Maswali Kutoka kwa Wasomaji
Je! usemi “ana zawadi ya roho,” unaopatikana kwenye 1 Wakorintho 14:37 NW, wamaanisha kwamba mtu amepokea roho takatifu katika maana ya kupakwa kwa roho, au wamaanisha kwamba ana zawadi ya kimuujiza kutoka kwa roho?
Katika New World Translation of the Holy Scriptures, mstari huo wasomwa hivi: “Ikiwa yeyote afikiri yeye ni nabii au ana zawadi ya roho, acha yeye akiri mambo ninayowaandikia, kwa sababu hayo ni amri ya Bwana.”—1 Wakorintho 14:37.
Msomaji angeweza kuchukua fungu hilo la maneno “ana zawadi ya roho” kuwa rejezeo kwenye jambo la kwamba Wakristo wa karne ya kwanza walizaliwa kwa roho wakawa wana wa Mungu wa kiroho. Au fungu hilo la maneno lingeweza kueleweka kumhusu mtu aliyekuwa amepokea zawadi ya pekee ya roho takatifu. Yaelekea kwamba ya pili ndiyo maana ya fungu hilo la maneno, kama vile muktadha usaidiavyo kuonyesha.
Hapo mtume Paulo alitumia neno la Kigiriki pneu·ma·ti·kosʹ, lililo na maana ya msingi ya “kuhusiana na roho, -a kiroho.” Namna-namna zalo zilitumiwa katika masimulizi kama vile “mwili wa kiroho,” “baraka ya kiroho,” “ufahamu wa kiroho,” na “nyumba ya kiroho.”—1 Wakorintho 15:44; Waefeso 1:3; Wakolosai 1:9; 1 Petro 2:5, NW.
Katika hali hizo, Biblia yataja kiima (mwili, baraka, ufahamu, nyumba) kinachosimuliwa na usemi “-a kiroho.” Lakini katika hali nyinginezo, maana na fasiri ifaayo ya usemi “-a kiroho” yapasa kuamuliwa kutokana na muktadha. Kwa mfano, 1 Wakorintho 2:14, 15 yatofautisha mtazamo wa mtu wa kimwili na ule wa ho pneu·ma·ti·kosʹ, ambalo humaanisha kimantiki “[the, katika Kiingereza] mtu wa kiroho.”
Wakorintho wa Kwanza sura ya 12 hadi ya 14 zakazia zawadi za kimuujiza za roho takatifu. Mungu alizitoa kwa Wakristo fulani wa mapema ili kuonyesha kwamba yeye hakuwa akitumia Israeli wa asili tena bali sasa alikuwa akibariki “Israeli wa Mungu,” wa Kikristo. (Wagalatia 6:16) Paulo aliandika hivi juu ya zawadi hizo: “Sasa kuna namna mbalimbali za zawadi, hata hivyo roho ni ile ile moja.” (1 Wakorintho 12:4, NW) Hekima, ujuzi, na imani ya pekee zilikuwa miongoni mwa zawadi za roho, kama vile kutoa unabii, kusema katika ndimi, na kutafsiri ndimi.—1 Wakorintho 12:8-11.
Wakristo katika Korintho walioandikiwa barua na Paulo walikuwa wamepakwa kwa roho takatifu ya Mungu. Paulo alisema: “Lakini mlioshwa, lakini mlitakaswa, lakini mlihesabiwa haki katika jina la Bwana Yesu Kristo, na katika Roho wa [roho ya, NW] Mungu wetu.” (1 Wakorintho 6:11; 12:13) Naam, wote walikuwa wamepokea ile “dalili ya kitu ambacho kitakuja, yaani, roho.” (2 Wakorintho 5:5, NW) Hata hivyo, si wote waliopokea zawadi ya pekee kupitia roho takatifu. Na yaonekana kwamba wengi walisisimuliwa na kule kusema katika ndimi, wakikutolea umaana wa kadiri isiyofaa. Paulo aliandika ili kusahihisha fikira zao akaonyesha kwamba ndimi hazingewanufaisha wengi kadiri ambavyo zawadi ya kutoa unabii ingewanufaisha. Mwisho wa sura ya 12, Paulo aliwashauri Wakorintho hivi: “Takeni sana karama [zawadi, NW] zilizo kuu.”—1 Wakorintho 12:28-31.
Halafu, mwanzoni mwa sura ya 14, alihimiza hivi: “Ufuateni upendo, na kutaka sana [ta pneu·ma·ti·kaʹ], lakini zaidi kwamba mpate kuhutubu [kutoa unabii, NW].” Kutaka sana nini? Wakristo hao hawakuhitaji kutaka sana kupakwa kwa roho, kwani walikuwa tayari wamepakwa kwa roho. Kimantiki Paulo alimaanisha “zawadi” za roho, ambazo alikuwa amewahimiza watake sana, mwishoni mwa sura ya 12. Kwa hiyo, New World Translation of the Holy Scriptures hufasiri 1 Wakorintho 14:1 hivi: “Endeleeni kutafuta zawadi za kiroho kwa bidii.” Hapo tafsiri nyingine za Biblia hufasiri neno ta pneu·ma·ti·kaʹ kuwa “[the, katika Kiingereza] zawadi za kiroho” au “[the, katika Kiingereza] karama za Rohoni.”
Tukiwa na muktadha huo, twaona kwamba karibu na mwisho wa sura ya 14, Paulo ahusianisha kutoa unabii na pneu·ma·ti·kosʹ. Kama vile katika mstari 1, muktadha wadokeza kwamba alimaanisha kuwa na zawadi ya roho. The New Testament in Modern Speech, cha R. F. Weymouth, chatumia fasiri hii: “Ikiwa yeyote ajihesabu mwenyewe kuwa nabii au mtu mwenye zawadi za kiroho, acha yeye atambue yale ninayoandika kuwa ni amri ya Bwana.”
Naam, Wakristo wote, wawe walikuwa na zawadi ya kutoa unabii au zawadi nyingine yoyote ya roho, walihitaji kukubali na kufuata lile shauri ambalo Paulo aliandika kuhusu jinsi mambo yapaswavyo kutendeka katika kutaniko.