “Haki huelekea uzima; afuataye maovu hufuata mauti yake mwenyewe.” Naam, baada ya waovu kuharibiwa, hakuna atakayekuwa na sababu ya kuhofia uhai wake au mali yake. Zaburi 37:11 yatupa sisi ahadi hii: “Wenye upole watairithi nchi, watajifurahisha kwa wingi wa amani.”
[Maelezo ya Chini]
a Baadhi ya majina yamebadilishwa.
[Sanduku katika ukurasa wa 5]
Kukabiliana kwa Mafanikio na Uhalisi wa Wizi
NYUMBANI—Kwa kuwa wezi waweza kushambulia nyumba yako uwe umo ndani, au la, weka milango ikiwa imefungwa na kutiwa kufuli. Wastadi hupendekeza kuwa na ving’ora au mbwa-mlinzi. Unapoenda likizoni, julisha jirani mwenye kutegemeka. Baki ukiwa mtulivu—wanyang’anyi hutenda kwa kasi, bila kutazamiwa, na waweza kubadili mipango mara moja wakipatwa na wasiwasi. Ikiwa wewe ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova, jitambulishe mwenyewe na ujaribu kutoa ushahidi. Huenda ukaweza kuvuta urafiki au huruma. Usikinze isipokuwa ukishambuliwa kimwili.
HADHARANI—Uwe chonjo kuona ikiwa mtu fulani anakufuata. Tembea katikati ya kijia kilicho kando ya barabara. Epuka barabara zenye giza na zenye watu wachache sana. Weka kibeti chako au vitu vyako vyenye thamani mahali palipo salama. Tembea upesi kana kwamba unaenda mahali hususa. Epuka kuvaa mavazi ya bei ghali au vito vinavyometameta. Enda dukani pamoja na rafiki hali zinapohitaji hivyo. Chukua fedha utakazohitaji tu, zilizogawanywa katika mifuko au sehemu mbalimbali.
KATIKA GARI—Ikiwa “kuiba gari pamoja na dereva walo” kumekuwa jambo la kawaida katika eneo lenu, usikae katika gari lako lililoegeshwa. Badili-badili njia unayofuata unapoenda na kutoka kazini. Fuata njia iliyo salama zaidi, hata ikiwa ni ndefu kidogo. Kabla ya kuegesha gari, tazama huku na huku kuona ikiwa kuna jambo lolote linaloonekana lenye kutilika shaka. Epuka kufungua mahali pa kuwekea mizigo ukiwa katika eneo lenye watu wachache sana. Usiache vitu vyenye thamani vionekane katika gari. Mnyororo wenye kuonekana uliofungwa kwa kufuli au kifaa kingine cha kulinda dhidi ya wezi chaweza kuwazuia wezi wanaoiba vitu vidogo-vidogo.
[Sanduku katika ukurasa wa 6]
“Msijiwekee hazina duniani, nondo na kutu viharibupo, na wevi huvunja na kuiba; bali jiwekeeni hazina mbinguni, kusikoharibika kitu kwa nondo wala kutu, wala wevi hawavunji wala hawaibi.”—Mathayo 6:19, 20